Kisanga kipya chamkuta Waziri Ngeleja D`Salaam

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,268
33,040
15th July 2009








headline_bullet.jpg
Wananchi wavamia mkutano wake
headline_bullet.jpg
Wataka kujua fidia yao itatoka lini
headline_bullet.jpg
Akatiza hotuba, kusikiliza kilio chao



Ngeleja1.jpg

Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja.



Shughuli ya uzinduzi wa mtambo wa kusindika gesi ya asilia wa kampuni ya Pan African Energy, ambayo mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja jana iliingia dosari, baada ya wakazi wa Ubungo maziwa jijini Dar es Salaam kuvamia walishinikiza kulipwa fidia ya kuhamishwa eneo hilo.
Wakazi hao wanaotoka kaya 137 walivamia eneo hilo wakiongozwa na mwenyekiti wao wa serikali ya mtaa, Jovin Ndimbo.
Waziri Ngeleja alifika katika hafla hiyo saa tano asubuhi na wakati akiwa amekaa meza kuu, ghafla wakazi hao walitinga eneo hilo na kuzua tafrani ambapo waandishi wa habari walilazimika kutoka nje ili kwenda kusikiliza kilio cha wakazi hao.
Wakazi hao walisema kuwa wamechoka kusubiri ahadi ya serikali tangu mwaka 2004 walipoahidiwa kulipwa fidia ili kuhama eneo hilo kwa ajili ya kupisha uwekaji wa mitambo ya gesi.
Eneo hilo lipo jirani na mitambo ya gesi ya Songas, Aggreko na Pan African.
Mwenyekiti wa serikali ya mtaa huo, Ndimbo, alisema gharama ya kuwalipa fidia ya mwaka 2004 zilikuwa ni Sh. bilioni 2.2 na kuongeza kuwa kwa sasa fidia hiyo itakuwa imepanda mara tatu.
Ndimbo alisema kutokana na ahadi hiyo ya serikali, hivi sasa wananchi hao wameshindwa kufanya kitu chochote, ikiwemo kuendeleza maeneo yao kwa kuwa bado wanasubiri kulipwa.
Wananchi hao walifika na mabango yaliyokuwa yameandikwa maneno ya malalamiko dhidi ya serikali na Ngeleja. Baadhi yalisomeka hivi:
“Mheshimiwa tangu ukiwa naibu waziri, leo waziri, hutukuoni. Songas sisi, Aggreko sisi na gesi asili sisi. Tutaponaje?”
Mengine yalisomeka kuwa: “Mheshimiwa Waziri sikiliza kilio chetu, Ubungo Maziwa tunateketea, nini hatma yetu?”
Wananchi hao walisema wanapata matatizo mengi kwa kuishi eneo hilo lenye mitambo hatari ya gesi yakiwemo makelele pamoja na kuishi kwa kuogopa kwani ikitokea ajali ya moto wanaweza kupoteza maisha.
Waziri baada ya kuona wananchi hao hawana mpango wa kuondoka, akaona hakuna jinsi ila dawa ni kwenda kuwasilikiza ndipo alipotoka nje na kuwasikiliza.
Hata hivyo, licha ya Waziri Ngeleja kuwapa majibu ya matumaini huku akijitetea kwamba serikali itawalipa, lakini wao waligoma na kusisitiza kwamba serikali inawadharau kwani kilio chao ni cha muda mrefu na kwamba inafanya makusudi kwa kukataa kuwalipa.
Ngeleja aliwaambia kuwa serikali inajua saula hilo, lakini akasema hawezi kutamka ni lini itawalipa fidia hiyo, badala yake aliwaomba waendelee kuvuta subira.
Baada ya kusikia majibu hayo wananchi hao hawakuridhika tena na walichachamaa mbele ya Ngeleja na kutoa maneno makali.
Baadhi ya kauli walizotoa mbele ya waziri ni pamoja na kumwambia kwamba uchaguzi ujao mwaka 2010 hawampi kura mbunge wao wa sasa, Charles Keenja, kwa kuwa ameshindwa kwenda katika eneo hilo kufuatilia matatizo yao. Keenja ni Mbunge wa Ubungo (CCM).
Walidai kuwa mwakani watamchagua aliyekuwa mgombea wa kiti hicho mwaka 2005 kwa tiketi ya Chadema, John Mnyika, badala ya Keenja kwa kuwa hakuna kitu anachowasaidia.
Majibizano kati ya Ngeleja na wananchi hao yalidumu kwa takribani dakika 10 kabla ya kukubali kuondoka kwa shingo upande.
Wiki chache zilizopita, Ngeleja alikumbwa na matata mengine wakati alipoandamana na kamati ya wabunge iliyokwenda Tarime kuchunguza madai ya mgodi wa North Mara, kumwaga kemikali za simu katika mto ambao wananchi wanatumia maji yake kwa mahitaji ikiwemo kunywa na kupikia. Wananchi walimlalamkia kwa kutoonekana kutatua tatizo lao licha ya kumfikishia malalamiko.
Kadhalika, wakati wa kampeni za jimbo la Busanda waziri Ngeleja aliripotiwa kuandamwa na wachimbaji wadogo wadogo waliohoji ahadi za kupata maeneo ya kuchimba.
Kuhusu mradi wa Pan African Energy, imeelezwa kwamba Awamu ya kwanza ya mradi huo imegharimu dola za Marekani milioni tatu ambapo nyumba 30,000 jijini Dar es Salaam zitaunganishwa ili zitumie gesi hiyo.
Aidha, magari 8,000 yanatarajia kubadilishwa ili yatumie gesi asili kutoka mradi huo badala ya mafuta.
Ngeleja alisema serikali imepata mapato ya dola za Marekani milioni 74.3 kwa kuuza gesi ya asili na kuongeza kuwa imeokoa kiasi cha dola za Marekani bilioni 1.91 ambazo zingetumika kama wananchi wangetumia mafuta ya kawaida.
:: IPPMEDIA
 
Tanzania wawekezaji ni muhimu kuliko wananchi,hii nimbaya sana.sijui kama watalipwa inabidi wananchi wawe ngangali kwenye kupata haki.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom