Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,319
- 33,125
UCHAGUZI mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 31 mwaka huu unaweza kuingia mushkeli baada ya mkazi wa Dar es Salaam, Denis Maringo kufungua kesi ya kikatiba akihoji sheria inayozuia matokeo ya rais kupingwa baada ya kutangazwa na Tume ya Uchaguzi (Nec). Katika kesi hiyo ya madai namba 86 ya mwaka 2010 iliyofunguliwa juzi,
Maringo anataka mahakama itoe ufafanuzi wa mambo hayo kabla ya kufanyika uchaguzi huo. Maringo pia anadai kuwa Rais Jakaya Kikwete alivunja katiba kwa kulivunja Bunge kabla ya kumalizika muda wake wa miaka mitano. Kwa mujibu wa Maringo, Bunge la Tisa la Jamhuri la Muungano wa Tanzania lililoingia madarakani mwezi Desemba mwaka 2005, lilipaswa kuvunjwa Desemba 5 mwaka huu badala ya Julai 17 kama alivyofanya rais.
"Tunaitaka Mahakama itamke kuwa kifungu 41(7) cha katiba kinapingana na kifungu namba 13(6)(a) kinachohusu mgawanyo wa madaraka na uhuru wa mahakama kwa kueleza kuwa matokeo ya urais baada ya kutangazwa na Nec hayawezi kupingwa," inasema sehemu ya madai hayo. "Kitendo cha rais kulivunja Bunge tarehe 17 Julai ni kinyume na kifungu namba 65(1) cha katiba ya Jamhuri ya Muungano ambacho kinaeleza kuwa kipindi cha muda wa Bunge ni miaka mitano," imesema sehemu ya hati hiyo.
"Kifungu cha 46A cha katiba kimetamka bayana kuwa rais hatalivunja Bunge wakati akijua kuwa mwenyewe (rais) bado yupo madarakani kwa lengo la kuleta uwiano wa madaraka." Maringo amefungua kesi hiyo dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Nec akiwa ni Mtanzania aliyejiandikisha kupiga kura.
Katika kesi hiyo, anashirikiana na Kituo cha Haki na Demokrasia (CJD). Mbali na madai hayo ya awali, walalamikaji wametaka wabunge kurejesha fedha za walipa kodi walizopewa kwa ajili ya mafao yao, wakidai kuwa hawastahili kulipwa kwa kuwa hawakulitumikia Bunge kwa muda uliotakiwa. Madai mengine yaliyotolewa na walalamikaji hao ni pamoja na kupinga umri wa mgombea urais kuwa miaka 40. Walisema Mahakama inapaswa kuirekebisha sheria hiyo kwa kuwa ni ya kibaguzi.
Walalamikaji hao pia wameiomba Mahakama kuondoa zuio liliolowekwa na baadhi ya vyama vya siasa kwa wagombea wake kushiriki midahalo ya uchaguzi kwenye vyombo vya habari wakisema hatua hiyo inawanyima wagombea hao fursa ya kujieleza; na wapigakura haki ya kujua sera za wagombea wanaopaswa kuwachagua.
Madai mengine yaliyoelezwa kwenye hati hiyo ni kupinga mipaka ya kijiografia ya majimbo ya uchaguzi na upigaji kura iliyowekwa na Nec kwa maelezo kuwa yataleta matokeo yasiyo ya haki kwa wapigakura.Walalamikaji wametaka pia Nec itafsiri sheria za uchaguzi kwa lugha ya Kiswahili kuwawezesha wapigakura wote kuzifahamu na kujua haki zao kabla ya kufanya uamuzi.
"Sheria inayomtaka mgombea kujua kuzumgumza Kiswahili tu ni mbovu kwani sheria zote huandikwa kwa lugha ya Kiingereza ingawa mijadala bungeni na mambo mengine ya serikali hufanyika kwa Kiingereza," anasema Maringo katika hati hiyo.
Chanzo: Gazeti la Mwananchi