Elections 2010 Kusema maisha yamekuwa bora baada ya miaka 5 ya CCM madarakani ni kejeli

Pax

JF-Expert Member
May 3, 2009
268
87
KUSEMA MAISHA YAMEKUWA BORA BAADA YA MIAKA 5 YA CCM MADARAKANI NI KEJELI.


Taifa lipo kwenye hekaheka za kampeni za uchaguzi, Taifa linarindima kwa vishindo na kelele za wagombea, vumbi linatimka kila mahali, ni wakati wa kuomba kura. Ni wakati ambao wananchi wananyenyekewa na kubembelezwa kupita kipindi chochote. Mchuano unaonekana baina ya vyama vikuu viwili, CHADEMA na CCM, japo pia CUF kinaonekana kina nguvu lakini kwa mtizamo wa wengi sio kama hivyo viwili. Baadhi ya viongozi waliokuwa madarakani na waliofanikiwa kugombea tena kipindi hiki, wa Uraisi,Ubunge na hata Udiwani wamerudi kwa wananchi kujitetea kuwa waliyoahidi kuyafanya wameyafanya kwa kiwango fulani na sasa wanataka waendelee kuwatumikia wananchi. Kwa upande wa pili wapo wanaowashitaki kwa kusema kuwa fulani hakufanya vizuri,nichagueni mimi na chama changu, tunao uwezo na mkakati mzuri zaidi kuwaletea maendeleo. Kwa Kiasi kikubwa CCM kama chama ndicho kinachojitetea kwa wananchi maana ndicho kilipewa uongozi wan chi ijapokuwa kwenye baadhi ya maeneo kipo kama mshitaki dhidi ya vinavyoitwa vyama pinzani.
Kauli mbiu ya CCM ya mwaka 2005 ya Maisha Bora kwa Kila Mtanzania ndiyo kwa kiasi kikubwa iliyowapa wananchi hamasa ya kuichagua CCM kuendelea kuongoza, wenyewe wanasema walishinda kwa kishindo. Ushindi wa kishindo hata hivyo unatakiwa uendane na mafanikio ya kishindo katika kuleta maendeleo kwa wananchi na si vinginevyo, kinyume cha hapo ushindi wa kishindo hauna maana yoyote. Wagombea wa mwaka huu wa CCM wanatakiwa katika uhalisia wake wawaeleze wananchi kila mtu aridhike kuwa maisha yake yamekuwa bora, maana ndicho kipimo cha kauli mbiu iliyovuma sana ya Maisha Bora kwa kila mtanzania ambayo yangetokana na Kasi mpya, Ari mpya na Nguvu mpya katika utendaji. Kwa kiingereza kauli mbiu ya Maisha Bora kwa kila mtanzania tunaiita vision ama unaweza kuiweka kama goal/aim. Maana ya vision ni kuwa kiongozi mkuu wa nchi na timu yake wanatakiwa kuwafikisha wale wanaowangoza. Ni sawa na ile habari ya kwenye Biblia kuwa waisraeli walitakiwa kwenda nchi mpya ya Kaanani, hivyo kufika Kaanani ndio ilikuwa vision ya Musa na Ndugu yake Haruni kama viongozi wa waisraeli. Swali la kujiuliza Je, CCM walifanya tathmini ya uhakika kuwa hii vision ya Maisha Bora kwa kila mwananchi inaweza kutimizwa ndani ya miaka mitano ya uongozi? Nasema inawezekana walijiamini hivyo kwa kuwa walikuja sasa na namna ya kufika hapo, kwa kiingereza tunaita mission. Mission ni namna utakavyoweza kutimiza vision, na CCM walisema mission yao ni Kasi Mpya, Ari Mpya na Nguvu Mpya katika utendaji. Mwisho wa miaka mitano ndio huu hapa, na hatuangalii kingine, hapana! Hamna cha kuangalia zaidi ya utimilifu wa ile vision ya Maisha Bora Kwa Kila Mtanzania. Je Raisi Kikwete na CCM yake wanaweza kusimama mbele ya watu pasipo shaka na kusema kwa ukamilifu wote kuwa Maisha ya Watanzania yameboreka?
Swali la kujiuliza hapa, Je tunapowaona watu kwenye kampeni za Kikwete, watu wazima na vijana, wengine wakirukaruka na kuimba, wengine wakiwa kwenye sare za CCM kuonyesha mapenzi kwa chama, ina maana maisha yao yameboreka kiasi kwamba wanataka mgombea huyu aendelee kukaa madarakani zaidi? Kama mtu angalifanya utafiti leo hii akamuuliza mtu mmoja baada ya mwingine, je maisha yako yameboreka miaka mitano baada ya Raisi Kikwete kutoa ahadi hii nahisi kwingine ungeweza kukandamizwa mangumi na mateke.Ni kejeli isiyovumilika. Cha kustaajabisha na kusikitisha tuliowaamini kuwa ni wasomi na wataalamu wa tafiti sidhani kama wamewahi kuuliza swali hili katika tafiti zao, REDET, Synovate na wengine mliuliza swali hili kwenye tafiti zenu? Kama hamkuuliza tafiti zenu hazina mantiki, ni upotevu wa rasilimali.
Katika makala hii nitatumia Ripoti ya Umasikini na Maendeleo (Poverty and Human Development Report,2009) kujenga hoja na upembuzi wa vision ya Maisha Bora. Ripoti hii ni hitimisho la kwanza la MKUKUTA (Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini Tanzania). Ripoti hii ya Desemba 2009 inatoa taswira nzuri ya sekta muhimu kwa nchi yetu na hakika ndiyo ambayo vyama vya siasa vinatakiwa kujikita katika kutengeneza ilani zao. Pia ndiyo ambayo CCM na viongozi wake wanatakiwa kuitumia kusema mafanikio ya kukamata dola tokea nchi ilipopata uhuru, na pia serikali ya awamu ya nne kusema walichofanya tokea imekaa madarakani. Ni takwimu hizi ambazo mgombea wa CCM anatakiwa awape wananchi na kuwaelezea pasipo hila wala kificho. Siwezi kuongelea kila kitu humu lakini kwa ufupi nitafafanua uchumi, afya, elimu majisafi n.k angalao kwa ufupi tu.

Uchumi wetu ulikua kutoka 4.1% mwaka 1998 mpaka 7.4% mwaka 2008 na ulitarajiwa kushuka mpaka 5% mwaka 2009 kabla ya kupanda tena mwaka 2012, sababu za kushuka ni mtikisiko wa uchumi wa dunia (Global economic crisis). Asilimia hizi sio rahisi mwananchi wa kawaida kuelewa ni nini hasa, lakini nikiendelea kwa kusema kwa wastani 98% ya watanzania wanatumia chini ya Shillingi 58,000 kwa mwezi ( takribani shilling 2,000 kwa siku) kwa chakula na mahitaji muhimu (Bei za mwaka 2007) na kwa ujumla wastani wa 80% ya watanzania wanatumia chini ya Shilingi 38,600 kwa mwezi (sawa na Shillingi 1,380 kwa siku) inaleta picha kwa mwananchi wa kawaida. Je takwimu hizi mbona wagombea wa CCM hawazisemi? Hii 2% ya watanzania wanaotumia zaidi ya Shillingi 2,000 kwa siku ya chakula ndio hawa wanaotaka watutawale milele, ndio hawa ambao wanaishi kwenye majumba ya kifahari,ndio hawa ambao hawajui joto ni nini maana nyumbani, kwenye magari yao mpaka ofisini ni viyoyozi, ndio hawa ambao hawajui bei ya mchele wala unga maana hela sio tatizo kwao, ndio hawa waliokejeli wananchi kuwa bora wale majani lakini wanunue ndege, ndio hawa wanaoshikilia karibia utajiri wote wa nchi . Hawa tunaowaona wamevaa fulana za njano na kijani, wanaocheza bongo flava kwenye kampeni, wanaosombwa kutoka eneo moja kwenda jingine kujaza idadi ya wanaohudhuria kampeni za Kikwete ndio waliorubuniwa ili kuwashawishi wananchi waendelee kuwapa wakubwa hawa maisha ya anasa huku wao wakiishi katika umasikini uliopindukia. Ndio hawa ambao kipindi hiki cha kampeni angalao wanaweza kutumia zaidi ya 2,000 kwa siku. Baada ya kampeni ni kilio na tabu kama kawaida. Wagombea wa CCM wanalijua hili fika, Raisi Kikwete analijua hili fika, ni kejeli isiyovumilika kudai ahadi ya maisha bora kwa kila mtanzania imetimia na wapewe miaka mitano tena madarakani.
Twende kwenye elimu, ni ukweli usiopingika kuwa shule zimeongezeka kwa kiasi kikubwa, kuanzia shule za msingi, sekondari mpaka vyuo vya elimu ya juu. Lakini je, majengo ndio elimu? Ripoti hii Poverty and Human Development Report 2009 inasema hivi, nanukuu “ …the enrolment of the poorest children in secondary and higher levels of education- and hence the benefit they derive from government spending for education-remains far behind that of the least poor. Tafsiri yake ni kuwa watoto wanaotoka kwenye familia zenye uwezo wanapata nafasi zaidi kwenye shule za sekondari na elimu ya juu na hivyo kuneemeka kwa kiasi kikubwa na uwekezaji wa serikali kwenye elimu kuliko watoto wanaotoka familia masikini. Ripoti hii inazidi kufafanua kuwa ubora wa elimu umeshuka na kwa siku za karibuni serikali haijawekeza kwenye elimu ya ufundi ili vijana waweze kupata utaalamu ili waweze kujiinua kimaisha. Nanukuu “ Key indicators – including examination pass rates and primary to secondary transition rates have also deteriorated recently, highlighting the persistent challenges of achieving education quality. Moreover, increases in education funding in recent years have not flowed through to technical and vocational training so that young people develop the skills required to secure decent livelihoods”. Hii inaonyesha wazi wanaofaidika ni watoto wa wenye uwezo na sio kila mtanzania kama ambavyo CCM inataka tuelewe na tuamini. Takwimu hizi hawataki wananchi wazijue, wanataka kuwaambia tu kuwa shule zimeongezeka, zaidi ya hapo siri.
Tuangalie upande wa Afya. Kuna taswira mchanganyiko kwenye sekta ya afya. Vifo vya watoto wachanga na wale wenye umri chini ya miaka mitano vimeendele kupungua, hata hivyo vifo vitokanavyo na uzazi havijabadilika karibia muongo mmoja sasa. Mwaka 1996 vifo vya uzazi vilikuwa 529/100,000 , mwaka 2009 takwimu zinaonyesha vimeongezeka mpaka 578/100,000. CCM haiwezi kuzungumzia takwimu kama hii kwa kina mama. Idadi ya watanzania wanaokwenda kwenye vituo vya afya wakiugua nayo pia haijabadilika pamoja na kuwa wagonjwa wameonyesha kutumia vituo vya afya vya serikali kuliko vya binafsi. Mwaka 2001 takwimu zinaonyesha kuwa kuridhishwa kwa wananchi na huduma za afya (Public satisfaction with the health care services) ilikuwa 50% ikapanda mpaka 73% mwaka 2003, ikaporomoka mpaka 70% mwaka 2005, ikaporomoka zaidi kwenye utawala wa awamu ya nne mpaka 64% mwaka 2008. Tunakumbuka vizuri mkakati wa serikali hii wa Zahanati kwenye kila kata, hata hivyo mkakati huu umeshindwa kutokana na kukosekana kwa wataalamu wa afya. Siku za karibuni wengi tumeshuhudia kupungua kwa ufanisi na umakini wa wataalamu wa afya, aidha pia Madaktari wengi wamekimbilia nchi nyingine na wengine wamebadili fani. Wengi wanasema udaktari haulipi,ni kazi ya wito ambayo mtu unaishia kwenye maisha duni. Jambo la kufedhehesha ni kwamba viongozi hawaziamini taasisi za afya za hapa nyumbani, wengi wanakimbilia nje ya nchi kutibiwa maradhi ambayo wangeweza kutibiwa hapa nyumbani, ipo sababu moja tu kuelezea hili, ni kwa sababu hawaiamini sekta ya afya ya hapa nchini. Hawako tayari kupasuliwa kichwa badala ya mguu, hawako tayari kupanga foleni kwa daktari, hawako tayari kuweka maisha yao rehani.
Sekta ya maji safi nayo haiku vizuri, na hamna ushahidi wa wazi kuwa kwa ujumla kuwa kuna unafuu kwa wananchi walio wengi. Katika miaka saba, ripoti inasema hakuna ongezeko la usambazaji wa maji na katika miji kiwango kimepungua cha watu wenye kupata maji ya bomba kutokana na miji kukua kwa kasi kuliko uwezo wa kupanua huduma za usambazaji maji. Baadhi ya maeneo ya mkoa wa Dar es Salaam kuna usambazaji mpya wa mabomba lakini huduma hii haikufika pembezoni au nje ya jiji. Kipindipindu kimeendelea kusumbua wananchi na hiki ni kiashiria kikubwa cha ukosefu wa maji safi.
Kwa ufupi ni kuwa Maisha Bora kwa kila mtanzania ambayo ndiyo vision ni ndoto kwa CCM kuweza kuifanikisha, na ripoti hii imeweka wazi kuwa malengo ya MKUKUTA mengi ni ndoto kuyafikia. Napotoa hitimisho turudi kwa Musa na wana waisraeli. Safari ile iliwachukua miaka 40 jangwani, miaka 9 pungufu ya ambayo CCM imeshindwa kuwaletea watanzania Maisha Bora. Musa aliambiwa hata yeye hatafika kwenye vision (Nchi ya Kaanani), waliowafikisha wana wa Israeli kwenye vision walikuwa wengine kabisa. Pamoja na Musa kufa, vision haikubadilika. Maana yake ni kwamba vision ya Maisha Bora kwa kila mtanzania itaendelea kubaki lakini kwa kuwa CCM imeshindwa kuitimiza inabidi watanzania wapate kiongozi mwingine kutufikisha Kaanani, awe CHADEMA, CUF, NCCR, TLP au chama chochote kingine. Ni kejeli kwa CCM na viongozi wake kusema maisha ya watanzania yameboreka. Wanatumia takwimu lakini takwimu zenye maana halisi ya maisha kuboreka hawazisemi, wamekimbia midahalo wakihofia wapo watu makini watakaowauliza maswali yasiyo na majibu. Wanafahamu watanzania wengi ni masikini wa kutupwa, wakipewa fulana na vijiesenti vidogo wapo tayari kuanika miili yao wakicheza na kuwaimbia ili waendelee kukaa madarakani. Wanafahamu watanzania wengi ni wavivu wa kusoma, wanahitaji kutafsiriwa kila kitu. Wananchi msidanganyike, CCM hawako na ninyi.:israel:
 
Back
Top Bottom