Mgao wa Umeme Wamalizika!

nyengo

JF-Expert Member
Oct 27, 2010
454
184
Serikali ya Tizamia ambayo imekuwa kizani tangu kuzaliwa kwa nchi hiyo hatimae imefanikisha kumaliza tatizo hilo lililokuwa likiuvuta shati uchumi wake kwa miongo kadhaa sasa. Hayo yalisemwa jana na Mkuu wa Mamlaka ya Nishati wa Tizamia, Mh. Wiliamson Geresha, katika hotuba aliyoitoa katika moja ya vijiji ambako alikwenda kuzindua mradi mkubwa wa nishati mbadala (jua na upepo).

Huku akishangiliwa na wanakijiji waliokuwa wakisikiliza taarifa yake kwa shauku kubwa, na pia akiwa amezingirwa na vyombo lukuki vya habari, Mh. Geresha alisema, "Kwa mara ya kwanza tangu dunia kuumbwa hatimae kijiji hiki cha Msonyo, na vijiji vingine 700 nchini kote, taa zinawaka na watoto wetu wanaweza kujisomea hadi usiku wa manane, baadhi ya wanakijiji wameweza kufungua saluni za kike na kiume, wapo waliofanikiwa kuanzisha biashara za kuuza vinywaji baridi na vikali na kutengeneza faida nzuri kutokana na kuwa na majokufu, baadhi ya vijana wameanzisha biashara za kuchaji simu, hongereni" Alisema Geresha huku akisikika kwa taabu kutokana na ushangiliaji wa muda wote wa wanakijiji.

"Haya yote yamewezekana kwa usimamizi makini wa Serikali yenu ya Tizamia, ukusanyaji sahihi wa kodi ambazo badala ya kwenda kulipa posho za watawala, kununua magari ya kifahari, na kwenda kuwatibu watawala nje ya nchi na kufanya shopping baada ya matibabu, tumeweza kuwekeza kodi hizo katika manunuzi ya vifaa vya umeme-jua na upepo na kuvifunga bila malipo ya ziada katika nyumba ya kila mwanakijiji, zahanati, nyumba za ibada, bila kusahau sehemu za starehe kama bar na kumbi za muziki." Aliendelea kusema Mh. Geresha.

Mbali na mambo mengine, Mh. Geresha pia alisema, "Serikali ya Tizamia kwa miaka nenda rudi imekuwa ikipiga maktaimu kukimbizana na vyanzo vya nishati ambavyo vimeshatutupa mkono, ila kwa kudra za Mwenyez Mungu, uongozi bora, na maono wa wananchi na watawala wa Tizamia, hatimae tumefunguka akili zetu na kuona ni kwa jinsi gani tulivyoacha jua linalowaka siku 365 za mwaka kupotea bure. Ni jambo lisilofichika kwamba kwa upatikanaji wa nishati hizi mbadala hakika tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuongeza ukusanyaji wa kodi za serikali kwa sababu sasa wananchi wetu mmeweza kuanzisha miradi kadhaa inayowaingizia kipato, wananchi wanapata na serikali inapata, mambo waaaa!" Aliesema Mh. Geresha huku wanakijiji wa Msonyo wakimshangilia kufa na kupona.

Upatikanaji wa nishati ya umeme ya uhakika katika nchi ya Tizamia ni hatua kubwa kuwahi kufanikishwa na serikali yake katika kipindi kisichopungua miongo minne. Matumizi ya nishati mmbadala ya umeme katika makazi ya watu kumetoa mwanya kwa umeme wa gridi ya taifa kutumika kwa matumizi makubwa kama ya viwandani na mashirika makubwa ya serikali.

Viwanda vingi vikubwa vilivyokuwa vimefungwa vimeanza kufufuliwa tena na vingi vimekabidiwa kwa wawekezaji ambao ni wazawa wa nchi ya Tizamia. Pia pamekuwa na mfumuko wa kasi wa uzalishaji toka katika viwanda vidogovidogo ambavyo vingi viko maeneo ya vijijini. Viwanda hivi vidogo ni vile vya usindikaji matunda (ambayo awali yaliozea shambani), mbogamboga, vinywaji vitokanavyo na matunda n.k. Hii imewezesha Tizamia kuwa nchi ya wazalishaji na walaji, tofauti na hapo awali ambapo nchi hiyo ilikuwa ni soko na jalala la vyakula vya sumu pekee.

Nilipopata wasaa wa kuzungumza na mwenyekiti wa kijiji cha Msonyo, baada ya Mh. Wiliamson Geresha kukamilisha hotuba yake, alinieleza haya, "Tangu kukamilika kwa mradi huu wa uwekaji wa umeme mbadala katika majumba yetu, kwa ruzuku ya serikali, tumeshuhudia wimbi kubwa la vijana wetu waliokimbilia mjini wakirejea na kutengeneza ajira hapahapa kijijini."

"Ndungu mwandishi, jina la kijiji hiki ni Msonyo, jina hili lilitokana na hasira watu walizokuwa nazo kwa serikali yao ambayo ilikuwa ikiahidi tu kutuletea huduma hii na wasifanye hivyo. Msonyo ni jina lilitokana na usonyaji wa wanakijiji kila walipokuwa wakiona chochote kinachowakilisha serikali, iwe ni gari la mkuu wa wilaya, awe mwenyekiti wa kijiji, mjumbe wa nyumba kumi, au hata ofisi ya serikali za mtaa. Watu walikuwa wakisonya kuonesha dharau kwa ahadi za uongo za serikali ya Tizamia. Lakini sasa ni tofauti, tumepata nishati hii tuliyokuwa tukiisikia tu kwa wenzetu wa mjini, ambao nao hawakuifaidi sana pia kutokana na mgao. Kwa hili la kutupatia umeme ni jambo jema sana na hata uhasama kati ya raia na serikali yao sasa basi" alisema mwenyekiti huyo ambaye jina lake tumelipiga kabari.

Naye Mh. Wilamson Geresha, Mkuu wa Mamlaka ya Nishati alikuwa na haya ya kusema, "Kwa kitambo sana serikali yetu ya Tizamia ilichukulia tatizo la ukosefu wa nishati ya umeme kama tatizo la msimu, tatizo linalotukumba wakati wa kiangazi na kusababisha ukosefu wa maji ya kusukumia mitambo ya kuzalisha nishati hiyo. Lakini baada ya miaka mingi serikali ikishirikiana na mchango wa kimawazo wa raia wake (ambao kwa miaka mingi tuliamini ni mbumbumbu), tuligundua kuwa tumekuwa tukipoteza sana kiuchumi na hivyo kuamua kulivalia njuga suala hiki kwa dhati kabisa."

"Siyo serikali pekee iliyofanikisha hili, wananchi ndio hasa wahusika wakuu kutokana na kodi zao na mchango wa mawazo yao, halafu kuna wataalamu wa makampuni binafsi ya nishati hizi mbadala, ambao ndio waliofunga umeme huu nchi nzima, serikali mchango wake umeegemea zaidi katika kutengeneza sera za kumuinua mwananchi wake na kusimamia kwa dhati dhana ya uongozi bora na uadilifu wa viongozi."

"Umeme huu wa jua na upepo ni ukombozi wa kweli kwa mwananchi wa Tizamia kwanu hawatatozwa tozo la mwezi zilizokuwa zinakusanywa na shirika la umeme la TANZU. Jua na upeo tunapata bure toka kwa Mungu kwa nini tuwatoze wananchi wetu? Sisi tutatoza kodi za haki zitakazotokana na uzalishaji wao. Tizamia Oyeee!" Alimaliza Mh. Geresha huku wanakijiji wa Msonyo wakimbeba juu juu kumpeleka kwenye gari lake. Nilishuhudia gari la Mkuu huyu lilisukumwa na wanakijiji hao hadi katika mpaka wa kijiji hicho.


Tizamia Oye! (Itikia Oyeeee!). Swadaktaaa, tukutane wakati mwingine.
 
Nimeipenda hiyoo. Ungeiweka ktk gazeti kusudi na wengine waisome
 
Back
Top Bottom