Let Zanzibar Go! - Kwanini Zanzibar hawahitaji kuwashawishi Watanganyika ili watoke kwenye Muungano

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,476
39,995
zanzibar2.jpg


Msitunyonye bana nyie! Msitunyonye mnatudhiri! Tuachaneni angalau tujikung'ute kidogo! Tumekuwa mafukara; mtu mwenye miaka kumi na tatu amepinda mgongo kama mtu wa miaka sabini na tano! … tunachotaka sasa hivi mtuachie tupumue!
– Mhadhara wa Uamsho Zanzibar Machi 4, 2012.


Nimekuwa mtetezi wa Muungano kiasi kwamba nimegundua nimebakia peke yangu. Wengine wanautetea Muungano kwa kutumia vitisho na wengine wanautetea kwa kutumia dharau. Binafsi ninaamini muungano unaweza kutetewa kwa hoja maridhiwa zenye kuonesha kuwa Zanzibar na wananchi wa Zanzibar wananufaika na wataendelea kunufaika zaidi katika Muungano kuliko nje ya Muungano. Kwamba hoja za kupinga muungano kwa madai kuwa Wazanzibari wanaonewa na kuwa Zanzibar inakaliwa kama koloni na Tanganyika haina mshiko, ni ya kupuuza na ina uwezo wa kuteka akili za watu wasiotaka kufikiria.


Baada ya muda mrefu kuwa mtetezi pekee wa Muungano kelele za hivi karibuni zimenibadili kabisa mawazo yangu na sasa nimekuwa na nitaendelea kushakizia muungano uvunjwe ili wale wanaoitaka Zanzibar yao wapewe na ili watu wa bara tuhangaike mambo mengine kuliko kuonekana tunawakandamiza Wazanzibari. Ile hofu ya Mwalimu kiasi cha kuachilia mambo mengi ya Zanzibar kuwa tukiungana kuwa nchi moja kamili kabisa Zanzibar watajiona wamemezwa imetimia kwani pamoja na kuwapa kila kitu Zanzibar bado wapo ambao wanaona wanamezwa!


Ni kutokana na ukweli huu kwamba hakuna kiongozi au mwanasiasa wa Tanzania awe mzee au kijana mwenye uwezo wa kuutetea Muungano kisomi na kisiasa na kuwapinga wenye hoja dhaifu ndio maana leo naendelea na hoja yangu ya kuwasaidia Wazanzibar watoke kwenye Muungano, wawe na nchi na taifa lao na zaidi ya yote waweze baada ya kutoka kwenye Muungano kuanza mahusiano mapya na bara kama nchi mbili zilizo sawa. Ninaamini tunaweza kuhusiana vizuri zaidi baada ya Zanzibar kutoka na kuwa taifa lao wenyewe kuliko ilivyo hivi sasa ambapo Muungano hauteteleki – zaidi ya kutumia vitisho vya dola.


Tunawapenda sana ndugu zetu Wazanzibari kiasi kwamba hatutaki kuwang'ang'ania. Wapo kwao wenye kutuchukia sana kiasi kwamba hawataki hata kufikiria sisi ni ndugu zao. Wanatuangalia kwa dharau na kebeki wao wakiamini utukufu wao wa "Zanzibar" isiyokuwepo ndiyo tunu waliyonayo. Ukiwaskiliza sana baadhi ya wapinga muungano kwa kweli kabisa wamejawa chuki isiyo na kifani na chuki hiyo imezaa matunda meusi katika madhihirisho ya chuki dhidi ya watu wa Bara na Wakristu.


Lakini kitu kimoja ambacho watu wengi hawataki kukifikiria ni kuwa hawa watu wanaopinga Muungano wao wanadai "nchi". Sasa hakuna aliyewauliza kwamba mbona katiba ya Zanzibar imefanyiwa mabadiliko na kuitangaza kuwa Zanzibar ni nchi? Sasa kama tayari Zanzibar ni nchi wanachodai hawa ni nini? Haiwezekani kuwa wanachodai ni nchi kwani nchi tayari wanayo na Katiba ya Zanzibar inasema hivyo! Wanachotaka siyo nchi! Wanachotaka ni kuwa nje ya Muungano! Hivi ni vitu viwili tofauti.


Ndio maana basi katika makala ya leo nataka kuwasaidia Wazanzibari hawa na wale ambao wanaamini kuwa muungano haustahili kuteteewa kwa hoja bali kwa vioja. Pendekezo langu ni njia nyepesi za Wazanzibari kujiondoa kwenye Muungano bila kufanya maandamano, mihadhara wala kuwashtumu watu wa Tanganyika. Wazanzibari wakitaka kutoka kweli kwenye Muungano wanaweza kufanya hivyo ndani ya wiki chache tu na wakawa nchi. Nina uhakika serikali ya Muungano haitotumia nguvu kuwalazimisha kubakia! Nyerere mwenyewe alishasema kuwa hawezi kuwalazimisha Wazanzibari kubakia kwenye Muungano.


Njia ya kwanza
Njia ya kwanza na nyepesi zaidi ya kuweza kujitoa kwenye Muungano ni kwa wananchi wa Zanzibar wakiongozwa na hawa wana- uamsho wawatake watendaji wote wa Muungano wenye asili ya Zanzibar kuachia nafasi zao mara moja na kurudi Zanzibar!


Hii ni pamoja na majaji, wabunge, mawaziri, maafisa wa polisi na vyombo vingine vya usalama, na wantedaji wengine ambao wako kwenye Muungano. Badala ya kuililia Tanganyika kila kukicha kuwa inawabana mashehe wa Zanzibari wenye kuongoza vuguvugu la kutoka kwenye Muungano waanzishe mihadhara ya kuwataka Wazanzibari wenzao ambao wanatumikia Muungano waachilie nafasi hizo.


Binafsi ningependekeza kama wataniruhusu waanzishe harakati hizo ili viongozi wote hawa waachilie nafasi zo ifikapo Disemba 10, 2012. Hii ni pamoja na Makamu wa Rais Ghaib Bilal, jaji mkuu na wengine.
Hawa wote wakishawishiwa kuondoka Wazanzibari wajiandae ama kuwapatia pensheni au kuwatafutia nafasi kwenye serikali ya nchi ya Zanzibar.


Sasa hawa wote wakikubali kuondoka kwenye nafasi zao za Muungano Zanzibar itapata wataalamu wengine wengi ambao wamekuwa wakitumikia Muungano na hivyo kujiongezea hazina ya wataalamu mbalimbali. Lakini pia itafungua ajira za Watanganyika wengi ambao wangeweza kushika nafasi zinazoshikiliwa na Wazanzibari hasa kwa vile Wazanzibari hao wako kimya na hawajitokezi kuutetea Muungano ambao wanautumikia.


Pamoja na kuwataka viongozi wao na watendaji mbalimbali watoke kwenye Muungano katika harakati za mwanzo za Zanzibar kujitenga wana uamsho hawastahili kulalamikia Watanganyika. Hawahitaji kuendelea kuwaghilibu vijana wa Kizanzibari kuwa inanyonywa na sasa wanahitaji kupumua. Mashehe wa uamsho waende mbali zaidi katik akudai nchi yao. Waanze kuwahamasisha Wazanzibari walioko bara kuamua kuondoka bara na kurudi Zanzibar ili kuendesha shughuli zao huko.


Watu kama kina Bakheresa wenye biashara kubwa bara itabidi watiwe hamasa waamue kuondoka bara. Siyo hawa tu bali pia wale Wapemba na Wazanzibari waliona maeneo ya ardhi Bara. Hivi ndivyo ilivyotokea Sudan ya Kusini ambapo baada ya nchi hiyo kujitenga Wasudan ya Kusini waliokuwa wanafanya kazi Khartoum waliacha kazi zao na wengi wao wameamua kurudi kwenye nchi yao kuanza kuijenga.


Wengi tunakumbuka kuwa baada ya Rwanda chini ya Kagame kutulia kwa kiasi Wanyarwanda wengi ambao wengine waliishi kama Watanzania waliacha kazi zao na kurudi kwao Rwanda kuijenga nchi y ao. Nakumbuka baadhi ya wahadhiri kwenye taasisi mbalimbali nchini ambao tuliwadhania ni Wahaya au Waangaza walipoamua kuacha kazi zao kumbe walikuwa ni Wanyarwanda.


Hili pia litakuwa na faida kubwa sana kwa Zanzibar kwani itapata watu wengi zaidi wenye uwezo na utajiri mkubwa na vile vile itabidi iwaandalie viwanja vipya vya kilimo na makazi maana vile vya bara itabidi waviachilie kuwapisha Watanganyika ambao wanalalamikia kukosa ardhi au kupatiwa ardhi isiy nzuri. Na pia wafanyabiashara hao wa Kizanzibari watakaporudi Zanzibar na kama watataka kuja kufanya biashara Tanganyika itabidi waje kama wawekezaji na hivyo watasaidia katika ukuaji wa uchumi wa Tanganyika kama wageni wengine. Na kama watakuwa wajanja kama wageni wengine wanaweza kutengeneza mamilioni zaidi kuliko wanavyofanya sasa kama raia wa Tanzania!


Hivyo hilo ni jjambo la kwanza nawashauri wana uamsho; hamasisheni Wazanzibari waondoke Tanzania bara ili warudi Zanzibar ambako watapatiwa nafasi bora zaidi za ajira. Mtakapofanya hivyo, na watu wa Bara nao itabidi waanze kuondoka Zanzibar japo hapo nina uhakika kutakuwa na kazi kidogo. Watu wa Bara ni kina nani Zanzibar?


Njia ya pili
Kuna maneno na kauli za baadhi ya watu wachache wakizungumza kana kwamba wanawakilisha "wengi". Utasikia mtu anayepinga Muungano anasema,"Wazanzibari hatuutaki Muungano" na wakati mwingine kudai "Wazanzibari wengi hawautaki muungano". Sasa mara nyingi wanaposema "wengi" mtu wa kawaida (asiyetaka kufikiri sana) anaweza kuamini kabisa kuwa ni kweli "wengi" hawautaki Muungano.


Mfano unaotolewa siku za hivi karibuni ni "sahihi 500,000" za wanaodaiwa "Wazanzibari" wasiotaka Muungano.
Sasa kwenye mahali ambapo pana watu milioni 1.5 hivi idadi hiyo ni kubwa sana; ni theluthi moja ya watu wote wa Zanzibar. Sasa kama kweli wapo watu wengi hivi njia rahisi ya kutaka kujitoa kutoka kwenye Muungano siyo mihadhara wala hawahitaji kabisa kuwalalamikia watu wa Bara au Serikali ya Muungano.


Kwa wanaokumbuka wananchi wa Zanzibar walishinikiza vyama vyao viwili vya CCM na CUF kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na waliweza kufanya hivyo baada ya kupitisha sheria ya kura ya maoni ambayo hatimaye iliandika upya Katiba ya Zanzibar.


Wananchi wakaweza kujitokeza na kupiga kura ya maoni. Walifanya hivi bila kuomba kibali Muungano na kiasi cha kuweza kuandika kwenye Katiba Yao vitu ambavyo ni kinyume na Katiba ya Muungano.

Sasa kama waliweza kufanya hili ni kitu gani kinawashinda kutaka viongozi wao wa kisiasa kuandia sheria ya kupiga kura ya maoni kama wanautaka Muungano au la?


Kwa vile hoja ya kupinga MUungano inadaiwa inakubaliwa na watu wa vyama vyote ni wazi kuwa ni rahisi sana kwa watu wa Uamsho na Wazanzibari wengine kuhakikisha kuwa BLW linapokaa linaazimia kupitisha kura ya maoni kuhusu Muungano na kutaka sheria iletwe ya kuuliza swali la Muungano.


Swali liwe rahisi tu:
Je unataka Zanzibar ibakie kwenye Muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania?


a. Ndio ibakie - Ikibakia kero na matatizo ya Muungano kutatuliwa ifikapo Julai 1, 2014 na yasipotatuliwa basi kipengele cha "b" kitatimia.

b. Hapana isibakie - isipobakia Zanzibar itajitoa kwenye Muungano ifikapo Julai 1, 2014.



Ijulikane mapema kuwa ikisemwa kuwa "ndio ibakie", maana yake ni kuwa masuala ya muundo na mfumo wa Muungano yatajadiiliwa na kushughulikiwa kwenye Katiba Mpya na yatakuwa tayari kumalizwa yote ifikapo 2014. Baadhi ya watu ambao wamesoma hoja yangu hii ya pili wamedai – na mimi nikakubali – kuwa mwaka 2014 ni mbali sana. Hivyo, Wazanzibari wakitaka kujitenga wanaweza kuja na sheria kwenye kikao kijacho cha baraza la wawakilishi na ninapendekeza Mjumbe Jussa alete muswada wa swali la kura ya maoni ili Wazanzibari wafanye hima ya kujitoa kwenye Muungano.


Nina uhakika wapo Watanganyika ambao watashukuru sana kwa wao pia kupewa nafasi ya kupumua kuliko kila siku kuimbiwa "Zanzibar, Zanzibar"; kama kweli inavyosemwa Muungano ni kama koti likibana unalivua ni wazi kuwa wanaobanwa na koti hilo sasa siyo Zanzibar tena bali ni watu wa bara na sasa wameamua kuwapa Wazanzibar uwezo kamili (absolute power) kujitoa kwenye Muungano bila kufanya mihadhara mingi wala kushindana na dola.
Njia hizo hapo juu zitawasaidia Wazanzibari wanaotaka kujitoa watoke salama hasa kwa vile inaonekana hakuna Wazanzibari wanaoutaka Muungano. Watu wa Bara hatutaki kuonekana tunawang'ang'ania Wazanzibari wakati nguvu yote ya kutoka kwenye Muungano wanayo wao.


Ni matumaini yangu serikali ya Rais Kikwete ambayo imeshindwa kujenga hoja na kuwajibu kwa hoja wana uamsho haitotumia nguvu kuzima harakati za kujitoa kwenye Muungano. Tena ningependa kabisa kutoa pendekezo kwa serikali ya Muungano kukataza kabisa Polisi na JWTZ kuingilia kati mikutano ya wanauamsho na badala yake waache kazi hiyo kwa Valentia, JKU na KMKM.


Vikosi vya Muungano vikae pembeni kabisa kwani vitaonekana vinalazimisha watu kuupenda Muungano. Kama Muungano haupo moyoni, muungano hauwezi kuwepo ulimini! Kama watu wanataka mfumo wa Muungano au mambo fulani yabadilike basi tungeona juhudi za haraka za kutatua kero zote za Muungano badala ya hili la "subirini mkatoe maoni kwenye tume". Watanzania wameshatoa maoni ya kutosha kuhusu Muungano kiasi kwamba kama CCM na serikali yake wangekuwa na uwezo wa kuyatatua basi wangekuwa wamekwishayatatua.


Nidhahiri kuwa hakuna mwenye uwezo huo na sasa kilichobakia ni sote kwa pamoja kutoka Bara tuseme nasi pasi ya shaka kuwa LET ZANZIBAR GO- Iacheni Zanzibar iende.

Itaenda wapi zaidi ya kuwa kwenye kivuli cha Tanganyika ndani au nje ya Muungano


HUU NI MWANZO WA "LET ZANZIBAR GO MOVEMENT 2012"; Kama unaunga mkono kuwaacha Wazanzibar wajitoe kwenye Muungano weka kwenye sahihi yako "I support Let Zanzibar Go Movement 2012"! Tuwasaidie waharikishe wajitoe kwani hakuna kiongozi yeyote ambaye amekuwa na uwezo wa kuutetea Muungano kwa hoja maridhawa badala ya kutumia vitisho na mikwara.
 
MMJ

Umewalima si kawaida, ha ha ha mimi hata ile hotuba ya waziri wa Fedha wa Zanzibara kufoka kwa jamaa wa TRA kuwa atawafukuza na aone nani wa Muungano atawarudisha? sikuona busara hivi anajua katiba kweli?

Mimi nataka nione baraza la wawakilishi watasema nini? umewasidia saana kuweka mambo peupe
 
Mimi nimeshauchoka huu muungano. Ni muungano ambao haueleweki eleweki. Na uvunjike tu hata leo hii hii.

NN, unadhani basi hata umeuchoka Muungano? I bet kilichokuchosha ni manung'uniko yasiyokoma ya Wazanzibari. You are fed up with unending cries of oppression and exploitation kiasi kwamba unajisikia vibaya kuonekana unawaonewa Wazanzibar kama Mtanganyika so unasema bora waende zao tu "tumechoka kulalamikiwa"...

Kwa sababu Zanzibar kwa Tanganyika ni kama kupe mwenye kumlalamikia ng'ombe!!! kila kukicha anatishia kudondoka na kuondoka ili amkomoe ng'ombe ati kwa vile ng'ombe hatoi damu ya kutosha!!
 
Ya wazanzibar wenye asili ya mwarabu au watu weusi kama watanganyika? We unaonaje?
 
Binafsi sijauchoka muungano, ila kwa hulka yangu sipendi kuonea au kunyanyasa mtu na sipendi kusikia mtu akidai hivyo. Kwa kua wazanzibari wanatunung'unikia kua wanaonewa katika Muungano huu na wanataka nchi yao ni vema waende zao. Nasisitiza na waende waishi kwa amani yao.Let them go!!:wave:
 
jamani eeh, ile tar 26 Apr ambayo huwa holiday wasije wakaigusa hata huo muungano ukivunjika. Lol
 
Mzee Mwanakijiji,
Nitakwambia haswa shiriki za kihisia zilizowakumba Wazanzibar...Na naweza sema ni swala la kiasili ambalo limetokana na utamaduni wetu pale ambapo imetumika hata ktk ndoa zetu hivyo kuwafanya Wazanzibar waishi ktk maisha ya What if?...


Ni kwamba zamani ktk ndoa zetu mwanamke akiolewa huchukuliwa kama chombo cha kutotoa watoto, kulea na kutunza nyumba lakini mwenye jina na familia na mali zote ni baba. Na ilitokea hata wakati baba amefariki basi urithi huchukuliwa na wanandugu wa Baba, na kumwacha mke arudi kwao hana kitu, hivyo ktk fikra za utamaduni huu mchafu wanawake wengi siku hizi hutazama kwanza maslahi yao. hata ktk mahari ya ya ndoa tu, huomba wajengewe nyumba, wafunguliwe biashara, wengine wakitazama utajiri wa bwana yote haya ni katika kujilinda wao na nasaba yao.- kule kwa baba na mama zao.

Wapo wengine huwaibia waume zao fedha ama kuficha baadhi ya mapato na matumizi ili apate kujijenga kwao kwa sababu mke huyu huishi kwa fikra za What if mmewe akimwacha atabakia na kitu gani? hufikiria kwamba ndoa yoyote haina guarantee ya kudumu hivyo lazima ajiandae yeye kuachika na familia yake ni kwa baba na mama yake sii mume. Na ktk utekelezaji wa fikra hizi utakuta familia haiwezi kuendelea kwa sababu Ufisadi unatoka ndani na NDIVYO TULIVYO.

Hivyo Wazanzibar kwa fikra zao wanataka bara tuwajengee makwao (tupeleke maendeleo Zanzibar), tuwafikirie wao kana kwamba ipo siku Muungano huu utavunjika na wao hawatakuwa wamepata kitu isipokuwa Bara ambayo imejijengea jina la ubwana. Na ukisikia vilio vyao kwa makini utagundua ni tamaa ya fikra za What if, maana wanazungumzia vitu visivyokuwepo leo, sijui Mafuta yasiwe ya Muungano lakini wanatumia Umeme wa bara bure wakati ni ktk wizara zile zile wasizotaka ziwe ktk muungano. Kifupi ni madai ya mke alopata kazi hataki kuchangia ktk matumizi ya familia kwa madai ya kwamba wewe sii mume kazi yako nini?..mbona wataka hata fedha za mke kuiendesha familia hapo wakimwona mume sii mwana familia ila mtu wa nje alokaribishwa ktk familia - Ni asili ya Wangazija na watu wa Pwani!
 
Mmh, mimi naanza kuwatilia mashaka hawa jamaa, wasije kuwa wameamua kuendesha maisha yao kwa jinsi. Kuonyesha kuwa wanaonewa wakati wote ili waendelee kuonewa huruma tu, kama kweli hawautaki muungano na kuonyesha kasoro zote hizi zilizo kwenye muungano kwa nini wanachaguliwa kushika nafasi za uongozi katika muungano huu nao haraka haraka wanakimbilia.

Hawataki muungano au hawautambui ni kukataa nafasi yoyote ya muungano, au wakati huu wanaodai nchi yao ni kufuata mawazo ya mwanakijiji ya kuwaondoa watu wao kwenye nyadhifa zote za muungano wala hawatagombana na mtu na kila mtu atawaelewa.

Hii kila siku kutuonyesha kasoro imetosha, tumeziona ingawa hatuwezi kuwasaidia lolote kwani yote yako ndani ya uwezo wao. Ondoa watu wako wote kwenye uongozi, ita raia wako nyumbani uone kama tutakufuata huko pamoja na uzuri wa nchi yenu tukufu.
 
I support this movement na tena wafanye haraka.Ikiwezekana wabunge wao kutoka zanzibar wasije kabisa kwenye kikao kijacho. Tumewachoka na lazima walielewe hilo
 
MMKJJ, Mzee Mwanakijiji
Kwa mujibu wa katiba ya JMT, hoja yoyote ya kuuvunja muungano ni uhaini!.

Angalieni jf tusije nyooshewa vidole tuu wachochezi!.

Tukiamua kufuata sheria, taratibu na kanuni, muungano ni kwa bara tuu, kwa Zanzibar hauna legitimacy, hivyo kuuvunja from that side ni haki yao.

Naunga mkono hoja!.

Paskali
 
Muungano ulikuwa na matatizo toka siku ya kwanza ya kuundwa kwake.
Utavunjika tu siku ccm itatoka madarakani, kama ccm itaendelea kuwepo tusitegeemee mabadiliko yoyote yale.
 
Na waende wakapewe misaada na ndugu zao wa Oman!lkn for sure watatukumbuka na ukalimu wetu!!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom