Kinara wa ufaulu Chuo Kikuu Dar es Salaam 2010

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
SALOME Maro ni miongoni mwa wanawake wanaodhihirisha kwa vitendo ule usemi usemao, “mwanamke akiwezeshwa anaweza.”

Amedhihirisha kwa kuongoza kwa ufaulu miongoni mwa wahitimu zaidi ya 3,000 wa Shahada ya Kwanza katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam waliohitimu masomo yao na kufanyiwa mahafali Novemba 27, mwaka huu.

Salome, licha ya kusoma masomo magumu ya Sayansi ya Kompyuta, ameweka rekodi ya kuwa Mwanafunzi Bora wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa mwaka huu, kutokana na kufaulu kwa Daraja la Kwanza akipata pointi 4.7 kati ya 5 katika masomo.

Mafanikio yake katika masomo yalimwezesha kutambulishwa katika mkutano wa jumuiya ya wahitimu wa chuo hicho kikongwe kupongezwa na viongozi mbalimbali mashuhuri akiwamo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Akielezea mafanikio yake, Salome anasema hakuwa na lolote la ajabu zaidi ya kujitahidi kuwa makini na kuhakikisha kuwa anazingatia ratiba pasipo kukosa vipindi bila sababu maalumu.

Anasema alijiwekea mikakati ya kuhudhuria vipindi vyote kwa ukamilifu, yaani bila kuchelewa wala kutoka kabla ya kipindi hakijamalizika.

Hata pale alipolazimika kukosa kipindi, aliwasiliana na wenzake na kumfahamisha walichofundishwa kisha kuingia maktaba na kuchimbua zaidi juu ya somo hilo.

Pia alijiwekea ratiba binafsi ya kujisomea ambapo alisoma kwa wastani wa saa mbili kila siku kuanzia saa mbili hadi saa nne usiku.

Anasema kuwa, wakati wa majaribio na mitihani alikuwa anasoma kwa wastani wa saa tatu, kisha kupumzika ili kuepuka kuingia kwenye mitihani akiwa amechoka.

Anasema siri kubwa ya mafanikio ya kufaulu ni kujumuika na wenzake na kujadiliana juu ya masomo na kushirikiana kujibu mitihani iliyofanywa na wanafunzi waliowatangulia.

Baada ya Salome kutangazwa kuwa Mwanafunzi Bora wa Kike wakati wa mafahali ya 40 ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, baadhi ya watu walisikika wakisema huenda alikuwa akisoma muda wote na hakuwa na muda wa kupumzika wala kujichanganya na wenzake.

Hata hivyo Salome anasema anapata muda wa kupumzika, kujichanganya na wenzake pia kwenda katika maduka ya urembo ikiwa pamoja na saluni kwa ajili ya kujiremba.

“Kwa kweli nilipata muda wa kupumzika kwa kuwa sikuwa nasoma kila siku…pia nilitenga muda wa kwenda saluni angalau mara moja kwa wiki,” anasema na kuongeza kuwa, alikuwa pia anapata muda wa kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii na kushika nafasi mbalimbali za uongozi ikiwa ni pamoja na kusimamia mawasiliano ya ndani na nje ya umoja wa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wa Teknolojia ya Habari maarufu kwa jina la ITSADU.

Kwa kuwa Salome ni miongoni mwa kizazi cha jamii ya habari na mawasiliano, anapata muda wa kutosha kuwasiliana na kubadilisha mawazo na vijana sehemu mbalimbali duniani kwa kutumia mawasiliano ya kompyuta na hata simu yake ya mkononi.

Salome anasema, wanafunzi wanaotaka kufuata nyao zake na kufaulu kwa kiwango cha juu ni lazima wajiwekee mikakati ya kuhudhuria vipindi vyote.

“Mimi naona ili mwanafunzi aweze kufaulu ni muhimu ahudhurie vipindi…lakini nasikitika kusema kuwa niliona wanafunzi wengi wanatega vipindi hasa vile vya asubuhi sana au usiku,” Salome anasema.

Anataja jambo la pili lililomwezesha kufaulu kwa kiwango cha juu ni kujipangia muda wa kutosha kufanya mazoezi ya darasani ili kupata alama nzuri ambazo zinachangia katika matokeo ya mitihani ya mwisho.

Anataja jambo la tatu ni kuwa na nyenzo za kujifunzia, kwani alifanikiwa kumiliki kompyuta alipokuwa muhula wa pili mwaka kwanza wa masomo yake.

Anaeleza kuwa ni muhimu kwa mwanafunzi wa Sayansi ya Kompyuta kumiliki kompyuta kwa sababu inasaidia kufanya mazoezi kwa vitendo na kugundua vitu vingi na kuongeza uelewa.

Anasisitiza kuwa, mawasiliano ya kompyuta ni mazuri, lakini ni lazima yafanyike kwa kiwango fulani ili kuepuka kujitenga na jamii inayokuzunguka.

Anasema alitenga muda maalumu ili kuepukana na athari za matumizi ya kompyuta, akiamini kama angeganda mbele ya kifaa hicho, mwisho wa siku angeweza kujikuta bila marafiki wa kuonana nao, kula nao au kunywa pamoja.

Anasema kuwa watu wenye tabia ya kutumia kompyuta kwa muda mrefu bila kuwasiliana na watu wengine wanaomzunguka wanaweza kujitenga na jamii inayomzunguka na hatimaye kuchanganyikiwa.

Hivi sasa Salome ameajiriwa na Kampuni ya Sigara, Idara ya Habari na Mawasiliano ambayo inajumuisha wataalamu wa kompyuta.

Anasema anategemea kufanya kazi kwa muda ili aweze kupata uzoefu kisha kurudi shule kuisaka elimu ya juu zaidi.

Salome ambaye ni mtoto wa pili kwenye familia ya watoto wanne wa Mzee Honest Philip Maro alizaliwa Machi mwaka 1987, yaani miaka 23 iliyopita jijini Dar es Salaam.

Elimu ya Msingi aliipata katika shule mbalimbali kwa sababu baba yake alikuwa akihamishwa kikazi.

Alisoma darasa la kwanza mwaka 1993 katika shule ya msingi Town School Shinyanga na darasa la pili katika Shule ya Msingi ya Kambarage iliyopo Shinyanga.

Amesoma darasa la tatu hadi la nne katika Shule ya Msingi Mwenge iliyopo Kinondoni, Dar es Salaam na hatimaye akahamia Shule ya Msingi ya St. Marys ambapo alilazimika kurudia darasa la tano ili aweze kujiimarisha kwa mujibu wa viwango vya shule hiyo.

Hata hivyo, alikuwa na uwezo mkubwa wa kumudu masomo hivyo alipofika darasa la sita aliandaliwa kuingia kidato cha kwanza na kufanikiwa kuruka darasa moja.

Mwaka 2001 alifanikiwa kujiunga na shule ya Sekondari ya St. Mary’s High School na kuhitimu kidato cha nne 2004.

Anasema wakati akiwa sekondari aliamua kujikita katika masomo ya sayansi akiwa na ndoto ya kuwa rubani wa ndege za abiria, hasa zinazofanya safari za kimataifa.

“Nilipokuwa msichana mdogo nilikuwa na ndoto ya kuwa rubani…ingawa nilibaini kuwa watu wengi wanadhani wasichana hawawezi masomo ya sayansi niliamini nitaweza,” anaeleza.

Anafahamisha kuwa katika mitihani ya taifa ya kidato cha nne alifaulu kwa kupata daraja la kwanza na pointi 15.

Mwaka 2005 alijiunga na kidato cha tano katika Shule ya Loyola High School na kuchukua masomo ya mchepuo wa Sayansi ya Fizikia, Kemia na Hisabati (PCM).

Kwa kutambua kuwa kumcha Mungu ni chanzo cha maarifa, Salome alisoma pia somo la dini ili aweze kuishi katika maadili mema na kumtambua Mungu hata katika ulimwengu wa sayansi.

Akafanikiwa kuhitimu Kidato cha Sita mwaka 2007 ambapo alikuwa miongoni mwa wanafunzi waliong’ara kwa kufaulu vyema mitihani ya taifa ya kidato hicho kwa kupata alama 9, akifaulu kwa kiwango cha Daraja la Kwanza.

Anafahamisha kuwa siri ya mafanikio yake ni msingi imara aliojijengea akiwa shuleni Loyola ambapo walimu na uongozi wa shule ulikuwa karibu na wanafunzi kwa kuwapatia ushauri na hamasa ya kuisaka elimu bila kuchoka.

“Maisha ya shule yalikuwa mazuri na Loyola ni shule nzuri…tulikuwa tukipata ushirikiano mzuri kwa walimu, na uongozi mzima hivyo tulijenga moyo wa kusoma kwa bidii na kwa makini zaidi,” anaeleza.

Anasema tofauti na malalamiko anayosikia kuhusu ukosefu wa vitabu katika shule nyingine alibahatika kusoma shule zenye maabara na vitabu vya kutosha.

“Ingawa nilijitahidi kusoma kwa bidii na nilipenda kuona miujiza inayofanywa na kompyuta ndoto yangu ya kwanza ilikuwa kurusha ndege baada ya kusomea urubani,” anaeleza.

Anasema alifanikiwa pia kujifunza maisha ya kujiamini na kujitegemea kwa sababu alilazimika kujiunga na wasichana wenzake na kupanga katika hosteli ambayo haisimamiwi na shule.

Yeye na wenzake waliweza kujisimamia wenyewe na kuepuka vishawishi vya wanaume walaghai.

“Mwongozo wa walimu na wazazi ulituwezesha kuwa na msimamo na kusema hapana pale tulipokutana na vishawishi, hivyo naamini kuwa walimu na wazazi wakiwa karibu na wanafunzi wanaokaa hosteli nje ya shule itasaidia kujenga msingi imara kwa watoto wa kike,” Salome anasema.

Baada ya kuhitimu kidato cha sita, anasema alihangaika bila mafanikio kutafuta shule ya urubani, ndipo akajikuta akiangukia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

“Kusoma chuo kikuu lilikuwa chaguo la pili, namba moja kwangu ilikuwa urubani…hivyo baada ya kukosa chuo nilituma maombi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na nilifanikiwa kupata nafasi mwaka 2007,” anasema na kuongeza: “Miaka mitatu ya maisha yangu ya chuo yalikuwa ya furaha sana nilikutana na marafiki wengi, nikajifunza mengi ya kijamii na kimasomo sikutoa nafasi matatizo ya chuo kuwa sehemu ya maisha yangu.”

Hata hivyo anasema alikumbana na changomoto mbalimbali hususani upungufu wa kompyuta za kufanyia mazoezi.

Anasema pamoja na uhaba wa kompyuta hakukutana na vitendo vyovyote vinavyombagua mtoto wa kike. “Sikukutana na ubaguzi dhidi ya wanawake wala upendeleo wowote….wanafunzi wote walipewa fursa sawa,” anafahamisha.

Ili kuweza kukabiliana na changamoto za maisha ya chuo alifanikiwa kumiliki kompyuta mara alipoingia mhula wa pili.

Anasema ingawa alifaulu vizuri, alizingatia ratiba ya kawaida iliyotolewa na uongozi wa chuo. “Ushauri wangu kwa wanafunzi ni kuwa na malengo, waweke shule mbele na mambo mengine ndo yafuate, kwa sababu naamini mtu ukisoma inavyotakiwa ni rahisi kufaulu.

Anaiomba serikali, ijitahidi kuboresha miundombinu ya chuo kwa kuwa mabweni hayatoshi, wanafunzi wanateseka, pia iboreshe mfumo wa mikopo watu wapate mikopo kwa wakati muafaka.

Salome anasema mafanikio aliyopata yanatokana pia na msaada kutoka kwa ndugu, jamaa na marafiki na hasa wazazi wake ambao walifanikiwa kumpeleka katika shule zenye msingi mzuri wa elimu.

“Nawashukuru wazazi wangu kwa kunipeleka shule nzuri na kufuatilia kwa karibu mwenendo na maendeleo yangu kisha kunisaidia kila nilipokutana na changamoto mbalimbali,” anaeleza.

Anasema dada zake watatu wamechangia kwa kiasi kikubwa kuwezesha kukamilisha ndoto yake kwa kuwa walimpa moyo wa kuchukua masomo ambayo yanamwezesha kuidhihirishia jamii kuwa watoto wa kike wakiwezeshwa wanaweza.

Salome anapenda kuogelea, kujumuika na marafiki, kuwasiliana kwa kutuma ujumbe mfupi kwa kutumia simu na kompyuta. Pia anapenda kusoma vitabu vya ziada, kusafiri na kujifunza mambo mbalimbali.

Huyo ndiye Salome Maro, msichana aliyepata mafanikio zaidi kimasomo miongoni mwa wahitimu wa Shahada ya Kwanza katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Hakika ni mfano wa kuigwa kwa wasichana wengine, kwani mbali ya kuyavaa masomo ya Sayansi yanayoogopewa na wengi, ameweza pia kuwaburuza hata wanaume kimasomo.
 
Halafu kozi ya kompyuta sio sawa na Education wala fine arts ambayo niliisoma mimi.Yeye ni kinara wa kozi ya kompyuta na siyo vinginevyo. Lakini nampongeza kwa kufanya vizuri masomo yake. Tutegemee kuona anaongeza thamani na siyo kutuionyesha jinsi madesa yalivyo ya muhimu.
 
Halafu kozi ya kompyuta sio sawa na Education wala fine arts ambayo niliisoma mimi.Yeye ni kinara wa kozi ya kompyuta na siyo vinginevyo. Lakini nampongeza kwa kufanya vizuri masomo yake. Tutegemee kuona anaongeza thamani na siyo kutuionyesha jinsi madesa yalivyo ya muhimu.

HV MPAKA CHUO udsm WANADESA?
 
it is very nice...many congrats for her...hivi kumbe alikuwa anasoma mitihani ya nyuma ili ajue namna ya kujibu mitihani. inawezekana kabisa alikuwa ni bingwa wa kusomea mitihani na siyo bingwa wa ubunifu katika fani yake...huo ni mtazamo wangu tu masela, msijenge chuki.
 
Sina hakika na chanzo cha habari yako, mimi ni moja ya wahitimu wa mwaka huu na aliyetangazwa mwanafunzi bora kwa maana ya GPA ni MARTIN CHEGELE. Huyu alikuwa Tanzania One form4 na mwaka 2007 alikuwa Tanzania one form 6. Labda kama huyo dada aliongoza kwa kozi yake na si chuo kizima mkuu.
 
"....licha ya kusoma masomo magumu ya Sayansi ya Kompyuta...."

Masomo gani ni rahisi?
 
Nmpongeza sana Salome ila nimeshangaa huyo binti ameamua kufanya kazi sigara badala ya kufundisha
 
Sina hakika na chanzo cha habari yako, mimi ni moja ya wahitimu wa mwaka huu na aliyetangazwa mwanafunzi bora kwa maana ya GPA ni MARTIN CHEGERE. Huyu alikuwa Tanzania One form4 na mwaka 2007 alikuwa Tanzania one form 6. Labda kama huyo dada aliongoza kwa kozi yake na si chuo kizima mkuu.

This guy is good.
Looks retarded,not so social but insanely intelligent.
But whether the source is true or not,Salome is definitely smart and driven...that GPA seem very much her.
 
Computer science ni kati ya kozi rahisi sana kwani vitu vipo direct haviitaji uchambuzi sana wala ulinganifu kama masomo mengine mfano uchumi, sheria etc. Tatizo ni lile lile watanzania kuogopa Science. Pili ukiweza kusolve past papers (MADESA) za miaka 5 na kwa mfumo wetu wa semester lazima mitihani hutoka humo humo jinsi ilivyo. Hata hivyo kwa perfomance yake anastahili pongezi.
 
This guy is good.
Looks retarded,not so social but insanely intelligent.
But whether the source is true or not,Salome is definitely smart and driven...that GPA seem very much her.
Siku zote........ shule ipo invesare proposheno na sosho laifu................. Jaribu kuwatafakari vipanga wote unaowafahamu na uangalia how were they socially................
 
Congratulations sister. Wadau mnasema kadesa p'papers, mbona wengine wanadesa ila hawafiki hilo daraja. Ana uwezo, tumpe hongera zake ili na wengine wafuate huo mwenendo hasa Dada zetu. Heko SALOME,
 
Halafu kozi ya kompyuta sio sawa na Education wala fine arts ambayo niliisoma mimi.Yeye ni kinara wa kozi ya kompyuta na siyo vinginevyo. Lakini nampongeza kwa kufanya vizuri masomo yake. Tutegemee kuona anaongeza thamani na siyo kutuionyesha jinsi madesa yalivyo ya muhimu.

Acha wivu wewe,umeambiwa ni "KINARA" wa wahitimu wote tatizo lako nini?
kakufunika au?
mpe salut yake bana
 
sina hakika na chanzo cha habari yako, mimi ni moja ya wahitimu wa mwaka huu na aliyetangazwa mwanafunzi bora kwa maana ya gpa ni martin chegele. Huyu alikuwa tanzania one form4 na mwaka 2007 alikuwa tanzania one form 6. Labda kama huyo dada aliongoza kwa kozi yake na si chuo kizima mkuu.

kaongoza chuo kizima,bisha shauri zako ila ndo ukweli huo,swallow it
 
Tumpe hongera zake kwani kaonesha uwezo, gender si issue kwenye mafanikio....cha msingi ni committment!
 
What is the issue here. Je hakuna mwanamke aliyewahi kupata point 4.7 tangu chuo kianze, ameongoza kwenye kozi yake au ameongoza chuo kizima? Nyie watoto mliomaliza mwaka huu tuambieni basi, naona mnabishana wenyewe mara martin mara salome
 
Back
Top Bottom