Mapinduzi ya fikra!!

X-PASTER

JF-Expert Member
Feb 12, 2007
11,610
1,809
MAPINDUZI YA FIKRA!!

Ni muda sasa tangia kadhia ile ya refa alipoamua kukwatua! Na mi kwa sababu moja ama nyingine nikaamua kujikalia kando na kuwa msomaji tu wa kawaida. Lakini hali hile ya kukaa tu na kuwa msomaji haikudumu sana maana ilikatizwa na swahiba wangu mpenzi. Kwa lawama na maneno ya kunishawishi niwe nami mchangiaji wa jukwaa la mambo ya siasa.

Ni kweli haswa wala si utani, wala uongo kwamba nimechoka kufanyakazi ya uhandishi hususani huu uhandishi wa kwenye forum za majibishano. Maana kuna wenye kubisha na kupinga kila jambo hata lenye faida kwa jamii, wao ni kupinga tu sababu mwandishi ni fulani na wala upingaji si wa maudhui ya kwenye mjadala husika… Waswahili wanasema kuwa “Baniani m’baya kiatu chake dawa”.

JF sasa imekuwa kama jalala kila mwenye uchafu wake anautupa hapo. Labda wale wanao nifahamu wanaweza kushangaa imekuwaje leo XP amekuwa mtu wa kukata tamaa namna hii na si kawaida yake!? Basi labda nikudokeze kidogo yanayo jiri nyuma ya fikra zangu…!

Unapokuwa nyumbani au ofisini kwako ukiandika kile ambacho unaona kina faida kwa jamii unategemea wasomaji wako kuyazingatia yale ulioyaandika na kuboresha pale ambapo kuna mushkeri, ili kuinua mawazo chanya kwenye jamii yetu na kuweza kuyafanyia kazi... Wakati mwingine huwa najiuliza ‘Hivi ni kweli huwa tunasomwa na wasomaji makini?’ Vipi wale ndugu zangu wa kule vijijini, wanayasoma haya tunayo yaandika au yanaishia hapa hapa tu!?

Basi huko kuchoka kwangu kunatokana na hali hiyo ya kufanyakazi huku ukidhani kwamba kuna watu makini walio na fikra pevu za kimapinduzi. Kumbe maskini ya Mungu, pengine hakuna anayekusoma! Na ikitokea wakukusoma ni wale wale wenye nia hasi za kupinga kila jambo kwa kuwa tu mwandishi ni Fulani.

Hata hivyo mimi si mwandishi wa kiivyo bali nachukuwa mfano huo kuwafahamisha wasomaji wangu kuwa sipendi na si suala la kupenda tu bali imani yangu hairuhusu kukata tamaa. kushughulikia tatizo ndio suluhisho. Nafikiri nimekuwa nikifanyakazi bila ya ridhaa ya wasomaji wangu; kutafuta cha kuandika nakudhani kwamba walengwa wamepata ujumbe na wameufurahia au wameukubali. Kumbe nililoandika si tatizo kwao, au hata kama ni tatizo si kubwa kama nilivyolionesha. Mambo yamekuwa kiuvyogo uvyogo!

Wapo watakao shangaa sana kuhusu nini makusudio yangu haswa…! Haya yote yamekuja baada ya kukumbuka kisa kimoja nilichokisoma zamani kidogo. Kisa cha kijana Matata, basi tega sikio usikie jinsi kijana Matata alivyokuwa na matata.

“…Matata alikuwa akifikiria kuhusu sherehe ya siku yake ya kuzaliwa. Alikuwa anafikisha miaka saba. Alikuwa haamini kama mama yake atamfanyia sherehe nzuri kama siku za nyuma, kwa sababu walikuwa wakikwaruzana kidogo katika mambo ya kitabia. Alipoona siku yake inakaribia, akaamua aende kumkumbushia mama yake. Akamwambia:

"Mama, birthday yangu inakaribia. Katika birthday hii naomba uninunulie baskeli nyekundu". Mama yake akamwambia: "Siku hizi umekuwa mbishi sana, hata husikii. Huna adabu, hata Mungu humheshimu. Kwa hiyo mimi nimeamua kuwa safari hii sikununulii chochote, kwani hata Mungu atanikasirikia kwa kumshughulikia mtoto asiyesikia".

Matata alijaribu saana kumsihi mama yake aamini kwamba sasa hivi amejirekebisha. Mama yake akamwambia: "Sasa ni lazima umhakikishie Mungu kwamba umejirekebisha, Umuandikie barua na uahidi kwamba hutarudia mambo yako ya ukaidi, kisha uilete hapa nimpelekee. Nakwambia hivyo kwa sababu kila kitu anatoa yeye, Hata hiyo baiskeli huwezi kuipata mpaka yeye atake".
Matata akaona hii ni kasheshe. Hata hivyo akakubali. Akaenda zake chumbani kwake na kuanza kumuandikia Mungu barua. Barua yake ilikuwa kama hivi:

Dear Mungu.

Napenda kukujulisha kwamba mimi sasa hivi nimeacha ukorofi kabisa.
Kwa hiyo naomba unisaidie safari hii nipate zawadi ya birthday.
Ningependelea zaidi baiskeli nyekundu, tafadhali.
Ni mimi kiumbe wako mtiifu,
Matata.


Matata akaisoma barua yake, akafikiria jinsi Mungu alivyo Kufuatana na mafundisho aliyopewa, akagundua kwamba amemdanganya Mungu na kwamba hatapata kitu, kwani Mungu hadanganyiki. Akaichana barua ile. Akajaribu kufikiria jinsi ya kuweka maneno kumfanya Mungu amuamini, lakini akaona itakuwa ni uongo na Mungu atajua kuwa ni uongo. Akapata akili. Akarusha ngumi hewani, akisema: "Yes, nimegundua la kufanya. Lazima nipate baiskeli".

Matata akanyata akaenda ukumbini. Mama yake alikuwa ni mtu wa dini sana. Alikuwa na kasanamu kake anakapenda na kukaheshimu, na mara nyingi anapofanya maombi yake hukachukua kasanamu kale na kuwa kama anaongea nako, Siku moja Matata alimuuliza mama yake kale kasanamu kalikuwa ni ka nini, mama yake akamwambia, kale ni kasanamu ka Maria Mtakatifu, ambaye ni "mama wa Mungu". Kwa hiyo hapa Matata akawa amepata ujanja. Alipofika pale kasanamu kanapowekwa, akakachukua, akakaweka mfukoni, akaenda nako chumbani kwake. Halafu akaanza kumuandikia Mungu barua.

"Mungu.
Birthday yangu inakaribia. Kama nilivyotaka kukuambia saa ile, nahitaji zawadi ya baiskeli. Uilete hiyo zawadi, mama yangu aipate haraka, maana siku zinaenda mbio. Usipofanya haraka shauri yako. Hapa ninaye mama yako, naweza kumfanyia lolote nikikasirika. Naweza kumvunja au kumtupa cho oni, au kumsaga saga chini au kumficha usimuone tena!
Hakikisha kwamba baiskeli yenyewe inakuwa nyekundu, kama ya David.

Ni mimi unijuaye".


Sasa hivi katika jamii yetu kuna akina Matata, wanaotegemea kushereheka hivi karibuni. Hawa ni wale ambao walikuwa madarakani na kipindi cha madaraka kinakaribia kwisha. Watarudi sasa kuomba zawadi za birthday, yaani wachaguliwe tena. Kabla ya hapo, wamepewa madaraka, wameleta kibri, wanajifanya wababe, hawana nidhamu. Sasa hivi watarudi mikono nyuma. Watataka kutushawishi tuamini kwamba wameshakuwa watoto wazuri.

Matata alijaribu kumueleza mama yake kwamba kaacha ukorofi, kwa hiyo apewe zawadi. Akina matata wa siasa nao wataanza kuja wakisema kwamba pamoja na matatizo na ukorofi walioufanya, kutojali hali za wananchi, kutotimiza ahadi walizotoa kabla, kuwakejeli, kuwanyanyasa, na kuwakumbatia mafisadi na mambo mengine kadha wa kadha ambayo hawaja yatimiza, sasa hivi watajionyesha wamekuwa watoto wazuri, na kwa heshima na taadhima wanataka wapewe tena "zawadi", wako radhi kutembea kwa magoti hadi vijijini kwenda kuomba kura ili waendelee kula.

Matata wangu alikubali kumuandikia barua "Mungu", lakini ana nafuu, maana alijua uwezo wa Mungu, na akajua kwamba hawezi kumdanganya. Akina Matata wa kisiasa wao hawaangalii Mungu. Hofu ya Mungu hawana. Baada ya ukorofi mwingi wataanza kuingia kwenye nyumba zetu za ibada, Misikitini na Makanisani. Watawatanguliza Masheikh na Maaskofu mbele ili wawanadi kwa waumini wao. Sina uhakika sana na haya majumba mapya ya ibada yanayo chipukia kila kukicha, nahisi nayo hayata kosa kula. Vyombo vya habari visikose kutuhabarisha tu kama viongozi wetu wa ibada washa nunuliwa tayari ili kuwapigia debe akina Matata wa kisiasa, maana wao wenyewe akina Matata maji yako kwenye pua.

Matata wangu alikuwa na akili sana, maana alijua dawa ya ushindi ni moja tu, kumkamata mama wa mtoa zawadi, akijua kwamba kwa mapenzi ya watoto kwa mama zao, "Mungu" angetoa zawadi tu. Akina Matata wa Kisiasa nao wanatafuta kila waliwezalo kuhakikisha kwamba wanapata wanachokitaka. Akili yao inawatuma kwenye kuwapora Masheikh na Maskofu. Kwa mapenzi ya waumini kwa viongozi wao hawa, basi kura zitatoka tu.

Kama Matata wangu alivyomdhania "Mungu", kwamba baada ya kuporwa mama yake angetoa baskeli, ndivyo akina Matata wa kisiasa walivyokuwa na mawazo kama hayo. Sasa hivi wanapanga kupora utu wa watu kwa kuwanunua. Kuwafanya bidhaa. Nafuu Matata wangu alimfanya Maria mateka, Matata wa Kisiasa hawapati mateka, wanapata kondoo, maana kondoo ndio hununuliwa. Na wao wakitaka kukufanya kondoo hawaangalii kama wewe ni Sheikh au Askofu, au Imamu, au maamuma, au Paroko au mlei. Wanakununua tu. Nasikia tayari akina Matata wa kisiasa wameshapata kondoo zao mapema, na ndevu zao, wamewanunua kuwatumikia.

Hili ndilo linalonisumbua sana kuhusu siasa za nyumbani. Siasa za Afrika hazionyeshi kama wapo waliojitoa kuisaidia Afrika na waafrika. Nikionacho mimi ni wanaobahatika kutawala, muda wao wa kutawala ukiisha, wanatafuta mbinu za kuendelea kutawala, na watatawala tena hata kama nchi zao zinapiga rivasi, sio kwamba wanaotawaliwa wanapenda, bali ni kwa sababu ya rafu, na katikati ya watawala na watawaliwa kuna makondoo, yako tayari kununuliwa ili wengine wote waje waswagwe na akina Matata. Makondoo haya ni yale yanayo heshimiwa na wananchi, lakini yanatumia heshima na dhamana walio nazo kuwawekea njia akina Matata wa Kisiasa, katika jina la Mungu. Si unakumbuka misamaha ya bidhaa za kidini zilipoamuliwa kulipiwa ushuru? Wenyewe walivyokuja juu… walirudisha wenyewe baada ya kutishiwa kutonunuliwa baiskeli.

Tunajuwa kabisa kwenye hizi imani, ukipigwa shavu ili geuza shavu lile. Lakini kwenye siasa hakuna kugeuza shavu, kwa hiyo tukubaliane na sera ya "shavu kwa shavu" kama wale wanaosema "pua kwa pua", "jino kwa jino". Jingine niliotaka kufahamu kutoka kwa wasomaji ni ili la kila baada ya miaka mitano chama kinacho onekana kinapata kasi ya kukubalika na watu, basi, upesi upesi kuna watu waliokabidhiwa jukumu la kukipaka matope chama kama hicho.

Nakumbuka enzi zile za mwanzo mwazo kabisa En sisi ara ya Mageuzi ilipoundwa mwanzo tuliambiwa kuwa ni chama cha Wajaluo. Lakini baadaye Mheshimiwa Fulani wa inji hii mzee wa kibaragashia alipotoka Sisi emu na kujiunga na chama hicho watu wengi nao walitoka Sisi emu na kumfuata mzee wa inji hii. Na Wachaga wengi nao wakamfuata. Lakini katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 Nakumbuka Ensisiara ya Mageuzi ilipoonekana imekuwa tishio kwa Sisi emu basi watu hao hao walianza kukipakazia chama hicho eti kilikuwa ni chama cha Wachaga!

Na hata chama cha Kafu ilipoanzishwa Wapemba wengi na baadhi ya Waunguja wachache ndio waliokiunga mkono, tukaambiwa chama hicho ni cha Wapemba. Ingawa Kafu ni chama cha kisiasa si cha kidini, na kinaungwa mkono na Watanzania wa dini na rangi mbalimbali, lakini kwa vile safari ile kilipokuwa kimeanza kukubalika na kuungwa mkono na Watanzania wengi wa Bara, na kuonekana kimekwisha kuwa ni tishio kwa Sisi emu katika uchaguzi mkuu ulio fuata wa mwaka 2000, wale watu wenye kazi yao wakakipakazia chama hicho eti ni chama cha Waislamu!
Lakini ni kweli chama cha Kafu cha Waislamu kweli? Baniani kasema, "Domo jumba ya maneno!" Hiyo ina maana kuwa binadamu, kwa kutumia mdomo wake anaweza kutamka mengi, yanayofaa na yasiyofaa. Na Washihiri wakasema, "kama mwenye kusema ana wazimu, basi mwenye kusikiliza huwa ana akili!" Maana ya msemo huo ni kuwa mtu asiamini kila analoambiwa au kulisikia. Ni wajibu wa msikilizaji kupima lile analoambiwa au kulisikia kabla ya kuliamini.

Sasa kuna hiki chama cha Chaa dema nacho kinaonekana kinakuja juu, basi tushaanza kusikia kuwa hiki chama cha ukoo wengine chama cha Wachaga, japokuwa nasikia mwanzilishi wake ni Simon Madete ambaye ni Msukuma.
Basi kama kuna watu wanaodai kuwa Kafu ni chama cha Waislamu na Chaa dema ni Wachaga, En sisi ara nayo kama ipo hai... ni wajibu wa wale wanaoambiwa hivyo wachunguze madai hayo kabla ya kuyaamini. Wale wanaokipakazia udini chama cha Kafu wanadai kuwa chama hicho ni cha Waislamu eti kwa sababu viongozi wake wengi wa kitaifa ni Waislamu. Lakini kama hicho ndicho kigezo kinachokifanya chama cha Kafu kiwe ni chama cha Waislamu, basi tutaona kuwa karibu vyama vingine vyote vilivyobaki, ukiondoa chama twa wala, navyo ni vyama vya Wakristo, kwa sababu ile ile, ya kuwa viongozi wake wengi wa kitaifa ni Wakristo. Hawa watu wanataka kututenganisha kutumia udini, hivi hamuoni jamani, hayo macho na masikio mliyonayo yanafanyakazi gani?
Na ilivyoelekea ni kuwa kila chama kinachoonekana kinapata kasi ya kukubalika na watu, basi, upesi upesi kuna watu waliokabidhiwa jukumu la kukipaka matope chama kama hicho.

Nasikia uchunguzi wa gazeti la Raia aliye Mwema umethibitisha kufanyika kwa maandalizi ya kuanzishwa kwa chama kipya kinachoitwa ‘sisi je’ kwa kirefu ni Chama Cha Jamii (CCJ); ambacho rasimu ya katiba yake inadai kuwa kinakuja kukidhi kiu kubwa ya Watanzania wengi waliochoshwa na hali mbaya ya mahusiano ndani ya Sisi emu na mitafaruku isiyoisha ndani ya vyama vya Upinzani.

Wapendwa wasomaji haya yalikuwa ni maelezo baada ya habari, cha kuzingatia hapa ni kuwa zana za uwazi na ukweli zinaturuhusu kusoma na kusikika. Karne ya demokrasia inatutaka tuhoji kabla ya kukubali, basi kwa vigezo hiyo Nashauri kuwa, badala ya kunung'unika au kususa na kama ikitokea kujibu basi turekebishe pale tulipokosea na si kupinga tu kila kinacho andikwa na wale ambao tunaona tunapishana nao kifikra. Tuwe wana mapinduzi wa kifikra, tusikubali kutengwa kwa sababu za kidini, kikabila, kikanda, kimkoa au kirangi. Sote tu watoto wa baba mmoja... ! Oktoba si mbali... tetemelo la ardhi likija halichagui wewe ni wa dini gani au kabila gani... litazowa waliokuwemo na wasio kuwemo... Maoni na mapendekezo yako yanaweza kuwa ni amri kwa kina Matata na yanaweza kuondoa mtivyogo wa mambo! Ati nami si nimesikikaa !!!
 
Well said mkuu,

Akina matata wanapita kila kona sasa kuchukua mateka wao wa kifikra wanaweza kutumia silaha yeyote iliyo mbele yao Kwa mfano, akina matata wanaweza kwenda shinyanga kuwachukua mateka wasukuma kwa ahadi ya vyeo na miundo mbinu

Wanaweza kwenda pemba kuwachukua mateka kwa ahadi ya mseto, ambayo kumbe wangeweza kuifanya zamani miaka 9 iliyopita watasema baadaye ili ifikapo hiyo baadaye waje waseme hatuhitaji mseto ila umoja na amani na kuaminiana.

Akina matata, wapo huku JF kazi yao nikuangalia XYZ kasema nini? kwanini kasema?, wametumwa, msiwasikilize, subiri utaona watakavyojitokeza kwa wingi!. Walioko JF wao wana chama chao ukihoji na kudadisi usiwe msikilizaji tu...mmmm hawatakusoma ...wana akili mgando

Akina matata wanajua tabia zetu sisi wanadamu wenye asili ya bongo ..hatupendi kusoma, twependa kusikia tu..kupewa tetesi na taarifa...na tuna watu maalum wa kutupa taarifa kila mahali JF tunaye Mkjj, TBC tunaye JK, n.k. hatuwezi kwenda mbali zaidi ya hapo kutafuta ukweli..Matata hana shida ...kazi yake ni mchukue mateka Mwanakijiji umewamaliza wote hapa JF...wote wataku-support Lo! kondoo wetu wepesi kwelikweli.

Matata akisha teka JF nenda moshi, wateke wachaga kwa tender za biashara na kazi lo! hutapata usumbufu pengineko ambako hawana kazi sana wagombanishe kwa dini zao mbona watapambana na watakuita wewe matata msuluhishi na hiyo ikawa sifa yako ya kupata zawadi yako ya Birthday ..rahisi..Tanzania
 
Ama kweli kimya kingi kina mshindo mkuu! Karibu tena X plaster
 
Lakini tatizo hapa ni nani? Matata, au wale wanakubali kudanganyika kutokana na hila na vitisho vya matata?
 
Labda wale wanao nifahamu wanaweza kushangaa imekuwaje leo XP amekuwa mtu wa kukata tamaa namna hii na si kawaida yake!?


Pole sana kwa kukata tamaa! Na wewe uwe unakubali wanayokuelimisha wenzako na si kupinga tuuuuu kila wakati na kila jambo, ok?
 
Respect XP, jf imekuwa sehemu ya watu kukurupuka bila kudadisi mambo kiundani, kweli kabisa jf sasa inaboa!! usikate tamaa niwajibu wako na wetu kuelimisha
 
Well said mkuu,


Matata akisha teka JF nenda moshi, wateke wachaga kwa tender za biashara na kazi lo! hutapata usumbufu pengineko ambako hawana kazi sana wagombanishe kwa dini zao mbona watapambana na watakuita wewe matata msuluhishi na hiyo ikawa sifa yako ya kupata zawadi yako ya Birthday ..rahisi..Tanzania
Mi nadhani mkuu wa nchi ameamuwa kuwapa kisirisiri wananchi uhuru wa kusema na kuamuwa... Huu ndio muda wa kufanya mabadiriko... nahisi itafika wakati yeye amestahafu atakuja kutuambia kuwa milango ilikuwa wazi na hatukuitumia... wakati ndio huu, na wananchi wasipo amka ndio basi tena!
 
Back
Top Bottom