Zak Malang
JF-Expert Member
- Dec 30, 2008
- 5,404
- 234
·Makongoro Nyerere azitia doa kampeni za JK
Na Mwandishi wetu, Bunda
Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, ambaye ni motto wa Baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere, jana alizitia doa kampeni za Rais Kikwete, baada ya kuwahoji watu kama watampa kura mgombea huyo wa urais, lakini alijibiwa kuwa hatapewa kwa kuwa ameshindwa kuliondoa taifa kwenye lindi la umasikini.
Sakata hilo lilitokea jana kwenye uwanja wa stendi, wakati rais Kikwete akiwa katika kampeni wilayani Bunda akitokea katika jimbo la Mwibara, ambapo Makongoro alisimama limkaribisha mgombea huyo huku akitoa vijembe na maneno ya kejeli kwa vyama vya upinzani.
Makongoro alianza kwa kuigiza salamu za vyama vya upinzani, ambapo alianza na ile inayotumiwa na Chama cha Wananchi (CUF), kwa kusema: "Hakiii…" Wananchi wakanyamnyamazia na alipoona kimya, aliamua kuisema ile salamu ya Chadema ya ‘Peoples…' na kujibiwa ‘Power!'
Mwenyekiti huyo aliendelea na majigambo kwa kuwauliza wananchi kama watampa Kikwete kura zao, ndipo ziliposikika sauti kuwa hawampi, kwa sababu ameshindwa kuutokomeza umasikini.
Baadhi ya watu waliohudhuria kwenye mkutano huo walionekana wakionyesha alama ya vidole viwili, alama ambayo ipo kwenye bendera ya Chadema, jambo lililosababisha mkutano huo kutawaliwa na kelele za kupingana.
Makongoro pia aliutumia mkutano huo kuwabeza wagombea wa vyama vya upinzani kwa kuwafananisha na wapiga debe na makondakta wa daladala, ambao mwisho wa siku wataendelea kuishuhudia CCM ikishinda kwa kishindo.
"Si mnajua wapiga debe na makondakta? Kazi yao ni kupiga kelele za kuita abiria, hivyo hata kwenye kampeni kuna wapiga debe na makondakta nao wanataka kuwa marais," alisema.
Hata hivyo, Makongoro hakuweza kuendelea kunadi sera za mgombea wa CCM kutokana na kelele zilizokuwa zikipigwa na wananchi kuonyesha kukerwa na kauli zake, hivyo kuamua kumkaribisha Kikwete aendelee na mkutano huo.
Akiwahutubia wananchi katika mkutano huo, Kikwete aliwataka kuachana na waigizaji na wanung'unikaji, kwani CCM ina sera nzuri ambazo zinadumisha amani na utulivu nchini………..
Chanzo: Tanzania Daima.