Mbunge awapa shikamoo watoto akiomba kura;loh ujafa ujaumbika

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,148
MBUNGE wa Sikonge, Said Nkumba (CCM) juzi jioni alimuacha hoi Waziri Mkuu Mizengo Pinda, pale alipowapa salamu ya shikamoo watoto ili pamoja na wazazi wao wamchague tena kuendelea kuwa mbunge wa jimbo hilo katika uchaguzi mkuu ujao.

Tukio hilo lilitokea wakati Waziri Mkuu alipokuwa akiwahutubia wananchi wa Sikonge katika mfululizo wa ziara yake ya kuutembelea Mkoa wa Tabora.

Kabla ya Waziri Mkuu kuanza kutoa hotuba yake, Nkumba alipewa nafasi ya kuwasalimia wapiga kura wake, ndipo alipoitumia nafasi hiyo kutangaza nia ya kugombea tena ubunge katika uchaguzi mkuu utakaofanyika baadaye mwaka huu.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu, wakati ulipokuwa ukiahirisha kikao cha Bunge kilichopita ulisema sasa ni wakati muafaka kwetu kurudi kwa wapiga kura wetu ili kuwapa shikamoo.

“Leo ni siku ya bahati kwani watu wengi wamejitokeza katika mkutano wako huu na mimi naomba kuitumia nafasi hii kutoa shikamoo. “Kwa heshima na taadhima shikamoooni watoto wote mliopo hapa kuanzia mnaonyonya, watoto wa halaiki, watoto mliopo shuleni na shikamooni vijana na wazee wote mliopo hapa,” alisema Nkumba.

“Napenda sasa kutumia nafasi hii kutangaza nia kwamba nitagombea tena ubunge katika Jimbo la Sikonge na naomba wote mniunge mkono,” alisema Nkumba.

Tukio hilo lilimfanya Waziri Mkuu aliyekuwa amekaa jukwaani na viongozi wengine wa kitaifa, mkoa na wilaya, kuvunjika mbavu kwa kicheko.

Hata hivyo baada ya hotuba ya Waziri Mkuu, yalifuata maswali na kero kutoka kwa wananchi ambapo mkazi wa kijiji cha Tutuo, Hussein Juma, alimlalamikia mbunge huyo kuwa katika kipindi cha miaka 10 ya ubunge wake hajawahi hata kuchangia dawati moja katika shule ya kijiji chao.

“Ni sawa mbunge wetu kutangaza nia lakini na yeye anapaswa kuelewa kuwa hata wadogo zake wanapenda kusoma. Nasema hivyo kwa sababu katika kipindi chote cha ubunge wake hajawahi kuchangia hata dawati moja katika shule yetu,” alisema Juma.

Akizungumzia hilo, Waziri Mkuu, alisema ni dhana potofu kwa wananchi kudhani kuwa Mbunge anaweza kutoa msaada katika kila kijiji au katika kila mradi wa maendeleo.

“Mbunge ni mtumishi kama watumishi wengine wa serikali. Sidhani kama anaweza kuchangia kila mahali. Hata mimi ni Mbunge, yapo maeneo ambayo nimechangia lakini pia yapo maeneo ambayo sijachangia. Kikubwa hapa ni ushirikiano wa pamoja katika kutekeleza miradi ya maendeleo,” alisema Pinda.

Waziri Mkuu amehitimisha ziara yake ya siku saba mkoani Tabora jana kwa kutembelea Wilaya zote sita za Igunga, Nzega, Tabora, Uyui, Urambo na Sikonge.
 
Back
Top Bottom