Kuna Wasafiri Na Wabeba Mabuli

Sumaku

Member
Feb 17, 2009
53
1
Na Maggid Mjengwa,

RAIS MSTAAFU Mzee Ali Hassan Mwinyi amejaliwa kipawa cha kutumia vema lugha ya Kiswahili anapowasiliha ujumbe wake. “ Ndugu zangu, kuna wasafiri na wabeba mabuli!”. Nilipata kumsikia Mzee Mwinyi kwenye moja ya hotuba zake alipokuwa madarakani.

Wabeba mabuli ni wale wanaotumiwa safarini kwa kazi ya kubeba hiki na kile na kufanya hiki na kile kwa kuamrishwa, ni kama wapagazi. Wabeba mabuli ni watu wa kuamrishwa safari bila kujua inakwenda wapi. Lakini wabeba mabuli anaowazungumzia Mzee Ali Hassan Mwinyi ni viumbe wenye kufikiri.

Bondia Mohammed Ali alipata kuvuliwa ubingwa wa uzito wa juu duniani kwa kukataa kwenda kupigana vita Vietnam. Alipotakiwa aende vitani Mohammed Ali alikataa na kusema; “ Siwezi kwenda Vietnam kwa vile sijui hao tunaokwenda kuwapiga wana kosa gani”

Mohammed Ali akaambiwa , kuwa wenzake wameshakwenda huko Vietnam, naye akajibu; “ Hao waliokwenda huenda wameshaambiwa kosa walilofanya Wa- Vietnam, miye bado sijalijua”.

Naam. Mohammed Ali hakwenda Vietnam, ni kiumbe anayefikiri na alikataa kuwa mbeba mabuli. Waliompa Mohammed Ali adhabu ya kunyang’anywa mkanda wake wa ubingwa na hata kufungiwa kucheza ngumi kwa muda fulani bado wanamuheshimu Mohammed Ali kwa msimamo wake ule.

Inasemwa, kuwa heshima ni kitu cha bure. Lakini mjinga ni yule anayefikiri, kuwa akiipoteza heshima yake, basi, atakwenda kuichukua nyingine bila gharama yeyote, maana ni kitu cha bure! Hapa duniani binadamu hupewi heshima .

Binadamu unajitengenezea heshima kisha unaheshimiwa. Hii itatokana na kauli na matendo yako. Kuna wanaoogopewa huku wakidhani wanaheshimiwa. Heshima ni zaidi ya mtu kuitwa mheshimiwa.

Nchi hii imejaliwa kuwa na watu wengi waliojitengenezea heshima na wakaheshimiwa. Mwalimu Nyerere ni mfano wa watu hao. Kuna wakati, walitokea watu waliovumisha ufisadi wa uongo wa Mwalimu Nyerere.

Ikasemwa kuwa Mwalimu alikataza majarida ya kigeni kama vile ‘News Week’ kwa vile yalibeba habari juu ya Mwalimu kumiliki viwanda kama kile cha nguo cha URAFIKI. Tuliokuwa shuleni wakati huo bado pia tuna kumbukumbu za uvumi kuwa Mwalimu alikuwa na shamba kubwa la mahindi kule California, Marekani.

Kama binadamu wengine, Mwalimu alikuwa na mapungufu yake, lakini , hata baada ya kifo chake, jambo moja tunafahamu, kuwa Mwalimu hakuwa FISADI. Aliitanguliza Tanzania na aliwapenda Watanzania. Hakuwa na shamba katika mkoa wowote wa nchi hii mbali ya lile la kijijini kwake Butiama.

Katika wakati wake, Mwalimu anngejilimbikizia mali nyingi kama angetaka. Mobutu wa Zaire alijenga Ikulu ya marumaru kijijini kwake Bbadolite, Mwalimu alijengewa nyumba kijijini kwake kwa msaada wa Wachina. Watoto wa Mwalimu tunawaona wanavyoishi, Mwalimu angetaka tusingeiona familia yake kama ilivyo sasa. Lakini hayo na mengineyo, ndiyo yenye kumfanya Mwalimu aendelee kuheshimika ndani na nje ya Tanzania.

Leo tuna aina ya viongozi wenye kufikiri mambo makubwa mawili; familia na jimbo lake ( kama ni mbunge). Jimbo ni kama mgodi, ataupigania ili aendelee kubaki bungeni na huku akiunyatia uwaziri. Hilo la mwisho linalipa zaidi. Kwa kiongozi huyo, waliobaki ni wabeba mabuli.

Naam. Wabeba mabuli wa nchi hii wameanza kuamka, wanahoji mwelekeo wa safari. Na wana uwezo, sababu na nia ya kuanzisha safari yao.
0788 111 765


CHANZO: kwanzajamii.com
 
Back
Top Bottom