Mafisadi wa vipato vyao

IsangulaKG

JF-Expert Member
Oct 14, 2010
706
386
MAFISADI WA VIPATO VYAO

Na Kahabi wa Isangula

Kila ninaposikiliza hotuba za wanasiasa zote zimejikita kutuaminisha kuwa Serikali ndiyo tiba pekee ya matatizo yetu ya maendeleo ya kiuchumi. Kwamba serikali ni tiba ya maendeleo ya uchumi wa mkubwa wa Nchi (macro) na Uchumi wa mtu binafsi ama familia (micro). Mfano mzuri ni ile kauli mbiu iliyokufa ya "Maisha bora kwa kila mmoja".

Wakati nakubaliana na wanasiasa kuwa serikali inawajibika kwa maendeleo ya uchumi mkubwa wa Nchi, kwa kiasi kikubwa sikubaliani na hoja kuwa maendeleo ya uchumi wa mtu mmoja mmoja ni wajibu wa serikali. Wakati pia nakubaliana na hoja kuwa serikali inawajibika kuweka mazingira wezeshi na rafiki kwa kila mmoja kufanikiwa kiuchumi na kuwezesha upatikanaji endelevu wa huduma za jamii bado nasisitiza kuwa ni wajibu wa kila mmoja kujiwezesha kiuchumi kwa kutumia fursa zilizopo katika mazingira hayo wezeshi yaliyoandaliwa na serikali.

Lakini pia, kwa kuwa mazingira wezeshi hayana viashiria vya jumla vya wazi, ni wajibu wa kila mmoja kutumia fursa zilizopo katika mazingira yoyote yale kujiendeleza kiuchumi. Najua kuna baadhi ya mazingira mfano Vita huwafanya utumiaji wa fursa kuwa mgumu, lakini upo ushahidi wa watu waliotumia fursa katika mazingira kama hayo kujiongezea kipato.Huu ulikuwa ni utangulizi tu.

Katika kutembea kwangu sehemu na Nchi kadhaa, nimejiridhisha pasipo na shaka kuwaaendele ya uchumi wa mtu mmojammoja ama familia ni wajibu wa mtu mwenyewe. Sikuona mtu ama familia ambayo imejengewa nyumba ya bure nzuri na serikali, isipokuwa makundi machache sana ambayo kutokana na sababu kadhaa mfano umri, ulemavu, ukimbizi n.k zinawafanya wasiwe na fursa sawa na watu wenye mwili na nguvu tele kujipatia kipato.

Kila mtu mwenye nguvu timilifu, mwenye familia yake ninayemwona anaishi maisha mazuri kwa maana ya makazi, chakula, usafiri n.k.ni kutokana na bidii binafsi. Hata mwanasiasa tunayemwona kuwa anaishi vizuri ni kutokana na bidii binafsi pasipo kujali ni ufisadi au la. Naam, ufisadi pia ni bidii binafsi ya kutaka kuwa na kingi kuliko wengine kwa kupora kilichostahili kuwanufaisha wote.

Kama mafanikio ni bidii binafsi, swali la kujiuliza ni kuwa; kwa nini watu wenye kazi na kipato kinachofanana au kukaribia kufanana wana maendeleo tofauti? Hapa ndipo hoja yangu ya ufisadi wa kipato inapohusika.

Ni kawaida sana kuona watu wenye kipato kinachofanana au kukaribia kufanana wakiwa na viwango tofauti vya maendeleo ya kiuchumi ama wao wenyewe ama familia za wahusika. Familia hapa namaanisha mke na watoto. Iwapo wewe ni baba wa familia, kipato chako chote kinastahili kuwanufaisha wana familia yako wote...iwe ni kuwajengea nyumba nzuri mtakayoishi wote, iwe ni kuwalipia watoto ada wasome vizuri na mavazi ama iwe ni kununua Gari mpande wote.

Iwapo watu wenye kipato sawa wana viwango tofauti vya maendeleo ya uchumi wa familia zao, hapa, inamaanisha kuwa mmojawapo ni fisadi wa kipato chake na mwingine siyo. Fisadi wa kipato chake ni mtu ambaye hutumia kipato chake ambacho kilistahili kuwanufaisha wanafamilia wake wote, kwa mambo ambayo yanamnufaisha au kufurahisha nafsi yake binafsi.

Yapo mambo kadhaa yanayomfanya mtu awe fisadi wa kipato chake na kuwadhulumu wanafamilia yake fursa ya kukua kiuchumi, naomba nitaje machache; Ulevi, Nyumba ndogo na starehe nyingine kupindukia ambazo wanafamilia yako hawazifaidi.

Katika kukua kwangu nimewaona mafisadi hawa wa kipato wengi sana. Ama nimeishi nao ama kufanya nao kazi. Watu hawa ni wepesi sana wa kuilaumu serikali kwa umasikini wao...ni wepesi pia kukata tamaa ya maisha..

Kwa kuhitimisha, lazima tutambue kuwa uchumi wa mtu mmoja mmoja ama familia ni wajibu wake mwenyewe. Wajibu wa serikali ni Uchumi mkubwa wa Nchi unaowezesha kupatikana na uendelevu wa huduma za jamii kama maji, barabara, umeme, afya, elimu n.k.

Ukiona watu wenye kipato cha aina moja au kinachokaribiana wana viwango tofauti vya maendeleo ya kiuchumi basi yule mwenye maendeleo hafifu ni fisadi wa kipato chake.

Ni hayo tu kwa leo.
 
Back
Top Bottom