Mgombea UVCCM Arusha atuhumiwa kuwa Chadema

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Monday, 08 October 2012 07:48


Mussa Juma, Arusha

MPASUKO ndani ya CCM Mkoa wa Arusha umechukua sura mpya baada ya Kamati ya Siasa kumsimamisha Mwenyekiti wa UVCCM, Wilaya ya Arumeru, Boniface Laizer akidaiwa kuwa na uhusiano wa karibu na Chadema.


Laizer ambaye pia ni mgombea wa nafasi ya Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Arusha katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Jumatano wiki hii, anadaiwa kuwa mfuasi wa kambi ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa.Hata hivyo, kusimamishwa huko kunaelezwa na baadhi ya watu walio ndani ya CCM kuwa ni mizengwe ya kisiasa dhidi yake.


Amesimamishwa siku 15 tu baada ya kuchaguliwa kushika nafasi hiyo ya uenyekiti wa UVCCM Arumeru.Laizer licha ya kugombea nafasi ya UVCCM Mkoa, pia alikuwa anagombea nafasi ya mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Baraza la Wazazi Taifa akiwakilisha jumuiya hiyo.Barua ya CCM Mkoa wa Arusha ya kumsimamisha kazi Laizer inaeleza kuwa uamuzi huo umechukuliwa na Kamati ya Siasa ya Mkoa ambayo ilifanya kikao chake Septemba 27 hadi Septemba 29, mwaka huu.


“Kamati ya Siasa ya Halmashauri Kuu ya Mkoa iliyokutana kuanzia Septemba 27 hadi Septemba 29, 2012, ilitafakari kwa kina tuhuma zinazokukabili na kwa mamlaka iliyonayo kwa mujibu wa Katiba ya CCM ya 1977, toleo la 2007-Ibara ya 96 (7) iliazimia kukusimamisha uongozi,” inaeleza sehemu ya barua hiyo ya Oktoba Mosi, mwaka huu iliyosainiwa na Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda.


Mtuhumiwa ajitetea Akizungumzia uamuzi huo wa Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Arusha kumsimamisha kwa tuhuma kwamba alishiriki mikutano ya Vuguvugu la Mabadiliko la Chadema (M4C) mkoani Lindi, Laizer alisema ilifikia hatua hiyo baada ya kuona picha gazetini ikimwonyesha Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akishiriki shughuli za chama mkoani Lindi huku nyuma akionekana mtu ambaye anafanana naye.“Wanalo gazeti moja ambalo kuna sura ya mtu tunafanana naye na tayari mimi nimefuatilia nimemjua kuwa ni mlinzi wa Mbowe anaitwa Swai, sasa wanasema ni mimi, wamenisimamisha...


Huu ni uonevu,” alisema Laizer.“Sasa vijana wamenichagua (Arumeru) kwa kuwa wana imani na mimi, nimekuwa katika chama hiki muda mrefu tunafanya kazi, sasa wao wanaibuka sasa na siasa za makundi,” alisema Laizer.Hata hivyo, alisema kwamba ana imani kubwa na vikao vya juu vya chama kwamba vitarejesha jina lake ili agombee nafasi alizoomba mbali ya kuwa amesimamishwa kazi yake mpya aliyoshinda hivi karibuni.


NagoleMwenyekiti wa CCM Mkoa wa Arusha, Onesmo Nagole alipoulizwa kuhusiana na suala hilo jana alikiri kusimamishwa uongozi kwa Laizer akisema anafanyiwa uchunguzi. Hata hivyo, alisema suala hilo litakamilika mapema na haki itatendeka.


Chadema nako moto

Wakati hali ikiwa hivyo ndani ya CCM, harakati za kuwania urais mwaka 2015 ndani ya Chadema zimepamba moto baada ya kada mwingine wa chama hicho kutangaza kuwa atawania nafasi hiyo kupitia chama hicho.


Aliyetangaza nia hiyo ni Katibu Baraza la Vijana Chadema (Bavicha) Mkoa wa Tanga, Deogratius Kisandu.Hivi karibuni, Naibu katibu Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe alitangaza kuwa atawania nafasi ya urais kupitia chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao.


Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini alisema hatagombea tena nafasi ya ubunge na badala yake anaelekeza nguvu zake katika kuwania urais kwani anaamini kuwa anazo sifa za kugombea nafasi hiyo.Kisandu katika taarifa yake iliyotumwa katika gazeti hili alisema kuwa sasa ni wakati wa kufanya mageuzi ya kiuchumi nchini.


Tayari Mwasisi wa Chadema, Edwin Mtei amekaririwa akikemea hatua ya Zitto kutangaza kuwania urais mapema akisema hali hiyo inachochea migogoro ndani ya chama.

 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom