nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
- Wateja hufutiwa madeni katika mazingira tata, BoT yachunguza
- Mtandao wa wezi wapambana kujiokoa
Raia Mwema | Toleo la 251 | 25 Jul 2012​
HALI si shwari ndani ya Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) baada ya Mkurugenzi Mkuu wa benki hiyo, Lawrence Mafuru, kusimamishwa kazi, Raia Mwema limebaini.
Habari za ndani ya benki hiyo, ambayo Serikali ya Tanzania inamiliki asilimia 30 ya hisa, zinaeleza kwamba, kuna shinikizo la kuitaka serikali, kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT) pamoja na Hazina, kuchukua hatua za haraka kulinda maslahi ya Tanzania katika benki hiyo.
Lakini wakati kukiwa na shinikizo hilo la kutaka hatua za haraka kuchukuliwa, uchunguzi wa Raia Mwema umebaini kuwa tayari vyombo vya dola, kwa kushirikiana na BoT, vimeanza kuitupia jicho NBC.
Hata hivyo, uchunguzi huo unafanyika katika benki hiyo yenye mtandao mkubwa nchini katika mazingira ya hadhari kubwa ikidaiwa kuwa, kuna juhudi kinzani zinazohusisha mbinu chafu ili hatimaye kuficha ukweli kwa malengo ya kuwalinda wahalifu wakuu dhidi ya mkono wa sheria.
Kwa mujibu wa uchunguzi wa gazeti hili uliohusisha watendaji mbalimbali wa NBC, kwa sasa raia wa kigeni ndani ya benki hiyo wamekuwa wakifanya kila aina ya hujuma kwa muda mrefu sasa, na kwa upande mwingine wakijitahidi kuwabana wazalendo wanaoonekana kuwa vikwazo kwao katika kufanikisha mbinu zao chafu.
Taarifa ambazo gazeti hili linazo zinaonyesha kuwa moja ya mambo yanayochunguzwa
na vyombo vya dola kwa sasa ni pamoja na ununuzi wa mtandao wa kibenki ambao ni maalumu kwa kuhifadhi kumbukumbu za wateja. Kitaalamu mtambo huo unajulikana kama Flexcube Data Base.
Mtandao huo ambao umenunuliwa na maofisa wa NBC ambao ni raia wa kigeni wanaofanya kazi katika benki hiyo inayoendeshwa kwa ubia kati ya Tanzania na Afrika Kusini, umeelezwa kugharimu Dola za Marekani milioni 30.
Lakini kinachoibua utata hadi kuhitajika uchunguzi ni taarifa nyingine kwamba, mtambo wa aina hiyo hiyo umepata kununuliwa na benki ya NMB kwa gharama ya Dola za Marekani milioni sita tu.
Mbali ya uchunguzi unaohusu bei kubwa katika ununuzi wa mtambo huo, uchunguzi pia unalenga kuangalia ubora wa mtambo huo ambao mara kwa mara umekuwa ukiigharimu NBC fedha nyingi kutokana na kuleta wataalamu kutoka nje ya nchi kuufanyia marekebisho kwa gharama kubwa.
"Flexcube ikifanyiwa marekebisho madogo tu (change request) kila hatua inagharimu Dola za Marekani 60,000 (Sh milioni 100) mbali ya gharama za kuwaweka wataalamu hao nchini katika nyumba za gharama na huduma nyingine," anaeleza mtaalamu mmoja wa mambo ya benki ambaye kwa sasa anajishughulisha na shughuli za kutoa ushauri wa kitaalamu (consultancy).
Raia Mwema liliwasiliana na Mkuu wa Kitengo cha Masoko NBC, Mwinda Mfugale kuhusu tuhuma zinazoelekezwa katika benki hiyo. Hata hivyo, Mwinda hakuwa na majibu ya kila hoja kama ilivyoanishwa katika habari hii na badala yake alimjibu mwandishi wetu akisema; "Tuhuma zilizotajwa ni za jumla, hazijaelekezwa kwa yeyote na wala mimi sina maelezo ya uchambuzi wa tuhuma hizo, kwa hiyo siwezi kuzungumzia masuala hayo zaidi ya taarifa tuliyotoa kwa vyombo vya habari kuhusu kusimamishwa mkurugenzi kwa ajili ya kufanyika uchunguzi."
Lakini pamoja na majibu hayo ya Mwinda, habari zaidi kutoka ndani ya NBC zinaeleza kwamba, benki hiyo imekuwa ikihujumiwa kwa makusudi na baadhi ya wageni ndani ya mfumo wa benki hiyo kiasi cha kuwafukuza hadi wateja wake wakubwa, akiwamo mfanyabiashara mmoja mkubwa nchini mwenye viwanda.
"Wanaiua (NBC) kwa makusudi, wanafukuza hadi wateja wakubwa. Wanajihusisha na mikopo mibovu, mambo ambayo yanasababisha mtikisiko mkubwa kwa benki kiasi cha kuishitua hata BoT," anaeleza ofisa mmoja katika moja ya matawi ya benki hiyo katikati ya Jiji la Dar es Salaam.
Kutokana na mtikisiko huo, huku tayari BoT ikianza kufuatilia kwa makini nyendo za benki hiyo kubwa nchini, Raia Mwema limeelezwa kwamba, wanahisa wa benki hiyo wanaweza kutakiwa kuongeza mtaji zaidi, jambo ambalo linaweza kuibua maswali juu ya kwa nini benki walimowekeza haizalishi faida tofauti na hali ilivyo katika benki nyingi nyingine nchini.
"Watanzania tumekuwa kama shamba la bibi, anakuja Mtanzania mwadilifu kama Mafuru anadhibiti uhalifu wengine wanamhujumu kwa kumfanyia vituko. Sasa wamefikia hatua ya kutaka kumharibia hata heshima yake katika jamii," anasema ofisa mmoja mwandamizi kutoka Wizara ya Fedha.
Mbali ya eneo la ununuzi, NBC pia imekuwa ikipoteza mabilioni ya fedha katika ukusanyaji wa madeni. Katika eneo la ukusanyaji madeni, mabilioni hupotea kwa kutumia mbinu ya kufuta baadhi ya madeni katika mazingira tata.
Ukiondoa wizi wa mabilioni katika mchakato wa ukusanyaji madeni na eneo la ununuzi, uchochoro mwingine wa wizi hufanyika katika uwasilishwaji wa fedha za mauzo ya mali za wadaiwa sugu.
"Uchunguzi usiishie kwenye ununuzi wa flex pekee, uende mbali zaidi hadi kwenye vifaa vingine kama vile milango, kamera na vifaa vingine ambavyo kwa kweli ni utata mtupu na pia usafirishaji wa fedha na masuala ya ulinzi," anasema ofisa mmoja ndani ya NBC, jijini Dar es Salaam.
Hofu kubwa kwa sasa imetanda ndani ya NBC kutokana na baadhi ya wafanyakazi kuanza kuhisi kuwapo kwa njama za kutaka hisa zote za benki hiyo kuchukuliwa na wageni.
Mtego unaosababisha hofu hiyo kwa wafanyakazi wazalendo unatajwa kuwa ni kujenga hoja za kuilazimisha Serikali ya Tanzania kuweka nyongeza ya mtaji katika benki hiyo na kama ikishindwa, basi hisa za serikali ziuzwe na katika kuuza, wanunuzi watakuwa wamekwishakuandaliwa na hatimaye benki kulimilikiwa kwa asilimia 100 na wageni.
Katika NBC kwa sasa, ABSA kutoka Afrika Kusini inamiliki asilimia 55 ya hisa na Serikali ya Tanzania ikiwa na asilimia 30, na asilimia nyingine 15 za hisa zinamilikiwa na International Finance Corporation (IFC-Shirika la Fedha la Kimataifa).
Hata hivyo, tayari ABSA imekwishauzwa na kununuliwa na Benki ya Kimataifa ya Backlays na taarifa nyingine mpya zikibainisha kuwa mmoja kati ya wamiliki watatu wa NBC, yaani IFC, iko tayari kuuza hisa zake.
Kutokana na IFC kuwa tayari kuuza hisa zake, baadhi ya wafanyakazi wa NBC wanashauri ni vyema Serikali ya Tanzania ikazichukua hisa hizo badala ya kuziuza.
Lakini wakati hayo yote yakiendelea kuhusu NBC, taarifa zilizolifikia gazeti hili la Raia Mwema zinaeleza kuwa Bodi ya Wakurugenzi wa benki hiyo inatarajiwa kukutana leo Jumatano kujadili hali ya benki yao, ikiwa ni pamoja na hatima ya Mafuru na wafanyakazi wengine.
Mafuru alisimamishwa na bodi ya NBC kwa madai ya kupisha uchunguzi huru, hatua ambayo yeye binafsi alisema anajiamini, ni msafi na anatarajia kuendelea na kazi baada ya uchunguzi huo.
Hadi kufikia Desemba mwaka 2010, NBC ilikuwa na mali zenye thamani ya Sh trilioni 1.47 amana za wanahisa kiasi cha Sh. bilioni 153.1, hiyo ni kwa mujibu wa tovuti ya benki hiyo.
NBC ilianzishwa nchini mwaka 1967 wakati Serikali ya Tanzania, chini ya Mwalimu Julius Nyerere ilipofanya utaifishaji wa taasisi za fedha, zikiwamo benki.
Mwaka 1997, NBC iligawanywa katika taasisi tatu tofauti. Taasisi ya kwanza iliitwa NBC Holding Corporation (Shirika Hodhi la NBC-Shirika lililokuwa na jukumu la kusimamia mali za NBC-mama), taasisi ya pili ikaitwa National Microfinance Bank (NMB) na taasisi ya tatu ikaitwa NBC (1997) Limited.
Baada ya mgawanyo huo, mwaka 2000, Kundi la kibenki la Afrika Kusini (Absa Group Limited) ilinunua hisa nyingi za NBC (1997) Limited zilizokuwa zikiuzwa, ununuzi ambao ulizua upinzani mkali nchini ikielezwa kuwa ni uuzaji wa bei ya kutupwa.
Uuzaji huo ulipingwa vikali na Mwalimu Julius Nyerere ambaye kwa ujumla, hakuwa akifurahishwa na mchakato wa ubinafsishaji na hasa unaohusu mashirika ya umma yaliyokuwa yakijiendesha kwa faida.
Katika ununuzi huo wa ABSA Group iliyochukua asilimia 55, Serikali ya Tanzania ‘ilijigawia' asilimia 30 ya hisa na IFC, shirika lililo chini ya Benki ya Dunia lilinunua asilimia 15 ya hisa. Katika ‘mauzo' hayo, NBC ikaitwa National Bank of Commerce (Tanzania) Limited.