Mawaziri tumbo joto; Wanaharakati wawasha moto

Kakke

JF-Expert Member
Dec 4, 2010
1,883
1,482
na Waandishi wetu

WAKATI Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (CHADEMA), amesema kuwa hakutumwa na Rais Jakaya Kikwete wala mtu yeyote, kuibua hoja ya kutaka Bunge lipige kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, mawaziri wengi sasa wanahaha kujaribu kujinasua na ‘fagio’ la mabadiliko ya uongozi.

Mawaziri walio katika wakati mgumu kuliko wengine wote ni wale waliotajwa na wabunge kuhusika na tuhuma za ufisadi na ubadhirifu wa mabilioni ya fedha za umma katika wizara zao.

Habari za uhakika kutoka serikalini, zimebainisha kuwa hofu ya mawaziri hao imekuja baada ya kuthibitika kuwa Rais Jakaya Kikwete atafanya mabadiliko makubwa ya Baraza la Mawaziri wakati wowote, ambapo inaelezwa kuwa atapunguza pia idadi ya wizara.

Taarifa zimesema kuwa baadhi ya mawaziri wameanza kukusanya vitu vyao, zikiwamo nyaraka na kuvihamishia majumbani mwao ama sehemu nyingine wanazoziamini kuwa salama.

Chanzo chetu cha kuaminika kutoka serikalini kimesema kuwa, hata baadhi ya mawaziri ambao hawakutuhumiwa moja kwa moja, wamekuwa wakikutana na wale wote wanaoaminika kuwa ‘watu wa karibu’ na Rais Kikwete, kwa nia ya kutaka wasaidiwe kubaki katika nafasi zao.

Hata hivyo, mmoja wa mawaziri aliyetajwa kuanza kuhamisha vifaa vyake alipoulizwa alikana kufanya hivyo na kwamba alikuwa mkoani kikazi.

Alipoelezwa namna ambavyo juzi alifika ofisini na kuondoka na rundo la vitu katika mkoba wake, waziri huyo kwanza alinyamaza, kabla ya kudai kuwa alifanya hivyo si kwa lengo la kuhama, bali ni kawaida yake kufanya kazi za ofisi nyumbani kwake.

“Si kweli, na hilo unalosema ni jambo la kawaida kwangu na hata dereva wangu anajua kuwa mara nyingi nachukua nyaraka zangu na kwenda kufanya kazi nyumbani.

“ Hata nikiwa ndani ya gari, badala ya kulala, huwa niko ‘bize’ na kufanya hiki ama kile. Kwa hiyo isichukuliwe kuwa nahamisha kitu,” alisema waziri huyo.

Zitto akana kutumwa
Akizungumza jana asubuhi katika kituo kimoja cha runinga, Zitto katika tuhuma za kutumwa na Kikwete, alisema yeye binafsi alisukumwa na taswira ya mabadiliko iliyoko kwa Watanzania wengi wanaotaka kuona hatua zikichukuliwa dhidi ya watendaji wabovu.

“Mimi nimetumwa na wananchi na ndiyo maana naishauri na kuisimamia serikali kama Katiba ya nchi inavyosema. Sasa kusema nimetumwa na Rais Kikwete, sidhani kama anaweza kufanya hivyo kwa lengo la kumwaibisha waziri mkuu wake,” alisema Zitto.

Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, alibainisha kuwa, viongozi wengi wanashindwa kusoma taswira hiyo ya watu kutaka mabadiliko.

Alifafanua kuwa alishangazwa na hatua ya waziri mkuu kuhitimisha Bunge pasipo kusema chochote kuhusiana na baadhi ya mawaziri wanaotakiwa kung’oka baada ya wizara zao kutajwa kwenye ripoti ya
Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kuhusika na ufujaji na matumizi mabaya ya fedha.

“Kwa kweli nilikuwa ‘disappointed’ na hatua ya waziri mkuu kuhitimisha Bunge bila kusema chochote, na hata nje mimi na Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe (CCM), tulimfuata na kumuuliza alimaaninisha nini? Na tulimfahamisha hatua yetu ya kuendelea na mchakato wa kutaka Bunge lipige kura za kutokuwa na imani naye,” alisema.

Alisema kwa miaka minne ripoti za CAG zimetoa mapendekezo ya kutaka watendaji wabovu wachukuliwe hatua lakini hazikufanyiwa kazi licha ya wabunge kupiga kelele.

Zitto aliongeza kuwa wazo hilo si lake binafsi wala chama chake cha CHADEMA, bali ni la Watanzania wote wenye mapenzi mema kupitia kwa wawakilishi wao bungeni na kwamba ndiyo maana aliweza kukusanya saini za wabunge 75 kutoka vyama vyote isipokuwa UDP.

Aliongeza kuwa tayari wamewasilisha hoja yao kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda, wakimtaka aitishe Bunge la dharura baada ya siku 14 ili kujadili na kupata muafaka.

“Mawaziri hawa si kwamba wengine wametajwa moja kwa moja kwenye ripoti hizo, isipokuwa wameshindwa kuwawajibisha watendaji wabovu wa chini yao na hivyo wao wanapaswa kung’oka kama sehemu ya uwajibikaji,” alisema.

Alisema kuwa Bunge halina mamlaka ya kumwajibisha waziri mmoja mmoja, hivyo njia pekee waliyonayo ni kwa waziri mkuu, kama walivyoamua kufikia hatua ya kukusanya saini ili wapige kura za kutokuwa na imani naye aondoke ama awachukulie hatua mawaziri husika.

“Tuliwapa muda mawaziri kuanzia Alhamisi hadi Jumapili ili wapime, wajiwajibishe wenyewe ama wamtose waziri mkuu, hivyo kwa kuwa hawakufanya hivyo basi sisi tunaendelea na mchakato wetu wa kumwajibisha Pinda,” alisema.

Aidha, Zitto amesema wabunge wote wa upinzani na wale wa CCM waliotia saini fomu ya kutaka waziri mkuu apigiwe kura ya kutokuwa na imani naye, wataungana na kufanya mikutano mikubwa kuhamasisha wananchi kuamua ikiwa Spika Anne Makinda atapuuza hoja yao.

Filikunjombe: Siogopi kufa
Katika hatua nyingine, Mbunge wa Ludewa, Deo Filikunjombe, ameapa kuwa yuko tayari kufa kwa ajili ya kutetea Watanzania wanyonge na kwamba haogopi vitisho uchwara vinavyotolewa na baadhi ya watu.
Alisema kamwe hawezi kukaa kimya akitazama namna Watanzania wanavyoporwa haki zao na viongozi wachache wenye uroho wa madaraka.

“Hatuwezi kufumbia macho wizi huu unaoliangamiza taifa kwa hofu kuwa ni chama changu. Ubunge wangu ni kwa manufaa ya Wana Ludewa na Watanzania wote, hivyo, wanaonishambulia wao ndio maadui wa CCM na Watanzania,” alisema mbunge huyo.

Alipuuza madai kuwa hatua yake ya kuungana na wapinzani katika suala la kutia saini kura ya kutokuwa na imani na waziri mkuu ni hatua za kukihama chama chake.

“Huo ni ujinga. Sina wazo la kukihama chama changu, nakipenda na nitaendelea kuwa mwanachama tu, labda wanifukuze,” alisema.

Wanaharakati waja juu
Nao Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) umesema kuendelea kwa ufisadi nchini ni aibu kwa serikali iliyoko madarakani, na umedai kutonyamazia aina yoyote ya ubadhirifu na matumizi mabaya ya fedha za miradi ya wananchi zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.

Katika taarifa yao jana, TGNP wamesema wanataka mawaziri na watumishi wa serikali wanaotuhumiwa kutumia vibaya fedha za umma kuchukuliwa hatua za kisheria.

“Ili kuonesha dhana ya uwajibikaji na utawala bora unaozingatia misingi ya haki za binadamu, tunaitaka serikali kuwawajibisha mara moja mawaziri, manaibu waziri na watendaji wakuu wa serikali na mashirika ya umma ambao wametajwa kuhusika na matumizi mabaya ya fedha za umma au kushindwa kusimamia rasilimali za taifa.

“Rais awafute kazi watendaji wanaotumia vibaya fedha za umma na kuwaongezea wananchi umaskini, ili liwe fundisho kwa watendaji wa serikali wenye tabia kama hiyo na wachukuliwe hatua za kisheria’ imesema taarifa hiyo iliyosainiwa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji,” Anna Kikwa.
 
Mimi sina imani kabisa na jk! Sijui kama atafanya kinyume cha tunavyomfahamu. Amefanikiwa sana katika kuongoza nchi kisanii
 
hamisi kigwangala, janauary makamba na tizeba wamo katika baraza jipya....ngereja nje
 
hamisi kigwangala, janauary makamba na tizeba wamo katika baraza jipya....ngereja nje

Niseme hivi, JK alete sura mpya bado mambo yatakuwa vile vile, kwa sababu chimbuko la matatizo sio mawaziri!
 
Huyuu anayetoa taarifa za baraza la mawaziri nusu nusu maana yake nini? Kama kitu unakifahamu kiseme chote kama kilivyo na kama hujui kaa kimya. mwenye taarifa za baraza jipya la mawaziri atujuze tafadhari.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom