Lembeli: Mafisadi hawana huruma hata kidogo

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,872
21,951
"NINAKUMBUKA na kamwe siwezi kuusahau mwezi Agosti, mwaka 2007, hii ni baada ya mimi kutokewa na tukio la kuzomewa na kikundi cha wananchi katika mkutano wa hadhara ambapo Rais Jakaya Kikwete alihutubia katika mkutano huo. Tukio hili halikuwa la kawaida na wala sikutegemea kunitokea maishani mwangu."


Hayo ndiyo yalikuwa maneno ya kwanza kusemwa na James Lembeli ambaye ni mbunge wa jimbo la Kahama wakati akifanya mahojiano maalumu na gazeti hili katika ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam hivi karibuni.


Hatua ya Lembeli kuzungumza maneno hayo ni kutokana na swali aliloulizwa la kuwa ni jambo gani hatolisahau katika miaka yake mitano ya kuwa mbunge hali kadhalika mwanasiasa.


Lembeli ambaye amezaliwa katika kijiji cha Bulugwa wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga anasema mbali na kupata mshituko na wasiwasi mkubwa mara baada ya kutokea kwa tukio hilo, Lakini lilimfunza mambo kadhaa kuhusu siasa.


“Na baada ya kutokea kwa tukio hilo, nilijifunza mambo kadhaa katika siasa na nikagundua masuala mengi yaliyokuwa yamejificha katika jimbo langu," anasema Lembeli na kuongeza;"Miongoni mwa mambo hayo ni kuwapo kwa vitendo vya ufisadi vinavyofanywa kwa siri na wanasiasa wenzangu.”


Anasema baada ya hapo ndipo alipoweka nia na kutangaza kupambana na vitendo vya ufisadi pamoja na watu wanaojihusisha na vitendo hivyo.


Mbunge huyo mwenye taalumu ya uandishi wa habari aliyoipata miaka 30 iliyopita katika chuo cha uandishi Kitwe nchini Zambia anasema ni bora afe kuliko kuwapigia goti mafisadi.


Akifafanua kauli hiyo anasema; "Kamwe siwezi kuwapigia magoti mafisadi kwa kuwa fedha wanazotumia zinatokana na jasho la Watanzania ambao kwa kiasi kikubwa ni walalahoi wanaoshindia mlo mmoja."


Mbunge huyo ambaye ni mmoja wa wabunge wanaojipambanua kupambana na vitendo vya ufisadi anasema anakusudia kuachana na masuala ya siasa mwaka 2015.


"Mwaka huu, 2010 nitagombea kama kawaida ili niendeleze kazi niliyotumwa na wananchi wa Kahama, lakini 2015 nitaachana na masuala ya siasa," anasema Lembeli


Lembeli alifanikiwa kuingia bungeni kwa mara ya kwanza mwaka 2005 mara baada ya kushinda katika uchaguzi mkuu mwaka huo.


"Kutokana na jinsi nilivyojijenga kisiasa jimboni mwangu na kuwa na maelewano mazuri na wananchi hakuna wa kuning’oa katika uchaguzi wa mwaka huu. Natumai nitarudi bungeni nikiwa na nguvu na ari mpya," anasema.


Lembeli (53) anasema hakujiingiza katika ulingo wa siasa kwa ajili ya maslahi bali aliingia kwa ajili ya kutaka kuwatumikia wananchi wa Kahama na Tanzania kwa ujumla.


Anasema kabla ya kujiingiza katika siasa alikuwa ni mtumishi wa serikali pamoja na mashirika binafsi lakini aliachana na yote hayo kwa ajili ya wito wa kuwatumikia wananchi.


Anasema hali hiyo inatokana na kuwa alilelewa katika mfumo wa kiutawala kutokana na baba yake mzazi kuwa chifu. Chifu, Daudi Lembeli wa Kahama ndiye baba yake na hivyo amekulia katika misingi ya uongozi.


Lembeli aliyewahi kuwa mtangazaji wa idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani (DW), pia anasema kutokana na utashi wa kutaka kuwatumikia wananchi, alilazimika kuachana na ajira yake katika Shirika la Hifadhi ya Taifa Tanzania (TANAPA), alipokuwa akilipwa mshahara mkubwa.


"Nililazimika niachane na ajira yangu ya meneja uhusiano wa Tanapa ambapo kwa wakati huo nilikuwa ninalipwa mshahara takribani Sh2 milioni," anasema. Alifanya kazi Tanapa kuanzia 1993 hadi mwanzoni mwa 2005.


Anasema mwaka 2005 alipoingia Bungeni alikuta mshahara wa Wabunge ni Sh800,000 yaani mara mbili ya kile alichokuwa akilipwa Tanapa.


Lembeli, baba wa watoto watatu anasema mara kabla ya kusomea taaluma ya uandishi alikuwa akifanya kazi kama karani wa benki katika Benki Kuu (BoT). Na hapo alifanya kazi kwa muda wa mwaka mmoja ( 1978).


Baada ya hapo alijiunga na chuo cha uandishi wa habari Kitwe na kuhitimu mwaka 1980 ambapo alitunukiwa stashahada ya uandishi.


Mwaka 1981/82 alikuwa ni muaajiriwa katika Baraza la Maaskofu Tanzania(TEC). Na mwaka 1983/84 alifanikiwa kwenda barani Australia katika nchi ya Papua New Guinea na kufanya kazi katika gazeti Katoliki.


Kutoka mwaka huo hadi 1987 alikuwa ni Afisa mwandamizi wa habari wa Jumuiya ya Muungano wa vyama vya Ushirika (C.U.T.).

Na baada ya hapo (1987-1992) alijiunga na idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Ujerumani akiwa kama mhariri na mtangazaji.


Lembeli aliyezaliwa Desemba 26, 1956, alipata elimu ya msingi katika shule za Buhungwa, Ibelansuha na Wigehe kati zote za Kahama.


Elimu ya sekondari aliipatia Wilayani Njombe mkoa wa Iringa
 
hakuna lolote zaidi ya njaa tu huo ufisadi kauona leo? yeye alipokuwa TANAPA hakufanya ufisadi?
 
Back
Top Bottom