Ustaadh
JF-Expert Member
- Oct 25, 2009
- 413
- 19
Spika wa Bunge, Samuel Sitta, amesema suala la mawaziri sita na wabunge wanne wanaotuhumiwa kuwa na vyeti vya taaluma vyenye mushkeli, atalipeleka serikalini ili likaamuliwe huko, kwa vile vyuo vilikopatikana vyeti vyao vimeonekana kuwa havitambuliki.
Tuhuma dhidi ya mawaziri na wabunge hao, ziliwasilishwa ofisini kwa Spika na Mwanaharakati, ambaye kitaaluma ni Mwanasheria, Kainerugaba Msemakweli, kwa njia ya barua na viambatanisho, Septemba 15 na 16, mwaka huu.
Akizungumza na Nipashe kwa njia ya simu kutoka mjini Dodoma jana, Spika Sitta, alisema barua na viambatanisho hivyo viliwasilishwa ofisini kwake, amevisoma na kujiridhisha kwamba, hakuna kosa la jinai, ambalo Bunge linastahili kuchukua hatua dhidi ya wabunge hao.
Sitta alisema ofisi yake itavipeleka vyeti hivyo serikalini na kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) atajua nini la kufanya.
Itabidi tulirejeshe serikalini ili waamue huko la kufanya. Kwa sababu vyeti wamepewa, lakini vyuo havitambuliki. Ni tofauti na kughushi kwamba, mtu kaamua kujitengenezea cheti. Ila vinaonekana ni vyeti havitambuliki. Sasa tutalirejesha serikalini wakaonyane wenyewe huko, alisema Spika Sitta.
Alikemea kitendo cha mtu kumiliki vyeti vya taaluma, ambayo hakuisomea.
Sijambo zuri kwa mtu kuwa na vyeti, ambavyo wengine wamesomea, alisema Spika Sitta.
Pamoja na hivyo, kibunge, hakuna kitu chochote cha kufanya kosa la jinai. Kiserikali Mwanasheria Mkuu wa Serikali atatizama nini la kufanya.
Mawaziri na wabunge hao walihusishwa na kashfa hiyo kufuatia utafiti huru uliofanywa na Msemakweli kwa msaada wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU), katika kipindi cha mwaka mmoja na kubaini kwamba wanasiasa hao walitumia vyeti vya kughushi na kuwasilisha katika ofisi za umma kwamba wana elimu hiyo, kitu ambacho si kweli.
Kwa mujibu wa Msemakweli, utafiti huo ulianza kufanyika Juni 25, mwaka jana hadi Oktoba 9, mwaka huu katika nchi za Marekani, India na Uingereza, ambako vigogo hao wanadaiwa kuwa walisoma na kupata shahada hizo.
Baada ya kubainika kwamba, hawana sifa za elimu wanazodai kwenye wasifu wa elimu zao, Msemakweli alisema ripoti hiyo ilikabidhiwa kwa Ofisi ya Spika wa Bunge.
Alisema kitendo cha kuwasilisha nyaraka za hizo katika ofisi ya umma ni kinyume cha Ibara ya 68 na 56 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia, ni kuvunja sheria ya Vyuo Vikuu ya mwaka 2005 (58) na sheria ya makosa ya jinai sura ya 16 (333).
Msemakweli alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Oktoba 18, mwaka huu na kusema kwamba, alilazimika kufanya utafiti huo baada ya kuingiwa na wasiwasi kuhusu elimu ya vigogo hao.
Alidai vigogo hao walighushi taaluma kwa baadhi yao kujiwasilisha kuwa wana shahada za masuala ya kimataifa na diplomasia, biashara na utawala, wengine shahada za uzamili, udaktari wa falsafa, na wengine shahada za ualimu nakadhalika, wakati si kweli.
Msemakweli alisema katika taarifa aliyowasilisha kwa Ofisi ya Spika wa Bunge, aliomba iwawajibishe vigogo hao kwa kashfa hiyo na kwamba, anaendelea na utafiti kwa vigogo wengine tisa na kwamba, atauarifu umma mara tu atakapokamilisha.
Alidai vigogo hao waliwaghilibu wananchi wa majimbo wanayoyawakilisha na kuwafanya wapate ubunge na kwamba, kwa kutumia shahada hizo za kujipachika, wameweza kuaminiwa na kupewa nafasi za kisiasa na kiutawala.
Msemakweli alidai ana ushahidi wa kutosha juu ya madai anayoyatoa dhidi ya vigogo hao kwani amefanya utafiti wa uhakika na kwamba, kigogo yeyote atakayehisi kuwa ameonewa aende kwenye vyombo vya sheria na yuko tayari kwenda kuthibitisha madai yake.
CHANZO: NIPASHE