Marekani yaonya raia wake kutoenda Zanzibar

MaxShimba

JF-Expert Member
Apr 11, 2008
35,772
4,054
Na Claud Mshana

MAREKANI imetahadharisha raia wake kuepuka safari zote zisizo za lazima visiwani Zanzibar kutokana na hofu ya kuibuka kwa zinazohusiana na uchaguzi wakati visiwa hivyo vikiwa kwenye zoezi la kuandikisha wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwakani.

Tahadhari hiyo, ambayo inaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa uchumi wa visiwa hivyo unaotegemea utalii, imetolewa wakati Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) ikiwa imesimamisha zoezi hilo la kuandikisha wananchi kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura baada ya kutokea vurugu zilizosababisha watu kadhaa kujeruhiwa kisiwani Pemba.

Taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani iliyotolewa jana imesema kuwa zoezi la kuandikisha wapiga kura limesababisha machafuko na hivyo kuwataka Wamarekani kuwa makini wanapotaka kufanya safari kwenye visiwa hivyo.

“Wizara ya Mambo ya Nje inawatahadharisha raia wa Marekani uwezekano wa kuwepo vurugu zinazohusiana na uchaguzi kwa sababu Zanzibar inaanza kuandikisha wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kuwa Oktoba 2010,” inaeleza taarifa hiyo iliyotumwa kwenye tovuti ya wizara hiyo.

“Wizara (ya Mamo ya Nje) inashauri kwamba raia wa Marekani waepuke safari zisizo na umuhimu za kwenda kisiwa cha Pemba cha Zanzibar. Tahadhari hiyo ya safari itadumu hadi Desemba 20,2009.

“Tangu uandikishaji wapiga kura kisiwani Pemba uanze Julai 6, 2009, kumekuwepo na taarifa nyingi kuhusu kutetereka kwa amani. Chaguzi zilizopita Zanzibar zimekuwa na matukio ya vurugu wakati wa msimu wa kampeni na wakati wa uchaguzi, na hasa katika siku na wiki zinazofuata baada ya matokeo kutangazwa.

“Vikosi vya usalama vya serikali vimeongezwa kaskazini mwa kisiwa cha Pemba, hasa kwenye wilaya za Wete na Micheweni. Uandikishwaji wapiga kura kwenye kisiwa cha Pemba unatarajiwa kumalizika Desemba 14.

Uandikishaji wapiga kura kwenye kisiwa kikubwa cha Unguja (pia kinajulikana kama Zanzibar) unatarajiwa kuanza Septemba na unaweza kugubikwa na mvutano wa kisiasa.“

Taarifa hiyo imeongeza kuwa Wamarekani wanaosafiri kwenda Zanzibar katika kipindi hiki wanakumbushwa kuwa katika tahadhari kubwa ya usalama wakati wote na kuepuka mikutano ya kisiasa, maandamano na mikusanyiko ya aina yoyote ile

Taarifa hiyo imewataka Wamarekani kufuatilia matukio ya hali halisi kupitia vyombo vya habari.

Wizara hiyo pia imewashauri hata raia wa Marekani wanaosafiri wanaokuja Tanzania, kujiandikisha kwenye ubalozi wa nchi hiyo kw akupitia tovuti ya serikali ili wapewe taarifa kuhusu safari na usalama wakati wakiwa Tanzania na kwamba wale ambao hawana huduma ya internet waende moja kwa moja kwenye ofisi za ubalozi.

Hali ya kisiasa Zanzibar imekuwa tete tangu zoezi la uandikishaji wapiga kura lilipoanza baada ya wananchi kupinga sheria iliyowekwa kuwa wanaoandikishwa ni wale tu walio na vitambulisho vya ukaazi wa Zanzibar, wakisema kufanya hivyo ni kukiuka katiba ambayo inamtambua Mzanzibari wenye nyaraka nyingine kama vyeti vya kuzaliwa.

Ilifikia wakati wananchi wa Pemba waliamua kufanya vurugu kukwamisha zoezi hilo na walifanikiwa baada ya serikali kutangaza kusitisha uandikishwaji wapiga kura.

Chama kikuu cha upinzani visiwani humo, CUF, kimekuwa kikipinga utaratibu mzima wa uandikishwaji na kimetishia kukwamisha zoezi hilo kama serikali haitaondoa suala la kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi kama sifa kuu ya kuandikishwa kupiga kura.

CUF inadai kuwa hali ni mbaya kisiwani Pemba kutokana na ukweli kuwa katika eneo lenye watu 400 ni idadi ndogo sana ya watu kati ya 40 na 50 walioandikishwa kutokana na wengi kukataliwa kwa kukosa kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi.

Utalii umekuwa na mchango mkubwa kwenye uchumi wa Zanzibar, ukitoa takriban ajira 200,000 na malengo ya serikali ni kuhakikisha visiwa hivyo, ambavyo vina historia ya aina yake na vivutio vingi, vinakuwa kituo kikuu cha watalii duniani kote.

Naye Mkinga Mkinga anaripoti kuwa Serikali ya Mapinduzi (SMZ) imeishutumu Marekani kwa onyo ililolitoa kwa wananchi wake kuhusu kutotembelea kisiwa cha Pemba kwa madai ya kutokuwepo uhakika wa usalama.

Akizungumza na Mwananchi jana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma alisema Marekani watakuwa na agenda yao ambayo hawataki kuiweka wazi ili ulimwengu ufahamu.

“Marekani wanashangaza... na kitu ambacho hakiingii akilini hata kidogo kusema kwamba Pemba hakuna aman,” alisema Juma.

Aliongeza kusema: “Pemba kuko shwari sana; nashangaa kusikia hata hiyo ‘warning (onyo)’ yao inatokana na kitendo gani hasa kilichofanywa huko Pemba?”

Alisema kuwa anawakaribisha Pemba watu wa mataifa mbalimbali kuona jinsi hali ilivyo shwari na kwamba wananchi wanaendelea na shughuli zao kama kawaida na wala hakuna vurugu kama ambavyo imesemwa na Marekani katika taarifa yake.

“Huko Pemba kuna raia wengi wa kigeni ambao wanaendesha biashara zao, mbona nchi zao hazijalalamika kuwa kuna vurugu kama inavyodaiwa na Marekani?,” alihoji Juma.

Alisema Zanzibar haiwezi kukubali uongo unaoenezwa na Marekani hata kidogo.

Imetoka: Gazeti la Mwananchi
 
Huu ndio utamaduni wa Wapemba, kuleta fujo na kuharibu jina, lol
 
Wapemba walikufanya nini? Hivi ni lazima uweke unazi katika jibu lako?
 
Marekani na wenyewe ni wanazi maana kuna nchi nyingi zenye vurugu kuliko zanzibar na hawajatoa tahadhari bali wanaona zanzibar kama ndiyo yenye matatizo.

wapemba wanatafuta haki yao wakati waunguja wanawakandamiza na kuwanyonya wapeni haki zao za kupiga kura na sio kuwanyanyasa, waandikisheni CUF ishinde mwakani ili zanzibar iendelee na kuwa nchi peke yake na sio kuungana muungano wasioutaka.
 
Marekani na wenyewe ni wanazi maana kuna nchi nyingi zenye vurugu kuliko zanzibar na hawajatoa tahadhari bali wanaona zanzibar kama ndiyo yenye matatizo.

wapemba wanatafuta haki yao wakati waunguja wanawakandamiza na kuwanyonya wapeni haki zao za kupiga kura na sio kuwanyanyasa, waandikisheni CUF ishinde mwakani ili zanzibar iendelee na kuwa nchi peke yake na sio kuungana muungano wasioutaka.

Ilianza Watanganyika wanaikandamiza Zanzibar haya sasa ikija Z'bar pekee yake Wapemba wana sema wana nyanyaswa na Waunguja. Mh! Maneno ya Mwl Nyerere yasije yakawa prophetic.
 
CUF inadai kuwa hali ni mbaya kisiwani Pemba kutokana na ukweli kuwa katika eneo lenye watu 400 ni idadi ndogo sana ya watu kati ya 40 na 50 walioandikishwa kutokana na wengi kukataliwa kwa kukosa kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi.

Kwa kweli hali ni mbaya sana pemba.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom