Mgodi Kiwira changa la macho

ipyax

JF-Expert Member
Nov 1, 2010
4,040
6,291
WAFANYAKAZI WASEMA HAUJAREJESHWA SERIKALINI



WAFANYAKAZI wa mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira wilayani Kyela, mkoani Mbeya, wametoboa siri kwa kueleza kuwa mgodi huo haujarudishwa serikalini kutoka kwa mwekezaji, kampuni ya Tanpower and Resources inayohusishwa na rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa.

Wamedai licha ya serikali kuutangazia umma miaka mitatu iliyopita kuwa imeuchukua mgodi huo unaodaiwa kuuzwa kwa bei chee ya sh milioni 70 hadi kufikia sasa hakuna makabidhiano ya kimaandishi yaliyofanyika kati ya mwekezaji huyo na serikali.

Kufuatia hali hiyo wamemwandikia barua Waziri Mkuu wakitaka kukutana naye Januari 18 mwaka huu, jijini Dar es Salaam ili kumweleza kilio chao hicho na endapo hawatasikilizwa wataandaa maandamano makubwa jijini humo na baadaye Februari mwaka huu wataelekea mkoani Dodoma kufanya tena maandamano ambako vikao vya Bunge vitakuwa vikiendelea.

Hayo yaliibuliwa mwishoni mwa wiki na mwenyekiti wa chama cha wafanyakazi wa migodini na ujenzi (Tamico), Daniel Kibona, wakati wa mkutano wa wafanyakazi uliokuwa na lengo la kujadili mustakabali wao kutokana na serikali kuwatelekeza bila kuwalipa mishara kwa miezi sita, hali inayofanya waishi maisha magumu.

Katika mkutano huo uliohudhuriwa na wafanyakazi wote wa mgodi huo wapatao 430 na kufanyika kwenye ukumbi wa Chen ulioko mgodini hapo, walisema kitendo cha serikali kutoujali mgodi huo na kuacha mitambo yenye thamani ya mabilioni ikiteketea ni dalili za wazi kuwa haijaurudisha serikalini mgodi huo.

Wakieleza kwa masikitiko makubwa, wafanyakazi hao walidai kusikitishwa na kitendo cha Waziri wa Nishati na Madini, William Ngereja, kwa kushindwa kutekeleza ahadi ya kuwajali kwa kuwalipa mishahara yao ambayo malimbikizo hayo yamefikia zaidi ya sh milioni 600.

Walisema katika Bunge la Bajeti la mwaka 2010 /11 Waziri Ngereja aliliomba Bunge hilo kupitisha bajeti ya wizara yake ili iweze kulipa wafanyakazi hao ambao wamekuwa wakiishi maisha magumu na yasiyo na matumaini, lakini tangu bajeti hiyo ipitishwe serikali haijawalipa mishahara yao.

Akizungumza kwa machungu, mmoja wa wafanyakazi mgodini hapo Frank Andrew, alisema kutokana na serikali kushindwa kuwalipa malimbikizo ya mshahara wao kwa zaidi ya miezi sita, hivi sasa wanaishi kwa kutegemea kuuza mkaa na maembe.

“Hali ni mbaya; sisi na familia zetu, huwezi amini tunaishi maisha ya mlo mmoja kwa siku, lakini pia hivi sasa tunashukuru msimu wa maembe kwani angalau wake zetu wanaenda kukusanya maembe na kwenda kuuza walau tunapata fedha ya mboga na chumvi,” alisema Andrew.

Katika barua hiyo waliyomwandikia waziri mkuu yenye kumbu namba TAMICO/KCM/VOL.2/01/011, wamelalamikia serikali kutowajali kwa kushindwa kuwalipa mishahara kwa miezi sita, kukosa huduma za kijamii ikiwemo matibabu bora, lakini pamoja na kunyimwa fursa ya kwenda kujitafutia kazi nyingine ili kutafuta fedha za kujikimu na familia zao.

Meneja wa mgodi huo, Adam Abdu, alikiri kuwa wafanyakazi hao wanakabiliwa na hali ngumu ya maisha kwa kuwa serikali haijawalipa mishahara ya miezi sita zikiwemo na stahili nyingine.
 
There is no fool so great a fool as a knowing fool. But to know how to use knowledge is to have wisdom. Spurgeon -
 
Back
Top Bottom