Maadili ya uchaguzi yanailinda CCM

Zak Malang

JF-Expert Member
Dec 30, 2008
5,404
233
Maadili ya uchaguzi yanalinda CCM

Na NdimaraTegambwage

YALE yanayoitwa "maadili," ambayo vyama vya siasa vinatakiwa kusaini na kufuata wakati wa kampeni na uchaguzi mkuu Oktoba mwaka huu, hayatekelezeki.

Hayatekelezeki kwa kuwa ni mtego ulioundwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kukabidhiwa kwa wateule wake ili kuangamiza hata uhuru kiduchu wa kujieleza na kutoa maoni uliokuwepo.

Tuchukue mifano michache ya baadhi ya yanayoitwa maadili kwenye orodha ndefu ambayo tayari vyama kadhaa vimesaini na kujifunga kuyatekeleza. Tufuatane.

Vyama ambavyo havijawahi kushika serikali, vinaambiwa kuwa "vikosoane" na hasa hapa ni kukosoa CCM "kwa kuonyesha kazi walizofanya."

Hili ndilo CCM inapenda sana na imelikuza kwa kulileta mwanzoni. Ni hili pia ambalo Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, John Tendwa anapigia vuvuzela.

Tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini (1992), viongozi wa CCM wamekataa ukweli; wamekumbatia ghiliba.

Wamekuwa wakizunguka nchi nzima kuwaambia wananchi kwamba "wapinzani wakija waulize wamewafanyia nini."

Hawakomei hapo. Wamekuwa wakiwaambia wananchi kwamba CCM imeleta barabara, zahanati, shule, hospitali na kwamba sasa wananchi wawaulize "wapinzani wameleta nini?"

Katika hali ya kawaida, huu ni ujuha. Lakini pia ni matusi makubwa kwa wananchi; kwamba ni wajinga na hawawezi kung'amua nani hasa anapaswa kukabwa koo kwa kufanya au kutofanya lolote.

Hii ni hatari. CCM ndiyo inaunda serikali. Ni serikali ya CCM iliyoko ikulu. Ni serikali hiyo inayokusanya kodi za wananchi. Sasa imuulize nani aliyefanya nini?

Ni utaratibu; hapana! Ni kanuni na sheria kwamba serikali ndiyo inakusanya kodi kutoka kwa wananchi. Hivyo ndiyo inawajibika; inalazimika kutumia kodi hiyo kwa manufaa ya wananchi – walipakodi.

Sasa badala ya CCM na serikali yake kutoa maelezo ya matumizi ya kodi za wananchi, wanataka vyama wanavyoita vya upinzani vieleze vilifanya nini. Vilifanya nini kwa kutumia nini?

Huu ndio ukora wa kisiasa, kwani ni chama chenye serikali kinachopaswa kueleza kilikusanya kodi kiasi gani; kilizitumia wapi; zimetumika shilingi ngapi; zimebaki ngapi; zilizobaki ziko wapi.

Hapa ndipo chama chenye serikali, kinachotoza kodi, kinapopaswa kueleza kwa nini kinajenga madarasa yanayoanguka baada ya wiki mbili – CCM.

Kwa nini kinanunua mashangingi badala ya matrekta? Kwa nini kinalipa watu wachache mishahara minono kupindukia na wengi wanaodai Sh. 315,000 tu kwa mwezi wanafokewa, wanatishiwa kuwekwa ngeu na kufukuzwa kazi – CCM?

Chama chenye serikali ndicho kinapaswa kutoa maelezo juu ya mapato kutokana na maliasili na raslimali nyingi za taifa (madini, mbuga na misitu) na jinsi mapato hayo yalivyotumika – CCM.

Chama kilichoko ikulu – CCM, ndicho kinapaswa kuulizwa kwa nini hakijaweka mipango hii au ile.

Kwa mfano, kwa nini serikali yake haitaki kuua mbu wanaoambukiza malaria na kuua mamilioni ya wananchi; na badala yake inatangaza na kukuza biashara ya chandarua chenye matundu makubwa kama mitego ya dagaa?

Ni hao walioko ikulu wanaopaswa kuulizwa na kujieleza, kwa nini zahanati, vituo vya afya na hospitali hazina dawa.

Waulizwe haohao, walipeleka wapi mabilioni ya shilingi waliyokusanya kwa watuhumiwa wa ufisadi kwa sharti la kuwasamehe; na kwa nini walisamehe watu waliokiri kuiba, tena bila shinikizo?

Katika hali hii, CCM itakosoana na nani? Ni yenyewe inayopasa kukosolewa na hasa kuandamwa kwa yale ambayo hayakufanywa au yalifanywa vibaya.

Kama kuna cha kukosoa vyama vingine ni kama vilifanya kazi ya kuamsha, kuelimisha, kushawishi na kuchochea wananchi kuondoa CCM ikulu kwa kuwa imeshindwa kazi.

Lakini hilo haliwezi kuulizwa na CCM kwa vile ingetaka wabaki wajinga, waoga na kimya!

Eti maadili yanataka "kuepukwa" kwa ukosoaji unaogusa tuhuma ambazo hazijathibitishwa. Hiki ni kichekesho. Bila shaka kuthibitishwa kunakohitajika ni hukumu ya mahakama.

Hapa kinachoitwa maadili kinalenga kukinga CCM. Kuna tuhuma nzito za ufisadi zilizoibuliwa miaka minne iliyopita, lakini serikali yake ilizifumbia macho.

Tuhuma hizi zingalipo; tena mbichi. Ushahidi ulioko mikononi mwa walioziibua unatosha kabisa kuwapeleka watuhumiwa mahakamani. Lakini hawajaguswa.

Katika kazi kuu ya kampeni, watu hao hawawezi kuachwa bila kutajwa; tena kwa majina yao halali na yale ya utani, kwamba wanatuhumiwa na umma unashangaa kwa nini tuhuma dhidi yao hazichunguzwi?

Kwa nini chama kilichoko ikulu kisikabwe koo na hata kuambiwa kuwa, ama kinashiriki ufisadi au kimewahi kunufaika nao? Kwa nini?

Kinachoitwa maadili kinataka "kusiwepo lugha ya matusi." Hii ni njia nyingine ya kuziba watu midomo.

Kutoa matusi ni kosa la jinai. Sheria iko wazi kuhusu hilo. Sasa kuchukua suala linalohitaji maamuzi ya kisheria na kuwakabidhi wanasiasa na watumishi wao, utakuwa msiba mkubwa.

Angalia hili: Eti kusiwe na "lugha ya matusi, kashfa, kejeli, udhalilishaji, vitisho au lugha inayochochea uvunjaji wa amani."

Mwenye uwezo wa kuamua juu ya haya ni mahakama; siyo Tendwa wala Jaji Lewis Makame.

Hii ni kutokana na ukweli kwamba hayo yaliyotajwa yanaweza kuwa na tafsiri tofauti kwa watu wa vyama tofauti, mirengo tofauti na maslahi tofauti.

Kwamba mtu amenyanyaswa au amedhalilishwa au ametishiwa, hilo iachiwe sheria kuchukua mkondo wake.

Hii ina maana kwamba mtu kama Tendwa au hata msimamizi wa uchaguzi, popote alipo, hana uwezo wa kushughulikia hayo kupitia mkondo wa sheria na vyombo husika – polisi na mahakama.

Kwa hiyo, Tume ya Uchaguzi na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa hawana uwezo wa kumsimamisha yeyote aliye katika mbio za uchaguzi kwa madai ambayo hawawezi kuyathibitisha kisheria.

Kitendo chochote cha kuzima mbio za yeyote anayeshindana, kitachukuliwa kuwa ni hujuma; tena kwa manufaa ya CCM.

Kuna hili la "kukubali na kuheshimu" uamuzi wa Tume uliofanywa kwa mujibu wa sheria za uchaguzi.

Hili nalo lina mgogoro. Kukubaliana na Tume siyo suala la utashi. Kunategemea mazingira husika ambako hata kama tume ilifanya kwa mujibu wa sheria; huenda taratibu za kufikia hapo hazikuwa sahihi.

Siyo lazima vyama na wagombea wakubaliane na kila uamuzi wa tume. Vilevile, hakuna sababu kwa tume kuanza kujikinga. Ikifanya kazi yake vuzuri, hata ikilalamikiwa, hatimaye ukweli utajulikana.

Yanayoitwa maadili ya uchaguzi, hakika yana walakini na yanalenga kujenga mazingira ya woga miongoni mwa vyama vingine na kuikinga CCM. Hayatekelezeki.

Chanzo: Mwanahalisi

 
Hakuna mtu mwenye akili timamu atakayebishia umuhimu wa vyama vya upinzani kwenye maendeleo ya Taifa lolote.
Ni CCM na Serekali yake peke yake iliyopofuka kuhusu hilo!!!!! Inasikitisha na ni aibu kubwa!!
 
Niliisoma ile makala ya Ndimara pale Mwana Halisi mara tu baada ya kuwa nimesoma kuwa Serikali inailipia CCM vifaa vya kampeini. Nilisikitika kuwa huenda gazeti hili halisomwi na watu wa vijijini, au hata kama linafika huko huenda makala zake zinaweza kuwa ni ndefu kwao kuzisoma zote. Vinginevyo nilifurahi sana kuona CCM inachambuliwa vizuri namna hiyo. Strnghold ya CCM ni huko vijijini kama ambavyo ilivyo kwa Mugabe huko Zimbabwe
 
Makala hii inanikumbusha tukio moja miaka ya mwanzoni mwanzoni tu mwa utawala wa JK. Katika mkoa wa Kigoma eneo ambalo madiwani wengi tu ni wa Chadema -- Muungwana aliwaambia wananchi kwamba sababu kubwa ya matatizo yao ya kukosa maendeleo ni kwa sababu wailwachagua madiwani wa upinzani, akimaananisha wapinzani kwa kuwa hawaundi serikali, basi hawana nyenzo za kuwaendeleza!

Punde tu hoja hii ilijibiwa na kiongozi mmoja wa Chadema aliyemkumbusha JK kwamba jee maeneo mengine mengi ya nchi yaliyokosa maendeleo hali yakiwa chini ya chama tawala - CCM - miaka nenda miaka rudi?

Kwa kuona embarrassment hiyo baada ya siku chache Ikulu ilitoa tamko eti alinukuliwa vibaya!
 
kukubaliana na ujuha uliojikita katika maadili haya ni sawa na kujinywesha sumu. Iweje tuafiki kila uamuzi wa tume hata kama sio sahihi au wa upendeleo? Hapa hatudanganyiki
 
Inawezekana upeo wa viongozi chama tawala una walakini.Kuuliza wananchi ati vyama vya wapinzani vimeleta maendeleo gani kwa wananchi,wakati toka uhuru mpaka leo wapinzani hawajaongoza serikali ni batili.Ebu jiulize wakati tunadai uhuru toka kwa wakoloni Waingereza waliotutawala zaidi ya miaka 70,wangeuliza wananchi kuwa wanaharakati wa kudai uhuru wamewaletea maendeleleo gani? Kwa muda mrefu wapinzani wamedai Tume huru lakini wamekataliwa.Ni kweli usiopuuzwa kwamba watawala hawako tiyari kuyaona mabadiliko ya kisiasa.Ila wanalazimishwa na taasisi za kimataifa na nchi za Magharibi.Wapizani si dhaifu kama chama tawala kinavyodai,ndio maana wataingia uchaguzi mkuu ujao wakiwa wamefungwa miguu na mikono.
 
Back
Top Bottom