Malecela apigilia msumari kashfa ya ufisadi bungeni

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Agosti 1, 2012 | Mwananchi

KADA mkongwe wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye pia ni Waziri Mkuu Mstaafu, John Malecela ameitaka Serikali kuchukua hatua kali za kisheria endapo itathibitika kuwa kuna wabunge wanaojihusisha na vitendo vya rushwa.

Kauli hiyo ya Malecela mmoja wa wanasiasa wanaoheshimika nchini, imekuja kipindi ambacho tuhuma hizo za baadhi ya wabunge kuhongwa zikiwa zimetikisa Bunge na nchi kwa ujumla.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Chuo Kikuu Huria (OUT) jana, Malecela alisema: "Ni aibu kubwa kwa Bunge kama mhimili wa dola wa kutunga sheria na kuisimamia Serikali kuhusishwa na rushwa."

"Wabunge ndiyo wanatunga sheria ya kupiga vita rushwa sasa inakuwaje na wao tena wanajihusisha na uozo huo? Ningeshauri hatua kali zichukuliwe dhidi yao endapo kweli tuhuma hizo zitathibitishwa," alisema Malecela na kuongeza:

"Tuhuma hizi nzito zinaelekea kulichafua Bunge hivyo, kama Spika Anne Makinda alivyoahidi uchunguzi wa kina ufanyike ili kurudisha imani ya wananchi dhidi ya viongozi wao."

Sendeka, Msafiri wanena

Hatua ya Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu kuwataja wabunge saba wa CCM kuhusika na tuhuma za ufisadi, zimechafua hali ya hewa bungeni baada ya Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka kuomba mwongozo wa Spika kama anaweza kumshtaki mahakamani kwa madai kuwa amemdhalilisha.

Wakati Ole Sendeka akieleza kusudio lake hilo, Mbunge wa Viti Maalumu, Sara Msafiri ambaye Lissu alimtuhumu kufanya biashara ya matairi na Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) na kumwomba Katibu Mkuu wa Nishati na Madini Eliakim Maswi, rushwa ya Sh50 milioni alisema anasubiri matokeo ya uchunguzi unaofanywa na Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge.

Ole Sendeka na Msafiri ni miongoni mwa wabunge saba wa CCM waliotajwa na Lissu juzi, kwamba wanalichafua Bunge kutokana na kujihusisha na mambo yenye mgongano wa kimasilahi Wabunge wengine waliotajwa na Lissu ni Nasir Abdallah (Korogwe Mjini), Mariam Kisangi na Vicky Kamata (Viti Maalumu), Charles Mwijage (Muleba Kaskazini) na mbunge mmoja ambaye hatutamtaja kwa sababu hajapatikana kuzungumzia tuhuma zake.

Wabunge hao wote walishazungumzia tuhuma zaona kukanusha kuhusika. Lakini, jana Ole Sendeka baada ya kipindi cha maswali na majibu, aliomba mwongozo wa Spika kutaka ufafanuzi endapo kauli hizo za Lissu zina kinga ya Bunge ili aende mahakamani na kama hazina alitaka mwongozo wa Spika.
"Mheshimiwa Spika, jana Lissu aliitisha mkutano na waandishi wa habari na akanitaja mimi na wabunge wengine wa CCM kwamba ndiyo tunaohusika na tuhuma hizi za ufisadi. Sasa naomba mwongozo wako. Kauli hizo zina kinga ya Bunge au la ili niweze kwenda mahakamani," alisema.

Katika mwongozo wake, Spika Makinda alisema kwa kuwa kauli hizo zilitolewa ndani ya maeneo ya Bunge zina kinga... "Ila napenda kuwaambia kuwa Bunge hili liwe na subira. Kuhusu aliyoyasema jana Lissu sisi tutamtaka yeye ndiye awe shahidi wa kwanza katika vikao vya Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge. Atupe ushahidi tupate pa kuanzia."

Kwa upande wake, Msafiri alisema ana imani kwamba kamati husika itatenda haki na kwamba yeyote anayemtuhumu apeleke ushahidi katika kamati hiyo.
"Siwezi kuzungumza kitu kwa sasa maana tuhuma ni tuhuma tu, mara huyu kasema hili mwingine kasema lile, kwa hiyo tusubiri tu matokeo ya Kamati ya Bunge na tumeambiwa inafanya kazi kwa kasi sana," alisema Msafiri.

Msafiri pia anadaiwa kwenda kwa Maswi kumwomba radhi na kumsihi asitoe ushahidi dhidi yake mbele ya Kamati ya Bunge.

Habari kutoka kwa baadhi ya maofisa wa Wizara ya Nishati na Madini zimedai kuwa baada ya mjadala wa ufisadi kulipuka bungeni mwishoni mwa juma, mbunge huyo aliamua kuomba radhi kama njia ya kujinusuru na adhabu inayoweza kutolewa dhidi yake kama Bunge litathibitisha kuwa aliomba rushwa.

Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge namba 3 ya mwaka 1988, inataka Mbunge anayethibitika kutumika na watu kutoa michango au kuandika bungeni kwa masilahi ya mtu huyo ama kujihusisha mwenyewe katika masuala ya rushwa, afukuzwe ubunge na kufungwa kifungo cha miaka mitano.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, mbunge huyo anadaiwa kufika Ofisi za Nishati na Madini zilizoko Mjini Dodoma Jumapili asubuhi, ikiwa ni siku moja baada ya Bunge kupitisha azma hiyo. Akaonana na Maswi na kuomba radhi katika kikao kilichowashirikisha watu watatu.

Habari zaidi zimeeleza kuwa lengo la mbunge huyo kuomba radhi ni kumshawishi katibu huyo ili asishirikiane na mamlaka zinazofuatilia tuhuma hizo ikiwamo Bunge katika kutoa taarifa kuhusu suala hilo.

Kuhusu suala hilo, Msafiri pia alisema anaiachia Kamati hiyo ya Bunge kufanya kazi yake.

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo alipotakiwa kuzungumzia hatua ya mbunge huyo kuomba radhi, alisema asingependa kuzungumzia masuala ya watu, bali utendaji wa kazi katika wizara yake.

Hata hivyo alieleza kuwa anachofahamu siku ya Jumapili, katika Ofisi za Wizara ya Nishati na Madini Dodoma, kulikuwa na kazi ya watendaji wa wizara hiyo kuonana na wabunge.

Nape aitega Chadema
Katika kile kinachoonyesha ni kuchukizwa na tuhuma hizo, CCM kimetoa tamko la kulaani juhudi zinazofanywa na baadhi ya wanasiasa na vyama vya siasa kujaribu kupotosha na kuuficha ukweli juu ya tuhuma za rushwa zinazowakabili baadhi ya wabunge.

Akizungumza na waandishi a habari Dar es Salaam jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye alisema zipo juhudi za baadhi ya wanasiasa na vyama vya siasa kujaribu kulifanya suala la tuhuma za rushwa kwa baadhi ya wabunge kuwa la kisiasa kwa malengo yao.

"Mfano mzuri wa juhudi hizi ni kitendo cha Tundu Lissu ambaye ni Mbunge wa Chadema na Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni cha kutoa aliyoiita orodha ya wabunge wanaotuhumiwa kufanya biashara na Tanesco na kwamba, ndiyo watuhumiwa wa rushwa inayozungumziwa," alisema Nape na kuongeza:
"Cha kushangaza orodha yake ilikuwa na wabunge wa CCM peke yake wakati wote tunajua kuwa yapo majina ya baadhi ya wabunge wa vyama vingine hasa Chadema, yanayotajwa katika orodha ya wabunge wanaotuhumiwa kwa rushwa hii."

Nape alisema juhudi hizo za Lissu na wenzake zina lengo la kuuficha ukweli na kujaribu kuwalinda watuhumiwa wa uhalifu wanaotokana na Chadema.

Alisema CCM inalaani vitendo vya rushwa hasa vinapowahusisha viongozi ambao wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa kwani vinavuruga uchumi wa nchi na kwamba haitoshi kuwaita wala rushwa tu, bali ni zaidi ya wahujumu uchumi... "Wakikithibitika ni muhimu hatua kali zichukuliwe kulikomesha kabisa hili na iwe fundisho kwa wengine," alisema Nape.

Nape alisema CCM kinawapongeza watendaji wakuu wa Wizara ya Nishati na Madini wakiongozwa na Waziri wao, Profesa Sospeter Muhongo, Manaibu wake, Stephen Massele na George Simbachawene na Katibu Mkuu, Maswi kwa uzalendo, ujasiri na umahiri wao mkubwa waliouonyesha kwa muda mfupi waliokaa kwenye wizara hiyo.

"Tunaamini uzalendo walioonyesha katika kusimamia wizara hii utaigwa na watumishi wengine wa umma katika kuhakikisha matumizi mazuri ya rasilimali za nchi zinalindwa ili kuhakikisha maisha bora kwa kila Mtanzania yanatimia. Tunaunga mkono jitihada zao," alisema Nape.

 
Na wewe Maleclela kwanini wewe na Rais Mstaafu Mwinyi Mliazimia kuweka kuvunja KUZO ZA UONGOZI ndani ya

AZIMIO LA ZANZIBAR? hauoni huo ndio sababu ya UFISADI ndani ya BUNGE? Umewafunya WABUNGE kuwa walafi?

 
We mzee hujua alichokikataa baba wa taifa, madhara ya siasa na biashara ndi hayo sasa
 
Heee, haya ni maneno ya buldozzer au mwingine? kwani huyu mzee naye si anakale ka kashafa ka stand ya Dodoma? na alikapata haka ka kashfa wakati akiwa mbunge, au ndo ya Nyani halioni .....!

Kuhusu issue ya nape, Tundu ametaja majina ya wana magamba, kama naye anayo majina ya CDM, si naye ataje? (hapa sina maana kama CDM hawapo, mtu kama shibuda, ninahakika akipata nafasi lazima aitumie tu) maelezo aliyoyatoa ni jumla mno, angetwambia kabisa kwamba mbona na fulani wa CDM au CUF nao wan scandle hii au ile, but akumbuke yeye hana kinga ya bunge, so awe na ushahidi ili wakienda mahakamani awe na ushahidi (pia hapa simtishi) kwa vile anatoka magamba ambayo akina Jack Zoka wana report huko, anaweza kupata full infor kupitia wao, vinginevyo hatuna usalama hata wa magamba.
 
Sijui huyu mzee kasahau au anajifanya kusahau. Ebu atuambie mwaka 1995 kwa nini Baba wa Taifa alihakikisha hapati nafasi ya kupigiwa kura kuwa mgombea urais kwa tiketi ya ccm. Akitufumbulia fumbo hilo ndipo tutajua kama yeye ni msafi wa kuweza kuwanyooshea kidole wenzake - au ndio mavi ya kale hayanuki?
 
Michango ya harusi yake nayo vipi? Si tuliambiwa akina nanihii walimchangia! Tena taarifa iko kwenye Hansard za bunge
 
Back
Top Bottom