Elections 2010 Kwanini ni vigumu kuiba kura katika Uchaguzi Wetu - Tusitafute visingizio

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,475
39,987
Na. M. M. Mwanakijiji

Mojawapo ya mada ambazo sijazigusa kabisa kwenye mtandao huu na hata kwenye makala zangu nyingine ni suala la wizi wa kura. Watu wengi wana wasiwasi sana kuwa kuna uwezekeno kuwa kura zikaibwa. Wengi wanapozungumzia suala la wizi wa kura wanazungumzia mfumo wa kihalifu ambao unaweza kutumika:

a. Kuongeza kura kwenye masanduku ya kura
b. Kuficha masanduku mengine ya kura na kuyaongeza baadaye
c. Kuhesabu kura kwa kuongeza namba
d. Kutumia teknolojia kubadilisha idadi ya kura. n.k

Ipo imani ambayo imejengeka kuwa ni rahisi kwa kikundi cha watu au watu kuiba kura na kumuongezea mtu mwingine kura kinyume cha sheria. Watu wenye imani hii (naiita imani kwani hakuna ushahidi wowote kuwa kura zimewahi kuibwa, yaani ushahidi unaoweza kusimama Mahakamani!) huwa na wasiwasi kuwa uchaguzi unapofanyika basi kuna makundi ya watu ambayo yanakula njama kuiba kura na kubadilisha matokeo.

Mtu yeyote ambaye anaweza kutumia muda kufikiri ataona kuwa kama kuna wakati ambapo CCM ilihitaji kuiba kura ni katika uchaguzi wa Dr. Slaa ambapo mara tatu amewaangusha Karatu (na madiwani akapata), Uchaguzi wa Mzee Ndesamburo (Moshi Mjini) au hata uchaguzi wa Arfi kule Mpanda Mashariki. Katika sehemu zote hizo CCM ilikuwa na sababu kubwa zaidi ya kuiba kura kuliko majimbo mengi nchini, kama kweli upo wizi wa kura, kwanini sehemu hizi nyingine na muhimu wameshindwa?

Siyo hapo tu, kama kweli Kura zingekuwa zinaibwa kirahisi hivyo, kwanini wameshindwa kuiba kura Pemba ambapo CUF imeendelea kutesa kwa miaka 15 sasa tangu mfumo wa vyama vingi uende na kwanini kura za Jimbo la Darajani (ambalo nadhani sasa limegawanywa - niko tayari kusahihishwa) haziibwi na matokeo yake zinakuwa za karibu sana?

Ukweli ni kuwa wenye hofu hii ya "wizi wa kura" ni kwamba hawajui upigaji kura wetu ulivyo na kwanini hatua zilizochukuliwa mwaka huu na Tume ya Taifa ya Uchaguzi zitachangia sana kuondoa wasiwasi wa wizi wa kura. Bahati nzuri nina uzoefu wa kushiriki kama mwangalizi wa Uchaguzi Mkuu katika mojawapo ya chaguzi zetu nchini na kuweza kutembelea maeneo ya Shinyanga, Mwanza na Musoma wakati wa kampeni na wakati wa Uchaguzi kuweza kutembelea vituo vya uchaguzi zaidi ya hamsini vya Mwanza. Nimeshiriki toka kituo kinafunguliwa hadi kura zinamalizwa kuhesabiwa. Kwa hiyo, siandiki kinadharia bali kwa uhakika wa ushuhuda wangu mwenyewe ambao nina uhakika unaweza kurudiwa na mtu mwingine yoyote aliyepata nafasi kama yangu.

Ninachofanya hapa (kuelezea hili) ningependa kungefanywa na Tume ya Uchaguzi ili kuwaondoa watu wasiwasi.

Kwanza kabisa, ieleweke kuwa kura zinapigwa, kuhesabiwa na matokeo yake kutangazwa kituoni (kwa kura za wabunge). Hii ina maana ya kwamba, mwisho wa kura washindi wa kila kituo watajulikana kituoni hapo kwa utaratibu uliowekwa wazi ambapo fomu mbalimbali zinatakiwa kujazwa mbele ya watu wote.


Masanduku yanaletwa kituoni na yote yanakuwa na mihuri (seals). Mihuri inapovunjwa kwa utaratibu maalum na mbele ya watu wote (wawakilishi wa vyama, waangalizi wa ndani na wa kimataifa kama wapo). Masanduku yakishafunguliwa hayahami tena hadi mwisho wa kura na kuhesabu kura na hayaruhusiwi kabisa kutoka hata kwenye jengo yalipo. Masanduku hufunguliwa hadharani, wawakilishi wa wagombea na waangalizi wanaruhusiwa kuyakagua si kwa macho tu hata kwa kuyashika na kuyapapasa ili waone kuwa hayaharibiwa au kuchezewa, wakisharidhika na hatua zote za ufunguzi wawakilishi wote hujaza fomu ya kuonesha kuwa wameridhishwa. Masanduku huwekwa mahali pa kupigia kura ambapo panampa mtu hifadhi. Lazima yawe mahali ambapo yanaweza kuonekana, hivyo hayawezi kuwekwa kwenye chumba kilichofichwa.

Mpiga kura baada ya kujithibitisha kuwa ni yeye (mwakilishi yeyote anaweza kutaka kuangalia uthibitisho huo) anaenda na kupiga kura kwa uhuru wake na kutumbukiza kura yake mbele ya hadhara ya wote waliomo humo ndani, kumbuka kuwa karibu watu nane (au zaidi) wanaruhusiwa kuwemo kwenye chumba cha kupigia kura! Kura zikishapigwa kituo kinaendelea kubakia wazi hadi muda rasmi wa kufunga vituo unapofika, kama mjuavyo wale waliokuwepo kwenye mstari tu ndio wataruhusiwa kupiga kura.

Baada ya muda rasmi kufika, Msimamizi wa Kituo atawatangazia kuwa kituo kimefungwa na mara moja protocol ya kufunga kituo na kuhesabu kura huanza mara moja. La kwanza kabisa (natumia kumbukumbu yangu tu hapa - nitawaacha wengine wasahihishe nikipotoka) ni kuyafunga masanduku yote pale pale yalipo na kuyatia muhuri tena. Hili lina lengo la kuhakikisha kwamba ni masanduku yale tu yaliyotumika kupigia kura ndio yanafunguliwa tena baadaye ili kuhesabu kura. Kama kuna sanduku lisilotumika linaeleweka na upo utaratibu wa kuhakikisha halihusiki.

Watu wote kwenye kituo wakiridhika (kumbuka yote haya yanafanyika hadharani! hakuna siri au kwenda chumba kingine) basi masanduku huanza kufunguliwa hadharani na kura huanza kuhesabiwa. Kila kura inahesabiwa kwa sauti (hakuna kuhesabu kimoyo moyo) na mtu yeyote akiona kuna utata fulani basi wawakilishi na maajenti wa vyama wanaruhusiwa kuiangalia hiyo kura. Kwanza kura hutengwa kwa kufuatana na wagombea na zikishatengwa huanza kuhesabiwa na idadi inatangazwa hadharani kwa kila mtu kusikia. Kama kuna mtu ana tatizo basi upo utaratibu wa kurudia kura hizo kuzihesabu hadi waridhike.

Kura zote (za Ubunge, Urais na Udiwani) zikishahesabiwa na watu wote kituoni wakaridhika na utaratibu basi huitwa kujaza fomu mbalimbali zikiwa na idadi na msimamizi wa kituo naye anajaza fomu zake mbele ya wote na wote wakiridhika kuwa taratibu zote zimefuatwa basi kuna nakala zinawekwa kwenye kila sanduku na masanduku ya kura hufungwa tena na kupigwa mhuri tena na hayatafunguliwa isipokuwa kwa agizo la mahakama! Matokeo yote yaliyopatikana yanaandikwa hapo hapo na kubandikwa kituoni na mtu yeyote atajua nani kwenye kituo fulani kashinda.

Hii ina maana mtu yeyote akitembelea vituo kadhaa kwenye eneo fulani wakati wa matokeo kutoka ataweza kupata picha ya mwelekeo wa ushindi. Sasa, hapa kura zitaibwa katika mazingira gani? Zamani tulikuwa na tatizo la kura za Rais kuhesabiwa kituoni lakini matokeo kutotangazwa hata majimboni isipokuwa hadi Tume ya Taifa ya Uchaguzi itangaze. Baada ya matukio ya Kenya ambayo nao walikuwa na mfumo kama wa kwetu Tume yetu ya Uchaguzi imebadili utaratibu na sasa matokeo ya kura za Rais yatatangazwa majimboni. Hii maanake ni kuwa wakati Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo (ambaye ni Afisa Mkuu wa Uchaguzi wa Jimbo) atakapotangaza kura za wabunge walioshinda mwaka huu atatangaza vile vile kura za Urais.

Hii ina maana ya kwamba, mtu akifuatilia kukusanya kura za urais kwenye majimbo mbalimbali ataweza vile vile kupata picha za nani anapata kura za Urais kwa wingi. Kinadharia basi inatakiwa iwe hivi kuwa majumlisho ya chombo chochote huru cha kura za Rais kutoka majimbo yote nchini ni lazima zilingane na hesabu za majumlisho rasmi ya kura za Rais yatakayofanywa na Tume ya Uchaguzi. Endapo kura za Urais kutoka majimbo yote zitaonesha kuwa mtu mmoja kapata kura milioni 1 halafu Tume ikasema amepata kura milioni 1.5 basi tatizo HALIWEZI KAMWE kuwa kwenye Jimbo isipokuwa kwenye Tume.

Hivyo, hata wakitumia kujumlisha kwa kompyuta, calculator au kwa kuhesabu visoda kura za Rais zitakazotangazwa katika majimbo ni LAZIMA ziwe sawa sawa kabisa na kura zitakazohesabiwa na Tume ya Uchaguzi kwani Tume ya Uchaguzi haihesabu kura za Rais yenyewe inatangaza tu baada ya KUPOKEA namba kutoka majimboni. Kama mwalimu wangu wa Hisabati alivyoniambia kuwa 2 + 2 ni 4, iwe Bigwa, Chunya au Tokyo!

Lakini, kura zaweza kuchezewa lakini ili zichezewe kunahitaji ushirika wa zaidi ya mtu mmoja. Yaani, msimamizi wa kituo, wawakilishi wa wagombea, waangalizi wa ndani na wa nje na vile vile wapiga kura wenyewe. Kwa Chadema kwa mfano itajikuta kwenye matatizo endapo tunajua kuwa kutakuwa na vituo vya kupigia kura zaidi ya 50,000 kinadharia kila kituo kinahitaji angalau mwakilishi mmoja ambaye atakaa kituoni kuanzia mwanzo hadi mwisho (ina maana lazima umlipe posho ya kula au umuandalie kula). Sasa Chadema ina wawakilishi labda wapata 30,000. Hii ina maana itakuwa haina macho kwenye vituo 20,000. Lakini hili lisitushtue kwa sababu haina maana kwenye vituo hivyo hakuna wawakilishi wengine na sheria inaruhusu kabisa mwakilishi wa chama kimoja kuwa mandate ya wagombea zaidi ya mmoja.

Lakini kama kila kituo kitakuwa na wapiga kura wasiozidi 500 ina maana ya kuwa ili mtu ahongwe inahitaji ushiriki wa watu wengi kweli kuweza kufanikisha wizi hasa ukizingatia kuwa masanduku hayaondolewi kituoni, mambo yote yanafanyika hadharani n.k. Hii ndio sababu sikutaka kuchangia suala la "lori lililobeba kura zilizopigwa za JK". Habari hii japo inavutia hisia lakini kwa mtu asiyejua atajiuliza hivi hizo kura zitaingizwa vipi kwenye upigaji kura? Baada ya kutoa maelezo hayo hapo juu labda mtu aniambie ziingizwe kwa njia ya mnunurisho.


Ninachotaka kusema ni kuwa kati ya visingizio ambavyo binafsi siko tayari hata kuvisikia ni hiki cha "wameiba kura". Chadema imepewa nafasi ya kihistoria kushinda uchaguzi, ilijua kwa miaka mitano kuwa mwaka huu kutakuwa na uchaguzi na inajua taratibu zote za uchaguzi - hivyo walitakiwa wawe wamejiandaa vya kutosha. Kama hawakujiandaa vya kutosha kupata wawakilishi wa kutosha kwenye kila kituo hili si tatizo la NEC wala CCM! Chadema inahitaji kushinda kisiasa kwa kuwafanya watu wengi wakipigie kura kwani ni kura zilizopigwa tu NDIZO zinazohesabiwa siyo zinazoombewa, kunuiwa au kusubiriwa mawazoni.

Ili iweze kupata watu wengi wakipigie kura ni lazima itumie mbinu za kisiasa (mbinu ambazo walidokezwa toka awali na chache wamezitumia!). Chadema bado wana nafasi kubwa sana ya kuweza kuwafanya hata wana CCM waichague na ninaamini watafanya yale yanayotakiwa kufanya kati ya yale mambo "matatu manne". Ila hili la kudai kuibiwa kura binafsi nalibeza na kulipuuzia kwani kwa miaka 15 sasa ya mfumo wa vyama vingi hakuna afisa au mtu hata mmoja ambaye ameweza kushtakiwa na kuthibitishwa kuwa ameshiriki katika kuiba kura.

Hata hivyo, baada ya kusema hayo ninaelewa kitu ambacho siwezi kuita "wizi wa kura" bali "kuvuruga upigaji kura" jambo ambalo linaweza likaathiri upigaji kura kwenye baadhi ya maeneo. Kwa mfano, endapo sehemu nyingine watu wanapiga kura na halafu mtu akaanza kueneza ujumbe kuwa x keshashinda katika eneo hilo basi baadhi ya watu wanaweza wasiende kupiga kura au wakapiga kura kwa kufuata mshindi au wakaamua kupiga kura tu ya kumpa yeyote. Mbinu nyingine ni vitisho na kuwafanya watu aidha wasiende kupiga kura wakihofia kuwa wakipiga kura watajulikana. Mbinu hizi ni za kisiasa na hutumiwa sehemu nyingi duniani. CCM ina uwezo mkubwa wa kutumia mbinu kama hizi lakini ni jukumu la CHadema na vyama vingine vya upinzani kujifunza jinsi ya kupangua mbinu hizi.

Mkikaa ati kusubiri "kulinda kura zenu" msishangae mnalinda ambacho hakitishiwi kuibwa ila wote mmekaa na kusahau kwenda kupiga kura kwa sababu mnalinda kura za wenzenu waliopiga ambao yaweza kuwa siyo wale wa chama mnachokitakia ushindi. Hivyo, badala ya kuhofia wizi wa kura, Watanzania wajitokeze wapige kura zao kwa kujiamini na pasipo kukubali ghilba na vitisho vya aina yoyote ile. Kura ndio sauti ya mwananchi kwa viongozi wake na ndiyo lugha pekee wanayoilewa. Sauti hiyo haiwezi kuibwa wala kutekwa nyara. Kama umejiandikisha kupiga kura, PIGA!


Hakuna wa kuiba kura yako isipokuwa wewe mwenyewe ukikataa kupiga kura unayotaka utakuwa umeiiba haki yako mwenyewe. Ni kwa kutokupiga kura wakati mtu kajiandikisha na ana uwezo, muda na nafasi hapo ndipo WIZI WA KURA UNATOKEA!
 
Kaka story yako ndefu sijaimaliza lakini believe or not kura huwa zinachakachuliwa kwa wale mawakala either kubadiri kura au kutohesabu kama ipasavyo. Sasa ukizungumzia katika majimbo ambayo wapinzani wameweka mizizi saana ukiiba utaleta machafuko. So hapo naona umechakachuliwa mwanakijiji.
 
Mwanakijiji,
Hawa jamaa kuiba kura wanaweza hasa za Urais ambazo zimetapakaa Nchi nzima. Maalim Seif hajawahi kushindwa Zanzibar lakini hajawahi kuwa Rais wa Zanzibar. Mbaya zaidi ni vyombo vya DOLA vinavyotumika kuifanya kazi hiyo sio watu wa kawaida.
 
wizi wa kura upo dunia nzima na mbinu zipo nyingi za kuiba kura, Technologia imekuwa sana, Prof Mvungi na Cheyo Momose ni mashahidi wa hilo, Mkuu WIZI WA KURA UPO NA UTAFANYIKA MWAKA HUU
 
Kaka story yako ndefu sijaimaliza lakini believe or not kura huwa zinachakachuliwa kwa wale mawakala either kubadiri kura au kutohesabu kama ipasavyo. Sasa ukizungumzia katika majimbo ambayo wapinzani wameweka mizizi saana ukiiba utaleta machafuko. So hapo naona umechakachuliwa mwanakijiji.


I know the perception.. wanaibaje kura? Mawakala hawahesabu kura!
 
wizi wa kura upo dunia nzima na mbinu zipo nyingi za kuiba kura, Technologia imekuwa sana, Prof Mvungi na Cheyo Momose ni mashahidi wa hilo, Mkuu WIZI WA KURA UPO NA UTAFANYIKA MWAKA HUU


jamani.. zinaibwaje? zamani ilikuwa rahisi kwa sababu sanduku linapakizwa kwenye baskeli kwenda kuhesabiwa sehemu nyingine.. siyo mnasema "wizi upo" kinadharia inawezekana lakini mtu aniambie unawezekana vipi? Wildcard anasema kuwa Zanzibar waliiba ah wapi!, kuna suala la Tume ya Uchaguzi kuingiliwa hilo limetokea Kenya na ninaamini ndilo lenye uwezekano mkubwa wa kutokea Tanzania mwaka huu..
 
Mzee Mwanakijiji, nadhani wizi unaouzungumzia hapa ni wa kupitisha au kuongeza kura ili kuongeza namba ya kura alizopata Mgombea Mmoja, naungana na wewe wizi wa namna hiyo ni mgumu sana maana wananchi wanaona kinachoingia na kinachotoka. Lakini Mkuu mwanakijiji mimi nasema kabisa kama hakuna uangalizi mzuri namaanisha kama waangalizi wakiwa ni njaa ni rahisi sana kile kilichobandikwa Ukutani kisiwe kile kilichohesabiwa
 
jamani.. zinaibwaje? zamani ilikuwa rahisi kwa sababu sanduku linapakizwa kwenye baskeli kwenda kuhesabiwa sehemu nyingine.. siyo mnasema "wizi upo" kinadharia inawezekana lakini mtu aniambie unawezekana vipi? Wildcard anasema kuwa Zanzibar waliiba ah wapi!, kuna suala la Tume ya Uchaguzi kuingiliwa hilo limetokea Kenya na ninaamini ndilo lenye uwezekano mkubwa wa kutokea Tanzania mwaka huu..
Kwa Zanzibar hasa ule wa mwaka 2000 ni masanduku yaliyojazwa kura za Karume ndio yaliyobadilishwa na yale ya kura halisi kijeshi kabisa. Staili hii ilitumika pia DRC kumsaidia Kabila kushinda uchaguzi ule dhidi ya Bemba.
 
Kwa Zanzibar hasa ule wa mwaka 2000 ni masanduku yaliyojazwa kura za Karume ndio yaliyobadilishwa na yale ya kura halisi kijeshi kabisa. Staili hii ilitumika pia DRC kumsaidia Kabila kushinda uchaguzi ule dhidi ya Bemba.

hii ni imani ilijengeka.. watu wengi najua wanaingia kwenye kituo cha kupiga kura na wanatoka lakini hawajui nini kimetokea kabla yao au baada yao. KUtokana na imani hii nadhani kwa kweli Tume ya Uchaguzi lazima itoe tamko la maelezo ya jinsi kura zinavyopigwa na nini kinapaswa kufanywa au kufanyika maana naona watu wengi kweli wanaaminii wizi hutokea kwenye kituo cha kupigia kura. Hili wazo ni la hatari.
 
Then tatizo lipo kwa mawakala kama ndo hivi,sina experience yoyoyte zaidi ya kusikia "kura zinaibwa".
Kama ulivo onesha,kama vyama vitakuwa na mawakala waaminifu basi wizi hautakuwepo
 
Mwanakijiji;

Sidhani kama ni uwizi wa kura bali ni kwa sababu ya katiba yetu inayosema kuwa NEC ikitangaza matokeo ya U-Rais HAYAWEZI PINGWA POPOTE PALE;kipengele hiki ndani ya katiba ni cha kishetani!

Wasiwasi wangu ni huu,majumuisho ya mawakala wa CHADEMA unaweza ukaonyesha labda uchaguzi ni too close to call na hata labda Dr Slaa akashinda kwa kura chache lkn majumuisho ya mawakala wa Dr Slaa yakitangazwa vingine na NEC na huku wakilindwa na sheria ya kshetani kama"wakitangaza matokeo hayapingwi"tutafanyaje?

CCM wanaweza wakafaidika na sheria hii ya kishetani maana NEC sio huru!
 
Mimi naamini kabisa mara zote Maalim Seif anashinda Zanzibar,
Mimi naamini kabisa 2005 MNYIKA alishinda Ubungo

MIMI NAAMINI KABISA KUNA WIZI WA KURA
 
jamani.. zinaibwaje? zamani ilikuwa rahisi kwa sababu sanduku linapakizwa kwenye baskeli kwenda kuhesabiwa sehemu nyingine.. siyo mnasema "wizi upo" kinadharia inawezekana lakini mtu aniambie unawezekana vipi? Wildcard anasema kuwa Zanzibar waliiba ah wapi!, kuna suala la Tume ya Uchaguzi kuingiliwa hilo limetokea Kenya na ninaamini ndilo lenye uwezekano mkubwa wa kutokea Tanzania mwaka huu..

Unless imethitibishwa kuwa karatasi zilizokamatwa Tunduma sio kweli naweza kuamini kidogo. Lakini kama ni kweli Mkuu Mwanakijiji ni za nini kama haziwezi kuingizwa vituoni?
 
Mwnaakijiji wizi wa kura upo wa namna nyingi.
Moja: zinaandaliwa karatasi nyingine za kupigia kura ambazo tayari zina tick kwa mgombea ambaye anatakiwa kushinda then wakati wa kuhesabu zinafanyiwa exchange na zile karatasi ambazo zina tick kwa mgombea mwingine 'wasiye mtaka'.
Namna nyingine ni kutumia ubabe kama uliotumika 1995 kule Zanzibar.
kashinda Seif lakini anatangazwa Salmin Amour na hakuna wa kuingilia kati.
 
hii ni imani ilijengeka.. watu wengi najua wanaingia kwenye kituo cha kupiga kura na wanatoka lakini hawajui nini kimetokea kabla yao au baada yao. KUtokana na imani hii nadhani kwa kweli Tume ya Uchaguzi lazima itoe tamko la maelezo ya jinsi kura zinavyopigwa na nini kinapaswa kufanywa au kufanyika maana naona watu wengi kweli wanaaminii wizi hutokea kwenye kituo cha kupigia kura. Hili wazo ni la hatari.

Hauamini Mwanakijiji? Nikuache tu. Ujumbe umefika.
 
Mzee mwenzangu unazeeka vibaya,unapoteza hii dhana ya UZEE DAWA,VILEVILE KUWA KIBARAKA WA CCM,KUMEKUCHAKACHUA KABISA.POLE.
 
Mwanakijiji;

Mwaka 1995 kulingana na takwimu za mawakala wa CUF kule ZNZ ilionyesha kuwa Maalim Seif kashinda kwa asilimia kubwa dhidi ya incumbent Dr Salmin Amour lkn matangazo ya ZEC yalimpa ushindi Dr Salmi kwa aslimia 50.1 dhidi ya 49.9 za CUF!

CUF walienda hata kwenye jumuia za kimataifa kuomba warudie tena kujumlisha matokeo ya kura ya vituo vya uchaguzi lkn ZEC ikasisitiza tena na tena kuwa matokeo waliyotangaza ni halali na hawatarudia tena kujumlisha matokeo;machafuko yaliyotokea hapo baadae hamna asiyeyajua!

Wasi wasi wangu ni kuwa hata kama Dr Slaa atashinda,na hata kama mawakala wa CHADEMA watafanya kazi nzuri sana ya kuwa makini kwenye vituo vya kura,lkn je kama NEC ikatangaza matokeo jinsi wanavyotaka wao na kwa hiki kipengele kinachosema NEC haipingwi popote pale tutafanya nini?
 
Back
Top Bottom