Kifo cha Gaddafi na maajabu ya Watanzania

Mwamikili

JF-Expert Member
Mar 24, 2011
417
137
Kifo cha Gaddafi na maajabu ya Watanzania
ban.blank.jpg


Prudence Karugendo

amka2.gif

MAPINDUZI ya umma ya Libya yaliyoung’oa utawala wa miaka 42 wa Kanali Muammar Gaddafi na hatimaye kusababisha kifo cha mtawala huyo yanayo mengi ya kuwafundisha Watanzania. Kiuhalisia mapinduzi ni mabaya kwa sababu mara nyingi huambatana na umwagaji wa damu na upoteaji wa roho, lakini kwa vile mapinduzi yanayo mengi yaliyojificha, kama kilivyo kifo, hatunabudi kuyaona mapinduzi ni mazuri hususan yale yanayochochewa na umma kama yalivyokuwa haya ya sasa ya Libya.

Nimetoa mfano wa kifo, kifo ni kibaya na tunakiogopa. Ubaya wa kifo unaletwa na ukweli kwamba aliyekufa anakuwa ametenganishwa moja kwa moja na ndugu zake ambao hawana uhakika kule anakokwenda kukoje.
Lakini wakati tunakiogopa kifo tunaamini kwamba kuna pepo ambayo kila mwanadamu anaitamani, na huwezi kwenda peponi mpaka ufe kwanza. Kwa mantiki hiyo ya kwamba kifo tunachokiogopa ndiyo njia pekee ya kuelekea peponi tunakokutamani basi kifo ni kizuri.
Kifo ndicho kinachotupeleka kwenye starehe ya milele ambako kila aendaye hatamani hata mara moja kurudi nyuma alikotoka. Mapinduzi nayo yako hivyo hivyo, yanafanyika, damu inamwagika na hata roho zinapotea wakati mwingine, lakini kinachotafutwa kinapatikana.

Mapinduzi yanabaki kuenziwa bila kujali damu iliyomwagika wala roho zilizopotea sawa na walioingia peponi wasivyokikumbuka kifo wala wapendwa wao waliowaacha nyuma. Kama ni hivyo basi kwa nini mapinduzi yasionekane mazuri?
Mifano ni mingi ya nchi zinazoendelea kuyaenzi mapinduzi yaliyotokea katika nchi hizo yakiwa yamemwaga damu na kupoteza roho. Libya yenyewe imeyaenzi mapinduzi ya mwaka 1969 kwa miaka 42.
Zanzibar inayaenzi mapinduzi ya mwaka 1964 huu ni mwaka wa 47, Cuba inayaenzi mapinduzi ya mwaka 1959 huu ni mwaka wa 52 na kadhalika nakadhalika.
Kwa maana hiyo kama mapinduzi yanaenziwa basi mapinduzi ni mazuri bila kujali athari zinazoambatana nayo. Ni kama ilivyo kwa pepo ambayo kuiingia ni lazima kwanza mtu afe bila kujali kitakuwa kifo cha aina gani.
Mapinduzi ya Libya yaliyoongozwa na Muammar Gaddafi mwaka 1969 yameenziwa mpaka wananchi wa Libya walipomchoka Gaddafi na kufanya mapinduzi ya sasa ambayo sina hakika watayaenzi kwa kipindi gani. Ila sote tumekuwa mashuhuda wa namna mapinduzi hayo yalivyopokewa kwa shangwe kuu na wananchi wa Libya.
Hapo kuna fundisho, nalo ni kwamba wanadamu, tofauti na wanyama, wanahitaji mabadiliko waliyojichagulia wao na siyo ya kulazimishiwa kitu wakipende watake wasitake hata kama kitu hicho ni kizuri namna gani.
Pamoja na mambo mengi aliyowafanyia Gaddafi watu wa Libya bado walikuwa wanajiona wanayo haki ya kuamua kama yeye ndiye aendelee kuwa kiongozi wao au la kuliko mwenyewe kuendelea kuwalazimisha kuwa yeye ndiye pekee anayewafaa.
Kushindwa kulitambua hilo au kulitambua na kulibeza ndilo kosa kuu alilolifanya Gaddafi lililomtoa kwenye utukufu na kumuingiza kwenye utukutu na hatimaye muadhama kuuawa kinyama na kwa aibu kama kibaka wa mitaani.
Fundisho jingine ni kwamba watawala walio wengi hasa wa bara la Afrika, wanaongozwa na pepo wachafu kufanya mambo ya ajabu. Tunaelezwa kwamba Gaddafi alikuwa amejilimbikizia utajiri wa ajabu. Mahesabu yaliyofanyika harakaharaka yanaonyesha kwamba pesa aliyokuwa ameificha katika mabenki ya ughaibuni kama angeamua kuitoa kwa nchi ya Tanzania ingeweza kuendesha nchi yetu kwa miaka 12 na ikabaki!

Kufuru yote hiyo ilikuwa ni ya nini kwa mtu aliyekuja kujikuta hana pa kukimbilia isipokuwa kujificha kwenye tundu la mtaro wa maji machafu kama nguchiro? Hiyo pesa, ambayo bila shaka alikuwa amewaibia wananchi wa Libya, imemsaidia nini?
Nani asiyeona kuwa Gaddafi aliongozwa na pepo wachafu kuiba pesa hiyo na kuificha nje ya nchi yake wakati akielewa kuwa hasingeweza kuitumia yote katika uhai wake uliokuwa umebaki wala kuitumia kujinusuru?
Katika moja ya mafundisho ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alisema kwamba zipo baadhi ya adhabu ambazo Mwenyezi Mungu ameziumbia ndani ya kosa. Unatenda kosa unapata adhabu palepale.
Mojawapo ya adhabu za aina hiyo ndiyo kaipata Gaddafi. Kufanya kufuru ya kuishi kama Mungu mtu lakini akaja kufa kama shetani mkuu.
Watu waliokubali kuishi bila makuu, kama alivyokuwa yeye Nyerere, ambao hawakuukubali mwongozo wa pepo wachafu, wamekufa kwa heshima na wanaendelea kuenziwa.
Sote ni mashuhuda, tuliona kifo cha Nyerere kilivyopewa uzito mkubwa duniani kote, uzito wa heshima, tofauti na uzito wa kifo cha Gaddafi ambaye ni kama wa kushangilia kuuawa kwa mdudu msumbufu.
Viongozi na watawala wajifunze, kuishi bila makuu wakafa kwa heshima au kuishi kwa makuu wakafa kwa dharau na aibu. Nyerere alijitahidi kuishi kiumasikini lakini akafa kiutajiri tofauti na Gaddafi aliyeishi kwenye kufuru ya utajiri lakini akafa kifo kilichopitiliza hata kwenye umasikini!

Kwa sasa yapo maneno mengi yanayosemwa kuhusu kifo cha Gaddafi, yapo madai ya kwamba sisi Waafrika tumelaaniwa kwa kushindwa kujiunga na Gaddafi pale majeshi ya NATO yalipoanza kuwasaidia wananchi wa Libya dhidi ya ukatili wa Gaddafi!
Sisi Waafrika! Kwa maana ya kwamba maumbile yetu na watu wa Libya ni sawa! Laana ninayoiona mimi hapa tuliyo nayo Waafrika ni ya kujiona sisi na Walibya tuko sawa wakati Walibya hawaoni hivyo.
Mimi naamini wale ni Waarabu, kama wanavyoona wao na huo ndio ukweli. Ndiyo, kisiasa tutawaita Waafrika kwa vile walilivamia bara letu na kuamua kuligeuza makazi yao, lakini kimaumbile hainiingii akilini kujichanganya nao na kudai sisi Waafrika.
Kama ambavyo mtoto aliyezaliwa Dar na wazazi Wahaya au Wachaga hageuki kuwa Mzaramo ndivyo na mimi ninavyoshindwa kuwageuza Waarabu wa Libya kuwa Waafrika. Sisemi hivyo kwa kuwabagua kwa rangi isipokuwa ni ukweli ambao wao wanauamini kuliko hata sisi tunavyouangalia.
Lakini hata hivyo kujiunga na Gaddafi dhidi ya mashambulizi yaliyokuwa yanaelekezwa kwake isingekuwa kuilinda Libya, nchi ya Kiafrika dhidi ya majeshi ya NATO, bali ingekuwa ni kuwasaliti Waarabu wa Libya waliokuwa wanajaribu kuondokana na mtawala wao aliyekuwa amejigeuza kirusi kwao.
Tungekuwa tumeyasaliti matakwa ya watu wa Libya na vilevile kukisaliti kinachoitwa demokrasia, utashi wa watu kuamua wanavyotaka waishi.
Ingetokea tukaitenda dhambi ya kuisaliti demokrasia kwa kwenda Libya kujaribu kuzizima harakati za kuisaka demokrasia nchini humo dhambi hiyo isingebaki Libya, ni lazima ingetufuata na kututafunia huku kwetu ambako nako kuna kila dalili za Ugaddafi.
Iwapo nguvu ya umma ingeshindwa kupata mafanikio kule Libya ni wazi ile dhana iliyowalewesha watawala wengi wa Kiafrika ya kwamba nguvu ya umma si lolote si chochote ingekuwa imepaliliwa na kuongezwa mbolea ili ikasitawi vizuri na kutuangamiza.
Umma ungeendelea kudharauliwa huku watawala wakijifanyia mambo jinsi wanavyotaka wakielewa kwa uhakika kuwa umma hauna lolote.
Kwahiyo kufanikiwa kwa umma wa Libya kuuondoa utawala king’ang’anizi ni mafanikio vilevile kwa nchi zote ambako sauti ya umma bado inakandamizwa na tawala dhalimu.
Kwa maana hiyo basi, kuanguka kwa utawala wa Gaddafi ni ishara nzuri kuelekea katika Afrika isiyo na tawala dhalimu. Afrika ambayo umma unasikilizwa unataka na kuamua nini. Afrika tunayoitaka.
Siku chache kabla ya kifo cha Gaddafi niliandika katika gazeti hili nikitabiri kilichokuwa wazi kama ifuatavyo, “Watawala wanaoamua kuiheshimu nguvu ya umma na kujisalimisha kwa nguvu hiyo au kuzikimbia nchi zao wanaweza wakapata msamaha.
Watawala wanaojifanya vichwa ngumu kama alivyofanya mwenzetu Muammar Gaddafi wa Libya, aliyejiaminisha kwamba zana zake zingeweza kumkinga dhidi ya hasira za wananchi, nguvu ya umma. Nilishasema kuwa sidhani kama ataweza kukiepuka kitanzi kama kilichomnyofoa roho Saddam Hussein wa Irak, pale nguvu ya umma itakapomtia mikononi akiwa hai.” Utabiri wangu huo ulitimia siku tatu baadaye!

Kwa upande mwingine, katika hali inayotutofautisha Watanzania na binadamu wa mataifa mengine, wapo Watanzania waliosikitishwa na kuyalaani sana mauaji ya Gaddafi. Walibya wanashangilia Watanzania wanalaani!
Nimejaribu kuwahoji baadhi ya watu walioonyesha kuguswa sana na mauaji ya Gaddafi. Nimepata majibu yanayotofautiana lakini yote yakionyesha wema wa mtawala huyo kwa Watanzania, wema ambao bila shaka hakuwahi kuuonyesha nchini kwake kwa Walibya wenzake waliokuwa wakikishangilia kifo chake. Wapo watu ambao wanasema kwamba Gaddafi alikuwa akijenga misikiti hapa nchini, hao wanamlilia kwa wema huo. Wengine wanasema alikuwa akituma zawadi za tende na halua!

Pia wapo wanaosema kwamba alikuwa akituma pesa kwa ajili ya vikundi mbalimbali hapa nchini bila kueleza malengo ya pesa hizo ambazo mara nyingi zimezua mitafaruko na uhasama miongoni mwa wanajamii.
Niliwahi kushuhudia tukio mojawapo ambalo watu walitaka kutoana macho kisa kikiwa ni fedha za Gaddafi kwenye kikao ambacho nilikuwa mwalikwa.
Kwahiyo tunaona kwamba utamu wa tende na halua vinatosha kumfanya Mtanzania asahau thamani yake! Kwa nini nasema hivyo? Tukumbushane kidogo.
Mwishoni mwa mwaka 1978 mtawala wa Uganda wakati huo, Idd Amin Dada, kwa ulevi wake aliamua kuivamia nchi yetu na kuteka sehemu ya eneo la Tanzania na kulifanya moja ya majimbo ya Uganda.
Wakati anafanya hivyo Amini akawachinja kinyama maelfu ya Watanzania waliokuwa wanaishi katika eneo hilo kabla ya Mwalimu Nyerere kuapa kwamba ni lazima amshikishe adabu Idd Amin kwa kitendo hicho ambacho Gaddafi hakukilaani.
Badala yake wakati Mwalimu ameanza kumchapa Amin, Gaddafi akamkemea Mwalimu kwamba aache mara moja vinginevyo angeingilia kati, mzee wa Kizanaki akamdharau. Ndipo Gaddafi akatuma majeshi na silaha nzito nzito kwa rafiki yake ili zikawamalize Watanzania.
Nakumbuka nilikuwa katika shule ya sekondari mwanzoni mwa waka 1979, tulipotembelewa na mmoja wa makamanda wa JWTZ, Luteni Kanali Victor Lusubi, aliyekuwa anapita katika shule za sekondari kuwaeleza wanafunzi maendeleo ya mapambano huku akiwapa hamasa juu ya mapambano hayo.
Lusubi ndiye aliyetueleza namna askari wa Gaddafi, ambao ndio kwanza walikuwa wameiona misitu badala ya jangwa la kwao, walivyokuwa wakikamatwa kama panzi na vijana wa JWTZ.
Tunalopaswa kulitilia maanani ni kwamba Gaddafi alikuwa amelenga kutuangamiza kwa kushirikiana na swahiba wake Amin kama usingekuwa ujasiri wa Amiri Jeshi wetu wa kutulinda bila kutetereka.
Hivyo kuukumbuka tu utamu wa tende na halua kutoka kwa Gaddafi tukiwa tumesahau jinsi alivyotaka kuyaangamiza maisha yetu kiubabe ni jambo linalotufanya Watanzania tuonekane ni viumbe wa ajabu. Na hayo ndiyo maajabu ya Watanzania yanayowatamanisha watu wa mataifa mengine kuja kwetu kufanya lolote wanalotaka tukiwa tumewatumbulia macho na kuwakenulia meno!


Source: Tanzania daima, jumapili 30 october 2011


h.sep3.gif

 
na wewe uko mule mule unastaajabisha

unataka na sisi jk akiotoka ridhwan atutwale sio?, wangapi mgekubariana na hilo? na asaidie nchi zingine kwa wealth zetu? na akina miraj wawe wakuu wa majeshi!
 
Back
Top Bottom