BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,792
- 287,994
Date::2/25/2009
Kikwete asema mfumo wa uchumi kimataifa unainyonya Afrika
Na Mwandishi Wetu
Mwananchi
Kikwete asema mfumo wa uchumi kimataifa unainyonya Afrika
Na Mwandishi Wetu
Mwananchi
RAIS Jakaya Kikwete amesema mfumo na taratibu kwenye ngazi ya kimataifa lazima zibadilike, ili kutoa nafasi kwa wakulima wa mataifa masikini waweze kushindana na wakulima ambao wanapewa ruzuku wa nchi tajiri na kwa namna hiyo kutoa nafasi ya kuendelea kwa Afrika na Tanzania kwa ujumla.
Hayo aliyasema na kunukuliwa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, alipokuwa akijibu swali kutoka kwa mwanafunzi mmoja ambaye alitaka kujua kwa nini Bara la Afrika limebaki nyuma kwa maendeleo, na kwa nini kasi yake ya kuendelea ni ndogo.
Nchi za Ulaya zinatoa ruzuku ya kiasi cha dola za Marekani bilioni 365 kwa mwaka kwa wakulima wao. Wakulima wetu hawawezi kushindana na wakulima ambao wanapewa ruzuku ya namna hii. Ndiyo maana tunasema kuwa mfumo na taratibu kwenye ngazi ya kimataifa lazima zibadilike, ili kutoa nafasi kwetu kuendelea,alisema.
Rais Kikwete alisema kuwa sababu hiyo pamoja na mfumo wa sasa wa kimataifa usiokuwa wa haki wa uchumi na biashara, wenye kuzipendelea nchi tajiri, zimechangia kwa kiasi kikubwa kudumaza maendeleo ya Afrika.
Mataifa yote duniani, wakati mmoja ama mwingine wa historia, yalikuwa masikini. Kuna sababu nyingi za hali ya sasa ya Afrika kubakia nyuma na moja ya sababu hizo ni ukoloni ambao uligeuza Bara hili kuwa chimbuko la malighafi na soko la bidhaa kwa ajili ya nchi tajiri zilizotutawala,alisema.
Alisema maendeleo ni mchakato na kwamba , hayawezi kuja ghafla kama ndoto, na kufafnua kwamba Afrika iko nyuma siyo kwa sababu uongozi mbovu bali nimfumo.
Haiwezekani kuwa uongozi wa nchi zote 54 za Afrika hauna uwezo. Unahitaji mfumo wa uchumi wa kimataifa wa haki na hili ndilo jambo tumelizungumza miaka mingi tangu wakati wa mazungumzo ya Uruguay na sasa tuko Doha.
Tunasema kuwa wakulima wote hawawezi kutoka kwenye umasikini wakati wanazuiliwa kuuza mazao yao kwa bei nzuri na za haki duniani kwa sababu ya nchi tajiri kulinda masoko yao kwa kutoa ruzuku kwa wakulima wao, alisema Rais na kuongeza.
Maendeleo ni mchakato, tena mgumu. Huwezi kuamka asubuhi moja na kujikuta tayari , Rais Kikwete aliliambia kundi la wanafunzi kutoka Tanzania na Ujerumani wakati alipokutana na kuzungumza na wanafunzi hao jana, Ikulu, Dar es Salaam.
Kundi hilo la wanafunzi 25 kutoka nchi za Tanzania, Ujerumani, Kenya, Ethiopia, Mauritius, Uganda na Rwanda linashiriki katika mpango wa kubadilisha uzoefu kati ya wanafunzi wa Afrika na Ujerumani wa Go Africa, Go Germany unaodhaminiwa na Rais wa Ujerumani, Horst Kohler.
Katika mazungumzo hayo na wanafunzi hao, Rais pia alijadili kuhusu uundwaji wa Serikali ya Afrika, mchakato wa kuunganisha uchumi wa nchi za Afrika Mashariki chini ya Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC), nafasi ya suala zima la ardhi katika ushirikiano wa EAC, na mikopo ya kugharimia elimu ya juu nchini.
Alipoulizwa na mwanafunzi kutoka Ujerumani kuhusu ni nini anadhani ni changamoto kuu kuliko zote ambayo inaikabili Tanzania kwa sasa, Rais Kikwete bila kusita alijibu, umasikini, na kuendelea kufafanua umuhimu wa kuongeza uzalishaji katika kilimo kama njia kuu ya kuwatoa wananchi walio wengi katika umasikini kwa haraka zaidi.