Kwa nini papa benedict xvi, alaumiwe?

ByaseL

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
2,225
247
Kuna mazoea kwamba waandishi wa Ulaya na Amerika ni watafiti zaidi katika habari zao. Lakini yanapokuja masuala ya Kanisa Katoliki ni rahisi nao kukumbwa na ugonjwa uleule unaoitwa “uvivu wa kutafiti”. Tumesikia jinsi kashfa za mapadri huko Ulaya na Amerika zinavyoendelea kutawala habari duniani. Vatican na majimbo husika wamekiri kutokea kutokea vitendo vile. Japo zimevuma sana duniani tuzijadili humu kwa kifupi kwa madhumuni ya makala hii. Zimetokea nchini Ireland, Ujerumani na Marekani. Nchini Ireland, chanzo ni Oktoba 2002, ambapo TV ya Ireland ilirusha kipindi kilichoonyesha unyanyasaji uliofanywa na baadhi ya mapadri wa Kanisa Katoliki nchini humo tangu mwaka 1975. Ireland iliunda tume iliyoongozwa na Jaji Yvonne Murphy kuchunguza madai yale. Tume ilitangaza ripoti yake 26 Novemba 2009 na ikaonekana ambavyo athari kwa waathirika hazikuzingatiwa kwa unyanyasaji uliotokea. Ndani ya siku 29 baada ya ripoti maaskofu wanne nchini humo walijiuzulu nao ni Eamonn Walsh, Raymond Field, Jim Moriarty na Donal Murray. Baadaye Machi 19, Papa aliandika waraka kwa wakatoliki wa Ireland kuhusu kashfa zile. Kama vile ni sinema, wakati Papa anaandaa waraka kwenda Ireland kumbe kashfa nyingine nayo inajiandaa kusambaa duniani. Hii inaelezwa kutokea Ujerumani mwaka 1980 wakati yeye mwenyewe (Papa) akiwa askofu wa jimbo la Munich akijulikana kama Kadinali Joseph Ratzinger. Papa humu ametajwa kwamba unyanyasaji wa Padri Peter Hullermann alijulishwa lakini hatima yake ni kuhamishwa kwa padri huyu kwenda parokia nyingine (Rejea gazeti la New York Times: www.nytimes.com/2010/03/19/world/europe/19church.html). Dunia ikatulia kwenye “kipindi cha mapumziko” kama timu za mpira. Mapumziko ya siku sita yalipoisha ikasambaa kashfa nyingine. Hii sasa ni nchini Marekani, ya unyanyasaji uliofanywa na Hayati Padri Lawrence Murphy wa Milwaukee kwenye miaka ya 1960. Hapa tena amehusishwa moja kwa moja Papa Benedict XVI akiwa bado Kadinali Ratzinger lakini tayari ameshahamia Vatican akiongoza idara inayosimamia Imani ya Kanisa Katoliki yaani CDF. Kwamba idara hii ilishindwa kumvua utumishi (laicization) Padri Murphy (Rejea gazeti la New York Times: www.nytimes.com/2010/03/25/world/europe/25vatican.html) Je, ni nini kimefanyika kanisani katika yote haya.Tumeona nchini Ireland tumeona maaskofu wanne wakiachia ngazi ya uchungaji. Kauli ya Kanisa kwa yaliyotokea Ireland ni vizuri kurejea baadhi ya sehemu za waraka ule wa Papa unaopatikana kwenye tovuti ya Vatican (www.vatican.va). Ndani ya waraka kwenye vifungu 14, Papa amekiri kusikitika kwa Kanisa kupatwa na aibu hii (..You have suffered grievously and I am truly sorry.. Kifungu 6, aya ya 1:). Pia ameeleza jinsi alivyowaita maaskofu wa Ireland pale Vatican wamueleze walivyoshughulikia masuala yale (...I recently invited the Irish bishops to a meeting here in Rome to give an account of their handling of these matters..... Kifungu 1, aya ya 2). Hapa tunaona kuwa kumbe suala hili ndiyo kwanza sasa linafika Vatican tena baada ya Papa kuwaita maaskofu badala ya wao kuwa wamelifikisha kwa utaratibu wa Mahakama za Kanisa. Ni nini walichoshindwa kufanya nchini Ireland? Tumnukuu tena Papa: ( ... Certainly, among the contributing factors we can include...resulting in failure to apply existing canonical penalties..... Kifungu 4, aya ya 2:). Kwamba Kanisa nchini Ireland lilishindwa kutumia kanuni za adhabu kama zilivyoainishwa kwenye Sheria za Kanisa. Sehemu ya 11 ya barua ile Papa amekumbusha wajibu wa maaskofu kutoa ushirikiano kwa vyombo vya dola vinapohitaji ushirikiano wao. Sitajadili sana lile suala la Ujerumani ambako Papa Benedict XVI alikuwa askofu kwani limejikita zaidi kwenye suala la mawasiliano ndani ya ofisi za jimbo yaani askofu na wasaidizi wake. Kuhusu ile kashfa ya Padri Murphy (Marekani), Padri Federico Lombardi ambaye ndiye msemaji wa Vatican amenukuliwa kwenye tovuti ifuatayo ya Catholic News Agency: (www.catholicnewsagency.com/news/fr._lombardi_explains_vatican_response_to_sexual_abuses_by_wisconsin_priest). Katika maelezo Maelezo yanatoa picha kwamba lengo la kesi iliyoanzishwa ilikuwa kwamba Padri Murphy apate adhabu kubwa anayoistahili hasa kuondolewa utumishini (laicization). Hata hivyo adhabu kama hii hii ni lazima itoke kama hukumu kwenye Mahakama ya Kanisa kwa mujibu wa Sheria za Kanisa. Hivyo Padri Murphy akawa mtuhumiwa akisubiri hukumu ya Mahakama hiyo. Utuhumiwa huo haumuondolei haki ya kusikilizwa utetezi wake wala haki ya kukata rufaa asipoyapenda maamuzi. Kesi kama hii si tu kwamba lazima ifike Vatican kwenye moja ya mahakama tatu zilizoko pale yaani 1: Roma Rota 2: 2: Apostolic Penitentiary na 3: Apostolic Signatura. Kesi hii lazima ifike kwa Papa ambaye ana jukumu la kumuondoa kasisi (padri/askofu) utumishini. Pamoja na kwamba unyanyasaji wa Pd. Murphy ulitokea miaka ya 1960/70 lakini kwa mara ya kwanza suala limefika rasmi Vatican mwaka 1996. Hapa gazeti la New York Times hawahoji kwa nini suala likae jimboni miaka yote ile. New York Times walibahatika kupata kopi ya taarifa za mawasiliano kati ya jimbo na Vatican. Iliyowashtua ni moja yenye maneno yafuatayo {.. But Cardinal Bertone halted the process after Father Murphy personally wrote to Cardinal Ratzinger protesting that he should not be put on trial because he had already repented and was in poor health and that the case was beyond the church’s own statute of limitations.} Tafsiri ni kwamba Kadnali Bertone aliamuru kesi ya Pd. Murphy isiendelee kwa sababu Padri Murphy mwenyewe aliandika barua kwa Kadinali Ratzinger akipinga kesi ile isiendelee kwani alishatubu, afya yake si nzuri na kwamba suala lile limeshachukua muda mrefu. Je hoja za mtuhumiwa huyu Padri murphy ni halali, kwamba ametubu na kesi isiendelee hata kama ingekuwa ndani ya muda wake? Kwa sura ya kijamii, Pd. Murphy anatuhumiwa kufanya kitendo cha unyanyasaji. Mahala kilipofanyika kitendo kile au dini ya mtuhumiwa na muathirika si msingi mkubwa kwa tuhuma zile. Hata hivyo mmoja wa waathirika Arthur Budzinski (60), ameripotiwa mitandaoni akieleza kunyanyaswa mwaka 1960 alipoenda kwa Padri huyu kufanya kwa maungamo {Rejea tovuti ile ya gazeti}. Kwa nchi kama Marekani kwa Pd. Murphy na hata Tanzania dini au imani ni suala la mtu binafsi. Nchi kama hiyo maungamo hayana nafasi yoyote kama msingi wa kesi. Lakini kwa mkatoliki Maungamo ni suala la imani kwani ni Sakramenti ya Kitubio (Sacrament of Penance). Hapa kosa la Pd. Murphy ni kosa la kiimani. Kuikiuka (Violation) Sakramenti ya Kitubio. Hivyo Sheria za Kanisa zinaweza kushindwa kutaja moja kwa moja ni adhabu gani itolewe kwa kukiuka Sakramenti hii kama alivyofanya Pd. Murphy. Padri Murphy anakiri alitumia vibaya Sakramenti ya Kitubio mwaka 1960. Mwaka 1998 analeta hoja kwamba ameshatubu kosa lile. Lugha kama hii haieleweki na sidhani kama inakubalika nje ya ukatoliki. Wala Pd Murphy hafikirii kupeleka hoja hii huko. Hata pale Vatican hakupeleka hoja hii pale Roman Rota ilikofikia kesi yake. Kapeleka hoja hii kwa anayesimami Imani ya Kanisa Katoliki duniani, Kadinali Joseph Ratzinger na Idara yake CDF. Hata ukiangalia hoja zingine za Pd. Murphy si rahisi kuzipuuza. Kwamba afya yake si nzuri na suala limechukua muda mrefu. Kwa misingi hii miwili suala lina sababu za kufungwa na kutoendelea kusikilizwa kama kesi ya inayosimamiwa na Roman Rota. Suala likahamishwa kwenda idara ya kusimamia Imani (CDF) ya Kadinali Ratinger kama suala la imani. Hapa ndipo wenzetu wa gazeti la New York Times waliposhindwa kubaini hali hii. Kwamba Kadinali Joseph Ratzinger na idara yake hawakupokea suala hili kama rufni kesi ya unyanyasaji. Wapolichukua na mawasiliano yote yaliyofuata lilikuwa ni suala la Imani, ukiukaji wa sakramenti ya kitubio (Violation of the Sacrament of Penance). Hata kama wanasheria wa Marekani wakiruhusiwa kufanya uchunguzi pale Vatican, sanasana wataishia Mahakama ya Roman Rota kwani pale ndipo rufani za kesi toka majimboni hufikia na hii ya Padri Murphy ilifia pale kwa hoja zile (Rejea: Sheria za Kanisa: Can. 1443). Idara ya CDF ya Kadinali Ratinger haitaguswa kwanza si mhakama kwani yenyewe ilikuwa inahangaika na hoja za Padri Murphy kuhusu Sakramenti ya Kitubio. Hata hivyo Padri Murphy alifariki miezi chache baada ya kuleta changamoto yake hiyo ikigonga vichwa vya wataalamu wa katekism/teolojia pale Vatican akiwemo Kadinali Joseph Ratzinger. Uamuzi wa Papa tu ndiyo hauna rufani ndani ya Kanisa Katoliki duniani { Rejea: Sheria za Kanisa: Can. 1442 na 333(3)}. Kadinali Ratinger hakuwa Papa wakati ule. Kama Padri Murphy aliweza kujenga hoja na shauri likahamishwa toka Roma Rota kwenda Idara ya Imani (CDF), je angeshindwa nini kukata rufani moja kwa moja kwa Papa John Paul II kupinga uamuzi wa CDF ya Ratzinger kama matokeo yasingemrishisha? Hivyo Kadinali Ratzinger na Idara yake ni lazima walitakiwa kuliangalia suala lile kwa umakini. Bila maelezo haya toka Vatican gazeti la New York Times limemuonyesha Kadinali Ratzinger kama yumo kwenye mtiriko wa Mahakama ya Kanisa unaofanya kazi chini ya Sheria za kanisa. Jambo ambalo waandishi wale (New York Times) hawakulifafanua na kuacha mwanya wa kuhoji uelewa wao kuhusu mahakama za Kanisa Katoliki. Uelewa ambao tunaujadili kuanzia aya ifuatayo. Baada ya kuzichambua kashfa zile tuone sasa uelewa wa watu kwa sheria hizi za Kanisa na mahakama zake. Mwezi Agosti 2008, Mahakama ya Kanisa Jimbo Kuu la D’Salaam iliweka barua kwenye ubao wa matangazo wa pale kanisani St. Joseph. Barua ile ikiwa na kumbukumbu namba JKD/MYM/016/2008 ilikuwa inawakumbusha waumini kupeleka kesi zao kwenye Mahakama hiyo hasa kesi za ndoa. Ninanukuu sehemu ya kipengele 1(iv) cha barua hiyo kinachosema hivi: “uzoefu unaonyesha kuwa watu wengi hawajui uwepo wa chombo hiki muhimu (Mahakama ya Kanisa) na kwamba kinafanya kazi gani na wapi na lini na kinapokea kesi kwa kiwango gani na kama kuna kesi za aina hiyo wazipeleke kwa nani. (Mwisho wa kunukuu). Anayenunua na kusoma vitabu vya Sheria za Kanisa ni rahisi kutambua kwamba adhabu za kanisa ziko kwenye kanuni ya 1311 hadi 1399 na Mahakama ya Kanisa imefafanuliwa kwenye Kanuni 1400 hadi 1752. Miaka 12 nyuma Padri Severine Niwe Mugizi alitafsiri Kitabu Cha Pili Cha Sheria za Kanisa katika lugha ya Kiswahili na kukiita ZIJUE SHERIA ZA KANISA. Kwenye ukurasa wa tano Padri Severine anamalizia aya ya pili ya utangulizi kwa kusema: “Bila shaka wapo wengi watakaoshangaa kusoma sheria hizi, maana ni kitu kipya kwao. (Mwisho wa kunukuu). Padri Niwe Mugizi sasa hivi ni askofu wa jimbo la Rulenge-Ngara. Mifano hii miwili ya Askofu Severine na ule wa Jimbo Kuu la D”salaam ni ishara ya tatizo kubwa la ufinyu katika uelewa wa Sheria za Kanisa (Canon Laws). Ufinyu unaosabisha kutojua rufani za kesi kutoka jimboni zinakwenda wapi. Hutajua rufani kwenda Vatican zinafikaje huko. Kwa mwandishiasiyei mkatoliki hali yaweza kuwa mbaya zaidi na matokeo yake ndiyo hawa ya kumtupia lawama Papa Benedict XVI bila kutafiti undani au unyeti wa suala husika. Je, Sheria za Kanisa ni adimu hivyo hadi kuleta uelewa huu mdogo? Sheria za Kanisa zinapatikana kwenye maduka ya Kanisa Katoliki kama lile Paulines Book Media lililoko pale kanisani St. Joseph jijini D”Salaam. Uelewa wa Sheria, Mahakama, Katekism ya Kanisa waweza kuwa bado ni mdogo. Hata hivyo vyote hivyo ni mambo ambayo yanasomwa na yanatafitiwa na kueleweka kama mambo mengine duniani. Tuhuma hizi si ndogo. Hivyo inatakiwa uangalifu mkubwa. Tukilishinikiza Kanisa lichukue hatua kila yanapotokea haya basi tuwe tayari kujibu maswali kadhaa baadhi tuyajadili hapa. Je Kanisa lichukue hatua mara tu minong’ono inaposemwa kuhusu tabia ya mtumishi wake? Je, lichukue hatua anapofumaniwa waziwazi lakini bado hajafikishwa polisi au mahakamani? Je, lichukue hatua siku anaandika maelezo mahakamani u pilisi? Je, lichukue hatua siku kesi inapotajwa mahakamani? Je, lifanye vile siku anapopatikana na hatia na kuingia jela? Kapatikana na hatia na sasa yumo gerezani. Hukumu ya Mahakam ndiyo ushahidi usiopingika. Je kanisa liutegemee huu na limuadhibu padri yule hukohuko jela aliko maana makosa yale hapa unaweza kufungwa maisha? Kumbe huko jela Padri anaendelea kimyakimya na mipango yake ya kukata rufani? Ghafla tunasikia kwenye vyombo vya habari kwamba yule padri si mfungwa tena kwani ameshinda rufani yake ngazi ya juu. Je, Kanisa lifanyeje kutokana na kutegemea hukumu ya ya mahakama zetu za uraiani. Kama moja ya hatua Kanisa liliomba msamaha je lirudi sasa lifute ule msamaha? Maswali yote yale yanajenga dhana kwamba kama muathirika amepeleka kesi mahakama za uraiani (Civil court) basi uamuzi wake uheshimiwe, mwenendo na maamuzi yatakayotolewa na mahakama yaheshimiwe. Muathirika akiamua asifikirie Mahakama za uraiani badala yake akapenda zaidi Mahakama ya Kanisa, basi na huyu aheshimiwe, na mwenendo na maamuzi ya Mahakama hiyo navyo viheshimiwe. Muathirika aliyeamua kukaa kimya licha ya kuwepo mahakama zote mbili, ya Kanisa au ya Kiraia. Kwamba kwa hiari yake mwenyewe ameamua yaishe, huyu pia ni uamuzi wake. Hoja ni pale baadhi haw kubadili mawazo baada ya miaka hata 30. Si kwamba baada ya kubadili mawazo wanaamua sasa kwenda kwenye moja ya zile mahakama mbili walizoziacha, bali wanaenda kwenda vyombo vya habari kusimulia unyanyasaji uliotokea miaka 30 iliyopita baadhi yao sasa wakiwa na umri wa miaka 60. Ukweli ni kwamba haki yao kufanya vile inakaribisha pia maswali kwamba kwanini wamesubiri miaka yote ile. Source: Tanzania Daima-Jumapili 11 April 2010
 
kwani hukuweza kuandika facts kwa ufupi maana haya maelezo ni marefu kwelikweli. Samahani huo ni mtizamo wangu
 
Sijui ni uvivu wa kusoma mambo mengi?
Hata mimi nimeshindwa kufika mwisho wa story hii. Na hasa kwa vile mambo mengine ni ya Rumi na hayahusiani na imani yangu yanakuwa kama msamiati mpya
 
Mwenzenu najiandaa kwa exams kesho so nimesoma kwa muda mrefu nikaamua kuwasha laptop ili nifungue kichwa kidogo na nilipoona Title ina muhusu bosi wangu nkasema ngoja niicheki dah, ni kama kuendelea ku revise strategic management. Ni ndefu na kwa sasa nimechoka nitachangia may be kesho baada ya kumaliza pepa hilo!
 
Mwenzenu najiandaa kwa exams kesho so nimesoma kwa muda mrefu nikaamua kuwasha laptop ili nifungue kichwa kidogo na nilipoona Title ina muhusu bosi wangu nkasema ngoja niicheki dah, ni kama kuendelea ku revise strategic management.

Ni ndefu na kwa sasa nimechoka nitachangia may be kesho baada ya kumaliza pepa hilo!

Kama ni ndefu wakati kazi ni kuisoma tu basi aliyeiandika ni geniuos.
 
Back
Top Bottom