Mchakato huu wa Katiba ufanywe kwa uwiano

Crashwise

JF-Expert Member
Oct 23, 2007
22,227
8,735
Mchakato unaoendelea sasa wa kutoa maoni ya nini kiwemo ndani ya Katiba Mpya ufanywe kwa kuzingatia uwiano wa walioko mijini na vijijini, na pia uhusishe jamii ambayo kwanza inaifahamu Katiba ni kitu gani na umuhimu wake, na kwamba jamii hiyo iwe na uwezo wa kutoa maoni ya kulifanya taifa liwe na Sheria hii mama itakayodumu kwa zaidi ya Karne moja ijayo.


Hoja za maingizo ya vipengere ndani ya Katiba mpya zisitolewe kwa jazba na shinikizo zitokanazo na imani za kisiasa, lazima ikumbukwe kuwa Katiba mpya ijayo isiegemee kuwagusa makundi maalumu tu kama ya wanasiasa, waumini wa dini mbalimbali, makabila, maskini, matajiri nk. Itakuwa ni kwa ajili ya Watanzania wote na wa rika zote.


Natambua kwa uhakika kuwa sehemu kubwa sana ya Watanzania hasa walioko vijijini hawajawahi kuiona Katiba iliyopo sasa, na hata pengine hawafahamu kwamba nchi zote za kidemokrasia duniani zinaongozwa na Katiba.


Wananchi wengi hawafahamu umuhimu wa kuchangia maoni ya kuiandaa Katiba mpya ambayo ndio dira itakayowalinda na kuwaongoza katika maisha yao wakiwa sehemu ya jamii inayowajibika katika kuleta maendeleo ya taifa.
Nina wasiwasi mkubwa sana kwamba wananchi wengi hawatapata fursa ya kuchangia ipasavyo kutokana tu na wao kutokujua nini fursa zitokanazo na Katiba zinavyoweza kuwapa haki zao Kikatiba.


Nchi hii haijawa bado na utamaduni wa kuendesha elimu ya uraia kwa wananchi wake, masuala pekee yanayowajumuisha wananchi wote katika maamuzi ya kitaifa ni wakati wa kipindi cha chaguzi mbalimbali za viongozi wa vyama vya siasa.
Ni kwa wakati huu tu ambapo wananchi wanahamasishwa kufanya maamuzi ya kupiga kura ili kuwapata viongozi wawakilishi wa maendeleo yao, ingawa katika hilo bado wananchi walio wengi hawatambui haki zao za msingi Kikatiba za kuwawajibisha wale wanaowachagua mara wanapokiuka ahadi wanazozitoa mara wanaposhinda katika chaguzi hizo.
Wanaoijua vizuri Katiba ni hao wanaoingia katika madaraka ya ama Ubunge, Uwakilishi, Udiwani nk. Lakini suala la kupata elimu ya kutambua na kujua haki za u-raia wa kila mwananchi ni haki ya msingi ya kila mwananchi.
Zipo gharama za msingi za kulifanya taifa lishiriki kwa asilimia kubwa katika mchakato wa kutoa maoni ya Katiba mpya, na serikali isione vibaya kupoteza fedha nyingi hizo kwa kazi hii muhimu ya kuwajumuisha wananchi wake wote katika kutoa maoni. Ingawa pia naliona hilo siyo jepesi sana kutokana na Jiografia ya nchi hii pamoja na mtawanyiko wa wananchi wengi waliojichimbia huko vijijini.


Nina imani kuwa baadhi ya wananchi wengine hawajui sasa kama ipo Tume iliyoteuliwa kwa ajili ya kazi ya kukusanya maoni ya Katiba mpya, na baadhi yao watakapofikiwa na Tume hiyo wanaweza kuchanganyikiwa wakadhani labda Tume hiyo ni wawakilishi wa chama cha siasa! Au wakadhani ni Tume inayopita nchini ili kutathmini ardhi yao kwa ajili ya wawekezaji. Inaweza ikawa huo ni mwendelezo wa suala lile lile la kukosa elimu ya kutokujua nini kinachoendelea nchini.


Maamuzi ya kuhusisha wananchi wote katika maamuzi makubwa yanayohusu uhai na ustawi wa taifa yanahitaji umakini na weledi wa hali ya juu. Tume iliyoteuliwa imekubalika na makundi yote nchini, siwezi kutoa kasoro katika hilo kwani mpaka sasa hakuna pingamizi la kuhoji uteuzi uliofanywa na Rais Kikwete kwa wajumbe hao.
Ninachokiona hapa ni namna wajumbe hao watakavyopata mikiki ya kuwafikia wananchi wengi waishio vijijini. Mawasiliano yatakayofanywa na ujumbe huo kwa baadhi ya wananchi yanaweza kuwakwaza katika maeneo mengine wasipate walichokitaka, na hilo linaweza kuwa pia ni tatizo lililosababishwa na kutotoa elimu mapema kwa walengwa.
Wananchi wanatakiwa kuijua kwa kina Katiba yenyewe, na hilo linawezekana kwa kuwatumia viongozi wa serikali za vijiji, ambao kama ilivyokuwa wakati wa operesheni ya Kisomo cha Elimu ya Watu wazima enzi ya miaka ya sabini, ambapo madarasa yaliendeshwa kwa utaratibu wa usimamizi maalumu, hatimaye wananchi wengi wakajua kusoma na kuandika.


Serikali iliingia gharama kubwa kufanikisha dhamira ya kufuta ujinga. Hata hili la kuelimisha wananchi kuhusu Katiba mpya linahitaji maelekezo na mawasiliano maalumu na viongozi walioko karibu na wananchi, na wala lisiwe la muda mfupi, kwani matokeo yake itakuwa kuibua Katiba mpya iliyokosa uwiano wa maoni ya wananchi wote.


Nalisema hilo kwa msisitizo kwani dalili za wananchi za kutokujua michakato inayofanywa ya kuwahusisha katika maamuzi iliwahi kujidhihirisha katika mkutano mmoja wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 kutokana na kutoelewa misamiati, ambapo mgombea mmoja wa jimbo moja mkoani Iringa wakati akijinadi aliwasihi wananchi wamchague kwa kuzingatia demokrasia.


Mwananchi mmoja akakurupuka na kuhoji kwamba "'demokrasia ' tena ni chama cha nani?". Hayo ni moja ya mapungufu ya kutopata elimu ya uraia kwa wananchi, mwananchi huyo hakujua neno hilo lina maana gani, pia si ajabu Tume hii iliyoteuliwa ya kukusanya maoni ikakumbana na maswali ya wananchi ya kutokujua maneno ya kawaida yanayotumika kama 'Katiba Mpya'.


Tusipokuwa waangalifu katika hili, tutazalisha Katiba mpya inayozingatia zaidi maoni ya wananchi walioko mijini, hata kama hao walioko vijijini watahusishwa bila wao kujijua.
 
...Hoja za maingizo ya vipengere ndani ya Katiba mpya zisitolewe kwa jazba na shinikizo zitokanazo na imani za kisiasa, lazima ikumbukwe kuwa Katiba mpya ijayo isiegemee kuwagusa makundi maalumu tu kama ya wanasiasa, waumini wa dini mbalimbali, makabila, maskini, matajiri nk. Itakuwa ni kwa ajili ya Watanzania wote na wa rika zote....

Mkuu umeongea point sana ila hapo kwenye red sijui kama wale majambazi wa Uamsho, mabwana zao, na vibaraka wao wataelewa somo kutokana na umimi/usisi uliowajaa.
 
Watakaoharibu mchakato huu wa katiba ni walewale tunaozan wanaifaham katiba, watakaotumia muda mwingi kujifanya wanawatafsilia wengine kwa mitizamo yao ili waungwe mkono,

Iikumbukwe kuwa mwaka 1992 waliowengi walikataa vyama vingi si kwamba hawakuona umuhim wake bali ni matokeo ya tafsiri za wale waliojivisha jukum la kuwaelimisha wengine juu ya vyama vingi,

Wakaweka tafsiri yao katika hali ya vitisho hatimaye wananch wa kawaida wakaogopa na kuvikataa ni 20% ndio waliokubali, hoja ya kutoijua katiba ya zaman haina mantiki kwani hatuihitaji katiba ya zamani kwa sasa, watu waulizwe ktk hali ya kawaida kabisa wanataka nchi yao iongozwe namna gani, rasilimali zimilikiwe vp.n.k

Hamna haja ya kuwatisha na kufikiri kwamba hawawezi kuwa na maamuzi mpaka wafundishwe mwishowe wanapotoshwa na hao hao wanaojifanya wanawaelimisha.
 
Back
Top Bottom