Kesi ya Cameron Todd Willingham: Baada ya kunyongwa yabainika hakuwa na hatia…….!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398
image.jpg

Cameron Todd Willingham.

story-willingham.jpg


ht_Grann_Arsonist_04_090916_ssv.jpg

cameron_todd_willingham1.jpg


090907_r18772_p465.jpg

Willingham akiwa gerezani kusubiri kunyongwa...............

fire.jpg

Nyumba ya Willingham ikiteketea kwa moto huku wanae watatu wakiwa ndani ya nyumba hiyo....

Ilikuwa ni Desemba 23, 1991, majirani waliona moto ukiwaka kwa kasi ya ajabu kutoka katika nyumba moja katika mji huo wa Corsicana, uliopo kaskazini mwa jimbo la Texas. Miali ya moto ilikuwa ikichomoza kupitia katika milango na milio ya kupasuka kwa marumaru za sakafu na samani za ndani ilikuwa ikisikika, moshi ulitanda kila mahali na kuharibu anga ya eneo hilo.

Buffie Beebee, binti wa miaka kumi na moja ambaye likuwa akiishi jirani na nyumba hiyo alikuwa akicheza uani mwa nyumba yao, ndipo aliposikia harufu ya moshi kuashiria kwamba kuna kitu kinaungua mahali. Alikimbilia ndani na kumweleza mama yake Diane ambapo walikimbilia katika nyumba hiyo iliyokuwa ikiwaka moto.

Walipofika katika eneo hilo walimkuta Cameron Todd Willingham akiwa amesimama nje ya nyumba yake ambayo ndiyo iliyokuwa ikiwaka moto. Alikuwa amevaa nguo za dangrizi maarufu kama Jeans. Alikuwa na masizi kifuani na alikuwa anapiga kelele alikilalamika watoto wake wanaungua ndani ya nyumba. Alidai kwamba ndani ya nyumba kulikuwa na watoto wake watatu, Karmon na Kameron mapacha wa kike wa mwaka mmoja na mwanae mwingine aliyemtaja kwa jina la Amber aliyekuwa na umri wa miaka miwili.

Willingham alimwambia jirani yake Diane apige simu haraka kuita zima moto, na wakati Diane anakimbia kwenda kupiga simu, Willigham aliokota fimbo na kuvunja kioo cha dirisha cha chumba cha watoto, lakini moto ulichomoza kwa kishindo kupitia katika tundu alilotoboa. Alitoboa kioo cha dirisha lingine lakini hali ikawa ni hiyo hiyo ya miali ya moto kuchomoza kwa kishindo. Willigham alirudi nyuma kukwepa moto ule na kupiga magoti chini mbele ya nyumba yake akiangalia nyumba hiyo ikiteketea kwa moto huku watoto wake wakiwa ndani asiamini macho yake. Akionekana kuchanganyikiwa Willigham alilia kwa uchungu huku akiwaita wanae na mwishowe akabaki kimya akiutumbulia macho moto ule uliokuwa ukiteketeza nyumba yake kwa kasi ya ajabu. Ulikuwa ni msiba mkubwa kwake.

Diane alirudi katika eneo hilo na alikuta eneo hilo likiwa lina joto kali kutokana na moto ule, baadae madirisha matano ya nyumba ile yalilipuka kwa kishindo na miali ya moto ikasambaa kiasi cha kuwafanya watu aliokuwa wameizingira nyumba hiyo kurudi nyuma kwa hofu ya kuungua au kujeruhiwa na moto ule. Muda mfupi baadae gari la kwanza la zima moto liliwasili ambapo Willigham aliwafuata na kuanza kufoka akiwaambia watoto wake watatu wamekwama ndani ya chumba chao cha kulala katika nyumba ile iliyokuwa ikiwaka moto katika hali ya kutisha.

Askari wale wa zimamoto walituma taarifa kwa njia ya simu ya upepo (Radio Call) kwenye kikosi cha uokoaji ili waje kuwaokoa watoto wale ambao kwa kweli kulikuwa na matumaini finyu ya kuwapata wakiwa hai. Muda mfupi baadae askari wa uokoaji walifika na kwa kushirikiana na askari wa zima moto walianza kuzima moto ule kwa maji baada ya kufanikiwa kuzima sehemu ya mbele ya nyumba ile. Askari mmoja aliyevaa mavazi maalum ya kuzuia moto pamoja na mtungi wa kuvutia hewa aliingia ndani ya ile nyumba kwa kupitia dirishani, lakini alisukumwa na maji yaliyokuwa yakirushwa na wenzie waliokuwa wakiendelea kuzima moto. Askari yule alirudi nyuma na kuingia tena katika nyumba hiyo kwa kutumia mlango wa mbele. Akiwa ndani ya nyumba hiyo alikutana na miali ya moto pamoja moshi lakini alimudu kupita katika kibaraza cha nyumba hiyo kwa shida hadi jikoni ambapo alikuta jokofu likiwa limezuia mlango wa chumba hicho.

Willingham alionekana kama amechanganyikiwa. Mmoja wa askari waliokuwa pale aitwae George Monagham alimchukua na kumpeleka nyuma ya gari la zima moto ambapo alimtuliza. Willingham alimweleza yule askari kwamba mkewe aliyemtaja kwa jina la Stacy aliondoka hapo nyumbani alfajiri na kumwacha kitandani akiwa amelala ndipo alipoamshwa na mwanae aitwae Amber aliyekuwa akipiga kelele kumwamsha akisema baba, baba, baba, moto……

"Binti yangu mdogo alijitahidi kuniamsha na nilipoamka, alinitaarifu kuhusu nyumba kushika moto, sikuweza kuwaokoa wanangu katika moto ule…" Alisema Willingam.

Wakati akiendelea kumweleza yule askari juu ya tulio lile, Askari aliyeingia katika nyumba hiyo alitoka akiwa amembeba bintiye aitwae Amber, na alipofika pale nje alipokelwa na askari wenzie na hapo hapo wakaanza kumpa huduma ya kwanza ya kumpulizia hewa mdomoni maarufu kama Cardiopulmonary resuscitation (CPR). Wilingham ambaye alikuwa na umri wa miaka 23 wakati huo, kijana mwenye mwili uliojengeka kwa misuli imara alikimbilia mahali alipokuwa mwanaye. Alipomuona mwanae, alikimbia kuelekea katika nyumba yake ambayo bado ilikuwa ikiungua akitaka kuingia ndani, lakini Monagham na askari mwingine walimzuia. "Ilibidi tumkamate na kumfunga kwa kamba kwa usalama wake na wetu pia." Alisema Monagham akiwaambia askari wa upelelezi.

"Kwa jinsi moto ulivyokuwa ukiwaka, ilikuwa ni ujinga kwa mtu yeyote kujaribu kuingia katika nyumba hiyo." Aliendelea kusema Monagham.

Baadae alipelekwa hospitalini ambapo alipewa taarifa kwamba mwanae Amber ambaye alikutwa kwenye chumba cha kulala cha wazazi wake (tofauti na malezo ya Willingham kwamba alikuwa kwenye chumba chao cha kulala) alikuwa amekufa kwa kuvuta hewa yenye moshi na pia watoto wake wawili Kameron na Karmon walikutwa wamelala kwenye sakafu ya chumba chao cha kulala wakiwa wamekufa. Miili yao ilikuwa imeungua sana na kwa mujibu uchunguzi wa madaktari ilithibitishwa kwamba nao pia wamekufa kutokana na kuvuta hewa yenye moshi (smoke inhalation).

Habari ya tukio hili lilotokea tarehe 23 Desemba 1991 ilisambaa kila mahali katika mmji huo wa Corsicana. Ulikuwa ni mji mdogo ulioko maili 55 kaskazini mwa mji wa Waco. Mji huo ulikuwa ndio eneo la kwanza nchini Marekani lililokuwa likichimbwa mafuta, lakini baada ya visima vingi katika eneo hilo kukauka zaidi ya robo ya wahamiaji kati ya wakazi elfu ishirini wa eneo hilo wamejikuta wakiwa katika lindi la umasikini.

Maduka mengi pamoja na shunguli mbalimbali za bishara zilizokuwa pembezoni mwa barabara zilifungwa kutokana na biashara kudorora na hivyo kuufanya mji huo kuonekana kama umehamwa. Willingham na mkewe aitwae Stacy aliyekuwa na umri wa miaka 22 wakati huo walikuwa hawana hela kabisa za kujikimu. Stacy alikuwa akifanya kazi katika baa ya kaka yake iliyokuwa ikijulikana kwa jina la "Some Other Place," na Willingham alikuwa ni fundi makanika ambaye hakuwa na kazi wakati huo, alikuwa na jukumu la kutunza watoto mkewe akiwa kazini.

Wakazi wa mji huo walichangishana fedha ili kumsaidia Willingham kugharamia mazishi ya wanae. Wakati huo huo, wataalamu wa uchunguzi wa moto walianza upelelezi wao ili kubaini chanzo cha moto huo. Willingham aliwapa wachunguzi hao ruhusa ya kupekua nyumba yake iliyoungua.

"Najua tunaweza tusipate majibu sahihi juu ya chanzo cha moto huo, lakini ningependa kujua kwa nini watoto wangu walikufa." Alisema Willingham.

Douglas Fogg, aliyekuwa afisa wa cheo cha juu wakati huo katika kitengo cha uchunguzi wa moto katika mji huo wa Corsicana ndiye aliyefanya uchunguzi wa awali katika nyumba hiyo. Alikuwa ni mrefu kwa kimo na sauti yake ilikuwa kavu na yenye mikwaruzo kutokana na kumeza moshi wa moto kwa miaka mingi akifanya kazi hiyo ya uchunguzi wa moto ikiwa ni pamoja na uvutaji wake wa sigara uliokubuhu. Douglas Fogg alizaliwa na kukulia katika mji huo wa Carsicana na baada ya kumaliza masomo yake ya elimu ya juu hapo mnamo mwaka 1963 alijiunga na na jeshi la wanamaji la nchini humo na alitumikia jeshi hilo nchini Vietnam akiwa kama tabibu, ambapo alijeruhiwa mara kadhaa katika vita hivyo. Alitunukiwa nishani kadhaa akiwa katika vita hivyo.

Baada ya kurudi kutoka vitani nchini Vietnam alijiunga na kikosi cha zima moto. Wakati wa tukio la kuungua kwa nyumba ya Willingham alikuwa ametumikia kikosi hicho kwa takriban miaka ishirini mbapo alipandishwa cheo na kuwa afisa wa cheo cha juu wa uchunguzi wa moto. Alishirikiana na mtaalamu mwingine wa cheo cha juu wa uchunguzi wa mtoto aitwae Manuel Vasquez (Manuel Vasquez alikuja kufariki hapo mnamo mwaka 1994).

Vasquez alikuwa ni mtaalamu aliyekuwa akiheshimika wa uchunguzi wa vyanzo vya moto, na mpaka tukio la kuungua kwa nyumba ya Willingham linatoke alikuwa amechunguza matukio yasiyopungua elfu kumi na mbili ya moto. Wataalamu wa kuchunguza chanzo cha moto walikuwa wakiheshimika sana katika jamii. Vasquez ambaye kipindi cha nyuma alilitumikia jeshi la nchi hiyo kama intelijensia alikuwa amejijengea heshima kubwa katika jeshi hilo. kutokana na uzoefu wake alikuwa na kanuni yake isemayo, "moto kamwe hauharibu ushahidi bali huutengeneza." Na kanuni nyingine isemayo, "Moto hukupa fumbo, mimi ni mfumbuaji tu."

Wakati fulani akihojiwa chini ya kiapo kama aliwahi kupotosha ushahidi katika kesi yoyote alijibu. "kama nimewahi kufanya hivyo mheshimiwa, kwa kweli sijui." Alijibu, kisha akaendelea, "kwa kweli sijawahi kuambiwa kama niliwahi kukosea mahali."

Uchunguzi wa awali ulibaini kwamba, moto ule ulikuwa umesababishwa kwa makusudi na Willigham, kwani kulikutwa mabaki ya aina fulani ya kimiminika ambacho husababisha milipuko. Hata hivyo nia (Motive) ya Willingham kusababisha moto huo ilikuwa haijajulikana, na hata mkewe Stacy alipoulizwa kama walikuwa na ugomvi yeye na mumewe usiku uliopita kabla ya tukio la moto, mwanamke huyo alikanusha kutokea kwa ugomvi kati yao.

Kulikuwa na maneno mengi mitaani juu ya tukio hilo, na hata baadhi ya wanafamilia walikuwa wakimlaumu Willingham kwa kuzembea kutowaokoa watoto wake wasiteketee kwa moto. Hata maelezo yake ya namna alivyoweza kujiokoa na moto ule yaliyochukuliwa na askari wa upelelezi yalikuwa yanajichanganya. Alisema alidhani mwanaye Amber alikuwa kwenye chumba chao cha kulala, lakini mwili wake ulikutwa kwenye chumba chao yeye na mkewe cha kulala.

Majeraha aliyodai kuyapata wakati wa jitihada zake za kutaka kuwaokoa wanae hayafanani na jinsi alivyoeleza, na hata uchunguzi wa kitabibu aliofanyiwa katika Hospitali hakuonekana kuwa alimeza moshi, jambo ambalo liliwashangaza wataalamu hao wa uchunguzi wa moto kwamba iweje mtu aliyejiokoa ndani ya nyumba iliyokuwa inaungua kiasi cha kushindwa kuwaokoa wanae atoke salama bila hata kumeza moshi...!

Shahidi mmoja alidai kwamba Willingham angeweza kurudi ndani ya nyumba yake ili kuwaokoa wanae kabla moto haujakuwa mkubwa wa kutisha lakini badala yake alikimbilia kuondooa gari lake lisiungue. "kitendo hicho si cha mtu aliye na uchungu wa watoto wake walioko ndani ya nyumba inayoteketea kwa moto." Alisema Sajenti Jimmie Hensley askari kiongozi wa upelelezi wa kutoka katika kituo cha Polisi cha Corsicana.
Pamoja na Willingham kusingizia hitilafu ya umeme kwenye kifaa cha kupashia vyakula moto (Microweve) lakini askari hao wa upelelezi hawakuona dalili yoyote ya hitilafu hiyo. Waligundua kwamba vifaa vyote vya umeme katika chumba cha watoto vilikuwa vimezimwa na mtungi wa gesi ya kupikia haukuonekana kuwa na hitilafu ya kuvuja lakini waligundua sampuli ya kitu kilichoungua kikiwa kwenye ukuta na sakafuni kuashiria kwamba kulikuwa na aina fulani ya kimiminika kinachosababisha mlipuko kilichotumika kuwasha moto huo.

Wakati huo huo wapelelezi wa Polisi walianza kusikia habari za ugomvi wa mara kwa mara kati ya Willigham na mkewe Stacy, zikiwemo tuhuma kwamba kuna wakati aliwahi kumpiga mkewe ili amsababishie mimba kutoka.
Pia Polisi walidai kwamba aliwahi kumwambia mama mkwe wake kuwa anaamini anaweza kulaumiwa kwa vifo vya watoto wake kutokana na majeraha yasiyo ya kawaida shingoni mwa mwanae Amber.

Willingam aliamatwa mnamo Januari 8, 1992, siku moja kabla ya kusherehekea miaka 24 ya kuzaliwa.. alinukuliwa akimwambia mama yake wa kambo, "sina nafasi ya kuepuka tuhuma hizi."

Je huyu Cameron Willingham Todd ni nani? Je kwa nini alituhumiwa kwa mauaji ya watoto wake mwenyewe……?

Willingham hakuwa mzaliwa wa mji ule wa Corsicana, alitokea katika mji mmoja ulioko maili 60 kusini mwa jimbo la Dallas. Tofauti na Willingham, familia ya Stacy ina mizizi katika mji huo wa Corsicana, kwani hapo ndipo chimbuko la familia yao lilipoanzia. Willingham alihamia katika mji huo na kuungana na Stacy baada ya kutoka katika jela ya watoto watukutu iliyoko Oklahoma (Oklahoma Juvenile Boot Camp) kwa kosa la kuvunja masharti ya kifungo cha nje ..

Kutokana na tabia zisizofaa Willingham alishindwa kuendelea na masomo. Pia katika kipindi hicho alishawahi kuhukumiwa kifungo cha nje mara kadhaa kwa makosa ya udokozi wa kuvizia majumbani (Buglary), wizi na kuendesha gari akiwa amelewa na pia aliwahi kufungwa jela kwa kosa la kukutwa na silaha.

Baba yake Willingham aitwae Gene, aliachiwa mwanaye huyo akiwa na miezi 13, pale mkewe alipomtelekeza na kwenda kusikijulikana. Kwa kushirikiana na mkewe mwingine aliyemuao aitwae Eugenia, walimudu kumlea Willingham akakua kwa umri na kimo.

Mama yake wa kambo aliyemlea Eugenia Willingham aliwaambia askari wa upelelezi kwamba, Willingham na mkewe Stacy walikuwa na uhusiano wenye vurugu.

Kesi yake ilianza kusikilizwa hapo mnamo Agost 1992 na ilisikilizwa kwa siku tatu tu. Waendesha mashitaka walimpa nafasi ya kukiri makosa ili ahukumiwe kifungo cha maisha badala ya kunyongwa lakini alikataa akidai kwamba hana hatia.

Waendesha mashitaka katika kesi hiyo walidai kwamba, Willingham alikuwa na nia (Motive) ya kuangamiza watoto wake ili kuepuka mzigo wa malezi kwa watoto hao. Waendesha mashitaka hao walidai kwamba, moto ule uliotekekeza watoto lilikuwa ni jaribio la tatu kufanywa na Todd baada ya majaribio yake mawili ya kumpiga mkewe wakati wa ujauzito wa kwanza wa mtoto Amber na wa pili wa watoto mapacha ili kumsababishia mkewe mimba kutoka.

Akitoa ushahidi wake mtaalamu wa uchunguzi wa moto Vasquez aliiambia mahakama kwamba kulikuwa na vidokezo vitatu ambavyo vilikuwa vinaonyesha dhahiri kwamba moto ule uliwashwa kwa makusudi na mikono ya mwandamu. Sampuli ya vifaa vilivyoungua vilivyokutwa kwenye mlango vilikuwa na viashiria vya aina fulani ya vimiminika vinavyosababisha mlipuko. Mtaalamu huyo aliendelea kusema kwamba Wilingham alijiokoa kutoka katika nyumba ile iliyokuwa imeshika moto akiwa pekupeku bila viatu, lakini hakukutwa na majeraha kuonyesha kwamba aliungua. Huo ni ushahidi tosha kwamba alimwaga kimiminika kile chenye kusababisha mlipiko akiwa anakimbia kutoka nje.

Hata hivyo pamoja na tuhuma hizo mwandishi moja aitwae David Grann, katika moja ya makala zake akizungumzia kesi hiyo alisema "ni kweli Todd aliwahi kumpiga mkewe mara kadhaa hata pale alipokuwa ni mjamzito, lakini kulikuwa hakuna ushahidi wa kipolisi au wa kitabibu unaothibitisha kwamba alikuwa na dhamira ya kutaka mimba ya mkewe itoke au ushahidi kwamba alitaka kuwaua wanae." Mwandishi huyo aliendelea kuandika, "hata mke wa Todd alipokuwa akihojiwa wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo alikanusha madai kwamba mumewe alikuwa na tabia ya kuwanyanyasa watoto kwa kuwapiga."

Stacy aliulizwa swali hiyo baada ya shahidi mmoja aliyekuwa gerezani kutoa ushahidi pale mahakamani. Shahidi huyo aliyetajwa kwa jina la Jonny Webb alikuwa anatumia chumba kimoja na Todd na katika mazungumzo yao alidai kwamba, Todd aliwahi kumweleza kuwa aliamua kuwasha moto ili kuwateketeza watoto wake ili kuficha majeraha au kifo cha mtoto wake mmoja ambaye aliumia kutokana na ugomvi wake na mkewe usiku uliopita. Kwa kawaida ushahidi wa aina hiyo hujulikana kama "jailhouse informant."


Mwendesha mashitaka aitwae John Jackson aliieleza mahakama kwamba Willingham alikuwa ni mwanaume mnyanyasaji aliyekuwa akimnyanyasa mkewe kwa kipigo au kwa kashfa zenye kuumiza hisia. Jackson pia alidai kwamba alikuwa ni mtesaji wa wanyama na alikuwa na tabia za kikatili zinazohusisha kuua. Lakini baadhi ya watu waliokuwa wanamfahamu Todd, walikuwa na mtazamo tofauti na waendesha mashitaka walivyomwelezea Todd. Afisa aliyekuwa akifuatilia mwenendo wake wakati alipokuwa akitumikia kifungo cha nje (Probation) aitwae Polly Goodin alikanusha kumuona Todd akiwa na tabia za kikatili zinazohusisha kuua. "alikuwa ni mmoja wa watoto niliowapenda sana wakati huo….." Alisema afisa huyo.

Pia Jaji Bebe Bridger ambaye ndiye aliyemhukumu kutumikia kifungo kwa kosa la kuiba alishindwa kuamini kama Willingham anaweza kuwa katili kiasi cha kuuwa wanae. "Alikuwa ni kijana mpole na anayeonekana kujali kuhusu uhai wa mwingine…." Alisema Jaji huyo ambaye kwa sasa amestaafu.

Mtuhumiwa hatiani na ahukumiwa kunyongwa...........!

Mnamo Octoba 29, 1992, Jopo la majaji na baraza la washauri katika kesi hiyo walitumia muda usiozidi saa moja kupitia kesi hiyo ambapo Todd alipatikana na hatia ya mauaji na kuhukumiwa kunyongwa. Kwa muda wa alitumia miaka kumi na moja na nusu kukata rufaa mara kadhaa ambapo rufaa hizo zilitupwa na hata maombi yake ya kutaka aonewe huruma nayo hayakukubaliwa. Baada ya mumewe kuhukumiwa Kunyongwa mkewe Stacy aliomba talaka rasmi na kuachana na mumewe Willingham.

Familia yake ilichanga fedha kwa ajili ya kumuwekea wakili, na pia kutaka kesi hiyo isikilizwe upya, lakini hilo halikuwezekana. Waendesha mashitaka na mashahidi wa upande wa mashitaka katika kesi hiyo walimuita muuaji kichaa na walifananisha mchoro wa fuvu la kichwa alilojichora katika mkono wake kuwa ni ishara ya imani ya kishetani.

Hata hivyo mnamo mwanzoni mwa mwaka 2004 Mwanasayansi mmoja na mtaalamu wa uchunguzi wa moto Dr. Gerald Hurst ambaye ana Ph.D. katika kemia, aliipitia ushahidi ulioandaliwa na Manuel Vasquez. katika taarifa yake alisema kwamba hakukuwa na ushahidi wa nyumba ile kuchomwa moto kwa makusudi kama alivyodai Manuel Vasquez. Dr. Hurst ushahidi uliomtia hatiani Willingham ulikuwa na makosa mengi ya kitaalamu na ulipitwa na wakati. Kesi hiyo pia ilipitiwa upya na wachunguzi kadhaa ambao ni mahiri katika taaluma hiyo ya uchunguzi wa moto na wote walikuja na majibu yanayofanana na ya Dr. Hurst. Repoti ya Dr. Hurst ilitumwa kwenye ofisi ya gavana wa jimbo la Texas Rick Perry pamoja na bodi ya inayotoa msamaha na kifungo cha nje (Board of Pardons and Paroles) ikiambatanishwa na maombi ya Todd ya kuomba aonewe huruma, lakini ripoti hiyo haikujibiwa. Taarifa iliyopatikana kutoka katika mradi wa kuwatoa hatiani watu waliohukumiwa kimakosa (Innicence Project) ulioasisiwa na mwanasheria mahiri na maarufu nchini humo Barry Scheck ilisema kwamba, mamlaka ya jimbo la Texas ilipokea rpoti hiyo lakini ilikaa kimya bila kuchukua hatua zozote zinazostahili juu ya kesi hiyo.

Hata hivyo bodi hiyo ilikiri kupokea ripoti hiyo ya Dr. Hurst lakini ilipinga kupokea maombi ya Willingham ya kutaka kuonewa huruma na bodi hiyo na kupunguziwa adhabu. Gavana Rick Perry alikataa kuongeza muda wa kunyongwa kwa Willingham. Msemaji wake alisema, "gavana alifanya uamuzi kwa kuzingatia ukweli wa kesi." Gavana Perry aliendela kusema, "Watu walidhani kwamba wataalam walikuwa na makosa, na nisingependa musikilize propaganda za wanaopinga hukumu ya kifo." Gavana Rick Perry ndiye aliyechukua nafasi ya Gavana George Bush aliyegombea urais wa nchi hiyo na kushinda kwa vipindi viwili. Rick Perry ndiyer Gavana wa jimbo hiolo la Texas hadi hivi sasa.

Akizungumza kupitia kwa msaidizi wake aitwae Mary Anne Gavana Perry alisema kwamba hata tume ya mwanasayansi Craig Beyler ambayo ilikadiriwa ingetumia kiasi cha dola 30,000 ilikuwa ni kupoteza bure fedha za walipa kodi. Baadhi wa wanaharakati walipinga kauli hiyo. "Haiwezekani, yaani serikali iko tayari kuua kuliko kupoteza fedha za walipa kodi..... Hii inamaanisha kwamba fedha ni bora kuliko uhai wa mtu........!" Alionekana kushangaa mwanaharakati mmoja.

Katika hali isiyo ya kawaida mmoja wa waendesha mashitaka aitwae Jackson alikiri kwamba ripoti ya kitaalamu iliyomtia hatiani Todd ilikuwa na kasoro kadhaa, lakini hata hivyo alisisitiza kwamba, kulikuwa na sababu nyingine imara zilizomtia hatiani.

Ushahidi mwingine wa Johnny Webb pia ulikuwa na kasoro. Mkumbuke kwamba huyu Jonny Webb ndiye aliyedai kwamba, Todd aliwahi kumweleza kuwa aliamua kuwasha moto ili kuwateketeza watoto wake ili kuficha majeraha au kifo cha mtoto wake mmoja ambaye aliumia kutokana na ugomvi wake na mkewe usiku uliopita. Webb baadae akiongea na mwandishi wa gazeti la The New Yorker alisema, "Inawezekana kabisa, kwamba sikuelewa kile alichonieleza. Kufungwa katika chumba kidogo inakufanya unakuwa kama mwendawazimu. Kumbukumbu zangu hazikuwa sahihi kwani nilikuwa niko kwenye matibabu ambapo nilikuwa natumia madawa mengi wakati huo. Kila mmoja anajua kuhusu hilo." Webb baadae alilazwa kwa matibabu ya yanayohusiana na ugonjwa wa akili,(Bipolar Disorder). Baada ya kutoa ushahidi huo mwendesha mashitaka Jackson alifanikiwa kumtoa jela mapema kabla ya kumaliza kifungo chake.

Pamoja na ushahidi uliomtia hatiani kugubikwa na utata, Willingham anyongwa.............!

Mnamo Februari 17, 2004 Cameron Todd Willingham akiwana umri wa miaka 36 alinyongwa katika gereza la Penitentiary gereza liliko katika mji wa Huntsville jimboni la Texas nchini humo. Wakati alipoulizwa kama anayo kauli yake ya mwisho, Todd alisema….. "Ndio. Jambo ambalo ningependa kusema ni kwamba, mimi ni mtu nisiye na hatia ambaye nahukumiwa kwa kosa ambalo sikulitenda. Nimewekwa gerezani kwa miaka 12 nikisubiri kutekelezwa kwa hukumu hii kwa kosa ambalo sikulifanya. Nilikuja kwa mavumbi na ninarudi kwa mavumbi…."

Baada ya kusema hivyo, alimgeukia aliyekuwa mke wake Stacy Kuykendall aliyekuwepo hapo kushuhudia akinyongwa na kumwambia........

"We mwanamke kahaba, natumaini utaozea jehanam………." Willingham alirudia kauli hiyo mara tatu.

Baada ya kusema maneno hayo alichomwa sindano ya sumu na kukata roho. Ilitangazwa rasmi kwamba Todd alikata roho saa 12:20 jioni, ikiwa ni dakika 7 baada ya kuchomwa sindano hiyo, inayoingizwa kupitia katika mshipa mkubwa wa damu kwa mtindo wa 'drip'.

Tangu kunyongwa kwa Todd, kumekuwa na maswali mengi kuhusiana na ushahidi uliomtia hatiani watu wengi nchini humo walidai kwamba, ushahidi uliomtia hatiani haukuwa na mashiko. Akijibu tuhuma kwamba ametia saini ya kunyongwa kwa mtu asiye na hatia Gavana Rick Perry alinukuliwa akisema, "Alikuwa ni mume mkatili kwa mkewe na kesi hii iliegemea zaidi kwenye ushahidi wa kisayansi zaidi." Akizungumzia jambo hilo msemaji wa Gavana huyo Bi, Katherine Cesinger alisema kwamba, Gavana Perry alipima ushahidi wote uliomtia hatiani Willingham, na pia anafahamu kuhusu tafsiri mbalimbali zilizotolewa na watalaamu kuhusiana na shahidi huo.

Dr. Gerald Hurst aliyeipitia kesi hiyo upya ikiwa ni pamoja mkanda wa video alisisitiza kusema kwamba ule moto haukuwashwa kwa makusudi kama wataalamu waliofanya nuchunguzi walivyodai…. Kwa maneno yake mwenyewe alisema…. "hakuna kitu chochote kinachoweza kunishawishi kuamini uchunguzi uliofanywa na wataalamu kwamba moto ule uliwashwa kwa makusudi. Kwangu mimi ule ulikuwa ni moto wa kawaida tu uliosababisha ajali ile…"

Taarifa hiyo ilipingwa vikali na mwendesha masitaka John Jackson.

Mwezi mmoja tangu Willingham anyongwe gazeti la Chicago Tribune, lilichapisha taarifa ya wataalamu wa uchunguzi wa kihalifu. Mradi wa kuwatoa hatiani watu waliohukumiwa kimakosa (Innocence Project) iliwakutanisha wataalamu mahiri watano wa kujitegemea wanaosifika kwa uchunguzi wa vyanzo vya majanga ya moto ili kupitia ushsidi huo kwa makini. Wataalamu hao walitoa ripoti yao ya kurasa 48 ambayo ilionyesha kwamba ushahidi wa kisayansi uliotumika kumtia Willingham hatiani ulikuwa umepitwa na wakati.

Mradi wa kuwatoa hatiani watu waliohukumiwa kimakosa (Innocence Project) waingilia kati na kuamuru uchunguzi urudiwe...........!

Mnamo mwaka 2006 Mradi wa huo wa kuwatoa hatiani watu waliohukumiwa kimakosa (Innocence Project) uliipeleka kesi hiyo kwenye tume ya kisayansi ya uchunguzi wa mauaji ya jimbo Texas ikiitaka tume hiyo itumie mamlaka yake kuamuru uchunguzi wa kesi hiyo ufanyike upya. Pamoja ripoti ya kesi hiyo, mradi huo pia uliambatanisha taarifa nyingine ya kesi ya uchomaji moto iliyowahi kutokea jimboni humo. Katika kesi hiyo ushahidi uliotumika kumtia hatiani mtuhumiwa huyo Ernest Willis na kuhukumiwa kunyongwa, ulikuja kutenguliwa baadae na mtuhumiwa huyo kuachiwa huru kwa sababu ushahidi huo ulikuwa umepitwa na wakati.

Mnamo June 2009 serikali ya jimbo la Texas lilamuru kupitiwa kwa kesi hiyo upya. Mnamo August 2009 ikiwa ni miaka 14 tangu tukio hilo la moto na miaka mitano tangu kutekelezwa kwa hukumu hiyo. Ripoti hiyo iliandaliwa na mtaalamu wa uchunguzi wa moto Dr. Craig Bayler ambaye alikodishwa na tume ya kisayansi ya uchunguzi wa mauaji ya Texas. Katika ripoti hiyo Dr. Craig alibainisha kwamba matokeo ya uchunguzi wa awali hayakuwa sahihi.

Mnamo mwaka 2008 tume ya kisayansi ya uchunguzi wa mauaji ya jimbo la Texas ilikubali kufanya uchunguzi wa kesi hiyo. Jopo hilo la wachunguzi waliokodishwa na tume hiyo lilitoa ripoti hapo mnamo mwaka 2009. Katika ripoti hiyo jopo hilo lilibainisha kwamba, wataalamu waliochunguza kesi hiyo na kutoa ushahidi mahakamani dhidi ya Willingham na kumtia hatiani, ushahidi wao haukuwa sahihi.


Mnamo August 2009 ilitolewa taarifa yakiwemo maelezo kutoka kwa kaka wa Stacy mke wa Willingham aitwae Ronnie Kuykendall ambaye alikuwa ni shemeji yake na Willingham. Maelezo hayo aliyaandikisha hapo mnamo mwaka 2004. Kwa mujibu wa maelezo yake alidai kwamba, dada yake, yaani Stacy Kuykendall aliyekuwa mke wa Willingham kabla hawajaachana aliwahi kumwambia kwamba Willingham aliwawahi kukiri kwake yeye Stacy kuwa ndiye aliyewasha moto.

Pia Stacy mwenyewe aliwahi kulieleza gazeti moja maarufu liitwalo Fort Worth Star-Telegram hapo mnamo Oktoba 25, 2009, wiki moja kabla kutekelezwa kwa hukumu ya kunyongwa kwamba Willingham alikiri mbele yake kwamba aliwasha moto kwa sababu yeye Stacy alimtishia kumuacha siku mmoja kabla ya tukio hilo.

Hata hivyo Stacy alikanusha taarifa zote mbili, ile ya kaka yake na ile yakwake akidai kwamba mahusiano yake na Willingham yalikuwa yako imara kabla ya moto ule. Mnamo mwaka 2010 Stacy alikiri kwamba Mumewe Willingham aliwauwa watoto wake Amber, Karmon na Kameron. Aliwachoma moto...! "Alikiri mbele yangu kwamba aliwaua na amehukumiwa kwa kosa hilo….." Alisema Stacy.

Jopo la watu wanne wa Tume ya kisayansi ya uchunguzi wa mauaji ya Texas ilichunguza kwa makini ushahidi uliotolewa katika kesi hiyo. Mnamo Julai 23 2010, tume hiyo ilikubali kwamba ushahidi wa kisayansi uliomtia Willingham hatiani ulitengenezwa kiujanja. Tume hiyo ilibaini kwamba Mkuu wa kitengo cha uchunguzi wa moto Manuel Vasquez (Ambaye ni marehemu) na naibu mkuu wa uchunguzi wa majanga ya moto katika mji huo wa Corsicana Douglas Fogg walighafilika au walipotoka katika uchunguzi wao wa kitaalamu walioufanya katika eneo la tukio.

Mnamo mwaka 2010 Mradi wa kuwatoa hatiani watu waliohukumiwa kimakosa (Innocence Project) ulifungua kesi dhidi ya jimbo la Texas ili kupinga hukumu hiyo ya ukandamizaji………

Kizungumkuti cha shauri hili bado kinaendelea................... .!

 
Last edited by a moderator:
Haya wadau kama kawaida, wiki hii nimekuja na kesi hii ambayo kwa kweli pamoja na mtuhumiwa kunyongwa lakini bado kuna utata mkubwa uliogubika ushahidi uliomtia hatiani........... Kuna mengi ya kujifunza katika kesi hii.

Kwa leo sina mengi ya kusema, naomba tukutane Ijumaa ijayo.................................
 

Kama Jamaa aliamshwa na mwanae kisha akaenda kusogeza gari lisiungue : Why hakuwafikiria wanae kwanza? Hata huyo aliyemuamsha bado aliachwa ndani ya nyumba?

This is indeed a weird case ambapo kama jamaa angewaokoa wanae asingedhaniwa na akanyongwa
 
hivi watu wengine ni mashetani au? unawahije kutoa gari, huku twins na dada yao wanaungua?? imeniliza wallah, nime-imagine ni twins wangu na dada yao wanateketea! lol hakika NITAKUFA, MUNGU APISHIE MBALI, AMEN!
 
It is so sad,
Kwa kweli hii kesi inautata mwingi sana but hili la kukimbiza gari badala ya watoto mhh???
Ufunguo wa gari ulikuwa wapi?

Lakini pia yawezekana mambo ya ukata aliokuwa nao, akili ilimpeleka moja kwa moja kwa kile alichokuwa anaona ndio mali aliyo nayo tu, na akitegemea kuwa angeweza kuwahi kubeba watoto kumbe huku nyuma moto ukawa umezidi.

Kuna mafuriko yametokea hapa bongo mama mmoja kakimbiza TV kaacha mtoto kitandani, kurudi mtoto kisha CHUKULIWA NA MAJI.

Sijui huwa akili zinakutoka ukipata janga hata sielewi maana huyu mama ingekuwa ulaya sijui angeshtakiwa kwa kuua makusdi? Nashindwa kuelewa.
 
Huyu muuaji bhna! tena ni bora wangemuwashia moto na yeye akaungua kama alivowaunguza watoto wake! ni wazi ameua, na ushahidi mmoja ni pale alipoenda kusogeza gari isiugue!
 
Halafu angalia ile picha ya juu kabisa! huyu jamaa muuwaji! amebeba mtoto shingoni, mtoto ndio ameshikilia vidole vya baba yake asianguke ! yeye ameachia ! hivi mtu kama huyu si muuwaji tu! je mtoto angachia hivo vidole si angedondoka na kufilia mbali! bhana huyu muuwaji ! hiyo picha inajionesha !
 
jamani dunia ina mambo!
na hao mawakili wanaosema moto haukuwashwa na Cameron...sasa chanzo cha moto ni nini?!?!?
 
Duh!...
Inasikitisha sana lkn mm sidhani kama huyo jamaa anahusika wazi inautata sana hii kesi na huyo mama mara anapinga wkt mwingine anakubali kwamba jamaa alimwambia alifanya makusudi ninamashaka nae.
Pia naona kuna kitu huyo jamaa alikufa nacho tu hakutaka kukisema kama mke wake anakiri walikuwa na uhusiano imara ilikuwaje amwite kahaba na kumwambia ataozea jehanam?...
full utata!...
 
Hapa mungu ndie anaejua ukweli. Ila kibinadamu ni hivi;
Kwa nn Todd baada ya kuamshwa na mtoto wake kitandani akafanikiwa kutoka nj'e peke yake bila hata na mtoto mmoja?
Kwa nn Todd hakukutwa na majeraha ya moto ili kudhihirisha alijaribu kwa hali na mali kuokoa familia yake lakin ilishindikana?
Kwa misingi hiyo Todd hasingeweza kunusulika ktk hii kesi.

Kwa mimi ningeshauri Todd afungwe kifungo cha maisha badala ya kunyongwa.
 
Duh!...
Inasikitisha sana lkn mm sidhani kama huyo jamaa anahusika wazi inautata sana hii kesi na huyo mama mara anapinga wkt mwingine anakubali kwamba jamaa alimwambia alifanya makusudi ninamashaka nae.
Pia naona kuna kitu huyo jamaa alikufa nacho tu hakutaka kukisema kama mke wake anakiri walikuwa na uhusiano imara ilikuwaje amwite kahaba na kumwambia ataozea jehanam?...
full utata!...

Mimi nadhani hiki kitu WALIKIPANGA WOTE yeye na mkewe kuangamiza hawa watoto, nadhani ni hivo
 
the power of innocence........Todd kosa lake lilikua sio la kuua bali alikosea priority ktk uokoaji....ningekua gavana ningempiga hata 10 yrs bt hakustahili kunyongwa au kifungo cha maisha...
 
hivi kwa nini hawa watu weupe aka wazungu hawawezi kuimili ugumu wa maisha!.....kwa fikra za harakaharaka tu jamaa nahusika na mauaji wa watoto,huwezi thamini gari ukaacha watoto wanaangamia, Mungu azilaze roho za marehemu pema peponi
 
No doubt Billy ndiye aliechoma hiyo nyumba, maneno yake ya mwisho ni kujitetea tu hana lolote. Anaonesha tu kuwa ni hard criminal tu.
 
It is so sad,
Kwa kweli hii kesi inautata mwingi sana but hili la kukimbiza gari badala ya watoto mhh???
Ufunguo wa gari ulikuwa wapi?

Lakini pia yawezekana mambo ya ukata aliokuwa nao, akili ilimpeleka moja kwa moja kwa kile alichokuwa anaona ndio mali aliyo nayo tu, na akitegemea kuwa angeweza kuwahi kubeba watoto kumbe huku nyuma moto ukawa umezidi.

Kuna mafuriko yametokea hapa bongo mama mmoja kakimbiza TV kaacha mtoto kitandani, kurudi mtoto kisha CHUKULIWA NA MAJI.

Sijui huwa akili zinakutoka ukipata janga hata sielewi maana huyu mama ingekuwa ulaya sijui angeshtakiwa kwa kuua makusdi? Nashindwa kuelewa.
inachekesha na kuhuzunisha at the same time!! asingeshtakiwa maana hakusababisha mafuriko.
 
mi naona huyu jamaa alikuwa mgonjwa wa akili .. inawezekana moto hajawasha yeye lakini kuna screw imeloose kichwani haiwezekan ukaokoe gari yako na kuacha watoto ndani ..? either alikuwa high kipindi moto ukiwaka ...


R.I.P willie
 
Inawezekana jamaa hahusiki kabisa ila kilichomponza ni historia yake ya matukio yasiyo ya kawaida, na hiyo ndo iliyopelekea akachunguzwa zaidi kuliko mkewe. Kwa nini moto uliwaka baada ya Stacy kuondoka?:baby:
 
Back
Top Bottom