Madudu Mengine ya Wizara ya Maliasili na utalii haya hapa

The Emils

JF-Expert Member
Apr 16, 2011
568
124
WAKATI Wizara ya Maliasili na Utalii ikihaha kuwabeba Wazungu kwenye ugawaji vitalu vya uwindaji wa kitalii, suala hilo sasa limeelekezwa kwa Waziri Mkuu na wabunge ili waweze kuihoji Serikali juu ya ukiukwaji wa kanuni na sheria.

Taarifa ya wadau wa uwindaji wa kitalii, pamoja na kuandaa waraka maalumu kwa wabunge hao, wamemwomba Waziri Mkuu afuatilie kwa makini mwenendo mzima wa ugawaji vitalu ambao wamesema umejaa upendeleo kwa wageni.

Baadhi ya wabunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wameshathibitisha kupokea waraka wa wadau, na wanajiandaa kudai majibu ya Serikali. Kama ilivyoandikwa na MTANZANIA jana, mkakati wa kuwabeba wageni umebarikiwa kwa tangazo la Wizara
ya Maliasili na Utalii, kwenye magazeti kadhaa ya jana yanayotaka wadau waombe vitalu 22. Katika orodha hiyo mpya, kimo kitalucha Maswa Mbono ambacho kinatakiwa kwa udi na uvumba na bilionea mmoja wa Marekani. Kimsingi ameshapewa hata kabla ya kutolewa kwa tangazo hilo.

Hata hivyo, kwa kutambua kuwa tayari Wizara kupitia Kamati ya Ushauri wa Kugawa Vitalu ilishavunja sheria kwa kutoa vitalu kwa kampuni za kigeni zaidi ya asilimia 15 inayotakiwa kisheria, sasa bilionea huyo anawatumia Watanzania kujipatia eneo hilo la daraja la kwanza na lenye utajiri mkubwa wa wanyamapori. Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009, kifungu 39 (3) (b) imeainisha wazi kuwa kampuni za kigeni ziwe asilimia 15 na za wazalendo ziwe asilimia 85. Imeelezwa kwamba sheria hiyo imevunjwa kwa makusudi kwa lengo la kuwabeba wazungu ambao wamefanya kila liwalo kwa kuingia ofisi zote kubwa na kuwatumia watu wenye ushawishi na madaraka.

Wiki hii viongozi waandamizi wa Wizara ya Nishati na Madini wanasafiri kwenda Paris, Ufaransa kubariki ugawaji vitalu. Mkutano wa Paris, kama mingine iliyowahi kufanyika Marekani na Hispania, unatarajiwa kutoa msimamo wa kuwabeba wageni hao. "Watatangaza vitalu baada ya kutoka Paris, kisheria ilikuwa Waziri atangaze Juni 12, mwaka huu lakini imeshindikana," imesema sehemu ya barua hiyo. Kamati ya Ushauri wa Kugawa Vitalu iliyoongozwa na Bakari Mbano, pamoja na kusheheni wataalamu wa sheria na wasomi wa hali ya juu, haikutambua kipengele hicho cha sheria, na matokeo yake yakaanza kujaza kampuni za kigeni. Mapendekezo yake ya mwisho kwa Waziri wa Nishati na Madini yanaonyeasha kuwa kampuni 57 zilipata sifa ya kupewa vitalu.

Kati yake, kampuni za wageni ni 17; ilhali za wazalendo ni 40. Kwa idadi hiyo, kampuni za wageni zilizopata vitalu ni asilimia 29.82; ilhali za wazalendo ni asilimia 70.18. Kwa mgawo huo, ni wazi kuwa kifgungu cha sheria namba 39 (3) (b) kimevunjwa. Kwa mujibu wa sheria hiyo, na kwa mgawo wa kuiheshimu sheria, kampuni za kigeni zilizostahili kupata vitalu ni tisa pekee. Suala la kuziacha kampuni nyingine nane limekuwa gumu kutokana na mvutano wa maslahi kutoka kwa maofisa wa Wizara ya Maliasili na Utalii na nje ya wizara hiyo.

Kila ofisa alikuwa na ‘kampuni zake' alizoapa kuzibeba. Kutokana na mparaganyiko huo, ndiyo maana Waziri mwenye dhamana amepata kigugumizi cha kutangazakampuni zilizoshinda kwa mujibu wa sheria inayomataka awe amefanya hivyo ndani ya siku 90. Tarehe ya mwisho kisheria aliyotakiwa kutangaza ni Juni 12, mwaka huu. Mbinu ilityotumika kuzima mpango huo ni kurejea kutangaza vitalu 22 kama ilivyofanywa kupitia magazeti kadhaa ya jana. Hata hivyo, vitalu vingi vilivyotangazwa tena na Waziri vilikuwa kwenye orodha ya awali ya Machi, mwaka huu lakini havikuombwa kutokana na uchovu wake.

Kwa wafanyabiashara wanaoitambua vema tasnia ya uwindaji wa kutalii, vitalu hivyo ni mzigo kwao kibiashara. Kutangazwa kwa vitalu hivyo 22 kwa mara ya pili kumelenga kupata kampuni zaidi za Watanzania, ili kwa kuongezeka kwake, wageni waweze kubaki na vitalu vinono walivyokwishapewa kwa msaada mkubwa wa wakubwa serikalini. Kwa mkakati huo wa Wizara ya Maliasili na Utalii, kama vitalu vyote 22 vitapata kampuni za Kitanzania, mabadiliko yanayotarajiwa ni kama ifuatavyo:

Idadi ya kampuni itaongezeka kutoka 57 hadi 79. Kama itatokea kwamba vitalu hivyo vimechukuliwa na kampuni za Kitanzania (mkakati ambao ndio lengo lake), kampuni 12 za kigeni zitabaki na vitalu. Waraka wa wadau wazalendo kwenda kwa wabunge unasema kwamba mkakati ulioandaliwa ni wa kuhakikisha kwa namna yoyote ile, wageni wanabaki na vitalu ambavyo sasa vinasubiri saini ya waziri tu. "Itambulike kuwa vitalu 22 havikupata waombaji kwenye duru ya kwanza kutokana na kuwa vichovu kibiashara, ndiyo maana hakuna aliyeviomba," imesema sehemu ya barua ya wadau hao.

Kwa mujibu wa nyaraka za wasifu wa vitalu ambazo MTANZANIA inazo, kitalu pekee katika kundi hilo ambacho ni kinono ni Maswa Mbono ambacho ni cha daraja la kwanza. Vitalu vya K4 na M2 ambavyo ni vya daraja la pili, si vizuri. Vitalu hivyo vimetangazwa kugawiwa wakati vilitengwa kwa ajili ya mafunzo na uwindaji unaofanywa na wageni maarufu, wakiwamo viongozi wa mataifa wanaozuru hapa nchini. Kutolewa kwa vitalu hivyo, hasa kwa wageni, kunaendelea kuwahakikishia wageni kuwa kampuni zao 17 na nyingine zitakazoongezeka, zitamiliki vitalu vyote vinono.

MASWALI YANAYOULIZWA Kamati ya Ushauri wa Kugawa Vitalu ilikuwa na wanasheria na wasomi waliobobea. Hata hivyo, bado inatia shaka kutambua ni kwa nini hawakuzingatia Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009 inayotaka kampuni za kigeni ziwe asilimia 15 pekee?

Kuna habari kwamba Kamati hiyo iligundua dosari kubwa kwenye idadi ya kampuni za kigeni na za wazalendo, lakini ilikuwa imesalia wiki moja tu kabla ya kuwasilisha mapendekezo yake kwa waziri. Awali, kuliandaliwa mpango wa kutaka mapendekezo yapelekwe bungeni kwa ajili ya kubadili sheria ili ikiwezekana kampuni za kigeni zitakazopewa vitalu ziwe zaidi ya asilimia 15, ikibidi ifike asilimia 30.

Wazo hilo limeonekana kuwagawa baadhi ya wajumbe na wataalamu wa wizara kwa kuamini kuwa wizara ingepata wakati mgumu kuwashawishi wabunge. Wadau wanahoji, "Imekuwaje waziri apate kigugumizi cha kutangazamatokeo wakati akitambua kuwa muda wa kufanya hivyo kisheria umepita? Kama kuna matatizo ya kuzingatia sheria na kanuni, kwa nini suala hilo halikurejeshwa kwenye Kamati? "Kuongeza muda wa kugawa vitalu maana yake ni kwamba anatafuta kile anachotaka na si kupata kile kinachotakiwa kwa mujibu wa Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009. "Kutotangaza matokeo ya awali hadi matokeo ya duru ya pili yatoke, ni hatua yenye nia mbaya inayolenga kuwabeba na kuwapendelea watu fulani (hasa wageni) kinyume cha utawala bora unaozuia aina zote za upendeleo (kifungu 38 (11 cha Sheria). "Tunamshauri Waziri atangaze matokeo ya awali…

Tunamwomba Waziri Mkuu aingilie kati kuhakikisha kuwa haki inatendeka kwa mujibu wa sheria na kanuni. Tunaamini kuwa kutotangaza matokeo ya awali ni kuandaa mazingira ya kuchakachua. " YALIYOKWISHAWATOKEA MAWAZIRI WALIOTANGULIA Kuna matukio kadhaa yanayothibitisha kuwapo kwa usiri na upendeleo kwenye ugawaji vitalu vya uwindaji.

Aliyekuwa Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, alishapata msukosuko kutokana na kuzembea kutekeleza Tangazo la Serikali namba 159 la kuongeza ada za vitalu. Kanuni kwa ajili ya Sheria Namba 5 ya Wanyamapori ya mwaka 2009 ziliibua msuguano mkali baada ya kubainikakuwa kundi la wageni linakutana kwa siri na maofisa wa Wizara ya Maliasili na Utalii usiku wa manane kuingiza waliyoyataka.

Matokeo yake ni kwamba zilitolewa kanuni zilizokwenda kinyume kabisa na azma njema ya wabunge na Serikali ya kuhakikisha wazalendo wanapewa fursa ya kufaidi rasilimali ya wanyamapori. Aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Shamsha Mwangunga, aliingia kwenye mgongano mkubwa na wabunge baada ya kupuuza Azimio la Bunge kwa kuongeza muda wa uwindaji.

Hata hivyo, ilikuja bainika baadaye kwamba Waziri alikuwa ameghilibiwa katika mkutano ulioshirikisha wadau kutoka Chama cha Wenye Kampuni za Uwindaji wa Kitalii (TAHOA) ambao ulifanyika Reno, Nevada nchini Marekani. Mkutano mwingine ulioibua utata ni ule uliofanyika Hispania na kuamua kupunguza ada za tozo kwenye nyara na leseni. Baada ya kutolewa kwa tangazo la kugawa vitalu, TAHOA walikuja juu na kusema hawako tayari kuachia vitalu ambavyo wameviendeleza.

Hatua hiyo iliifanya wizara inywee na kulazimishwa kubadili baadhi ya vipengele. Miongoni mwa vipengele vilivyorekebishwa ni kile kilichokuwa kikitaka waombaji vitalu kuwasilisha Mpango wa Biashara pamoja na fomu za maombi. Kwa sasa mkutano mwingine umepangwa kufanyika Paris, Ufaransa, na kama inavyotarajiwa, uamuzi wa ugawaji vitalu unatarajiwa kubarikiwa huko na wazungu.

Wadau wazalendo wanaamini kuwa kile kitakachoamuriwa Paris ndicho kitakachokuja kutekelezwa na ujumbe wa maofisa waandamizi wa Wizara ya Maliasili na Utalii. Hatua hiyo itakuwa ni sawa nakutekeleza makubaliano ya kimkakati yaliyosainiwa miaka kadhaa kati ya TAHOA na wizara hiyo ambayo hayakuiopa mwanya Serikali kufanya mabadiliko yoyote kwa manufaa ya nchi bila kuwahusisha wazungu wanaomiliki chama hicho

Source:Mtanzania
 
Majungu majingu! hawa watu wanaojiita wafanyabiashara wazawa ni mzigo na mafisadi wakubwa. Wengi wao hawana uwezo wa kuendesha biashara ya uwindaji bali hutumiwa na kampuni za kigeni. Labda atokee malaika kuja kugawa hivi vitalu ndo malalamiko yataisha. Otherwise kila mwaka wizara ya maliasili itakua inabeba lawama.
 
Majungu majingu! hawa watu wanaojiita wafanyabiashara wazawa ni mzigo na mafisadi wakubwa. Wengi wao hawana uwezo wa kuendesha biashara ya uwindaji bali hutumiwa na kampuni za kigeni. Labda atokee malaika kuja kugawa hivi vitalu ndo malalamiko yataisha. Otherwise kila mwaka wizara ya maliasili itakua inabeba lawama.

Udalali kila mahali!!!
 
Wafanyibiashara wazawa wahindi/waarabu ???

Acha ubaguzi wewe. Kwani waarabu na wahindi hawawezi kuwa wazawa na raia kindakindaki wa Tanzania. Mbona mnao wabunge na hata mawaziri ambao ni waarabu na wahindi.

Kumbuka dhhambi ya baguzi ni mbaya na mkifanya mchezo WaTanganyika itawatafuna.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom