leseiyo
Senior Member
- Oct 25, 2007
- 116
- 3
Na Reuben Kagaruki
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kesho kutwa kinatarajia kufanya mkutano mkubwa wa hadhara mkoani Mwanza kutoa tathmini ya mapambano ya vita dhidi ya mafisadi.
Mkutano huo unaotarajiwa kuhutubiwa na Mwenyekiti wake, Bw. Freeman Mbowe, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya mwaka mmoja tangu CHADEMA itangaze orodha ya mafisadi 11 katika mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Mwembeyanga, Dar es Salaam, Septemba 15, mwaka jana.
Akizungumza na gazeti hili Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa CHADEMA, Bw. David Kapalila, alisema mkutano huo pia utahudhuriwa na viongozi wengine wa kitaifa wa chama hicho.
"Katika mkutano huo viongozi wa CHADEMA wataeleza mwelekeo wa vita dhidi ya ufisadi na jinsi CCM ilivyoshindwa kupambana nayo,"alisema Bw. Kapalila.
Alisema kutokana na CCM kushindwa kupambana na vitendo hivyo, chama chake kitatumia mkutano huo kutangaza mkakati maalumu wa kupambana na mafisadi ili kutokomeza vitendo hivyo.
Mbali na Bw. Mbowe, alitaja viongozi wengine watakaohutubia mkutano huo kuwa ni pamoja na Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dkt. Wilbroad Slaa, naibu wake, Bw. Zitto Kabwe na Mwanasheria wa chama hicho, Bw. Tundu Lisu
Bw. Kapalila alisema mkutano huo ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya kikao cha Kamati Kuu kilichokutana hivi karibuni jijini Dar es Salaam.
Katika mkutano uliofanyika viwanja vya Mwembeyanga, mwaka jana Dkt. Slaa akisaidiwa na Bw. Lisu walitaja orodha ya vigogo 11 waliodaiwa kuhusika na vitendo vya kifisadi.
Baadhi ya viongozi hao ni aliyekuwa Waziri wa Miundombinu, Bw. Andrew Chenge, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Bw. Nazir Karamagi, Katibu Mkuu Hazina, Bw. Gray Mgonja na aliyekuwa Waziri Mkuu, Bw. Edward Lowassa.
Baadhi ya vigogo waliotajwa kwenye orodha hiyo walitishia kumburuta Dkt. Slaa mahakamani, lakini hadi leo hakuna aliyethubutu kuchukua hatua hiyo.