Mbunge Titus Kamani CCM aua Shinyanga?

Candid Scope

JF-Expert Member
Nov 8, 2010
11,883
6,883
HATIMAYE Mbunge wa Jimbo la Busega wilayani Magu, mkoani Mwanza, Dk. Titus Kamani (CCM), amejisalimisha kwa Jeshi la Polisi mkoani Mwanza, kujibu tuhuma zinazomkabili za kula njama kutaka kumuua aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Dk. Raphael Chegeni (CCM). Kujisalimisha kwa Dk. Kamani kumekuja siku chache baada ya jeshi hilo kutangaza kutaka kutumia nguvu kumsaka na kumkamata, iwapo angeendelea kukaidi amri ya kuja jijini hapa kutoa maelezo ya tuhuma hizo zinazomkabili za jinai.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi ofisini kwake, Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza, na Kamishna Mwandamizi wa Jeshi la Polisi (ASP), Simon Nyakoro Sirro, alithibitisha kujisalimisha kwa mbunge huyo, ambaye alibanwa maswali ‘mazito' kwa muda kadhaa na maofisa wa polisi juu tuhuma zinazomtaja kuhusika kwake katika njama za kutaka kumuua Dk. Chegeni ambaye inadaiwa pia ni ndugu yake wa damu. Kamanda Sirro alisema mbunge huyo wa Busega alifika na kuhojiwa mwishoni mwa wiki iliyopita, na baada ya mahojiano aliachiwa na kwamba polisi wapo kwenye upelelezi wa kina na wakikamilisha upelelezi wao watampandisha mahakamani kuungana na watuhumiwa wengine wanne wa kesi hiyo ya jinai.

Tetesi zinadai kwamba, Dk. Kamani alijisalimisha katika Kituo Kikuu cha Polisi jijini Mwanza Jumamosi ya Juni 25 mwaka huu, na siku hiyo hiyo inadaiwa alianza safari kurudi Dodoma kuhudhuria vikao vya Bunge la Bajeti, ambapo inaelezwa alipofika mkoani Shinyanga gari lake lililokuwa likiendeshwa na dereva wake lilimgonga mzee mmoja na kufariki dunia papo hapo.

"Hakuna jinsi, tutamfikisha tu mahakamani, mbona wengine tuliwafikisha?", alisema Kamanda huyo wa Polisi, Sirro, wakati akijibu swali la Tanzania Daima ilipotaka kujua iwapo atafikishwa mahakamani na kuunganishwa na watuhumiwa wengine wanne waliopo mahakamani.
Mei 31 mwaka huu, inaelezwa kuwa Jeshi la Polisi mkoani hapa liliiandikia barua Ofisi ya Bunge kumwamuru haraka Dk. Kamani kuja Mwanza kwa ajili ya mahojiano maalumu na polisi juu ya tuhuma hizo za jinai ambazo ametajwa kuhusika kutaka kumuua Dk. Chegeni.
Kwa mujibu wa barua hiyo ya Jeshi la Polisi, yenye kumbukumbu namba MZR/CID/SCR/105/2011/4 iliyotumwa kwa Katibu wa Bunge la Jamhuri, ikimtaka Dk. Kamani kuja kutoa maelezo polisi katika jalada namba MW/IR/2607/2011-MR-CC.28/2011 lililofunguliwa kwa kosa la kula njama za kuua.

Barua hiyo iliyoandikwa na kutolewa nakala kwa Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai Makao Makuu jijini Dar es Salaam na Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza kwa taarifa, ilimtaka mbunge huyo wa Busega, Dk. Kamani kufika Mwanza mapema ili aweze kutoa maelezo juu ya tuhuma dhidi yake.

Iwapo mbunge huyo wa Busega, Dk. Kamani atafikishwa mahakamani kama alivyosema Kamanda Sirro, atakuwa ni mtuhumiwa wa tano katika kesi hiyo ya kula njama kutaka kumuua Dk. Chegeni.

Watuhumiwa ambao Jeshi la Polisi lilishawafikisha mahakamani kwa tuhuma hizo ni Dismas Zacharia Ndaki, Erasto Kazimili Kombe, Queen Joseph Bogohe na Ellen Joseph Bogohe, ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Siasa (CCM) Mkoa wa Mwanza na kesi hiyo imepangwa kutajwa Julai 6, mwaka huu.


Tanzania Daima


 
Mabaya yakishaanza kukuandama hakuna pa kukimbilia, bora tu kutuliza kichwa na kufuata mtiririko uende, vinginevyo ni kuruka jivu na kukanyaga moto
 
Back
Top Bottom