Kumbukumbu: Hotuba ya Freeman Mbowe - Agosti 2006

WOWOWO

JF-Expert Member
Aug 3, 2011
590
430
Hotuba ya Mwenyekiti wa CHADEMA, Mheshimiwa Freeman A. Mbowe katika uzinduzi wa chama

WAHESHIMIWA viongozi wezangu, leo Agosti 13 mwaka 2006, tunatimiza mwaka mmoja kamili tangu tulipoonana kwa mara ya mwisho.

Sina hakika kama wengi wenu mnakumbuka tulikutana tarehe kama ya leo kwenye mkutano wetu wa mwisho. Mkutano ambao ulinipa wajibu wa kupeperusha bendera ya chama chetu katika uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani.

Leo tumekutana mwaka mmoja baada ya kupewa wajibu na heshima hiyo, niliwashukuru na nawashukuru tena. Pamoja na mimi mlinipa mgombea mwenza wangu, hayati mzee wetu Jumbe Rajabu Jumbe. Mimi na Mzee Jumbe, mlitupa kazi ngumu na nilizungumza katika mkutano huu kwamba mmetutwisha jiwe.

Namshukuru mwenyezi Mungu aliniwezesha kufika najiwe lile. Lakini mapenzi yake yalitimia kwa mzee Jumbe Rajab Jumbe nae hatunaekatika mkutano huu. Mwenzetu amefariki katikati ya mapambano. Ametutangulia mbele ya haki.

Napenda kuamini mwenyezu Mungu na tunavyomuomba wote, ataiweka roho ya marehemu mahali pema peponi. Ndugu zangu, uchaguzi ni kazi ngumu sana. Hasa uchaguzi huo unapopambana na watu wasiotambua haki, maadili ama utashi wa binadamu wenzao.

Kampeni ina maumivu makubwa. Maumivu haya hayakumkumba mheshimiwa Jumbe pekee, bali wengine wengi. Tunampongeza mwenyekiti wetu wa mkoa wa Manyara ambaye nae tulikuwa pamoja nae katika ukumbi huu mwaka mmoja uliopita.

Mheshimiwa Jumbe na mheshimiwa Mulumbi, ambaye alikuwa pia mgombea wetu wa ubunge, nae mwenyezi Mungu amemwita mbele ya haki. Tunatambua wapiganaji wetu wengine ambao pengine tulikuwa nao na sasa hawako nasi tena. Hata kama si wajumbe wa mkutano mkuu, tunawakumbuka.

Tunawakumbuka pia watanzania wengine ambao wamepoteza maisha yao katika kipindi hiki cha mwaka mmoja, pengine kwa sababu ya harakati za siasa. Wapo pia watu walipoteza maisha yao kule Tarime, wakipambana kutafuta haki kwa Watanzania.

Kwa heshima na taadhima naomba mkutano mkuu huu utambue jasho lao na damu yao iliyotangulia mbele ya haki, kwa sababu ya ukombozi wa taifa letu na kwa maana hiyo ningeomba tusimame kwa dakika moja kwa heshima ya mashujaa wetu hawa.

Waheshimiwa viongozi, napenda nimshukuru sana mama yangu kwa kukubali kuziba pengo la mzee Jumbe Rajab Jumbe wakati wa uchaguzi. Naomba pia niwapongeze wagombea wote wa ubunge na udiwani wa chama chetuwakiwemo nyinyi mliomo katika mkutano huu, kwa kukubali kazi ya kutetea haki katika taifa letu, katika mazingira magumu na ya kutisha; katika mazingira yaliyojaa vitisho na uzandiki wa kutisha.

Pamoja na yote hayo, wote kwa pamoja tulisimama kidete, kuwa mawakala wa mabadiliko. Nashukuru sana na naamini mwenyezi Mungu anatambua kazi tunayoifanya hata kama watawala hawaheshimu tunayoyafanya.

Tulifanya kampeni katika mazingira magumu sana. Tulifanya kampeni katika mazingira ya vitisho sana. Wako wengine waliosema kwamba, upinzani ulikuwa dhaifu katika uchaguzi, na wanatuhukumu kwa matokeo ya kuiba kura, lakini wanatuhukumu hivyo hawatuhukumu kwa kauli tulizotoa kwa niaba ya watanzania milioni 36. Viongozi wenzangu tusikate tama a wala msikate tama. Ujasiri uko palepale, malengo yako palepale na hakuna kulala.

Waheshimiwa viongozi, siku tunakwenda kupokea matokeo ya uchaguzi katika ukumbi wa Diamond Jubileekatika mazingira ambayo watu wengi walikuwa na hasira za matokeo yale wakaniambia mheshimiwa mbowe usiende kupokea matokeo haya, kwani utakuwa unahalalisha wizi wa kura na uchaguzi usiokuwa wa haki katika nchi yetu.

Niliheshimu ushauri wao, lakini nilijua ninawajibika nchi yangu, ninawajibu katika chama changu nikaenda. Kwani hata kushuhudia watu wakitunukiana heshima kubwa ya uongozi wa taifa hili kwa vigelegele vya kinafiki na kizandiki, wakati wakijua kweli kwamba kura zao,ushindi wao haukuwa halali. Na hata kama ulikuwa halali, haukuwa wa kiwango kile, niliona vema niwe shuhuda wa kitendo kile, kwani mabadiliko katika nchi yetu ni mchakato, hata kama tuliteleza kwa sababu mbalimbali.

Tuliwajibika kusimama na kuonyesha ujasiri wetu kwamba,kila penye ushindani pana mshindi na mshindwa hata kama kwenye mazingira ya rafu. Tunaitakia kheri nchi yetu. CHADEMA hatukubali kuwa mawakala wa kumwaga damu ya Watanzania ama kuleta machafuko ya njia yoyote katika taifa hili.

Wakati naondoka kwenye mkutano ule waheshimiwa sana viongozi wenzangu, waandishi wa habari walinizonga wakiniambia Mbowe pole. Nikawaambia sina hakika kama anaestahili kupewa pole ni Mbowe, pengine nyinyi waandishi wa habari na Watanzania ndio tuwapeni pole.

Kwa sababu tulichokifanya sio cha Mbowe wala sio cha viongozi wa CHADEMA, ni cha taifa letu la Tanzania, tunapoona demokrasia inanyongwa na haki inanyongwa katika taifa letu, tunawajibika kwenda pabaya, na waandishi wale wakaniuliza swali la pili. Wakaniambia Mheshimiwa Mbowe, huoni hawaelewi maana ya vyama vingi vya siasa? Nikawajibu nikawaambia: Watanzania wanafahamu vizuri sana haki zao, na kama kuna watu wa kuwapa mafunzo ya elimu ya siasa, kama kuna watu wa kuwapa mafunzo ya uraia,basi mwanafunzi namba moja katika darasa hilo angekuwa Mheshimiwa rais mstaafu, Benjamini Willium Mkapa.

Angekuwa Mkapa na serikali yake, wangekuwa viongozi wote wa chama cha mapinduzi, wangekuwa makamanda wetu wa majeshi ya ulinzi na usalama. Hao ndio wanaostahili kupewa elimu ya uraia.

Waheshimiwa wananchi, tulishuhudia matumizi makubwa ya nguvu za serikali katika uchaguzi huo. Tulishuhudia matumizi makubwa ya majeshi yetu katika kuvuruga demokrasia na haki ya wananchi kuchagua. Tulishuhudia matumizi yasiyo na mipaka na fedha katika uchaguzi mkuu. Uchaguzi mkuu ulikuwa ndio mnada wa kura, badala ya fursa ya Watanzania kuchagua viongozi wanaowataka.

Tumeona wazi tume ya uchaguzi ikifanya kazi kwa upendeleo na hawakuheshimu haki na demokrasia katika taifa hili. Kwa hiyo, waheshimiwa viongozi wenzangu nikubali matokeo nikujua hayako.

Nikijua kiongozi nina wajibu wa kufikiria zaidi ya mchakato wa uchaguzi, kwamba kuna maisha baada ya uchaguzi. Ndugu zangu sikuhalalisha kwamba uchaguzi ulikuwa huru na wa haki. Kwa hiyo naomba leo tutoe tamko kama chama, nyinyi kama mkutano mkuu mkiwa kama kikao cha juu kabisa katika chama chetu, tukubaliane kwamba chetu kiliendesha kampeni za kistaarabu, kiliendesha kampeni za kisera na kampeni za kihoja.

Wale wenye kulingia ushindi leo, hao hao walidai kwamba upinzani hauna sera, hao hao walidai kwamba wapinzani hawana jipya, tunawaona wakikumbatia sera zetu, Wakitoa kauli mbali mbali kuwa wanatambua kuwepo kwa CHADEMA, hoja za chadema na hata sera za CHADEMA.

Wanachadema wenzangu, kwa niaba ya Watanzania tusiwe wachoyo wa fikra. CHADEMA ni kisima cha fikra na ni fikra zinazoongozwa na dhamira tahabiti, wasione haya kuchukua sera zetu, tutaendelea kufanya utafiti wa kuibua sera mbadala kwa sababu ya ustawi wa jamii ya Tanzania.

Matokeo yalitoka, tukapewa yale waliokusudia kutupa kwa minajili yao, pamoja na kufanya kazi katika mazingira magumu sana, na pamoja na kupewa matokeo ambayo hayakuwa stahili yetu, bado chama chetu kimeweza kupanda kutoka kilipokuwa.

Tulishiriki uchaguzi wa rais kwa mara ya kwanza na tuliendelea kushiriki katika chaguzi za wabunge na madiwani, walinipa kura zilizoniwezesha kushika nafasi ya tatu. Na pengine ndugu, waheshimiwa viongozi wenzangu, kama msingekuwa makini pengine hata hizo laki mbili zisingepatikana. Lakini nilipata laki sita kwa sababu hizo mlizihenyea kwelikweli nawashukuruni sana.

Lakini chama chetu kiliweza kuongeza wabunge,awali tulikuwa na wabunge 4 katika bunge lililopita. Tulikuwa wabunge 5 katika bunge lililopita, wanne walikuwa wa majimbo na mmoja viti maalumu. Kazi yenu viongozi na waheshimiwa wenzangu, tumeweza kuongeza wabunge hadi 11 katika bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania.

Wabunge hawa 11 kwa wale wanaofuatilia mienendo ya bunge wakishirikiana na wabunge hawa wa upinzani kule bungeni wanawakilisha jamii kubwa ya Watanzania wenye uchungu na kilio. Hawa ndio watetezi pekee wenye dhamira ya kweli katika bunge letu la kuwakomboa Watanzania wakiwemo wa kada wa Chama Cha Mapinduzi ambao huenda kwenye uchaguzi wakishabikia vyma bila kusikiliza hoja.

Wakishabikia fulana na kofia bila kujua ni masikini wa kutupwa, hawa wanahitaji ukombozi, wanahitaji elimu ya uraia. Tumeweza kuongeza madiwani wa chama kutoka 49 kuwa madiwani 99. Ni mafanikio sio haba, kwa sababu wapo madiwani wengine wengi walishinda, lakini ushindi wao ukapokwa.

Wapendwa viongozi wenzangu nilizuiwa kufanya kampeni katika visiwa vya Pemba na Zanzibar, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), kwa kibali cha Serikali ya Muungano wakati wakijua kabisa kwamba, ratiba yangu ilikuwa kufanya mikutano 10 kwa siku.

Mara mbili tulijaribu kufanya juhudi za kuweza kufanya mikutano Zanzibar walitukatalia. Naomba radhi sana, viongozi wetu wa Zanzibar makosa hayakuwa ya kwetu, makosa ndio hayohayo tunajitahidi kuyarekebisha ya uzandiki wa watawala wetu.

Lakini pamoja na kushindwa Zanzibar, na pengine niseme wangeniruhusu kutua Zanzibar wangepata shuhuri. Bado nina usongo nao. Tuliweza kuwa kwanza chama cha tatu katika ushindi Zanzibar pamoja na kwamba hatukusimamisha mgombea urais, chama chetu sasa kinajipanga kuwa muhimili wa siasa wa tatu katika Zanzibar.

Tunafanya hivyo tukiamini kwamba, kwa kuwa na nguvu mbadala ya kisiasa katika visiwa vile, utengano wa amani wa ndugu zetu katika visiwa vya Zanzibar utakuwa kamili.

Kwa hiyo leo tunapofanya mabadiliko yetu ya katiba, ndugu zangu wa Zanzibar mtaona kuna mkazo mkubwa umewekwa katika kuimarisha ofisi ya Zanzibar ili wafanye kazi za siasa kama watu walio huru na ambao wana haki katika nchi yetu.Sisi ni chama makini, hatukurupuki.

Ndugu zangu sasa ni miezi minane baada ya uchaguzi. Baada ya uchaguzi ni wajibu wa watu walio makini, na watu walio na dhamira ya kweli kama waliteleza wasimame wajipange waanze tena safari. Tumekaa kimya kwa miezi minane, hatukuwa wendawazimu.Watanzania wengi wakiuliza chadema mnafanya nini kwa miezi minane, mbona mmekuwa kimya? Mtu yeyote mwenye busara humpa mwenzake nafasi ya kufanya kazi. Sisi ni chama makini hatukurupuki katika hoja zetu.

Tangu uchaguzi mkuu leo ni mara ya tatu naongea rasmi na waandishi wa habari,mara ya kwanza niliongea siku 100 za rais Kikwete, mara ya pili nilizungumza na waandishi wa habari kuwaelezea kikao chetu cha baraza kuumwezi wa tano na leo naongea mbele ya mkutano wangu, kwa misingi ya watanzania wenzangu tulikaa miezi hii 8 tukitafakari tulikotokea, tulipo na tunapokwenda, tumetumia mudahuu kufanya tathimini ya kina ya mfumo wetu wa uongozi wa chama, tumetumia fursa hii kutafuta nguvu zetu ziko wapi, udhaifu wetu uko wapi, fursa zetu ziko wapi na nini tishio kwa mustakabali wa taifa letu.

Tumefanya makongamano ya ndani ya wagombea ubunge, baadhi wagombea udiwani katika baadhi ya maeneo. Tumefanya utafiti wa kina katika wilaya 69 katika nchi yetu. Tumefanya makongamano ya kamati kuu (CC) Baraza kuu (NEC) katika mchakato mzima wa kutathimini. Tumegundua tuna udhaifu wetu ambao sambamba na mkakati wa makusudi wa kukandamiza upinzani, unawanyima watanzania fursa ya maisha bora.

Mtu jasiri ni yule anayekubali ukweli na udhaifu wake. Yote hayo tumeyafanya bila mgogoro,bila mivutno, kwa hoja na kwa mashauriano.

Tumeshirikiana na viongozi wote wa makao makuu, wabunge wetu, sekretarieti ya taifa, wajumbe wa baraza kuu, wajumbe wa kamati yetu, bodi ya wadhamini ya chama.

Tumewashirikisha wataalamu mbalimbali kutoka taasisi mbalimbali za elimu na jamii, na mnapenda kujua wenzetu wa nje wanaitafakari vipi CHADEMA.

Leo tuko na nyinyi tutawapa kile ambacho tumekipata na tutakiweka kwenu kama wajumbe wa mkutano mkuu mkitafakari, tukifanyie maamuzi, tukijua kwamba umma wa Watanzania wengi walio maskini na fukara wanakilio. Tukijua kwamba, tumaini jipya linahitajika katika nchi yetu, kwani Watanzania wasnaelekea kukata tamaa. Viongozi wananeemeka, wananchi wanataabika. Tunawajibu mbele yetu leo tufanye maamuzi. Tunahitaji kuboresha katiba yetu ya chama.

Waheshimiwa viongozi,kwani nyinyi ndio wadau wakubwa wa kuongoza mapambano haya katika hatua za baadae. Tutajadili kwa kina mwelekeo wetu wa katiba na nini tukirekebishe ili kuongeza ufanisi na ushirikishwaji wa umma wa Watanzania katika harakati za ukombozi wa taifa letu.

Leo tutajipanga kwa ajili ya uchaguzi wa 2010 tumesikia kauli za viongozi. Nimesikia kauli za viongozi. Nimesikia kauli za kebehi zikisema kwamba, upinzani nchi hii utakufa.Je,mnakubali upinzani nchi hii ufe? Hapana.

Upinzani hauwezi kufa wakati watawala wameshindwa kuleta neema kwa Watanzania. Upinzani hauwezi kufa kwa porojo na mbwembwe za majukwaani. Upinzani hauwezi kufa kwa ahadi zisizotekelezeka.

Upinzani utakufa pale Watanzania watakapoona kwa vitendo umasikini wao umeondoka. Takwimu za kukua kwa uchumi, ni mchezo wa takwimu. Watanzania maisha yao yameporomoka kwa kiwango cha kutisha.

Kwa miezi nane ya utawala wa awamu ya nne. Leo tunapitia mkakati wa miaka wa mitano tukitengeneza program (Mpango) wa chama kwenda katika uchaguzi mkuu. Sio kama wasindikizaji, lakini iliyodhamiria kukamata dola ya Tanzania.Hatutaogopa polisi, hatutaogopa usalama wa taifa. Tutaheshimu haki ya Watanzania bila woga, bila ajizi.

Wapendwa ndugu zangu, serikali ya awamu ya Mheshimiwa Jakaya Kikwete, hawa kwa lugha nyepesi ya kigeni unaweza kuwaita smooth operator.Kuna mikakati ya makusudi ina sukwa kunyonga upinzani. Na malengo yao makubwa ni kunyonga CHADEMA. Sijui na Mbowe? Sina hakika. Pamoja na vyama vingine vyote vya upinzani.

Ni watu wanaotoa kauli majukwaani kwamba, wanania ya kujenga upinzani, lakini wanarudi kwenye vikao vya ndani na kuweka mkakati wa kunyonga upinzani. Ni mambo ya hatari.

Zinafanyika juhudi za makusudi za kutumia fedha za walipa kodi wa taifa hili, kuwarubuni viongozi wa upinzani warudi ndani ya Chama Cha Mapinduzi. Hakuna taifa lolote linaloweza kurejista maendeleo ya kweli, ikiwa vyombo vyake ama taasisi zake za kidemokrasia hazipo.

Hatumkomoi Mbowe wala Mbatia. Hatumkomoi Mrema, wala Lipumba, wala viongozi wetu wengine wa vyama vya upinzani. Tunawatesa baba zetu, ndugu zetu, watoto wetu, ambao ni taifa la kesho.

Na ndiyo sababu mbinu zilezile za ufisadi na unafiki,tunazoziona ndani ya bunge, ambapo nimekuwa nikisema siku nyingikuwa bunge la Tanzania kwa misingi ya chama Cha Mapinduzi, ni mchezo wa kuigiza. Wabunge wa Chama Cha Mapinduzi wanakemea rushwa, rais wao anasimama anakemea rushwa, wakati wote tuna uhakika wameingia katika uchasguzi kwa misingi ya rushwa.

Sasa wale wqanaobariki rushwa,leo wana madaraka ya kuitokomeza rushwa. Taifa letu lina kilio. Upinzani ulishinda halmashauri kadhaa, ikiwapo Halimashauri ya Karatu.

Napenda kuwapongeza wapiganaji wenzetu wa karatu, Halmashauri ya Kigoma, ambayo tupo katika ubia. Napenda kuwapongeza wapiganaji wenzetu wa Karatu, Halmashauri ya Kigoma, ambayo tupo katika ubia. Napenda kuwapongeza sana waheshimiwa wa Kigoma.

Halmashauri ya Bariadi, chini ya UDP. Napenda kuwapongeza waheshimiwa wa UDP, na wale wapinzani wenzetu walioshinda katika visiwa vya Unguja na Pemba. Napenda kuwapongeza sana.

Aidha, mheshimiwa Kabuye mbunge wa Biharamulo kupitia TLP, napenda kumpongeza sana. Maana hawa ndiyo mabalozi wetu ndani ya Bunge la jamhuri ya Muungano. Hizo halmashauri chache tunazoziongoza zinawakera CCM. Hawalali wanafikiria jinsi ya kuzinyonga.Leo bila aibu serikali imeandaa muswada wa kupeleka ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Muswada ambao wanausema ni wa kurekebisha sheria namba 7 na namba 8 ya mwaka 1982. Hii ni local Govement Act ya mwaka 1992. Na mojawapo ya vipengele wanavyosema ni kwamba, waziri mwenye dhamana ya Tawala za Mikoa na Serikali Mitaa(TAMISEMI), eti anapewa sasa mamlaka ya kuteuwa madiwani watatu kwa kila halmashauri.

Wakijua kwamba, katika halmashauri ya Karatu, CHADEMA tunaziada ya madiwani watatu, wakijua halmashauri ya Bariadi, UDP ina ziadaya madiwani wawili, wakijua Kigoma tumefungana na Chama Cha Mapinduzi.

Sasa waziri huyu atateua madiwani wa CCM watakuwa wengi, watapindua halmashauri zinazoonozwa na upinzani. Hii ni aibu! Naomba wote tuseme aibu!

Rais Kikwete kama unaheshimu haki na demokrasia katika nchi hii, sitisha mpango huu wa kunyonga demokrasia.
 
Hizi ndio hotuba ambazo zinaweza kudumu hata miaka Mia bila kuchosha ukizisikiliza sio za mwenyekiti wa Chama cha mabwepande ukisikiliza unatapika Kama vile umekunywa gongo ya kigogo
 
Brainy speech Imetulia sana nimeipenda hii hotuba kamzidi Kikwete kwa mbali sana aisee
 
Tanzania ina viongo na huyu ni mmojawapo. Tunamshuku sana kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuwaamsha watanzania ambao tulishaibiwa mpaka basi!
 
Viongozi makini always hupatikana katika chama makini, sasa naomba mtoa mada aweke hotuba moja ya mh. Jk tulinganishe viwango....M4C forever...
 
Nimeipenda hotuba wakati huo Chadema kilikuwa chama makini.

wine ina kuwa nzuri jinsi inavyokula miaka.Sidhani kwanini CDM with same people are gaining experience iwe dhaifu.Inaelekea kipindi hicho akili yako ilikuwa timamu zaidi.
 
Mbowe ni mpiganaji wa kweli, na alianza kuwapigania watanzania muda mwingi sana Ongera sana Mbowe tuko pamoja.
 
Kama hotuba hii makini na tamu ingepata nafasi ya kusomwa leo hii katika vyombo vya habari
ama kwa hakika watu wangemkana JK na kusema tunataka Raisi wetu Mbowe akabidhiwe
nchi leo leo.

Chama makini siku zote hujengwa na watu makini ama kwa hakika 2015 Chadema lazima ichukue
kutoka kwa serikali hii dhalimu ya chama cha magogoni.

GOD BLESS CHADEMA (M4C Songa mbele daima)
 
Back
Top Bottom