Kikwete amtosa Warioba

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
Na Saed Kubenea
MwanaHALISI


CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimemtosa Jaji Joseph Warioba. Kimekana kumiliki kampuni ya CCM Trust ambayo imekuwa ikitajwa kumilikiwa na chama hicho kikongwe cha siasa nchini. CCM Trust ni moja ya makampuni manne yanayounda kampuni ya Mwananchi Trust Limited yenye hisa katika kampuni ya Mwananchi Gold Limited (MGL) ya Dar es Salaam.

CCM imekana pia kumiliki Mwananchi Trust ambayo ni mbia katika Mwananchi Gold Limited. Warioba ndiye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya MGL.

Gazeti hili lina taarifa kwamba CCM imekana kumiliki makampuni hayo mawili – Mwananchi Trust na CCM Trust na imeanika orodha ndefu ya makampuni yake.

Wachunguzi wa mambo wanasema hatua hiyo inamweka pabaya Warioba kwani amekuwa akidai kampuni hiyo inamilikiwa na chama tawala.

Taarifa kutoka serikalini zinasema baadhi ya viongozi wa ngazi ya juu wa CCM tayari wamehojiwa na vyombo vya dola nchini kuhusiana na umiliki wa CCM Trust, Mwananchi Trust na kampuni mwavuli ya Mwananchi Gold Limited.

Kupatikana kwa taarifa za hatua hiyo ya CCM kumekuja takriban wiki mbili tangu Warioba atuhumu Rais Jakaya Kikwete kuingilia mkondo wa mahakama, hasa katika kesi zinazohusu ukwapuaji wa mabilioni ya shilingi kutoka Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

MwanaHALISI limegundua kuwa waraka wa CCM unaokana kampuni ya Warioba ulijadiliwa katika kikao cha Kamati Kuu (CC) ya chama hicho, tarehe 2 na 3 Mei mwaka huu.

Waraka huo wenye kurasa 22 unaitwa, “Mkakati wa Chama Cha Mapinduzi kujiimarisha kiuchumi mwaka 2009 – 2012” na kampuni ya CCM Trust haionyeshwi kuwa mali ya CCM.

Kikao cha CC kilichojadili mkakati wa CCM kilifanyika Ikulu, Dar es Salaam, chini ya uenyekiti wa Rais Kikwete.

Tarehe 13 Januari mwaka huu, Jaji Warioba alinukuliwa na waandishi wa habari ofisini kwake Masaki, Dar es Salaam, akisema kuwa Kampuni ya Mwananchi Trust inamilikiwa na CCM na kwamba ina hisa 15.

Mwananchi Trust ina hisa katika Mwananchi Gold Limited ambayo anaongoza Warioba na ambayo imekuwa ikituhumiwa kutumia vibaya mabilioni ya shilingi kutoka BoT. Fedha hizo zililenga “kusaidia wachimbaji wadogo” wa dhahabu nchini.

Kwa mujibu wa nyaraka za Wakala wa Usajili wa Makampuni na Biashara (BRELA), wenye hisa katika Mwananchi Gold Limited ni BoT yenye hisa 500, Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) lenye hisa 375 na Chimera Company Limited, ya anayetajwa kuwa “raia” wa Italia, yenye hisa 500.

Taarifa zinaonyesha kuwa kampuni ya CCM Trust inamilikiwa na Jaji Warioba na Yusuf Mushi. Pamoja na kuwa mwenyekiti wa bodi MGL, Warioba pia ana hisa katika kampuni hiyo.

Hisa za Warioba katika MGL zinapitia kampuni ya familia yake inayoitwa Umoja Entertainment Limited (UEL).
Nayo kampuni ya Mwananchi Trust inabeba hisa za Vulfrida Mahalu kupitia kampuni ya VMB Ltd.; Yusuf Mushi kupitia kampuni ya Y.M. Limited na CCM Trust.

Warioba alipoombwa na gazeti hili kufafanua juu ya CCM kukana kampuni ya Mwananchi Trust na CCM Trust alisema, “No comment” (Sina la kusema). Aliendelea kusema, “Ninyi andikeni wanayosema, lakini kwangu mimi, no comment.”

Awali Warioba alimwambia mwandishi kuwa madai juu ya makampuni hayo aliishayajibu mara nyingi na kuuliza, “Kuna nini?”
Hadi sasa Rais Kikwete hajasema lolote juu ya Warioba na makampuni husika; bali wiki mbili zilizopoita, rais alisema kesi tatu kubwa za ufisadi zitafikishwa mahakamani. Haijulikani iwapo katika hizo kuna inayomhusu Warioba.

MwanaHALISI liliwasiliana na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba juu ya suala hilo; naye alisema si Mwananchi Trust wala CCM Trust kuwa ni mali ya chama hicho.

“Hiyo CCM Trust si kampuni yetu. Hatuifahamu na wala haimo katika orodha ya makampuni ya CCM,” alisema Makamba.

Alipoulizwa kama kampuni ya CCM Trust haina uhusiano na chama chake, iweje hawajachukua hatua ya kuwashitaki waliotumia jina hilo kwa vile wanaweza kuingiza chama katika migogoro, Makamba alisema, “Hayo mengine ya baadaye. Kwa sasa nakueleza hivyo. Hii si kampuni yetu.”

Katika kukana kumiliki makampuni hayo, CCM imetoa kwa wajumbe wa CC, orodha ya kile ilichoita “makampuni yake yote” inayomiliki.

Makampuni hayo ni Shirika la Uchumi na Kilimo (SUKITA), ambalo lilisajiliwa 15 Machi 1978 kwa ajili ya kufanya biashara mbalimbali.

Kampuni nyingineni ni Uhuru Publications Company Limited (UPL) ambayo ilisajiliwa 9 Desemba 1991. CCM inamiliki asilimia 100 ya hisa za Modern Newspaper Printers (MNP) iliyosajiliwa1995. Ni kampuni tanzu ya UPL.

Nyingine ni Tanzania Trading and Investment Limited (TANTI) iliyosajiliwa 1992 kwa lengo la kufanya biashara ndani na nje ya nchi. Ilifanya kazi tangu 1992 hadi 1998 ilipositisha shughuli zake kutokana na madeni.

Waraka unataja kampuni nyingine ya uwakala wa mafuta kuwa ni Jitegemee Trading Company Limited iliyosajiliwa mwaka 1997.
Kampuni ya Jitegemee Trading Company imeweza kununua hisa zenye thamani ya Sh. 5 milioni kwenye makampuni ya bia na sigara na inapata gawio kila mwaka.

Nyingine ni National Marketing Company Limited. Ilisajiliwa tarehe 6 Mei 1999 kwa madhumuni ya kufanya shughuli za uzalishaji mali na biashara. Kampuni inafanya biashara na kukiingizia chama mapato Tanzania Zanzibar.

Kampuni ya Tanzania Green Company Limited ilisajiliwa mwaka 2003 kwa lengo kuzalisha na kuendesha miradi ya biashara; ilipoanzishwa ilikuwa na mpango wa kuanzisha miradi zaidi ya 10. Hata hivyo, hakuna hata mradi mmoja ulioanzishwa hadi sasa.

Kamati Kuu ilijulishwa kuwa CCM inamiliki kampuni ya People’s Media Communication Company Limited ambayo inamiliki Radio Uhuru. Ilisajiliwa 22 Septemba 2004.

Makampuni mengine ni Kinara Exporters and Importers Company iliyosajiwa mwaka 1998; Jitegemee Tours and Company Limited iliyosajiliwa mwaka 2005; Gaming Management Company Limited iliyosajiliwa mwaka 2003; Amico Holding Company Limited ya mwaka 2001 na Jitegemee Mining and Constructions Company Limited iliyoundwa mwaka 2003 kwa ajili ya ujenzi.

MwanaHALISI liliripoti, miezi minne iliyopita, kuwa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU), ilikuwa tayari imewasilisha jalada la uchunguzi kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kwa hatua za mwisho.

Tuhuma zinazomkabili Warioba zipo katika maeneo mawili. Kwanza, ni iwapo fedha zilizotoka BoT zilipitia mkondo sahihi na halali; na pili, kama fedha hizo zilitumiwa kama ilivyotarajiwa.

Bali kwa muda mrefu sasa, Warioba amekuwa akirudia kauli ileile: “…Taarifa kwamba mimi nimetafuna fedha za mradi wa Mwananchi Gold Company Ltd., si za kweli, sijatumia vibaya fedha za kampuni hiyo.”

Amesema, “Fedha zote tulizolipwa na BoT, ambayo ilitoa mkopo kwa mradi huo, zipo kwenye maandishi na ushahidi upo wazi, ila nashangazwa sana, sijui ni kwa sababu za kisiasa mradi huu unapigwa vita?”

Warioba amekuwa akiilaumu serikali kwa kupiga vita MGL kwa kuitoza kodi ya asilimia tatu, wakati ipo kwa mujibu wa sheria ya EPZ, inayotaka kampuni za aina hiyo zisilipe kodi.

Wakati serikali imekuwa ikiibana kampuni hiyo kwa kodi, imekuwa ikitoa misamaha ya kodi kwa miaka mitano kwa kampuni za kigeni ambazo zipo nchini kwa ajili ya kuwekeza, Warioba amekuwa akisisitiza.
 
Mwanakijiji aliwahi kusema hapa kuwa CCM watairuka hiyo kampuni! Na kweli wamefanya hivyo. Warioba aliingizwa mkenge na Mkapa ili kufungwa mdomo! Anachotakiwa ni kikiri upungufu na kuomba msamaha! Sio kutoa utetezi usio na kichwa wala miguu!
 
kuingizwa mkenge unamtetea, aliingizaje mkenge wakati yeye ni mwanasheria na sheria anazijua vizuri sana tu
 
Kwa wanaojua sheria za Usajili wa kampuni wanafahamu fika kwamba huwezi kutumia jina la CCM pasipo idhini ya shirika au taasisi husika. Pili ni ujinga mkubwa kufikiria kwamba CCM inaweza kukaa kimya mtu kama Warioba afungue kampuni au trust fund kwa kutumia jina la CCM pasipo wao kuidhinisha - HAIWEZXEKANI.

Unaposema yeye ni mwanasheria, budi ufikirie pia sheria gani inayo mwezesha yeye kufungua trust fund kinyume cha sheria na Utaratibu.. kama hakuna basi hakuna haja ya kupoteza muda wetu kujadili majibu ya chama CCM kwani majibu kama haya tumeyasikia sana.

Kukana kwao hakuwezi dhihirisha lolote isipokuwa CCM wenyewe wamshitaki Warioba kwa kutumia jina la CCM ktk usajili pasipo idhini yao, hapo tutajua nani mkweli baina yao..
 
Inawezekana HII CCM trust ina kirefu kingine zaidi ya Chama Cha Mapinduzi...pengine ndo maana Makamba anaikataa

Inawezekana kuwa sasa kuna Chama Cha Mapinduzi na pia kuna Chama Cha Mafisadi. Sasa inabidi utengenishe. Nafikiri hii ni Chama Cha Mafisadi Trust.
 
Tafakari:
'Katika siasa hakuna kitu kinaitwa urafiki au undugu; kwa kawaida ni chuki na fitina tu kwa kwenda mbele. Wanachokiita wao urafiki au undugu sicho wanachokimaanisha. Wanachomaanisha ni aidha unafiki au urafiki wa mashaka'.
'...Anakuwa rafiki 'as long as' anakufanya uendelee kuwa na kuendelea kuwa juu. Ukiona anakukwamisha kwa namna moja au nyingine; 'get rid of him/her' tena fasta. Wa nini wakati atakufanya usiendelee kuneemeka?'-Sanga, J.S.
 
Kazi ipo. Hapa mheshimiwa Warioba kama hana maandishi, kweli ataburuzwa mahakamani. Kama uliambiwa kwa mdomo kweli unalo mheshimiwa. Mheshimiwa Makamba ameshakujibu.
 
kuingizwa mkenge unamtetea, aliingizaje mkenge wakati yeye ni mwanasheria na sheria anazijua vizuri sana tu
huku ndiko tunakorudi nyuma..Jaji warioba aingizwee mkengee??? ni ngumu kuelewaaa..

Tusimtetee hana rekodi yeyotee ya kujivunia pamoja na taaluma yakee..Ripoti yake ya Rushwa Mkapa alimweleza nimekutuma kuainisha vyanzo vya Rushwa sio majina ya wala Rushwa..

Unaweza kupima uelewa wake na utendaji kwa pamoja..
 
Sasa nimejua kwa nini Makala, yule mweka hazina wa CCM alimjia juu Warioba. Kumbe kulikuwa na kitu nyuma yake? Kubenea tunaomba utueleze huyo aliyehojiwa na vyombo vya dola ni nani? Au ni uzushi? Kweli vyombo vya dola vya bongo vinaweza kuhoji viongozi wa chama tawala? Sijui!
 
YULE mwandishi wa habari mahiri, Saed Kubenea yupo nchini India akipata matibabu ya macho baada ya kushambuliwa na mafisadi na kumwagiwa tindikali mwanzoni mwa mwaka jana.

Taarifaa zilizopatikana sasa hivi kutoka India zinasema mwandishi huyo anatakiwa kufanyiwa upasuaji katika jicho lake la kulia ili kutolewa usaha. Haijulijani opresheni hiyo itafanywa lini, kutokana na ukweli kuwa gharama ya opresheni ni kubwa na malipo yanafanywa na Kubenea mwenyewe kutokana na wale wasaanii wa serikali ya JK kumtosa.

Tunamuombaa mwenyezimungu amponeshe haraka Kubenea na arejee nyumbani kuja kupambana namafisadi hasa katika kipindi hiki cha kiza cha umeme kilicholtwa na RICHMOND.
 
hii nchi bwana,ndio yamepita haya! Ama kweli yaliyopita si ndwele......!
 
Kwa wanaojua sheria za Usajili wa kampuni wanafahamu fika kwamba huwezi kutumia jina la CCM pasipo idhini ya shirika au taasisi husika. Pili ni ujinga mkubwa kufikiria kwamba CCM inaweza kukaa kimya mtu kama Warioba afungue kampuni au trust fund kwa kutumia jina la CCM pasipo wao kuidhinisha - HAIWEZXEKANI.

Unaposema yeye ni mwanasheria, budi ufikirie pia sheria gani inayo mwezesha yeye kufungua trust fund kinyume cha sheria na Utaratibu.. kama hakuna basi hakuna haja ya kupoteza muda wetu kujadili majibu ya chama CCM kwani majibu kama haya tumeyasikia sana.

Kukana kwao hakuwezi dhihirisha lolote isipokuwa CCM wenyewe wamshitaki Warioba kwa kutumia jina la CCM ktk usajili pasipo idhini yao, hapo tutajua nani mkweli baina yao..
\Kwa chama kama CCM hilo linawezekana.Kwanin sasa CCM ni kundi la watu wachache chini ya mwamvuli wa CCM wanagawana keki ya taifa kila mmoja katika kundi hilo ana haki ya kuuda kampuni yoyote na kujichotea pesa anavyotaka mradi akae kimya akianza kukosoa chama tawala ataundiwa mizengo.Ebu jaribu kuyachunguza hayo makampuni yaliorodheshwa yako katika hali gani na yanaendeshwa vipi miradi yote ya CCM ni upenyo wa kukwepu pesa zetu walalahoi yatizame makampuni yake ikiwemo TOT ya John Komba utapata jibu.MUNGU IBARIKI TANZANIA
 
YULE mwandishi wa habari mahiri, Saed Kubenea yupo nchini India akipata matibabu ya macho baada ya kushambuliwa na mafisadi na kumwagiwa tindikali mwanzoni mwa mwaka jana.

Taarifaa zilizopatikana sasa hivi kutoka India zinasema mwandishi huyo anatakiwa kufanyiwa upasuaji katika jicho lake la kulia ili kutolewa usaha. Haijulijani opresheni hiyo itafanywa lini, kutokana na ukweli kuwa gharama ya opresheni ni kubwa na malipo yanafanywa na Kubenea mwenyewe kutokana na wale wasaanii wa serikali ya JK kumtosa.

Tunamuombaa mwenyezimungu amponeshe haraka Kubenea na arejee nyumbani kuja kupambana namafisadi hasa katika kipindi hiki cha kiza cha umeme kilicholtwa na RICHMOND.

du hafadhal kwan hata waandish njaa watakoma
 
Sometime nashindwa kumshangaa kumsifia au kumponda JK kikwete.

Pole J.warioba hawa wa sasa CCM dot.com
 
Back
Top Bottom