Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,316
- 33,112
Dk. Batilda Burian
Shahidi wa pili upande wa ulalamikaji, katika kesi ya kupinga matokeo ya ubunge wa Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbles Lema (Chadema), Agness Gideon Mollel, ameieleza mahakama kuwa aliyekuwa mgombea wa CCM, Dk. Batilda Burian, alidhalilishwa na Lema kwa kuambiwa ana mimba ya Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, na hafai kuchaguliwa kuwa mbunge wa jimbo hilo kwa madai wananchi watakuwa wameliuza kwa Lowassa.
Aidha, aliiambia mahakma hiyo kuwa alimsikia Lema akiwahutubia wananchi katika mkutano wa hadhara kuwa, Dk. Burian alikuwa ameolewa Zanzibar na akipata ubunge ataifunga Safina Redio na kuufungua msikiti.
Alitoa madai hayo mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Sumbawanga, Gabiel Rwakibarila, anayesikiliza kesi hiyo iliyofunguliwa na watu watatu, ambao ni Mussa Mkanga, Agness Mollel na Happy Kivuyo.
Mahojiano kati ya shahidi na wakili upande wa walalamikaji, Alute Mugwai, yalikuwa kama ifuatavyo:
Wakili: Wewe unaishi mtaa gani?
Shahidi: Mtaa wa Roman Katoliki.
Wakili: Huo mtaa una mwenyekiti wa mtaa?Shahidi: Ndiyo ambaye ni mimi.
Wakili: Wewe una elimu gani?
Shahidi: Elimu ya msingi.
Wakili: Umemaliza mwaka gani?
Shahidi: 1983.
Wakili: Wewe ulihudhuria mikutano mingapi ya kampeni?
Shahidi: Nilihudhuria mikutano mitatu ya CCM, Chadema na TLP.
Wakili: Huo mkutano wa Chadema ulifanyika lini na wapi?
Shahidi: Ulifanyika Septemba Mosi eneo la Bigsister, Kata ya Olorieni.
Wakili: Ulianza saa ngapi?
Shahidi: Ulianza saa kumi jioni.
Wakili: Unaweza kueleza alichosema Lema katika mkutano huo?
Shahidi: Ndiyo, nilimsikia Lema akisema msimchague Dk. Batilda sababu ana mimba ya Lowassa na ameolewa na Mzanzibari, hivyo akichaguliwa mtaliuza jimbo kwa Lowassa na akiwa mbunge atafunga Redio Safina na atafungua msikiti.
Wakili: Huyo Lowasa ni nani?
Shahidi: Huyo Lowassa ni Mbunge wa Jimbo la Monduli na alikuwa Waziri Mkuu Mstaafu.
Wakili: Baada ya kusikiliza maneno hayo ulifanya nini?
Shahidi: Niliamua kuondoka.
Wakili: Sasa Mahakama ikithibitisha maneno haya yalisemwa na Lema,
unataka Mahakama ikufanyie nini?
Shahidi: Nataka avuliwe ubunge wa Jimbo la Arusha Mjini na atulipe gharama za kesi hii.
Baada ya mahojiano hayo ndipo alipoanza mahojino mengine na wakili wa upande wa mlalamikiwa, Method Kimomogolo na sehemu ya mahojiano yalikuwa kama ifutavyo:
Wakili: Hivi unakumbuka uliweka sahihi yako katika hati ya mashitaka ulipofungua kesi hii wewe na wenzako?
Shahidi: Ndiyo.
Wakili: Uliyosema hapa na katika hati ya mashitka mbona yanatofautiana, katika hati ya mashitaka sehemu uliyosaini wewe inasema ulimsikia Lema akisema asichaguliwe Dk. Batilda sababu ni
mwanamke na hafai kuwa kiongozi na ukadai aliyasema hayo eneo la
Fantastiki huko Olomatejoo kata ya Erelai?
Shahidi: Siyo kweli sikusema hivyo.
Wakili: Angalia haya maneno na sahihi hii siyo yako?
Shahidi: Ndiyo.
Wakili: Hapa mahakamani ni lazima useme moja ukubali moja tu, nakuuliza
tena hii hati ni yako au umeyakataa uliyobambikiziwa? Na ni kweli uliyoshuhudia ni ya Olomatejoo au Bigsister?
Shahidi: Nimeshuhudia ya Bigsister Kata ya Olorieni.
Hapo Jaji aliingilia kati na kuhoji kama ifuatavyo:
Jaji: Ulishuhudia wapi?
Shahidi: Bigsister kata ya Olorieni.
Jaji: Hakuongea chochote kuhusu eneo la Fantastic Olomatejoo?
Shahidi: Hapana.
Wakili Kimomogolo aliendelea na mahojiano kama ifuatavyo:
Wakili: Akija mtu akasema ulihudhuria mkutano Septemba 22 mwaka juzi saa 10.00 jioni eneo la Fantasitick Elerai atakuwa mwongo? Na mwongo Mkubwa?
Shahidi: Hata sifahamu eneo hilo.
Wakili: Wewe unafahamu Redio Safina ilipo na siyo ile ya kuambiwa?
Shahidi: Ndiyo na nilishasali pale.
Wakili: Hufahamu Redio Safina ipo Kaloleni na siyo Olasiti?
Shahidi: Mi najua Olasiti tu.
Wakili: Je, katika huo mkutano uliomsikia Lema akisema Dk. Burian ana mimba ya Lowassa na maeneo yote hayo ulikuwa na tepu ya kunasa hayo maneno?
Shahidi: Hapana sikuwa nayo.
Wakili: Ulikuwa na kalamu ya kuandika na kuweka kumbukumbu ya yale yaliyosemwa?
Shahidi: Sikuwa nayo.
Wakili: Je, ulishawahi kumuuliza Dk. Batilda kwanini hajafungua kesi au
aliwahi kukueleza sababu ya kutofungua kesi? Wakati yeye aliwahi kuwa Waziri na hivyo kama ulimweleza amedhalilishwa angekimbilia mahakamani kwa nini hakufanya hivyo?
Shahidi: Hakuwahi kunieleza.
Wakili: Sasa wewe kama mama lishe na tena darasa la saba, ukaamua kufungua
kesi je, wewe binafsi uliguswaje hayo maneno?
Shahidi: Yalinigusa kijinsia, kidini na kikabila.
Wakili: Je, ulishawahi kuona au kusomewa maelezo ya Lema ya kujibu malalamiko yenu?
Shahidi: Nilisomewa tu.
Wakili: Wewe huo ujasiri unaupata wapi wakati wewe mama lishe na Waziri akaogopa kufungua kesi hii?
Shahidi: Natetea haki zangu za kimsingi.
Kesi hiyo inayovutia hisia za watu na kujaza umati wa watu mahakamani hapo, inaendelea na utoaji wa ushahidi upande wa walalamikaji leo.
CHANZO: NIPASHE