Kung'ara kwa Kikwete kunategemea usafi alionao

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,720
21,779
Kung'ara kwa Kikwete kunategemea usafi alionao




amka2.gif

HARAKATI na pilika pilika za wananchi wenye moto wa kisiasa, hivi sasa zinaendelea kushamiri nchi nzima huku wakijipanga vizuri ili kuwapata viongozi katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika siku 14 zijazo.
Chaguzi za serikali za mitaa sio za kupuuzwa kama baadhi ya watu wanavyofikiria, zina umuhimu wake na kwa mazingira ya kawaida ndiko kunakotoa picha kamili ya muundo wa serikali zilizokaribu na wananchi na dhana ya utawala bora.
Serikali za mitaa zinazotoa picha ya kuwa na mfumo mzuri wa kiutawala unaoanzia ngazi za chini hadi juu na endapo chaguzi hizo zitaborongwa ile dhana ya kuwa na serikali bora inatoweka na kuwa na serikali legelege.
Kufanyika kwa uchaguzi huo nchi nzima ni kipimo tosha cha kutoa tathimini na taswira halisi ya kiutawala inayoongozwa na serikali ya awamu ya nne ya Rais Jakaya Kikwete.
Uchaguzi huo wa serikali za mitaa ndio kioo cha kuona, kuchambua na kujiridhisha ni kwa kiasi gani serikali ya awamu ya nne imeweza kutekeleza ahadi zake ilizozitoa kwa wananchi hasa ikizingatiwa ukubwa wa viongozi katika ngazi za mitaa wametoka kwenye chama tawala( CCM).
Pia ikumbukwe kuwa kwa asilimia kubwa viongozi wa CCM ndio walioweza kushika hatamu za uongozi kwa wingi kutokana na uhamasishaji wa sera na ahadi kadhaa ambazo wananchi wengi walipenda kuona zinatekelezeka kwa wakati.
Tatizo linakuja pale ahadi nyingi zinaposhindwa kutekelezwa, muda ukiendelea kuyoyoma huku dalili za mvua na kiangazi cha mwaka 2010 zikianza kuonekana.
Vyama vya upinzani haviko mbali ,vinajinadi kila kona vikiwaelimisha wananchi umuhimu wa kuchagua viongozi safi kupitia vyama vyao, wananchi wakielezwa upungufu uliofanywa na serikali ya CCM ambayo imeshindwa kutekeleza baadhi ya ahadi ilizozitoa.
Kwa mazingira hayo naanza kuona uangavu na mng’aro wa Rais Kikwete juu ya hisia na hoja zinazojengwa na wananchi wa ngazi za chini ambao mategemeo yao ni kuwapata viongozi wa mitaa watakaoweza kuongoza harakati za mageuzi ya kisiasa katika uchaguzi mkuu wa mwakani.
Hizo ndizo dalili zinazoweza kuthibitisha kung’aa kwa Rais Kikwete kama alivyong’arishwa mwaka 2005, wananchi walimpokea kwa matumaini makubwa, walijiridhisha wamempata kiongozi safi, bora na mchapakazi, waliamini kuwa ndiyo chaguo lao.
Walimpa ushindi wa ‘kishindo’ wakijua fika kuwa mkombozi wao amepatikana, atawatoa kwenye nchi ya kutaabika na kuwafikisha kwenye nchi ya ahadi, nchi ya maziwa na asali, wengi walijua wangefika huko mapema kabla jua halijachwa, lakini kadri siku zinavyokwenda tumaini lao linazidi kufifia.
Wanasiasa wanapita kwenye mitaa, wakijinadi kwa majina ya vyama vyao wakikumbana na maswali magumu kutoka kwa wapiga kura wanaohoji, kama serikali kuu haijawafikisha kule walikokuwa wanategemea, viongozi wa serikali za mitaa watawasaidia nini ?
Hapo ndipo maswali hayo yanapozidi kujenga uzio na kuanza kuififisha nyota ya Rais Kikwete iliyong’ara kwa nguvu mwaka 2005 lakini inawezekana kabisa mng’aro wake umefifishwa na wasaidizi wake kuanzia ngazi za mitaa hadi serikali kuu.
Wananchi wanazidi kujenga shaka, wanashindwa kuona umuhimu wa viongozi wa serikali za mitaa wakijua kuwa wanapoteza muda wa kuwachagua viongozi ambao mfumo wa kiutawala unashindwa kukidhi ahadi ilizozitoa.
Kumbe kwa kufanya hivyo, kususia kupiga kura ni kosa ambalo wananchi wengi hawapaswi kulitenda, kura zao ndio kipimo kikubwa cha kuonyesha ni vipi serikali ya awamu ya nne inavyokubalika kwa wananchi, vinginevyo kosa la upotoshaji wa demokrasia litaendelea kuwatafuna Watanzania.
Wapo wasioamini umuhimu wa viongozi wa mitaa.wakiwalinganisha na tuhuma nzito za ufisadi zilizofanywa na vigogo wa serikali huko juu, huku wakielezea uongozi wa kibabe na kidkteta unavyofanywa na watendaji wa vijiji, hicho kinakuwa kikwazo cha kushiriki uchaguzi ujao.
Wananchi wanataka kumpima Rais Kikwete kwa kupata picha halisi ya viongozi wa serikali za mitaa watakao chaguliwa kwa kuwa miongoni mwao wapo wanaouhitaji uongozi huo kwa gharama yoyote na haieleweki msukumo wa kutumia fedha unatoka wapi ?
Haieleweki viongozi hao ambao kwa kipindi cha miezi kadhaa nchi itakapoingia kwenye mchakato wa uchaguzi mkuu mwakani watakuwa na jukumu gani kubwa la kufanya kama walidiriki kuupata uongozi wa vitongoji, mitaa na vijiji kwa rushwa leo hii wanawezaje kumsafisha mgombea wa urais mwakani bila kuwa wapambe wa rushwa.
Ili uchaguzi mkuu ujao uweze kuwa huru na wa haki kuna kila haja na sababu ya kuondoa uchafu wote wenye harufu ya rushwa katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa kuwa vitendo hivyo vitazidi kuitia doa serikali iliyopo tukihofia kuwa imeshindwa kupambana na rushwa.
Katika hilo na matamanio ya Rais Kikwete kuendelea kung’ara kutategemea usafi alionao na uadilifu mkubwa anaopaswa kuuendeleza ili kuhakikisha kuwa anayavunja makundi ya wana mtandao, urafiki wa hila ndani ya serikali yake na anajenga mshikamano wa kitaifa.
Mshikamano wa kitaifa ni pamoja na kuondoa mtafaruku wa kisiasa huko Zanzibar kati ya chama anachokiongoza, CCM na Chama cha Wananchi (CUF) akifanya hivyo naamini nyota yake iliyoanza kufifia itang’ara upya.
Ikumbukwe kuwa kufifia na kusinyaa kwa mn’garo alioupata Rais Kikwete mwaka 2005, kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na maadui wa kisiasa waliokumbwa na kashfa za ufisadi ndani ya serikali yake na sumu mbaya ya ufisadi imesambaa hadi vijijini.
Huko vijijini ambako sumu ya ufisadi imefika imesababisha wananchi waichukie serikali, wakiamini kabisa kuwa shida na dhiki wanazozipata, kuzidi kuongezeka kwa umasikini kumechangiwa na ubadhilifu mkubwa wa fedha za serikali zilizochotwa na mafisadi.
Wanampenda Rais Kikwete, wakimuonea, jinsi maadui zake, mafisadi wanavyozidi kujiimarisha kwa sura nyingine bila aibu, hilo ni doa kubwa linaloweza kuongeza mng’aro wa Rais kuendelea kufifia na kudhoofisha nguvu za chama hicho kwenye serikali za mitaa.
Wananchi wanaomuonea huruma Rais hawajui ni kwa kiasi gani kuyumba kwa uchumi wa nchi kumechangiwa na mtikisiko wa uchumi wa dunia hasa kwenye mataifa makubwa yaliyokuwa yakitegemewa na nchi masikini kama Tanzania.
Hapo ndipo, Rais Kikwete anapaswa kujipanga upya, akifanya jitihada za dhati za kuwashughulikia mafisadi si kwa maneno bali kwa vitendo. Wananchi wanataka kuona ushujaa wa Kikwete katika kutekeleza ahadi zote alizozitoa kwa maana ya kuhakikisha ‘Maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana’ muda unazidi kwenda na kipindi cha uchaguzi mkuu mwakani unakaribia.
Ndio maana nasema hivi, kung’ara kwa Kikwete kutategemea usafi alionao. Macho ya Watanzania wote bado yana mtazama, wengi wanalia lakini mtu wa kuwasikiliza kwa karibu hayupo, wanataka kupoteza matumaini lakini dhamira ya kujenga nchi ya amani na utulivu bado inawasuta. Wanakufa kwa njaa huko vijijini, wanakosa huduma bora za afya, barabara, umeme, maji safi na salama, shule zenye mwalimu mmoja mmoja, matatizo hayo yote wanamuangalia Rais Kikwete ndiye mwenye jibu. Sasa wameamua kumpigia simu Rais wao wakimuuliza maswali kupitia kwenye vyombo vya habari, wanajibiwa papo kwa hapo, hawaoni utekelezaji


h.sep3.gif
juu
blank.gif
 
Back
Top Bottom