Masaburi kuchunguzwa Kamati Maadili ya Bunge

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797

Tuesday, 09 August 2011 21:16
Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk Didas Masaburi
masaburi.jpg


Mussa Juma, Dodoma

KAULI ya Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Dk Didas Masaburi kwa wabunge wa jiji hilo kuwa wanafikiria kwa makalio badala ya akili, imeanza kumgeukia baada ya Bunge kuagiza kwamba suala hilo lichunguzwe na Kamati ndogo ya Madaraka, Maadili na Haki za Bunge.

Dk Masaburi akiwa jijini Arusha wiki iliyopita, aliwashambulia wabunge hao wa Dar es Salaam kwa maneno makali akisema pamoja na mambo mengine, wameshindwa kufikiri kwa ubongo badala yake wanafikiri kwa makalio, kauli ambayo juzi ilijibiwa vikali na wawakilishi hao wakimtaka meya huyo awaombe radhi kwa kuwatusi, vinginevyo watamburuza mahakamani.

Hata hivyo, ikiwa ni siku moja tangu wabunge hao wampe muda wa kuomba radhi, jana Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai alisema Bunge imelichukua suala hilo kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Akitoa mwongozo jana jioni, Ndugai alisema amelipeleka suala hilo mbele ya kamati hiyo ili lichunguzwe zaidi kwani linahusu mambo yaliyozungumzwa bungeni.

Awali, Ndugai alisema kwamba sheria zinalinda uhuru wa mbunge kujieleza akiwa bungeni kwa kutumia Ibara ya 100, Ibara ndogo ya kwanza ya Katiba ya nchi ya mwaka 1977, ambayo inaeleza kinga na haki za Bunge na kifungu cha tatu cha Sheria na Madaraka ya Bunge.

Naibu Spika alisema kanuni ya 71 ya Bunge ambayo inaelezea haki za raia wasio wabunge inafafanua kwamba, “Raia wasio wabunge wanaweza kujitetea kwa kauli, maneno au shutuma zilizotolewa bungeni kwa kupeleka maelezo kwa Spika.”

Awali, akiomba muongozo huo, Mbunge wa Kinondoni, Idd Azzan alisema wakati wa uchangiaji wa bajeti ya Wizara ya Uchukuzi, wabunge waliochangia walielezea ubadhirifu wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA) na baadhi kutaja majina ya wahusika.

Alisema baada ya hali hiyo, Waziri Mkuu alitoa tamko kuhusiana na jambo hilo kwa kuagiza kufanyika uchunguzi juu ya tuhuma hizo kwamba zingechunguzwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP).

Hata hivyo, Azzan alisema: “Lakini cha kushangaza Agosti 5, Mstahiki Meya wa Dar es Salaam, alikutana na wanahabari katika mengi aliyozungumza alisema wabunge badala ya kutumia akili wanatumia makalio katika kufikiri, kauli hii siyo tu imewadhalilisha wabunge, bali ni Bunge zima na hata wananchi waliotuchagua.” Alisema na kuongeza:

“Kwa kuwa ni kinyume cha Sheria ya Kinga, Haki na Madaraka ya Bunge, naomba mwongozo wako kwa jambo kama hili linapotokea kwa mtu kama huyu kiongozi mkubwa ambaye aliwahi kupita hapa kuomba achaguliwe.”

Rage aigeukia Kamati ya Mazingira

Mbunge wa Tabora Mjini (CCM), Ismail Aden Rage jana aliomba mwongozi wa Naibu Spika juu ya kitendo cha Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira kwenda kutembelea Mgodi wa North Mara kwa kukubali kufadhiliwa ndege na wamiliki wa mgodi huo, Kampuni ya Barrick wakati walikwenda kutafuta taarifa mbalimbali.

“Kuna taarifa kwenye vyombo vya habari leo (jana), kwamba Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, ilikwenda kwenye Mgodi wa North Mara kwa kufadhiliwa na Kampuni ya Barrick, naomba kupata ufafanuzi je, utaratibu huu ni sahihi?”

Alisema kama siyo sahihi, ilikuwaje hata Waziri wa Mazingira awepo kwenye msafara huo lakini Mbunge wa Tarime, Nyambari Nyangwine aachwe kwenye uwanja wa ndege.Hata hivyo, Ndugai baada ya mwongozo huo, aliahidi kutoa taarifa baada ya kujipa muda wa kufikiria zaidi.

 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom