Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,810
- 15,398
Inawezekana hata wewe umeshawahi kuambiwa kwamba usihesabu vifaranga kabla havijatotolewa. Mara nyingi msemo huo hutumiwa katika jamii yetu ikiwa ni njia ya kumwonya mtu kwamba asiwe na matarajio makubwa na jambo ambalo halijafanyika kwa ukamilifu.
Kila mtu, labda ukiwemo na wewe, unajua kuhusu jambo hili na unaliogopa pia. Unaliogopa kwa sababu umeambiwa kwa muda mrefu sana kiasi kwamba limekuwa ni kweli akilini mwako.
Nikisema limekuwa ni kweli nina maana kwamba unaliamini kuwa ndivyo lilivyo. Hili ni tahadharisho kwamba mtu ukiwa na matarajio makubwa, utavunjika sana nguvu iwapo matarajio hayo hayatazaa matunda yanayotarajiwa.
Bila shaka, waliotuambia hivyo walikuwa wanasema kwa nia njema kabisa. Lakini je lilifikishwa kichwani mwako kwa njia nzuri, ambayo isingeweza kuzalisha maana tofauti kabisa? Kila mmoja wetu wakati anakua aliwekwa kwenye tahadhari, ambapo alitakiwa bila kujua, kujiweka kwenye mazingira ambayo yatamfanya awe salama kihisia muda wote.
Kwa mfano kutokujenga matarajio makubwa ni ili mtu asije akaumia sana kihisia pale matarajio hayo yakishindwa kufikiwa. Lakini leo ukubwani jambo hilo limekuwa ni sehemu muhimu ya tabia zetu. Hatuko tayari kuwa na matarajio makubwa kwa sababu tunaogopa kwamba kufanya hivyo ni kuingia mahali ambapo tutaumiza sana hisia zetu, pale ambapo jambo tunalotarajia likishindwa kuwa.