Mabishano Haya Kwa Faida Ya Nani!?

X-PASTER

JF-Expert Member
Feb 12, 2007
11,610
1,810
Mabishano Haya Kwa Faida Ya Nani!?

Wahenga walisema Kamwe usibishane Na Mjinga, Maana atakushusha Ili ulingane naye, kisha atakugaragaza chini kwa upumbavu wake.

Mara nyingi tunapoingia kwenye majadiliano, huwa tunategemea kuwini mioyo ya washindani kihoja na kisomi, na si kubishana tu kwa kuwa aliyetoa hoja si katika wale unao wapenda au wenye kuamini tofauti na wewe.

Je, unajisikiaje unapojadiliana na mtu kihoja ukitegemea naye atakuja na hoja, lakini badala yake unachokikuta ni kinyume chake? Kwa kweli hii ni kuwafukuza wasomi na wenye hoja yakinifu. Mara nyingi tumeshuhudia mijadala ikiharibika na kuingia kwenye mabishano yasio na faida, na matokeo yake uzi uliokuwepo kufungwa au kupoteza mweleo.

kimaumbile, si kawaida kwa mjinga kuweza kumpiku mwerevu, bali mwerevu ndiye mwenye fursa ya kumzidi mjinga kwa uwerevu wake. Lakini, ili mwerevu aweze kumshinda mwerevu mwenziwe hanabudi kutumia vizuri mianya na fursa muhimu zilizoko, ikiwemo kubakia kwenye hoja usika, na kutumia rejea za kweli na zenye mashiko.

Mwanachuoni mmoja aliwahi kusema kuwa "Alaiti ningeshindana na wanavyuoni (wasomi) 100 ningekuwa na tamaa ya kuwashinda kwa hoja, lakini mjinga au mpumbavu mmoja hakika angenishinda"

Na ni kweli maneno haya, kwani ujinga ni maradhi mabaya sana, japokuwa yana dawa na yanaweza kuondoka, lakini upumbavu wa mtu, ni maradhi sugu ambayo si rahisi kuondoka mpaka dhamira yake mtu iwe tayari kukubali ukweli, kujifunza na kukosolewa, kwani sehemu kubwa ya thamani ya ubinadamu inapatikana katika maadili mema na kujifunza yale yalio bora kwake na kwa jamii inayo mzunguka.

Tusisahau kwamba sifa hii tukufu ya kiutu inaweza kupatikana kwa ukuzaji roho na malezi maalumu ya kinafsi na kimaadili. Kwa sababu hii, wanasaikolojia na wataalamu wa elimu ya maadili na malezi wamejadilihali hii kwa urefu jinsi ya kuzuia na kupambana na ufisadi wa kimaadili na namna ya kukuza sifa na tabia njema na tukufu; na kwa mara nyingi wamesisitiza upande wa kimatendo. Na jinsi ya kuhusiana na watu kwenye mnakasha (majadiliano) mbalimbali.

Wakati mwingine kuto mjibu mtu haimaanishi kuwa umeshindwa, bali unachelea kumuumbua kwa kukosa kwake maarifa. Na hii umpelekea mpumbafu kujiona kuwa yeye ameshinda, lakini wajuvi wa mambo utambuwa wazi kuwa kunyamaa kimya kwa msomi ni tusi kwa mpumbavu. Lakini kwa kuwa mtu huyu huenda asifahamu matokeo mabaya ya tabia yake basi uendelea kujitutumua na kujiona kuwa amepatia. Lakini mwenye maadili na aliye lelewa vyema atakuwa ameepukana na radiamali na bidhaa ya matusi na ufidhuli wa yule mpumbavu.

Tabia hizi za kuto hishimiana kwenye mijadala husababisha nyoyo za watu kuvunjika, huleta chuki na hata uadui, na matokeo yake ni kuvunjika kwa amani.

Wahenga wamesema: "Maneno si kama njiwa ambaye anaporuka hurejea tena tunduni mwake. Au maji yakimwagika hayazoleki tena". (Hivyo basi, maneno yakikudondoka hayarejei tena mdomoni mwako).

Nilicho kigunduakuwa humu JF, mijadala mingi imekuwa haina mwelekeo mzuri japo kuwa kuna uwezekano wa huo mjadala kuwa na manufaa kwa wasomaji. Lakini mijadala mingi imearibika kutokana na wachangiaji kutumia lugha chafu. Na wengi wakiulizwa au wakiona mmoja wa mchangiaji ametumia lugha kali au lugha ya kejeri na kashfa basi kuna ambao watakuja na kumtetea kwa kisingizio cha uhuru wa kutoa maoni. Tuna sahau kwamba uhuru bila kuwa na mipaka ni sawa na maisha ya kihayawani mwituni. Ni wajibu wetu sisi wanadamu kujiepusha na kujitofautisha na maisha ya kiuhayawani, kwa maana sisi tumepewa akili, utashi na kikubwa zaidi tunajitambua.

Kama tumeamua kuingia kwenye mnakasha (majadiliano) basi mtu anatakiwa asiwe na mwendo au tabia ambazo zinavunja heshima za watu wengine na tujadiliane kwa misingi ya kiurafiki. Yeyote Yule atakayeacha kutoa lugha za kejeli, kashfa na matusi basi atakuwa amejenga msingi madhubuti wa mapenzi ya kidhati kati yake na wale anao jadiliana nao. Vilevile moyo wake na unyofu wa hoja zake zitaimarika zaidi atakapoona hoja zake zikipata watu wa kuzitetea.

Lakini akijadiliana kimabavu na kutoa hoja za kejeli na matusi, kama wengi wanaochangia humu, basi atakuwa amejidharirisha yeye na familia yake, na kuwatukanisha wazazi au walezi wake mwenyewe. Maana watu watajuliza, kama kweli huyu mtu amepata malezi bora uko anakotoka.
Uandishi ni taaluma, si kila mtu anaweza kuandika na kuficha ushabiki au hasira zake na kukiwakilisha kile ambacho kitaleta faida kwa jamii. Tatizo kubwa ndani ya tovuti baraza hizi ni kuingiliwa kwa kazi hii ya uandishi na wale wanao jiona kuwa wana uchungu sana na nchi hii... Uandishi unaharibika kwa sababu umeingiliwa na watu domo kaya, wasio ona tabu kuharisha kwa kupitia midomoni mwao... Ndio unashangaa nini!? Kwani ni uongo, mara ngapi vilanja (moderator) wamefuta au kuhariri baadhi ya mabandiko yetu!?

Wakati mwingine tunaosoma tu kwa mazoea lakini kinacho wakilishwa ni matapishi kama si uharo… ndio uharo yaani ni sawa na kuharisha kule unakokujuwa wewe na mimi, yaani kutokwa na kitu katika hali ambayo si ile ya kawaida.

Tunajuwa kuwa, Ukabila, Dini na Siasa ni sehemu ya maisha, mang'amuzi na maendeleo endelevu ya mwanadamu sanjari na haki zake zote za msingi zimeegemea katika mambo hayo. Na ndio ukamilifu wa kila kitu katika mustakabali wa maisha yake hapa duniani. Na hayo yote hayakamiliki kama hakuna mapenzi katika jamii. Mapenzi ninayoyaeleza hapa ni mapenzi yale ya kiroho, mapenzi yanayovutana kati ya nyoyo za wanadamu ndiyo msingi unaosimamisha ushirikiano, mapenzi na maelewano kati ya watu. Je aliye mpenzi wako unaweza kumrekebisha kwa matusi na kejeli, na kumwita majina ambayo si mazuri kwake? Ni hakika kabisa jibu lake litakuwa hapana.

Kitendo cha kuingia kwenye mijadala na kusahihisha fikra za watu mara nyingi huwa ni kazi ngumu, basi kwa nini ujitie zaidi matatani kwa kutumia mbinu isiyofaa na kujiwekea vizuizi vigumu zaidi? Unapotaka kuthibitisha jambo moja, angalia kwamba wengi unaojadiliana nao wana upeo tofauti na malezi tofauti, inaweza kupelekea wasitambue makusudio yako, na kuwafanya wakurupuke kwenye kutoa majibu yao yasio endana na ustaarabu wa kawaida wa kwenye mijadala. Ukiwa kama msomi basi ni wajibu wako kutumia maarifa na uhodari wako ili wengine wafahamu unalolikusudia. Kuna msemo mmoja unasema hivi: "Wafunzeni wengine bila ya kuwa wafunzaji"

Kuna hawa wanasiasa kutoka vyama mbalimbali kama vile CCM, CUF, CHADEMA na wenginewe. Hawa watu wote, ukiondoa itikadi zao za kisiasa, wanaunganishwa na dini zao. Na ni wenye imani za dini tofauti tofauti. Ukiondoa ukabila basi wanaunganishwa na siasa za vyama vyao. Lakini cha ajabu nilicho kigundua humu kwenye tovuti baraza hii watu wanabaguana si kisiasa tu hata kidini, imefikia kiasi ya kuchukiana kwa sababu tu fulani ni chama fulani au dini fulani.

Mimi nasema hivi, Kashfa na Kejeli za Kisiasa au kidini ni uvunjifu wa haki msingi za binadamu zinazohatarisha pia mafao ya wengi ndani ya jamii zetu. Wamiliki wa hizi tovuti baraza tunao wajibu wa kulinda na kudumisha haki za msingi za Kisiasa na Kidini, kwani hizi pia ni sehemu ya haki za kila mmoja wetu.

Mimi ambaye ni Muislam/Mkristo, na si mfuasi wa chama chochote kile cha kisiasa, nikisoma bandiko la mfuasi wa Chadema, CCM au CUF, na katika hoja zake akausema vibaya Uislam/Ukristo kwa ubaya, kwa kuwa tu muhusika wa ilo tatizo ni Muislam/Mkristo, atakuwa ajanitendea haki mimi ambaye ni mfuasi wa imani hiyo ya Kiislam/Kikristo. Vipi unausema Uislam/Ukristo wote, eti tu muhusika wa ilo tatizo ni Muislam/Mkristo? Inanishangaza sana watu wanaposhindwa kumjadili mtu kama yeye bila ya kumuhusisha na imani yake. Hii yote ni kutokana na kutojua misingi ya majadiriano, na kukimbilia kujibu hoja hata pale unapokuwa huna la maana katika kuchangia hizo hoja.

Utawakuta wenywe eti wanatetea haya kwa kusema hii ndio Demokrasia. Jamani eeh, Demokrasia ni neno pana sana, linaweza kutafsiriwa kwenye kanuni ya wengi wape au ikimaanisha kuwa watu wawe huru kujieleza au kuelezea hisia zao lakini kwa kutumia maneno yalio na adabu na nidhamu, bila ya kuvuka mipaka ya kisheria.

Kipindi ambacho hatukuwa na hizi tovuti, tulikuwa tukitegemea sana magazeti na wakati mwingine tukijadiliana kwenye vibaraza vya kahawa na baadae kwenye luninga. Mi bado nakikumbuka kile kipindi cha Kitimoto... Tulishuhudia washirika wake wakishindana kwa kuchangia hoja zenye nguvu. Hoja ambazo ziliweza kuamsha hari ya msomaji/mtazamaji kuchangamsha akili yake na kufanya utafiti kabla ya kuja kujibu hoja husika.
Lakini kutokana na kukua kwa teknolojia hivi sasa tunashuhudia kila aina ya matusi na maneno yasio na maana kiasi ya kutia shaka akili za hawa wanaochangia kwenye hizi blog na tovuti baraza.

Humo kwenye hizo tovuti, zinatembelewa na viongozi wa vyama, nikimaanisha CUF, CHADEMA, CCM, na vyama vinginevyo. Kama hakuna viongozi wa hivyo vyama basi kuna makada wake, ambao wanajulikana kwa majina yao, lakini cha ajabu sijawasikia wakikemea huu upuuzi unao endelea kila kukicha. Kwangu mimi inanipelekea kuamini kuwa wanayapenda haya yanayo endelea humu, kwa sababu ndio sera za vyama vyao. Na kama wanayakubali haya yaendelee kwenye hizo tovuti, basi yatashindikana vipi yasitokee huko nje kwenye utendaji!?

Tatizo ni kwamba, narudia, uandishi umevamiwa na watu wasio makini. Wako wapi wale ambao wana uwezo wa kujadiliana kwa hoja? Wakatuhabarisha sisi ambao tupo mbali na nyumbani? Hata viongozi wa siasa wanaogopa kuingia humu kwa kuhofia matusi, kejeli na kashfa zisizo na ukweli.

Viongozi wa Kisiasa wana uwezo mkubwa wa kupiga stop ujinga wowote ule. Lakini tabia ya viongozi wetu nao wamo kwenye ushabiki huo huo wa siasa na udini. Na kwa kuwa nao ni washabiki na kile kinacho andikwa kikihusu kile anacho kipenda na kukishabikia basi, hawali shughulikii, hata kama ni baya. Na pakitokea lolote lile ambalo ni kinyume na ushabiki wake, watalishughulikia, hata kama ni zuri.

Hata uko nje kwenye majukwaa yao, kwenye siasa zao sikiliza hotuba kwenye majukwaa ukawasikilize. Sera hamna, bali utasikia tu "fulani akiwa kiongozi ataleta udini, ataleta Waarabu, uku nako utawasikia ataleta ukatoliki, mara na huyu naye utamsikia nchi itakuwa haina amani, watu watachinjana kama Rwanda na Burundi na blah blah blah nyiiingi. Wengine utasikia, "si mnamuona, ana kitambi kama mtungi, ana ndevu kama gunzi la mhindi, kipara kama..." Yaani mipasho tu kama vile tupo kwenye taarabu za rusha roho "Hana nywele kichogoni, kapigwa pasi haendi saluni fyoko fyoko fyoko" Aaah! Inaudhi kusema kweli... Jamani mtanisamehe, lakini palipo na ukweli na usemwe.

Mtu wa maana mwenye mawazo maangavu huzipitisha jitihada na nishati zake katika mikondo inayofaa. Mtu mwenye heshima ya kiasi chochote kile ana haki ya kuheshimiwa na wengine; hivyo, hujiepusha kabisa na mambo yanayowaudhi watu, kwa sababu kitambulisho bora kabisa cha mwungwana ni tabia yake ya kila siku inayoonekana kwa kuingiliana na watu.

Siasa imekuwa ni uadui, yaani kila kukicha ni rafu tu, kutokupendana, kufanyiziana, kusimangana, kutukanana, na kila aina ya uharo ndio tunauita siasa.

Lakini hata uharo nao hukauka ukapoteza harufu. Bado tuna matumaini kuwa siku moja wataibuka waandishi na wanasiasa wanaojua kutoa hoja nzuri na mbaya. Wataondoa mbovu, na kuweka nzuri.

Sasa sisi wengine tusiokuwa na vyama, mnatuogopesha na siasa zenu za visasi. Mimi natarajia watu washushe nondo za uhakika na waeleze mazuri ya vyama vyao, na ikiwezekana waielekeze jamii nini cha kufanya, pale linapotokea tatizo na si kuleta matusi....!

Kwani uko CUF, CHADEMA au CCM hakuna mazuri...!? Na kama kuna mabaya tu, nyie wachambuzi mnarekebisha vipi ili kupata kilicho kizuri?
Tanzania ni yetu sote, sasa hawa wachache wasituhatarishie amani yetu. Mtakapoanza kuwatukana kuwa wanachama wa chama fulani i.e CHADEMA, CUF au CCM au watu wa dini Fulani kuwa ni wajinga au kuwaita wapumbavu, hawakusoma, makafiri au waswahili, unaye mtukana hapa kama si nduguyo ni nani!? Hivi kuna familia ambayo hakuna Muislam au mkristo?

Kuna ambao hawataki kabisa kubadilika, wao wanaona kuwa ni haki yao kutukana na kuwakejeli wale ambao wana mitazamo tofauti na wao...! Hawa mimi nawaona kuwa hawana hoja, na litakapokuja suhala la kutoa hoja, mtu kama huyu hana nafasi na kwanini tumpe nafasi ya kututukania imani na itikadi zetu... Kwani kuwa Muislam au Mkristo ndio tiketi ya kukufanya wewe uwe msomi au mwanasiasa bora uliye makini!?
Hiyo freedom of speech hisio na mipaka ndio freedom ya wapi? Nasema hivi: There is no Freedom without Self Discipline.

Enyi Watu wa Siasa! Njooni kwenye neno lilio sawa baina yenu nyote: Ya kwamba tupiganie maisha bora na ustawi wa kila Raiya wa Tanzania kwa hoja, tukiheshimiana na kuelimishana, bila kutumia matusi na kejeli wala tusifanyane sisi kwa sisi kuwa ni maadui.

Kumbukeni kwamba hata watu waovu hujiona wanayo haki ya kufanya maovu. Mwizi huona anayo haki ya kuchukua cha mtu mwingine. Mharibifu huona anayo haki ya kuharibu mali ya mwingine, vivyo hivyo mchokozi hujiona anayo haki ya kuchokoza. Fisadi hujiona ana haki ya kufanya ufisadi wake.... Ajabu sana, kuna ambao ujiona eti wamejitengenezea maadui na watu wa kuwachukia humu kwenye hii tovuti baraza, wanashangaza sana watu hawa. Kwa maana wamesahau kuwa kusema kweli ni sehemu ya uadilifu.... Na ukweli una tabia ya kujilipiza kisasi.

Namalizia kwa kusema hivi... "Mtu anayekuudhi hukupa fursa nzuri ya kumsamehe na kuona utamu wake. Tumefunzwa kuwasamehe maadui zetu lakini hatukuambiwa tusiwasamehe marafiki zetu. Hivyo, ni wazi kwamba ni lazima tusamehe na ikibidi tusahau mabaya tuliyotendewa na wengine. Unapomlipizia kisasi adui wako huwa ni sawa naye, lakini unapomsamehe huwa ni bora kuliko yeye, kwani yeye huwa ni mwovu, nawe huwa ni msamehevu.

Huenda tusifanikiwe tunapotaka kulipiza kisasi, lakini kusamehe ni njia bora kabisa ya kulipiza kisasi. Kwa kusamehe tunaweza kuwashinda maadui zetu bila ya kupigana na kuwafanya wainamishe vichwa vyao mbele ya utukufu wetu. Kwa hivyo, kuacha chuki na kukwepa uadui ni shambulio kubwa kabisa lenye kuwashinda mahasimu wetu. Tunapotendewa maovu, tuwatendee mema, kwani kulipa mema kwa mabaya uliyofanyiwa ni siasa nzuri ambayo kwayo hupatikana amani duniani."

"Shujaa mwenye nguvu kuwashinda nyote ni anayejimiliki nafsi yake wakati akihamaki. Na mstahamilivu kuliko nyote ni anayesamehe wakati ana uwezo wa kuadhibu."

'Nguvu si kwa kupigana mieleka. Bali mwenye nguvu ni yule anayezuiya nafsi yake wakati akishikwa na ghadhabu au hasira'


Natamani kuendelea kuandika, lakini aaah! Uzi mrefu kama huu, nani atausoma, utasikia si ufupishe tu, ngonjera ndeeefu ka reli, khaaaa.


 
Mi naona povu la jukwaa la dini mnahamisha huku kwa kukosa washabiki wengi

I am sorry bro x-paster, i dont trust you anymore, you are never neutral and you only become wise unapoguswa interest zako

Just another crap from mdini... wewe, maxshimba na makundi yenu you ahve nothing except mbegu za chuki na magawanyiko
 
tatizo si kuwa watu wanabishana-la hasha-
x-paster,tatizo ni kwamba mtu anaweza leta mada yake,then akafanyiwa counter argument yenye haki,huku ikiwa inatoa reference nzuri tu,ila az long ukweli mara zote unauma,ndipo malumbano na lugha chafu zinaanza hapo.
NI SAWA NA MTOTO WA SHULE ANAPOFANYA KOSA KISHA MWALIMU WAKE AKAMCHAPA VIBOKO,MTOTO HUYOHUYO ALIKUEKUWA AKISIFIA HIYO SHULE/MWALIMU HUANZA KUIPONDA KWA KUPEWA ADHABU AMBAYO YEYE ANAIONA SI HAKI,KUMBE NI HAKI YAKE,NA MWALIMU WAKE ANAJARIBU KUMFUNZA LIPI ZURI NA LIPI BAYA
 
Wakuu ni busara kwanza tukasoma na kuelewa uzi ulioko, kisha tukatafakari kabla ya kujibu hoja iliyoko mbele yetu, nahisi hapa kama baadhi ya watu wamekurupuka kujibu kwa kuwa tu walikuwa wanataka kujibu, tena kwa kusoma mistari miwili mitatu kisha wakakurupuka kwa kuwa wanahisi mtoa mada si katika wale walioko kundini...! Poleni sana... Mna safari ndefu sana katika ukimwenguu huu...!

Wakuu nasema hivi, ili kuhifadhi umoja wetu, tunapaswa na tunawajibika kuheshimu misingi ya adabu ya maisha na si vema kuwa na tabia ya kuumbua umbua na kubezana, tabia ambayo husababisha utengano na kuvunjika uhusiano wa kirafiki. Ni lazima Watu tuwekeane heshima zetu na tujiepushe kabisa na tabia ya kuhiziana, kudharauliana na kutukanana...!

Sisi binadamu tuna tofauti kubwa sana na wanyama, tena viwango vyetu na uwezo wa mwanadamu ni mkubwa mno na kila mtu ana fursa nzuri ya kuyaelekeza kwa busara matamanio yake katika maisha. Lakini basi hakuna kitu kilicho muhimu kwa mtu na kwa wakati huohuo kikawa kigumu zaidi kama kuidhibiti hisia na matamanio ya nafsi yake. Basi tunashauriwa kwamba yale tunayo yataka kuwa yasizidi kupita kiasi na kuondoa busara zetu, kiasi ya kwamba tukawacha kushirikisha akili zetu katika kuyaendea yale tunayo yataka yawe.

Kwanini tunashindwa kuondoa ubinafsi, kwanini tunashindwa kutumia bongo zetu, tukawavuta wale tunaowatenga na kuwaona kuwa ni maadui zetu, kwanini tunashindwa kuwavuta kwa maneno mazuri na yenye hikma...! Mara nyingi naona wachangiaji wengi upenda kutumia maneno ya kebehi na yenye kuudhi, katika kujibu hoja. Hali hii sidhani kama inaweza kumvuta mtu yeyote mwenye akili zake timamu.

Binadamu ukijipenda sana, kunakupelekea kuwa na kiburi na kujiona wewe ni bora kuliko wengine... na hali hii ni sawa na kujenga ukuta badala ya kujenga daraja la kutuunganisha na wale tunao waona kuwa si bora kama sisi... Na hali hii tukiiachia kuendela basi huwa ni muhali kupatikana mafanikio ya maisha kwa sababu kama hakuna nidhamu katika majadiliano basi hakuta kuwa na muwafaka, na siku zote tutakuwa kama kuku wa kienyeji kwenye banda, kwa maana hakuna masikilizano...!

Binadamu tumeumbwa ili tushirikiane kwa pamoja ili kufikia malengo na mustakabari wa maisha yetu... Kwa sababu kila binadamu anapenda kusikilizwa na wengine. Kila mtu anapenda kuishi kwa masikilizano na wengine na anachukia asiposikilizwa. Lakini ikitokea mtu kuwa na roho mbaya, yenye chuki zisizo na sababu, basi moyo wake ukosa utulivu na ukosa amani kwenye nafsi yake.... kiasi ya kwamba uwachukia hata wale wanao mpenda na kumwelekeza kwenye mafanikio yake mwenyewe.

Amani, upendo, masikilizano na ushirikiano na watu wengine, ndio msingi muhimu wa maisha ya katika jamii yoyote ile. Sharti la kwanza kabisa la kuwepo upendano na masikilizano ni kuheshimu hisia na haki za watu unaofanya nao majadiliano. Jambo hili ndilo linaloimarisha na kudumisha uhusiano kati ya kila mtu. Watu wasiokuwa na sifa kama hii husababisha kuvunjika masikilizano kati yao na kila mtu katika jamii, huregeza nguzo ya urafiki na upendo, na wala hawawezi kuhifadhi uhusiano wao na watu wengine katika hali inayokubalika.

Tabia ambayo ni mbaya kabisa na yenye kuondoa mafungamano ya kirafiki na umoja katika jamii ni kutosikilizana, kubezana, kutukanana kukebeihana, haya mambo uleta ugomvi. Mara nyingi mtu mgomvi uonekana mbele ya jamii kama hana sababu, lakini sababu kubwa kabisa ni yeye mwenyewe na nafsi yake kwa kuruhusu roho chafu kumtawala na kujiona kuwa yeye ni bora na mwenye kutaka kusikilizwa peke yake, kumpelekea kujenga kiburi ambacho uharibu na kuathiri hisia zake na kuuchafua moyo wake na kupoteza nishati inayotunza mwili wake, na kusababisha mtu huyu kuzeeka upesi na wakati mwingine kupata matatizo ya kiafya.

Lakini pia kuna ulazima wa sisi wenyewe tuelewe kwamba ubinafsi wetu uliopitiliza kiasi ndio sababu ya kutopendana kwetu. Kwani mmea wa ugomvi na chuki ukua kwa kumimiwa maji na kupaliliwa na mbolea ya ubinafsi.
 
Mi naona povu la jukwaa la dini mnahamisha huku kwa kukosa washabiki wengi

I am sorry bro x-paster, i dont trust you anymore, you are never neutral and you only become wise unapoguswa interest zako

Just another crap from mdini... wewe, maxshimba na makundi yenu you ahve nothing except mbegu za chuki na magawanyiko

Na watu duniani wanastuka, wanajua huu ni ulaji wa watu tu, kununua ma hummer na kujenga majumba ya kifahari.
Itakua wametumwa kuchota "kondoo" maana, bila kondoo, pesa hakuna, na hii na kwenye dini zote na madhehebu yote!
 
MKUU X-PASTER. Kumbuka kwamba SILENCE IS THE ANSWER FOR THE FOOL. Viva X-PASTOR. Viva JF.
 
Back
Top Bottom