Mag3
Platinum Member
- May 31, 2008
- 13,064
- 22,757
Zabuni ya Manji yaigawa Manispaa ya Kinondoni !
Na Richard Makore
Jinamizi la ufisadi limeendelea kuinyemelea Manispaa ya Kinondoni, jijini Dar es Salaam, baada ya kukubali kuuziwa matrekta 27 ya kuzoa takataka yasiyokuwa na viwango kutoka kwa mfanyabiashara, Yusuf Manji. Dalili za kuwepo vitendo vya ufisadi zimeonekana wazi baada ya Baraza la Madiwani la Manispaa hiyo ambalo ndilo lililopitisha zabuni hiyo kugawanyika katika makundi mawili.
- Naibu Meya asema matrekta wameyapokea
- Kauli yake yapingana na Kamati ya Uwekezaji
Upande mmoja unaoongozwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Uwekezaji ya Baraza hilo, Julian Bujugo, ulipinga waziwazi kuwa hawawezi kuyapokea matrekta ya Manji kutokana na kutokuwa na viwango vinavyotakiwa kwa kuwa, Manji alikiuka masharti ya tenda na yaliyotaka matrekta yanayokidhi viwango.
Bujugo alisema Manji alipewa zabuni ya kuagiza matrekta yenye matairi manane lakini yeye akawapelekea yenye matairi manne kinyume na walivyokubaliana.
Hata hivyo, kauli ya Bujugo jana ilipingwa vikali na Naibu Meya wa Manispaa hiyo, Ibrahim Kisoki, baada ya kuibuka na kusema kuwa matrekta hayo yana viwango na wamekubali kuyapokea.
Kisoki aliiambia Nipashe kuwa wamemwagiza Manji kuongeza idadi ya matairi katika matrekta hayo hadi yafikie manane ili yafanane na maelekezo ya zabuni waliyompa.
Kauli hizo mbili kutoka ndani ya Baraza la Madiwani ambalo ndilo lililopitisha zabuni hiyo, zimezua mkanganyiko na kujenga dhana kuwa huenda kuna upande mmoja umepata ushawishi na kumlegezea masharti mfanyabiashara huyo ili kuweka mambo yake sawa.
Baada ya kukabidhiwa matrekta hayo, Bujugo alitangaza wazi kuwa madiwani wa Manispaa hiyo hawadanganyiki hata mtu akiwapa rushwa, lakini siku moja baadaye Naibu Meya, Kisoki aliibuka na kumtaka afute kauli yake.
Wakati Bujugo akitoa kauli hiyo, pia alimtaka Manji kuyaondoa matrekta hayo katika eneo la Manispaa hiyo ndani ya siku saba, lakini matrekta hayo bado yanahifadhiwa katika eneo la Manispaa ya Kinondoni licha ya muda huo kupita.
Kisoki jana aliliambia gazeti hili kuwa, Bujugo hana mamlaka ya kuzungumzia suala hilo na kwamba yeye (Kisoki) ndiye aliyetakiwa kusema kama matrekta hayo yalikuwa hayafai au la.
Alisema Manispaa imeamua kuyapokea matrekta hayo licha ya kuwa yana mapungufu na masharti ya zabuni yamekiukwa.
Aliongeza kuwa wamempa Manji miezi miwili ili ayafanyie marekebisho ya kiufundi, ikiwemo kuyaongezea matairi kutoka manne yaliyonayo hadi kufikia manane kwa kila trekta.
Kisoki alisema matrekta hayo kwa sasa yapo kwenye yadi ya magari ya magari ya Manispaa hiyo yakifanyiwa marekesho na kuongeza kuwa yatakuwa tayari baada ya miezi miwili.
Naibu Meya huyo alisisitiza kuwa licha ya baadhi ya madiwani katika Baraza hilo kukataa kupokea matrekta hayo lakini yeye ameyapokea na akadai kuwa haoni kama yana matatizo yoyote. Mbali na tenda hiyo ya Manji ambayo imezua utata na kuwagawa madiwani, pia hivi karibuni Manispaa hiyo ilituhumiwa kuuza eneo la kituo cha mabasi cha Makumbusho.
Kashfa nyingine zilizowahi kuikumba Manispaa hiyo ni pamoja na kuuza kiwanja cha shule ya Msingi Kawe kwa mwekezaji.
Manji, Patel, Rostamu, Somaiya n.k. Mapanya yaliyoshiba - kaazi kweli kweli !!