Mbatia amepotoka

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
Mbatia amepotoka

Tahariri
Tanzania Daima~Sauti ya Watu​

TUMEPOKEA kwa masikitiko na mshtuko mkubwa kauli iliyotolewa mwishoni mwa wiki na Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, kuwa hakuna aliye msafi hata amnyooshee mwenzake kidole.

Sisi tunaamini ya kwamba, hiyo ni kauli ya kuvunja moyo, hasa ule wa kijasiri na kutoogopa vitisho kunakojenga utamamduni wa kutumia nafasi ya kidemokrasia katika kuwajibishana.

Tunaamini ama kwa kuwalenga watu fulani au kwa kutoa angalizo kwa wanaoingia katika vita ya kuwakemea mafisadi, kwamba wanaweza kuwa kwa namna moja ama nyingine, hawakuwa sahihi kutoa kauli hiyo katika chungu hiki kinachochemka kwa sasa.

Madhara ya kauli hiyo ni kujengeana mazingira ya woga kwa kuogopa kurushiana mawe kwa kuwa wote wamo katika nyumba za vioo, yaani wameshiriki katika vitendo vya kifisadi.

Kwa upande mwingine wa shilingi, imejenga picha kwamba sote ni mafisadi hivyo hatupaswi kuongea kauli inayoonyesha kukabiliana na tatizo hili ambalo kwa kiwango kikubwa limedumaza maendeleo ya taifa hili lililojaa maliasili za kutosha liendelee kuwa ombaomba kiasi hiki.

Ni kwa namna hii, Mbatia amejenga dhana ya kwamba kamwe hatuwezi kuwajibishana kwa lengo la kuijenga nchi.

Sisi Tanzania Daima Jumatano tuamini kwamba kuwajibishana ndiyo njia sahihi ya kuitakasa nchi yetu ambayo viongozi wake wengi kwa namna moja ama nyingine wamejihusisha na vitendo vya kuihujumu nchi. Pia watumishi, wafanyabiashara kwa namna moja ama nyingine wameshawishi vitendo vya kifisadi kuchukua hatamu na hata kuvifanya sehemu ya maisha yao kiutendaji.

Ni katika njia hii ya kunyoosheana vidole ambako Mbatia anaonekana kukinzana nako, ndiyo inayotuwezesha kuwatambua, kuwachunguza na kuwachukulia hatua kwa mujibu wa sheria wale wote wanaobainika kwenda kinyume na taratibu za utendaji kazi katika ofisi zetu za umma.

Mbatia anapaswa atambue kwamba, vita ya panzi ni faida kwa kunguru. Kwa msingi huu, vidole vinaponyoshwa kwa viongozi wa siasa, watumishi wa serikali, wafanyabiashara na viongozi wa serikali na madai hayo kuonekana yana ithibati, ni faida kwa umma. Na kupinga suala hilo, ni sawa na kulea uozo.

Tunaamini kwamba Mbatia hakuwa na nia kama taifa kuachana na harakati za kupinga ufisadi, lakini nadharia aliyotumia kamwe haitumiki kwa manufaa ya umma bali ni kwa maslahi ya mtu mmoja mmoja.

Tunachoamini ni kwamba, Mbatia alipaswa kutoa tahadhari ya kuwepo kwa umakini wa kulishughulikia suala hili la ufisadi. Kwamba nyuma ya harakati hizi, tusije tukawasahau. Lakini kutoa vitisho kama alivyovitoa kunamaanisha kwamba hata yeye kama Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi hapaswi kumtaja ama kukemea ufisadi.

Katika hili, tunawasihi Watanzania kuwa makini katika kauli kama hizi. Wasiyatumie maandiko ya vitabu vitakatifu kwa kujengea hoja kila eneo. Kuna wakati inapotosha na hata kulea uozo katika jamii.

Tuyasema hivyo kwa kujua kwamba katika utawala wa kuwajibishana kila mmoja ni mlinzi wa mwenzake. Ndiyo maana serikali inahamasisha wananchi kushirikiana ili kukabiliana na uovu wowote katika jamii.

Tujiulize swali; endapo watu wakikataa kuwataja wahalifu kwa kuwa nao watakuja kushiriki uhalifu, jamii itajengeka?

Kwa hali hiyo, tunasema kauli nyingine zitolewe kwa lengo la kuijenga nchi kwa utamaduni huu huu tulionao wa kukosoana ambao hatuna shaka kwamba ndiyo msingi wa kulijenga taifa letu.
 
Back
Top Bottom