"Mapenzi ni Maisha"

STK ONE

JF-Expert Member
Dec 31, 2011
627
184
Jamani nafahamu kuwa Jamii forums ina wadau wengi tena wenye taaluma tofauti na nyazifa mbalimbali. Mimi kwa taaluma ni Mwalimu, namalizia my first degree (Bed. Science (Chemistry & Biology)) katika chuo cha Mwenge kando kidogo ya mji wa Moshi, lakini pia nilimaliza stashahada ya elimu chuo cha ualimu MOROGORO (KIGURUNYEMBE). Mbali na ualimu, nimekuwa nikiandika hadithi za kiswahili, mashairi ya kiingereza na kiswahili. Nimeandika hadithi nyingi, lakini ambazo zimekamilika ni hadithi tatu, "MAPENZI NI MAISHA, SIYO MWISHO na NANI ZAIDI." Kutokana na umbali na jiji la Dar, ambako wengi tunaamini kuwa kila kitu kinafanyika huko, nimeshindwa kupata access ya kufanikisha hadithi zangu zinachapwa kwenye magazeti.

Ndoto zangu, ni kuona hadithi zangu zinachapwa kwenye magazeti na hatimaye kuchapa vitabu. Nitaweka sehemu ya kwanza ya hadithi yangu ya MAPENZI NI ZAIDI, naomba mwenye access ya vyombo vya habari, hususani magazeti ambayo yanaweza kunisaidia kutangaza hadithi yangu moja ya MAPENZI NI MAISHA, anisadie. Aliyetayari anitafute kwa contact zifuatatazo.

e mail - joenva1983@gmail.com au
0763 00 80 52


MAPENZI NI MAISHA.
Ulikuwa ni usiku wa kiza, mvua yenye ngurumo na sauti za radi pamoja na sauti za wanyama wakali zilikuwa zikisikika kutoka kila upande wake. Kwa hakika alikuwa hafahamu yupo wapi na sababu gani hasa ambayo ilifanya yeye kuwa mahali pale kwa wakati ule.
"Hii ni njozi au la!!?" Ni swali ambalo alikuwa akijiuliza mara kadhaa lakini bado lilibaki kama fumbo akilini mwake.

"Jipe moyo utashinda tu, kwani yana mwisho." Alihisi kama sauti ya mtu ikimwambia maneno yale. Na mara aligeuka huku na kule kujaribu kuona kama angeliweza kumuona mtu aliyetoa sauti ile. Lakini yale yalikuwa ni mawazo yake tu kwani kwa muda ule hakukuwa na mtu mwingine zaidi yake mahali pale. Kiza kilikuwa kinazidi kuwa kizito kadri mvua ilivyozidi kunyesha.

"Lakini kwa nini nipo hapa?" Hili ni swali ambalo lilianza kumpa picha halisi ya tukio lote japo hakufahamu tukio lile liliisha vipi.
"Nimekosa nini mbele za Mungu? Nimemkosea nini Beatrce?" Haya yalikuwa ni maswali ambayo yalimsababisha kutokwa na machozi.
"Nilikuwa nampenda kwa dhati Beatrice na nilikuwa wazi kwake kwa kumwambia kuwa kama kwa namna moja au nyingine nitakuwa simridhishi kimapenzi awe wazi ili iwe rahisi kwangu kujirekebisha. Niliamini kuwa alikuwa ananipenda kwa dhati kwa jinsi alivyokuwa anaonekana, lakini sasa naamini kuwa kweli usiusemee moyo wa mtu." Alikuwa anawaza akiwa anaendelea kutoteshwa na mvua ambayo bado ilikuwa inaendelea kunyesha kwa nguvu sana.

Hakukuwa na dalili yoyote ambayo ilionyesha kuwa mvua ile ingemalizika kwa muda mfupi mbele, ilikuwa bado inaendelea kunyesha. Baada ya baridi kuwa kali sana, ndipo alipong'amua kuwa hakuwa na shati wala suruali, lakini alikuwa na bukta fupi sana ambayo ilikuwa inaishia juu ya magoti. Miguuni hakuwa amevaa chochote kile. Alikuwa anajitahidi kwa nguvu zote za akili yake kujaribu kukumbuka ni kipi kilitokea kwa mara ya mwisho. Baada ya kama dakika tano za kutafuta jibu la swali lake, alikumbukuka kuwa kwa mara ya mwisho alikuwa nyumbani kwa Beatrice, lakini ni kipi ambacho kilitokea hadi yeye akawa mahala pale kwa wakati kama ule, ndilo swali ambalo lilibaki kama kitendawili ambaccho jibu lake kwa wakati ule lilikuwa kama almasi kwake. Alijaribu kuinuka na kutembea, lakini miguu yake haikumpa ushirikiano wa kutosha. Alikuwa anahisi maumivu makali sana hasa sehemu za magoti na kiuno. Aliamua kukaa tena chini japo palikuwa pametota sana kutokana na mvua ambayo bado ilikuwa inaendelea kunyesha kwa kasi ile ile.

"Hivi mimi ni nani?" Ni swali ambalo kwa mara ya kwanza lilimjia akilini mwake. Alijaribu kufikiri kidogo kana kwamba kulikuwa na mtu ambaye alikuwa anasubiri jibu la swali lile na hivyo alikuwa anatafuta uhakika wa jibu ambalo angelitoa. Baada ya kama dakika mbili hivi, hakukuwa na ambalo alikumbuka kuhusu swali lile zaidi ya kukumbuka jina lake tu.
"Mimi ni Bernard. Lakini akina Bernard wapo wengi sana duniani, mimi natofautiana na hao wengine kwa lipi? Sasa kama kweli mimi ni Bernard nafanya nini hapa muda huu?" Aliendelea kujiuliza maswali mengi ambayo yote kwa ujumla hakupata majibu yake.

Kwa haraka haraka alijaribu kuyakumbuka mambo na matukio muhimu ambayo yaliwahi kutokea kwenye maisha yake. Kwanza alikumbuka maisha ya kijijini kwao Machipi alipokuwa anasoma shule ya msingi Kining'ina. Halafu akakumbuka jinsi alivyo soma kwa shida katika shule ya sekondari ya Ifakara na baadaye kidato cha tano na sita katika shule ya sekondari ya Pugu jijini Dar es Salaam. Hakuweza kusahau siku ya kwanza alipofahamiana na Winnie na baadaye Beatrice. Pia haikuwa rahisi kwake kumsahau rafiki yake wa dhati Shija Zacharia. Kumbukumbu zake zilirudi kwa Winnie, binti ambaye aliwahi kumpenda sana, lakini kutokana na kutekwa na mapenzi kivuli ya Beatrice, Bernard hakuwa na ujanja.

"Sikia Bern, najua unaweza kusema kuwa namkandia Beatrice, lakini potelea mbali, mimi ni msichana kama alivyo yeye. Mimi namfahamu vizuri sana huyo Betrice kwa sababu nilisoma naye shule ya sekondari ya Kilakala mkoani Morogoro.Tabia zake hazifai kuwa na mvulana anayejiheshimu kama wewe." Bern aliyakumbuka maneno ya Winnie siku moja alipokutana na Bernard kwenye maeneo ya chuo kikuu cha Dar es Salaam. Lakini hayo yote hayakutosha kumfanya Bernard aone hatari ya kuwa na Beatrice. Bern aliyapuuza yale maneno na kufikiri kuwa ni kweli kwamba Winnie alikuwa anatafuta njia ya kumtoa Beatrice ili yeye achukue nafasi yake.

Mawazo yale yalipotea mara baada ya kuona kuwa kiza kilikuwa kimepotea kwa kiasi kikubwa na nafasi yake kuchukuliwa na nuru hafifu iliyotokana na miale ya jua kutoka upande ambao ndio kwanza aligundua kuwa ulikuwa ni Magharibi.

"Kweli maisha ni safari, safari ambayo mwisho wake hautabiriki. Siamini kama kweli leo hii Bernard nimelala nje, siyo nje ya nyumba, nje porini ambako hakuna mtu zaidi ya miti na hawa wanyama." ALikuwa anawaza Bernard huku akiwa bado amekaa pale ardhini. Alitulia kana kwamba alikuwa anafikiri au kukumbuka kitu fulani cha maana na muhimu sana.
"Hivi chanzo cha yote haya ni mapenzi tu? Kwa nini mapenzi haya yanaleta mambo magumu sana kwa baadhi ya watu wakati kwa wengine mapenzi yanawapa faraja na amani mioyoni mwao? Kwa nini mapenzi haya yanaleta maisha magumu kwa mtu kama mimi na kuwafanya watu kama akina Beatrice kuendelea kuwa wenye siha nzuri hapa duniani? Kwa nini mapenzi yanakuwa na nguvu ya kuharibu maisha ya mtu bila ya ridhaa ya muhusika? Inawezekana kweli mapenzi ni maisha?"Alikuwa anajiuliza maswali mengi sana Bernard, lakini hakuna ambalo alikuwa na jibu lake
.
 
Back
Top Bottom