Kikwete alimuokoa syoi sumari ktk cc

Mwanajamii

JF-Expert Member
Mar 5, 2008
7,063
68
Rungu la Kikwete lilimwokoa Siyoi Send to a friend
Monday, 05 March 2012 09:17


jk-miwani.jpg
Rais Jakaya Kikwete

NAPE, WASSIRA WADAIWA KUSIMAMA KIDETE ATOSWE, JK AKATUMIA 'RUNGU' KUZIMA HOJA,WABUNGE WOTE CHADEMA KUHAMIA ARUMERU
Joseph Zablon, Dar na Moses Mashalla, Arusha
USHINDI wa Siyoi Sumari kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki, unadaiwa kuitesa Kamati Kuu (CC) ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kukuna vichwa kuhusu mbinu na mikakati ya kutengua ushindi alioupata katika duru ya pili dhidi ya William Sarakikya.

Katika Mkutano Mkuu wa jimbo hilo uliofanyika, Februari 20 ulimchagua Siyoi ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo, marehemu Jeremiah Sumari kwa kura 361, akifuatiwa na Sarakikya aliyepata kura 259. Hata hivyo, CC ya CCM iliyoketi Februari 27, iliagiza kurejewa kwa upigaji kura kati ya wagombea hao.
Katika duru hilo la pili la uchaguzi uliofanyika Machi Mosi mwaka huu, Siyoi alipata ushindi wa kishindo wa kura 761 na kumtupa mbali mpinzani wake, Sarakikya aliyepata kura 361.

Juzi katika kikao hicho cha CC, ushindi huo wa mara ya pili wa Siyoi uliipasua tena kamati hiyo kuu yenye mamlaka ya juu ya uamuzi ndani ya chama hicho, baada ya baadhi ya wajumbe kudaiwa kutaka atoswe na apitishwe Sarakikya kutokana na tuhuma za matumizi makubwa ya fedha wakati wa kampeni.

Vyanzo vya habari vya kuaminika kutoka katika kikao hicho cha CC, vilifafanua kwamba waliosimama kidete kutaka Siyoi atoswe ni Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira.

Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, Nape alipinga Siyoi kurejeshwa akizingatia matukio mbalimbali ya tuhuma za matumizi makubwa ya fedha yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watu ili wamchague mgombea huyo, kitu ambacho hakikupaswa kuvumiliwa.

Hoja hiyo ya Nape iliungwa mkono na Wassira ambaye naye alitaka Siyoi atoswe kutokana na tuhuma hizo za matumizi makubwa ya fedha kutoka kwa baadhi ya wapambe wake waliotaka mgombea huyo achaguliwe.

Lakini inadaiwa kuwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alisema kikao hicho kisingeweza kumkata Sumari kwa sababu tu ya tuhuma hizo za rushwa zilitolewa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), mkoani humo.

Chanzo kingine kilimnukuu mwenyekiti huyo akisema kwamba, Arusha ni mkoa wenye siasa za aina yake hivyo ni muhimu kuwa makini kwani siku za nyuma kuliwahi kuibuka tuhuma za rushwa kwa wabunge wa CCM kukamatwa lakini, mahakama ikawaachia huru.

Chanzo hicho kiliongeza kwamba, Rais Kikwete alisisitiza kuwa hata tuhuma za rushwa zilizotolewa zilikuwa zikigusa wengine kwani iliwahi kupendekezwa kwamba Elishalia Kaaya ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC), ndiye apitishwe na wengine wang'olewe.

Katika kikao hicho, Rais Kikwete pia alinukuliwa akihoji kuwa endapo Siyoi angekatwa jina kungekuwa na uhakika wa chama kushinda kwa kumsimamisha Sarakikya? Hakupata jibu kama mgombea huyo wa pili angeweza kushinda kiti hicho.

Hata hivyo, chanzo hicho kilisema baada ya mwenyekiti kutumia rungu kumpitisha Siyoi alimpa angalizo: “Basi na wewe usiende kutamba huko mitaani kwamba umeangusha watu, fanya kampeni, ushinde jimbo tuangalie mambo mengine mbele.”

Ilielezwa zaidi kwamba Rais Kikwete aliungwa mkono na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, aliyeeleza kuwa haoni sababu ya kumwondoa Siyoi katika kinyang'anyiro hicho kwani ushindi wake ulikuwa mkubwa.

Waziri Wassira jana alikataa kuzungumzia suala hilo akasema: “Hili linahusu chama na mambo ya chama mwulize Nape.”

Hata hivyo, Nape alipoulizwa alisema: “Si kweli kwamba kulikuwa na mpango wa kumtosa Sumari na sijui mambo hayo umeyapata wapi?” Mambo hayo ni fitna, majungu na uzushi ambavyo vinapandikizwa ndani ya chama chetu. Nakuhakikishia hakuna jambo hilo kabisa.”

Kikao cha Sekretarieti

Awali, katika kikao cha Sekretarieti Katibu Mkuu, Wilson Mukama aliwanyooshea vidole wajumbe wengine waliokuwa wakitaka kukatwa kwa jina la Siyoi akiwaambia kwamba hakuna ambaye yumo katika chombo hicho bila kuwa na kambi yake.

Mukama alinukuliwa akisema katika sekretarieti hiyo, kila mjumbe ana kambi na zinajulikana hivyo akataka wajumbe kufanya uamuzi ambao utakuwa na maslahi kwa chama na si ya kambi.

Kunusuru mpasuko
Wakati huohuo, CCM mkoani Arusha kimesema kitayapatanisha makundi yote yaliyotofautiana wakati wa mchakato wa kura za maoni za kumpata mgombea wa kupeperusha bendera ya chama hicho huku kikisisitiza kwamba kazi ya kuyapatanisha makundi hayo ni ndogo tofauti na inavyodaiwa.

Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda alisema jana kwamba mkakati uliopo kwa sasa ni kuyapatanisha makundi ya wafuasi hao kwa kuyaweka chini na kuyafanya kuwa kitu kimoja ili kunyakua ushindi .

Alitamba kwamba CCM kina uhakika na ushindi katika jimbo hilo kwa kuwa lilikuwa likishikiliwa na chama hicho.

Bila kutaja mbinu za ushindi, alisema wamejipanga kushirikiana na kamati ya kampeni ya chama hicho itakayoongozwa na Rais mstaafu, Benjamin Mkapa ambayo itashirikiana na kamati za kampeni kuanzia mashina, matawi hadi kata kuhakikisha ushindi unapatikana.

Mbowe na kampeni tulivu

Kwa upande wake, Chadema kimeahidi kufanya kampeni tulivu katika uchaguzi huo kikiliomba jeshi la polisi kuhakikisha unakuwepo utulivu wakati wa kampeni na siku ya kupiga kura.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe aliwaambia waandishi wa habari juzi mjini hapa kabla ya kukamilika kikao cha Kamati Kuu ya chama hicho, alisema wamejipanga kufanya kampeni tulivu na watashinda bila kuiba kura wala kupiga mtu.

“Chadema tunawaahidi wakazi wa Arumeru kushuhudia kampeni tulivu kabisa, hatutamtukana mtu wala kupiga mtu na hivyo tunaomba vyombo vya dola vihakikishe uchaguzi huu unakuwa tulivu” alisema Mbowe.

Alisema imani kubwa waliyonayo wananchi wa Jimbo la Arumeru Mashariki kwa chama hicho, inawapa nguvu kujiamini kuwa watashinda uchaguzi huo bila ya hofu yoyote.

Mbowe pamoja na wajumbe wa kamati kuu ya chadema, ambao waliwasili mjini hapa juzi na kupata mapokezi makubwa, alisema mgombea wa chama hicho, Joshua Nassari anakubalika zaidi katika jimbo hilo na hivyo anawapa imani kubwa ya ushindi.

Katika kuhakikisha ushindi, wabunge wote wa Chadema, wanatarajiwa kushiriki katika kampeni za nyumba kwa nyumba katika uchaguzi huo na wamepangwa katika kata zote 17 za jimbo hilo.

Habari za uhakika kutoka katika timu ya kampeni ya Chadema, ambayo katika hatua za awali, iliratibiwa na Mkurugenzi wa Bunge na Halmashauri, John Mrema zimeeleza kuwa mara baada kuzinduliwa kwa kampeni Machi 10, wabunge hao watatawanyika katika maeneo yao.

Natse na Nyerere

Mbunge wa Karatu, Mchungaji Israel Natse na Mbunge wa Msoma Mjini, Vicent Nyerere wameteuliwa na Kamati Kuu ya Chadema kuongoza timu ya kampeni ya chama hicho.

Habari za uhakika kutoka ndani ya kikao hicho, zimebainisha kuwa wabunge hao wataongoza timu za kampeni katika kata mbalimbali ili kuhakikisha Chadema inashinda.

Mrema alithibitisha jana akisema: “Ni kweli kwa sasa Mchungaji Natse na Nyerere wataongoza timu ya kampeni na tunatarajia ushindi mkubwa katika jimbo hili kwani tumejipanga kuhamasisha wapiga kura wengi na kulinda kura zetu.”

Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa amewataka viongozi wa chama hicho wa vijiji vyote kuwa na fomu maalumu za kujua wanachama wao.

Wagombea watamba

Wakati Siyoi akiwataka wana CCM wa jimbo hilo kusahau yaliyopita na kusonga mbele, mgombea ubunge kwa tiketi ya Chadema,Joshua Nassari ametamba kwamba anasubiri kuapishwa ifikapo Aprili mosi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti kuhusu kuteuliwa na kamati kuu za vyama vyao mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM, Siyoi alisema kwamba ameshukuru uamuzi uliofanywa na kamati za CCM wilaya, mkoa hadi taifa huku akiwataka wanaCCM kusahau yaliyopita ili wasonge mbele.
Siyoi alisema pamoja na kufurahishwa na uamuzi wa CC ya CCM kupitisha jina lake kupeperusha bendera ya chama hicho, chama hicho kinapaswa kutoa ushirikiano wa dhati katika kuhakikisha wanalitetea jimbo hilo.
Hata hivyo, alisisitiza kwamba changamoto zote alizozipitia katika hekaheka za uchaguzi wa kuteua jina lake zikiwemo tuhuma mbalimbali za rushwa ni misukosuko ya kisiasa ambayo haiwezi kuepukwa zaidi ya kukabiliana nayo.
Uongozi wa Radio 5

Katika hatua nyingine, uongozi wa Radio 5 umeeleza kusikitishwa na kitendo cha maofisa wa Takukuru Arusha kuvamia jengo lao na kumchukua kwa nguvu Meneja wake, Jimmy Mtemi Machi 2, mwaka huu.

Taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi wa Redio hiyo, Robert Francis ilieleza kuwa maofisa hao waliwatisha na kuwanyanyasa wafanyakazi wa kampuni jambo ambalo limesababisha wafanye kazi kwa wasiwasi mkubwa.
 
0 Reactions
Reply
Back
Top Bottom