Mauaji ya Usa River na Kisa cha Mtego wa Panya

maggid

JF-Expert Member
Dec 3, 2006
1,084
1,246
Ndugu zangu,


Kuna kisa cha mtego wa panya uliosababisha madhara hata kwa wasio panya.
Panya kwenye nyumba aliubaini mtego wa panya uliowekwa uvunguni mwa kitanda na mwenye nyumba.


Panya yule akamwendea jogoo wa mwenye nyumba. Akamwambia; " Ewe jogoo, kuna mtego umewekwa uvunguni mwa kitanda. Tusaidiane namna ya kuutegua kabla haujatudhuru wote".


Jogoo akajibu; " Ondoka zako, mie mtego wa panya unanihusu nini wakati sina kawaida ya kufika uvunguni mwa kitanda!"


Panya yule akaenda hadi kwa mbuzi wa mwenye nyumba. Akamwambia; " Ewe mbuzi mwema, unajua kuna mtego wa panya uvunguni mwa kitanda cha mwenye nyumba. Tusaidiane mawazo ya kuutegua kabla haujatudhuru sote".


Mbuzi akajibu; " Hivi tangu lini ukaniona nikiingia chumbani kwa mwenye nyumba? Mtego huo wa panya haunihusu mie mbuzi".


Panya akaenda hadi kwa ng'ombe wa mwenye nyumba. Akamwambia; " Ewe ng'ombe wa bwana, kuna mtego wa panya umewekwa uvunguni mwa kitanda. Tusaidiane mawazo namna ya kuutegua kabla haujatuletea madhara"


Ngombe akajibu akionyesha mshangao;
" Sijapata kusikia jambo la ajabu kama hilo. Yaani, mie ng'ombe nidhurike na mtego wa panya ulio uvunguni mwa kitanda! Hilo halinihusu."


Basi, ikatokea siku moja, nyoka akaingia chumbani kwa mwenye nyumba. Katika kutambaa kwake uvunguni mwa kitanda, mkia wa nyoka ukanasa mtegoni. Kishindo kilisikika.


Mwenye nyumba alikwenda kwa furaha akiamini hatimaye panya aliyekuwa akimsumbua sasa amenaswa. Hapana, ni nyoka aliyenaswa mkia. Na ni mwenye hasira pia. Akamng'ata mguu mwenye nyumba. Sumu kali akamwachia. Mwenye nyumba akafa.


Jirani wakafika msibani. Siku ya kwanza watu walikuwa wachache. Wakahitaji kitoweo . Akakamatwa jogoo wa mwenye nyumba achinjwe.


Siku ya pili watu wakaongezeka. Kilihitajika kitoweo pia. Akakamatwa mbuzi wa mwenye nyumba ili achinjwe.


Na siku ya maziko watu wakawa wengi zaidi. Akakamatwa ng'ombe wa mwenye nyumba ili achinjwe.


Ni jogoo, mbuzi na ng'ombe wa mwenye nyumba walioamini kuwa madhara ya mtego ule wa panya yasingewahusu wao. Walikosea. Panya alikuwa sahihi, na wala mtego haukumdhuru panya!




Naam, Watanzania tunazidi kupokea habari mbaya za matukio ya mauaji ya kutisha. Vuguvugu la mapambano ya kisiasa linasemwa kuwa ni moja ya sababu za matukio ya mauaji na hata watu kujeruhiwa kwa mapanga.


Na vuguvugu la mapambano ya kisiasa halipawi kuandamama na vitendo vya mauaji au kujeruhiana kwa mapanga, bali, liwe ni vuguvugu la mapambano ya hoja.


Kule Nyamagana tumeshuhudia wabunge wamepigwa mapanga. Na jana kiongozi wa Chadema pale Usa River amechinjwa kama kuku.


Inasikitisha sana kuona vitendo hivi vya kinyama vinazidi kuongezeka. Inasikitisha pia kuwa polisi wanashindwa kwa haraka kuwatia nguvuni wahusika wa mauaji na kuwafikisha mahakamani. Labda idara za upelelezi wa kipolisi zinahitaji kuimarishwa zaidi.


Na huu ni wakati, kwa Watanzania, bila kujali tofauti zetu za kiitikadi, kidini au rangi, tukemee kwa sauti moja vitendo hivi viovu. Kamwe tusikubali ikawa ni vitu vya kawaida.


Ni wakati sasa kwa wananchi wakiongozwa na viongozi waandamizi wa vyama vya siasa. Viongozi wa kidini na wanaharakati wa haki za kibinadamu, kusimama kwa pamoja, na kwa kauli na vitendo, kulaaani maovu haya na mengineyo yenye hata kupelekea roho za wanadamu wenzetu kutoweka.


Hakika, kama mtego ule wa panya, tutafanya makosa makubwa kama kuna watakaodhani, kuwa haya ya watu kuchinjwa na kujeruhiwa na mapanga yatawakuta watu wa kundi fulani tu. Tukiacha yaendelee, basi, yeyote yule, bila kujali dini, rangi, itikadi au hata wadhifa wake, anaweza kuwa mhanga wa maovu haya. Kama taifa, kwa pamoja tuwalaani wauaji hawa.


Na hilo ni Neno Fupi la Usiku Huu.


Maggid Mjengwa,
Iringa.
0788 111 765
Mjengwa Blog::Habari,Picha,Matangazo

 
Mdharau mwiba mguu huota tende, viongozi wasikae kimya kwa hili tena askari waamke kwa hali zote wahusika wakamatwe na wasiwachekee na kuanza kuwabembeleza kama vile wanatoa posa kwa mabinti wao. Inauma sana tena sana Mungu isaidie sana Tanzania maana viongozi wanajifanya wamevaa miwani ya mbao.
 
Mkuu heri ungeendeleza hadithi bhana,huku chini umenikata stim
 
Kweli Mtupu Mkuu, leo kwao lakini kesho kibao kitageuka na kumwelekea mtegaji. Ndipo utawasikia wakilalamika amani inatoweka, wanahatarisha amani yetu na kadhalika. Yatawafika tu!
 
Mwenyekiti mimi ni mmoja wa mashabiki wako wakubwa sana kule kwenye jukwaa letu kule. Mauaji ya Arumeru ni ya kupangwa na yana malengo maalum. 'PROVOCATION' AND 'INCITE OF VIOLENCE' Yaliyofanywa na watu wenye akili kama za jaogoo, mbuzi au ng'ombe kwenye hadithi yako.

Malengo hasa ya watu hawa ni kuiprovoke CDM kama alivyofanya kwa CUF miaka ile kwa lengo ya kukifanya kuwa ni chama ni cha kigaidi au cha vurugu. Kwa jinsi karata zinavyoenda CCM wamepoteza kila kitu kutoka mioyoni mwa watanzania na njia pekee ya kuwin their hearts and mind ni kuanzisha mauaji ya kimbari 'targeted killing' kwa lengo la kufanya upande wa pili uanze nao kufanya hivyohivyo ili wapate njia ya kuzuia maandamano yanayoendelea sasa ambayo kwa vyovyo vile hawana sababu za 'kiintelijensia' za kuyazuia.

Kwa kufanya hivyo wanajisahau kuwa siku watanzania wenye subira ndogo na uelewa mdogo wakisema sasa basi watakapoanza nao kufanya 'targeted killing' hakuna atakayekuwa salama, yaani wote tutakuwa kitoweo. Jeshi la polisi limeonesha wazi kabisa kuwa halipo kwa ajili ya Public safety bali ku-enforce CCM wills on people. Igunga waliuwawa wafuasi wawili wa CDM, Arumeru wamenyongwa watu wanne na kuning'inizwa kabla ya mwenyekiti wa CDM kushambuliwa na either panga au shka kali kwa nyuma na kukata spinal cord yake. Polisi kama wangekuwa wetu wote basi nina uhakika wauaji wote wangekamatwa kwani nina uhakika kuwa wanawajua, ndiyo maana kila wakati wanakanusha kuwa mauaji eti hayahusianai na siasa.

Pindi wananchi wakianza kujilinda wenyewe tutakuwa kama law of the jungle na hata hao polisi hawatatosha wala kuweza kurudisha amani ambayo haina itikadi wala chama bali ni tunu ya watanzania kwa kuwa tumeishi bila kuumizana huko nyuma hivyo hatuna roho za visasi 'vengeance mind set'. Sasa mambo kama haya yanapanda mbegu za visasi na tusishangae kusikia vitendo hivi vinakuwa ni normal. Mungu ibariki Tanzania na mungu tuepushe na ulafi huu wa madaraka wa CCM.
 
Duuuh! Inasikitisha sana ila polisi tumieni nafasi yenu na taaluma kuwatia nguvuni wa husika bila kujali nani ni nani Lasivyo....
 
Binafsi nimesikitishwa sana na mauaji ya kikatili ya kijana yule. Inawezekana kabisa kuwa wauwaji wako katika mkakati wa kudivert mawazo na mtizamo wa watu dhidi ya CDM hasa pale ambapo CDM wakiamua na wao kulipa kisasi.
Kumbuka yaliyofanywa na wafuasi wa CCM dhidi Mbunge Highness na Machemli.. kule mwanza, Pengine matarajio ya CCM ilikuwa CDM kufanya unyama kama walofanya wao. Kana kwamba hawakuridhika wamekuja na hili la Arusha.
CCM na serikali yake wakati wao madarakani umefikia tamati,, wanachokifanya ni wao kufanya wananchi wawachukie zaidi..ni ukweli usiopingika kuwa kila serikali inayoondolewa madarakani hufanya jambo au mambo ambayo kwayo huifanya ikose uhalali wa kuongoza, kama jinsi ambavyo CCM wanafanya..
Nawasilisha!!!
 
This stuff is very educative. Thanks for your creativity guy. I like this stuff so to speak.
 
Maggid mjengwa, hii hadithi umeikosea kidogo! nimehiyari kukukumbusha, aliyetega mtego alikuwa mtoto wa mwenye nyumba, jogoo, mbuzi na ng'ombe walikataa kusaidia kuutegua mtego wakijikinai kuwa umemlenga panya ambaye kimsingi amekuwa msumbufu kwa mwenye nyumba!!! naye panya amewaambia hakika kwenye mtego huu wanaingia waliomo na wasiokuwemo, panya alidhihakiwa na kukejeliwa. ndipo alipoingia wa kwanza asiyekuwemo (nyoka) akafuata mtoto wa mwenye nyumba, akafuata aliyekuwemo jogoo, mbuzi, kondoo na ng'ombe kwa uzembe na roho mbaya zao walizodhani wanamuadabisha panya!!!!!

Najifunza:
yakiachwa kuendelea pale meza itakapogezwa juu chini, chini juu, na hili vuguvugu lisilo na mwelekeo wa kupoa la kuikataa ccm, kuikataa huku kukianza na hatimaye kukolea chumvi ya CHUKI iko siku kila mwana ccm atapaswa kulindwa na polisi watano, kwa kuendekeza siasa chuki za kina mwigulu nchemba.
 
Dah yaani hasira tupu na huzuni lakini mungu hamtupi mja wake. Wao wana hela sisi tuna mungu.
 
Mkuu, umeongea sawia.

Mwanafalsafa Socrates aliwahi sema kuwa 'binadamu wamezoea sana kuua wanyama. Tabia hii ikiendelea, wataona ni sawa kutoa uhai wa binadamu wenzao.'
Leo CCM na vyombo vyake vya dola wamenyamaza kimya kuona mauaji haya sababu walengwa ni CDM. Wakumbuke kuwa, hawa wanaowatuma kuua ipo siku watawaua hata wao CCM na familia zao sababu za kijinga kama hizi.

Na kweli, utakuwa mtego wa panya.
 
Napingana na hoja kuwa ni mauaji ya kisiasa!!! JE MAREHEMU HAKUWA DEREVA WA BODABODA?, BODABODA NGAPI ZINAIBIWA NA MADEREVA WAKE KUUAWA!!
THE HOME OF GREAT THINKERS DO NOT WANT TO THINK OUTSIDE THE RING!!
 
Na siku za mwizi ni Arobaini yote na wote wahusika na haya watabainika.Na walichofanya wauaji wa yule mwenyekiti usa-river baada ya kumpigia simu kwamba wanamwita hapo mahali walipotekeleza hayo mauaji yao walichukua simu ya marehemu ili eti kupoteza ushaidi ya nani mtu wa mwisho kuongea na marehemu wakasahau kuna server ipo Voda/Airtel inayoweka kumbukumbu zote.Kwa hiyo kwa kuanzia hapo tu napata matumaini waliohusika na mauaji hayo kama line waliotumia ilikuwa imesajiliwa wamekwisha.
Na ninaomba mungu isije ikawa walikaba mtu wakampora simu na wakatumia simu yake katika tukio hilo kwa sababu atateseka asiye kuwa na hatia.
 
Napingana na hoja kuwa ni mauaji ya kisiasa!!! JE MAREHEMU HAKUWA DEREVA WA BODABODA?, BODABODA NGAPI ZINAIBIWA NA MADEREVA WAKE KUUAWA!!
THE HOME OF GREAT THINKERS DO NOT WANT TO THINK OUTSIDE THE RING!!
Labda kwa kukusaidia tu wauaji hawakuchukua chochote toka kwa marehemu zaidi ya simu ya mkononi ikiwa ni kwa lengo la kupoteza ushaidi wa namba ya mwisho kumpgia marehemu.
Hivyo waliacha boda boda ya marehemu palepale.
 
Back
Top Bottom