Leo nimekaa nikiwaza nchi yangu inapoenda, nikaamua kujiuliza kama kweli tuna viongozi wenye nia ya kutuongoza na kutufikisha katika neema ya angalau milo mitatu kwa siku! Nimeshindwa kuelewa ni kwa sababu zipi kila siku inabidi mtu uondoke nyumbani saa kumi alfajiri ili kuwahi kazini na ukifika huko kazi zenyewe hazileti tija bali ni kukaa, kusoma magazeti ya udaku na kujaribu kuganga njaa kwa kutafuta semina na mikutano ili angalau uambulie posho itakayopelekea familia yako ipate mlo kwani mshahara hautoshi hata kidogo. Ni nchi ambayo hata zinaponyesha mvua umeme ni wa mgao na bei ya mafuta na gesi haishikiki! Nikajiuliza kama kweli Watanzania ambao kila siku ndugu zao wanauwawa na askari polisi, majambazi na ajali za barabarani bila kujali mabomu ya kijeshi wanaweza kuwapatia kura viongozi ambao aghalabu hawajali hali zao bali matumbo yao na ya vimada wao! Ndiyo maana nakuuliza, hivi kweli kura yako ilihesabika Desemba mwaka jana? Nipeni jibu labda akili yangu itatulia kidogo!