Komba atuhumiwa kwa ubadhirifu

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,011
Ufisadi mpya CCM

na Mwandishi Wetu
Tanzania Daima~Sauti ya Watu

MKURUGENZI wa Kikundi cha Sanaa cha Tanzania One Theatre (TOT), Kapteni John Komba, anakabiliwa na tuhuma za ubadhirifu wa mamilioni ya fedha katika kikundi hicho, kinachomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), Tanzania Daima imegundua.

Tuhuma hizo zimeibuliwa katika taarifa ya ukaguzi maalumu, uliofanywa na kitengo cha ukaguzi cha CCM, kwa maagizo ya Katibu Mkuu, Yusuf Makamba, kutokana na tuhuma zilizowasilishwa kwake dhidi ya Kapteni Komba.

Ukaguzi huo, ulifanyika kuanzia Machi 3 hadi 16, mwaka huu na baadaye Aprili mosi hadi hadi 6, na taarifa yake kuwasilishwa rasmi kwa Makamba Aprili 22.

Katika taarifa hiyo ya uchunguzi ambayo Tanzania Daima ina nakala yake, Komba anadaiwa kutafuna sh milioni 30 za mishahara ya wafanyakazi wa TOT ya miezi 14.

Uchunguzi huo ambao umepata baraka za chama, unadai kuwa CCM ilitoa sh 37,442,923 kwa ajili ya kulipa malimbikizo ya mishahara ya miezi 14 kuanzia Julai 2006 hadi Agosti 2007 kwa awamu, lakini ni sh milioni sita tu, ndizo zilizolipwa kwa wafanyakazi kwa mishahara ya miezi miwili.

“Ukaguzi umebaini kuwa, CCM ilitoa sh milioni 37.4 kwa ajili ya kulipa malimbikizo ya mishahara ya miezi 14 kuanzia Julai 2006 hadi Agosti kwa awamu mbili.

“Malipo ya awamu ya kwanza yalifanyika 21/ 11/ 2007 kwa hati ya malipo namba 056996 ya sh 18,532,458 na tarehe 21/12/2007 kwa hati ya malipo namba 1343 sh 18,910,465, jumla ni sh 37,442,923,” ilisema taarifa hiyo ya uchunguzi ambayo Tanzania Daima imeiona nakala yake.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Kapteni Komba pamoja na afisa...(anatajwa jina afisa mwingine), bado wanadaiwa malimbikizo ya sh milioni 30,514,625.

“Ukaguzi uliona orodha ya majina waliyosainishwa watumishi hao wa TOT kwa miezi miwili tu jumla ya sh 6,928,298, watumishi waliulizwa na ukaguzi, walithibitisha walilipwa malimbikizo ya miezi miwili tu,” ilisema taarifa hiyo.

Pia viongozi hao wa TOT, wanahusishwa na udanganyifu wa kulipa warithi wa marehemu wasio waasisi wa chama jumla ya sh 27.3 milioni, lakini baadhi ya waliotajwa kwenye orodha ya malipo, wamekana kupewa fedha zozote.

Kwa mujibu wa dokezo lililosainiwa na kiongozi mmoja wa TOT, linaonyesha jina la marehemu, jina la mrithi na kiasi cha pesa alicholipwa.

Dokezo hilo linaonyesha kuwa marehemu Godfrey Lugendo, mrithi wake Mwantumu Haji, alisaini sh milioni 4,320,000, marehemu Leyla Khatibu, mrithi wake Monica Robert, alisaini sh 6,750,000, Fred Mshana, mrithi wake Benson Mshana, alisaini sh 4,880,000, Hamimu Hemera, mrithi wake, Mwanakombo Ahamed, alisaini sh 4,240,000 na Salum Poogwe, mrithi wake Nuru Salum, alisaini sh 7,200,000 na hivyo kufanya kiasi cha fedha zote zilizolipwa kwa ajili ya warithi hao kufikia sh 27,200,000, jambo ambalo uchunguzi umebaini kwamba si la kweli.

Madai mengine anayotuhumiwa nayo Komba ni kuwapunja wafanyakazi wa TOT kwa kuwalipa posho ya sh 20,000 kwa siku wanapokuwa nje ya Dar es Salaam badala ya sh 40,000 zinazotolewa na chama.

Taarifa hiyo inasema wasanii wa TOT wanaposafiri kwa shughuli za chama, viongozi wanne hulipwa sh 40,000 kwa siku na waliobaki hulipwa sh 30,000.

“Wanaokwenda CCM kuchukua fedha hizo ni ama Kapteni Komba au Gasper Tumaini (ofisa mwingine wa TOT). Fedha hizi huwa haziingii katika vitabu vya TOT, wala wasanii hawasaini hati za malipo, bali husainishwa katika karatasi na mhasibu hausiki kulipa fedha hizo,” ilisema taarifa hiyo.

Mbali ya tuhuma za ubadhirifu wa fedha, Komba ambaye pia ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) na Mbunge wa Mbinga Magharibi, anatuhumiwa kusajili gari la CCM kwa jina la asasi yake isiyo ya kiserikali inayojulikana kwa jina la Educare Girls.

Inadaiwa kuwa alisajili gari jipya la chama hicho, aina ya NISSAN Civilian, Mini Bus lililosajiliwa kwa namba TZT 8978, kwa jina lake na baadaye akaliuza gari hilo kwa sh 2,300,000, wakati limenunuliwa kwa sh 16,200,000.

Pia anakabiliwa na tuhuma za kuuza gari la chama, aina ya Mitsubishi Canter, lenye namba za usajili, TZR 6056, kinyume cha utaratibu na wakaguzi wanasema hajasema alipata kiasi gani na fedha hizo zilitumikaje.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, gari hilo lilinunuliwa kwa ajili ya kubeba wasanii na vyombo vya muziki.

Imeelezwa kuwa kabla ya uchaguzi mkuu wa 2005, CCM ilitoa magari matatu kwa Komba kwa ajili ya TOT.

Magari hayo ni Scania lenye namba za usajili T596 ABJ kwa ajili ya kuvuta tela; Isuzu Forward namba T 488 AHD na basi dogo aina ya Coaster, namba T 203 ABC.

Kutokana na tuhuma hizo, uchunguzi huo umependekeza kuwa kuanzia sasa mali zote za TOT, zisajiliwe kwa jina la CCM na Kapteni Komba na Tumaini, warejeshe fedha zote walizopata kwa kuuza magari kinyume cha taratibu na chama kiwachukulie hatua za nidhamu.

Kwa mujibu wa mapendekezo hayo, lori aina ya Scania, ambalo Kapteni Komba anadai kuwa ni lake, kitengo cha maadili na usalama, kimeagizwa kichunguze zaidi kwa kuwahoji wahusika.

“Kuhusu magari ambayo kadi zake hazijulikani ziko wapi, CCM ichukue hatua za kufuatilia yalikonunuliwa na Kapteni Komba atakiwe kutoa maelezo na pia mali zote zilizoandikwa kwa jina la mmiliki Colleta Investment, zibadilishwe umiliki wake na kuwa chini ya CCM,” ilisema taarifa hiyo.

Akizungumza na Tanzania Daima, Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi wa CCM, Amos Makala, alikiri kupata ripoti hiyo, lakini akasema alikuwa bado hajaipitia, kwani wakati inatoka alikuwa masomoni nje.

Alisema hata hivyo ukaguzi uliofanywa ni utaratibu wa kila mwaka unaofanywa kwenye taasisi zinazopata ruzuku ya CCM, ikiwamo TOT.

Kwa upande wake Kapteni John Komba, alisema taarifa hiyo imejaa chuki na majungu na katika kuthibitisha hilo, Komba alisema binafsi hajaipata, lakini tayari vyombo vya habari vimesambaziwa ripoti hiyo.

Hata hivyo alisema kilichopo ndani ya ripoti hiyo, bado kinahitaji majibu kutoka kwake, ambayo atayawasilisha kwenye chama mara atakapopata ripoti hiyo.

“Mimi ni msafi, hakuna ufisadi hapa, hii ni chuki tu maana kama kungekuwa na ukweli, kwanini vyombo vya habari havijapewa taarifa za taasisi nyingine ambazo pia zinapata ruzuku ya chama?” alihoji.
 
Hawataweza kumchukulia hatua yoyote maana Komba meshakaa jikoni muda mrefu kiasi cha kujua dili nyingi za wakuu wake.
 
Unategemea nini kama ndiye mpiga kampeni wa mafisadi. Huyu anamjua fulani ni fisadi lakini anampigia kampeni as if yeye ni malaika. Watanzania tutumie nguvu ya umma kuirejesha nchi yetu
 
Ndani ya CCM hakuna wa kumnyoshea kidole mwenzake eti ni fisadi. CCM wote ni mafisadi hivyo watakuwa makini sana katika kulishughulikia suala la Kapten Komba ili kuepuka balaa zaidi kwani yeye pia anaujua ufisadi wa wanaCCM wenzake.
 
Sasa UFISADI unaanza kuwala CCM wenyewe, nadhani ni vizuri ili nao waone uchungu wa kuibiwa!! Hongera Komba ingawa hela uliyokula ni ndogo!! Wenzio wanakula mabilioni wewe unalamba ml 30 tu!! Lakini zinatosha kuwahonga kina Winnie Masanja..
 
Hawataweza kumchukulia hatua yoyote maana Komba meshakaa jikoni muda mrefu kiasi cha kujua dili nyingi za wakuu wake.

You can bet on it!Wakiona he is more than a threat watambalali mara moja tuu!
 
Hakuna mradi wa CCM au Jumuia zake unaoweza kuendeshwa kwa ufanisi bila kutafunwa! Mnaikumbuka SUKITA iliishia wapi? Mradi wa mabasi wa UVCCM? Mradi wa vijana hostel pale Kinondoni na bendi yake? Viwanja vya michezo vya CCM kule Kirumba Mwanza, Tabora, Songea.... vina hali gani? Halafu tunategemea Chama hikihiki kiongoze mapambano dhidi ya UFISADI?
 
Ndani ya CCM hakuna wa kumnyoshea kidole mwenzake eti ni fisadi. CCM wote ni mafisadi hivyo watakuwa makini sana katika kulishughulikia suala la Kapten Komba ili kuepuka balaa zaidi kwani yeye pia anaujua ufisadi wa wanaCCM wenzake.

komba atakuwa aliamua kujiudumia baada ya kugundua wenzake wana mtandao wanaitafuna EPA .......na mgao hawakumpa..akaona na yeye bora ale urefu wa kamba yake....yaani over all the monies kala hadi mirathi ya kina leyla khatib......ccm hawana dogo......

...saasa wamemkorofisha komba na uchaguzi tarime ndo huoo...nani ataenda kuimba kule..si unajuwa watu wanapenda kushangaa TOT..............HATAHIVYO I DOUBT KAMA TARIME WANABABAIKA NA TOT.......
 
Ufisadi TOT: CCM kwawaka moto

na Mwandishi Wetu
Tanzania Daima~Sauti ya Watu

SIKU moja baada ya kuwapo kwa taarifa za tuhuma za ufisadi ndani ya kikundi cha sanaa cha Tanzania One Theatre (TOT), kinachoongozwa na Kapteni John Komba, hali ya mambo katika Ofisi ndogo za Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), zilizopo jijini Dar es Salaam, si shwari baada ya chama hicho kuamua kusaka waliovujisha habari hizo.

Habari ambazo Tanzania Daima imezipata, zinasema kuwa hatua ya kuwasaka waliohusika na uvujaji wa taarifa hizo, imeungwa mkono na Katibu Mkuu, Luteni Yusuf Makamba.

Vyanzo vyetu vya habari kutoka katika ofisi hiyo, vinasema taarifa hizo ambazo bado zinachukuliwa kuwa ni tuhuma, zilifanywa kuwa ni za siri na ambazo zilikuwa zikisubiri hatua kutoka katika mamlaka za juu ndani ya chama hicho tawala.

Usiri kuhusu kuwapo kwa tuhuma hizo kunaelezwa kulikuwa kumesababisha hata Kapteni Komba mwenyewe kutokuwa na taarifa rasmi za kuwapo kwa tuhuma za namna hiyo dhidi yake.

"Kuna tatizo kubwa sasa ndani ya chama. Sasa hakuna tena siri, lakini pia inawezekana kuna chuki miongoni mwa viongozi na makada, kwani kulikuwa na taarifa nyingine za uchunguzi kutoka kwenye taasisi zinazopata ruzuku kutoka kwenye chama, lakini iliyochomolewa ni ile inayomhusu Komba," alisema ofisa mmoja wa juu wa chama hicho aliyezungumza na Tanzania Daima jana.

Katika hatua nyingine, wakati Kapteni Komba, akibebeshwa zigo hilo la tuhuma za ubadhirifu wa mamilioni ya fedha katika kikundi hicho, taarifa zinaeleza kwamba, Katibu Mkuu, Makamba ameshaanza kuchukua hatua ili kuepuka kile anachokielezea kuwa ni fedheha kwa chama kizima.

Taarifa za ndani zinaeelza kuwa, tayari Makamba ameshaandika dokezo kwenda kwa viongozi wa juu wa chama hicho akiwataka kuziangalia tuhuma hizo na kisha kuzishughulikia kwa taratibu za ndani ili kuepusha fedheha.

Katika dokezo hilo maalumu la Makamba ambalo Tanzania Daima imeliona, linasema kudhalilika kwa Kapteni Komba ni sawa na kudhalilika kwa chama.

Sehemu ya dokezo hilo, inasomeka kuwa: "Kwa kuwa Komba ni mwenzetu sana na kudhalilika kwake ni kudhalilika kwa chama, naleta kwako kwa maelekezo na tafakuri hadi hapo uamuzi wa kuchukua hatua utakapokubalika."

Akizungumza na Tanzania Daima kwa njia ya simu jana, Makamba hakutaka kukubali wala kukataa kuandika dokezo hilo zaidi ya kusema kuwa alikuwa katika hospitali moja mkoani Tanga, akimuuguza mama yake.

"Hizo habari una uhakika gani kama ni sahihi? Mimi niko hospitali namuuguza mama yangu," alisema Makamba na kukata simu.

Taarifa za kumhusisha Kapteni Komba katika tuhuma za ubadhirifu wa mamilioni ya fedha zinazozidi sh milioni 30 ndani ya TOT zimo katika taarifa ya ukaguzi maalumu, uliofanywa na kitengo cha ukaguzi cha CCM, kwa maagizo ya Katibu Mkuu, Makamba kutokana na tuhuma zilizowasilishwa kwake.

Ukaguzi huo, ulifanyika kuanzia Machi 3 hadi 16 mwaka huu na baadaye Aprili mosi hadi 6 na taarifa yake ikawasilishwa rasmi kwa Makamba Aprili 22 mwaka huu.

Katika taarifa hiyo ya uchunguzi ambayo Tanzania Daima imeiona, Komba anahusishwa na ulaji wa sh milioni 30 za mishahara ya wafanyakazi TOT ya miezi 14.

Uchunguzi huo unaonyesha pia kuwa, ulaji huo unatokana na kiasi cha sh 37,442,923 ambazo CCM ilizitoa kwa ajili ya kulipa malimbikizo ya mishahara ya miezi 14 ya wafanyakazi wa TOT, kuanzia Julai 2006 hadi Agosti 2007 kwa awamu.

Taarifa zinaeleza kuwa uchunguzi uliofanywa ulibaini kuwa kiasi ambacho kililipwa ni shilingi milioni sita, na hivyo kuacha fedha nyingine kwenda kusikojulikana.

"Ukaguzi umebaini kuwa, CCM ilitoa sh milioni 37.4 kwa ajili ya kulipa malimbikizo ya mishahara ya miezi 14 kuanzia Julai 2006 hadi Agosti kwa awamu mbili.

"Malipo ya awamu ya kwanza yalifanyika 21/ 11/ 2007 kwa hati ya malipo namba 056996 ya sh 18,532,458 na tarehe 21/12/2007 hati ya malipo namba 1343, sh 18,910,465, jumla ni sh 37,442,923," ilisema taarifa hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Kapteni Komba pamoja na ofisa mwingine wa kikundi hicho, bado wanadaiwa malimbikizo ya sh 30,514,625.

"Ukaguzi uliona orodha ya majina waliyosanishwa watumishi hao wa TOT kwa miezi miwili, jumla ya sh 6,928,298, watumishi waliulizwa na ukaguzi, walithibitisha walilipwa malimbikizo ya miezi miwili tu," ilisema taarifa hiyo.

Pia viongozi hao wa TOT, wanahusishwa na udanganyifu wa kulipa warithi wa marehemu wasio waasisi wa chama jumla ya sh milioni 27.3, lakini baadhi ya waliotajwa kwenye orodha ya malipo, wamekana kupewa fedha zozote.

Kwa mujibu wa dokezo lililosainiwa na kiongozi mmoja wa TOT (si Komba), linaonyesha jina la marehemu la mrithi na kiasi cha pesa alicholipwa.

Dokezo hilo linaonyesha kuwa, marehemu Godfrey Lugendo, mrithi wake Mwantumu Haji, alisaini sh milioni 4,320,000, marehemu Leyla Khatibu, mrithi wake Monica Robert, alisaini sh 6,750,000, Fred Mshana, mrithi wake Benson Mshana, alisaini sh 4,880,000, Hamimu Hemera, mrithi wake, Mwanakombo Ahamed, alisaini sh 4,240,000 na Salum Poogwe, mrithi wake Nuru Salum, alisaini sh 7,200,000 na hivyo kufanya kiasi cha fedha zote zilizolipwa kwa ajili ya warithi hao kufikia sh 27,200,000, jambo ambalo uchunguzi umebaini kwamba si la kweli.

Madai mengine anayotuhumiwa nayo Komba ni kuwapunja wafanyakazi wa TOT kwa kuwalipa posho ya sh 20,000 kwa siku wanapokuwa nje ya Dar es Salaam badala ya sh 40,000 zinazotolewa na chama.

Taarifa hiyo inasema wasanii wa TOT wanaposafiri kwa shughuli za chama, viongozi wanne hulipwa sh 40,000 kwa siku na waliobaki hulipwa sh 30,000.

Hata hivyo, Kapteni Komba, alisema taarifa hiyo imejaa chuki na machungu na katika kuthibitisha hilo, alisema binafsi hajaipata na kueleza kushangazwa kwake na taarifa hiyo kufikishwa kwenye vyombo vya habari kabla ya hata mwenyewe kuiona.
 
Kumbe na taasisi nyinmgine ndani ya ccm nazo kuna ulaji? Kumbe wanachunguzana? Mbona hawakulisema hili wakatiw a NEC? Kama alivyosema Komba, nadhani kuna njama za kuchafuana, vita vya wenyewe kwa wenyewe ndo inaanza sasa, tusubiri mengine mengi
 
Back
Top Bottom