Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
- Alipewa nafasi ya kujitetea, akatumia kujiuzulu
- Angejiuzulu kabla ya Kamati Teule kuundwa, angekuwa shujaa
- Wanaoamini kaonewa hawajui "natural justice"!
Kuna baadhi ya watu ambao wanaamini mioyoni mwao kuwa aliyekuwa Waziri Mkuu na Mbunge wa Monduli Mhe. Edward Lowassa alionewa na Kamati Teule ya Bunge na kuwa alilazimishwa kujiuzulu kutokana na kutotendewa haki na Kamati hiyo iliyoongozwa na Dr. Harrison Mwakyembe, Mbunge wa Kyela. Watu wenye imani hiyo wanaamini kabisa kuwa Lowassa hakutendewa haki na hivyo wanafanya kila jitihada ya kuhakikisha kuwa Lowassa anasafishwa na hatimaye kujengwa tena ili kuweka rekodi iwe sahihi.
Katika makala hii ambayo nimeitengeneza kwa mtindo wa maswali na majibu nina kusudio la kuonesha kuwa Bw. Lowassa hakuonewa na mtu yeyote, alitakiwa kujiuzulu hata kabla ya Kamati Teule kuundwa na kuwa mjadala way eye kuonewa na chombo chochote ni mjadala unaotokana na mtazamo finyu, wenye ushahidi dhaifu, na kwa kipimo chochote unajaribu kutengeneza kitu ambacho hakipo. Ni makusudio yangu kuonesha kuwa Bw. Lowassa alistahili kujiuzulu mapema zaidi na hata pale alipochelewa alitakiwa kukubali adhabu aliyojipa yeye mwenyewe kutokana na kutokuwajibika kwake, uzembe wa ofisi yake, na kutokuonesha usimamizi unaomstahili Waziri Mkuu katika jambo nyeti kama la nishati.
Lengo kubwa ni hatimaye kulazimisha kwa nguvu za hoja kufunga mjadala huu baada ya kuzipima hoja zote kama zilivyo. Fuatana nami ukiwa na fikra huru ili uweze kuona kuwa nafasi aliyonayo sasa hivi Bw. Lowassa ndiyo nafasi ya juu kabisa ambayo anastahili kuishika katika Jamhuri yetu, ceteris paribus.