Candid Scope
JF-Expert Member
- Nov 8, 2010
- 11,883
- 6,884
SPIKA wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Anne Makinda, amewataka wabunge wa Tanzania wanaowakilisha katika Bunge la Afrika Mashariki (EALA), kususia vikao na kutoka nje pindi wanapoona sheria zinazopitishwa na Bunge hilo, zinaweza kuhatarisha taifa. Spika Makinda alisema hayo juzi usiku wakati wa kufunga semina elekezi kwa wabunge hao iliyofanyika jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa kanuni ya kutoka nje kwa wabunge hao lazima izingatiwe pale wanapoona kushindwa kutetea jambo lenye masIlahi kwa nchi.
Spika Makinda, alisema kanuni ya kutoka nje lazima waitumie hasa pale wanapoona hoja walizotoa zimeshindikana kwa kuwa wasipofanya hivyo kuna uwezekano mkubwa wa kuuza nchi. Nyinyi mpo tofauti na wabunge wa hapa nchini kwa kuwa mnawakilisha zaidi ya Watanzania milioni 50 katika Jumuiya hiyo, hivyo suala la kutoka nje lazima mlitumie pale mnapoona inafaa, maana wale wenzenu wana umoja sana, alisisitiza.
Spika Makinda alitoa msisitizo huo baada ya mratibu wa Bunge la EALA kwa Tanzania, Justina Shauri, alipowasilisha mada akiwataka wabunge hao kutumia staili ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ya kutoka nje pindi wanapoona hawatoshi katika kura zao. Aliwataka wabunge hao kujitambua na kuwa wavumilivu katika kila jambo kwa kuwa wakiharibu wanakuwa wameivuruga nchi. Alisema kutokana na uvumilivu na kutokuwa mjuaji ndiyo maana ameweza kudumu katika ubunge na mwaka 2015 anatimiza miaka 40 ya ubunge wake.
Spika Makinda alisema kuwa kwa kawaida wabunge wapya wanakosa uvumilivu, huku akitolea mfano bungeni Dodoma ambapo kuna wabunge wengi vijana na wapya, ambapo tangu siku ya kwanza wanajua, wakati kiongozi si kila mara unatakiwa kusema. Alisema kutokana na kukosa kuzijua kanuni mara nyingi hujisikia vibaya pale anapomwambia mbunge akae chini wakati wananchi wake wanamtazama kupitia televisheni.Nilipoingia bungeni nilikuwa mdogo sana lakini kwa miezi sita sikuzungumza lolote...ili uweze kuzungumza ni muhimu kuzijua kanuni, kwa kuwa Bunge linaongozwa kwa kanuni, alisema.
Hata hivyo akichangia katika hoja ya kutoka nje, Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukhindo (CCM), alipingana na kauli hiyo na kuwataka wabunge hao kuwa waangalifu na kuacha kususia kila kitu, kwani wakifanya hivyo wenzao kwa umoja wao wataendelea kutekeleza majukumu yao. Naye, mbunge mteule, Makongoro Nyerere, alipinga staili hiyo ya CHADEMA na kusema kuwa kama kuna hoja basi wabunge hao hawatapaswa kutoka nje. Leo umepigania nafasi na kupata, sasa kama una hoja kwa nini utoke nje? Tumia nafasi hiyo kusema, maana ukitoka nje utakwenda kusemea kijiwenim, hivyo kususia hatuombei, tupo pale kujenga hoja na tutaweza...Mungu tusaidie, alisema.
Kwa upande wake mbunge wa EALA anayemaliza muda wake, Kate Kamba, alisema kuwa kutoka nje kunaruhusiwa kikatiba kwa ibara ya 13, hasa kwa suala lenye masilahi ya nchi. Hata hivyo Spika Makinda amekuwa akipingana na tabia hiyo inayotumiwa na wabunge wa CHADEMA ambao wamekuwa wakitoka nje ya vikao pamoja na kususia mijadala mbalimbali bungeni mjini Dodoma.