Kauli za Salim, Warioba zautikisa utawala wa Kikwete

Pdidy

JF-Expert Member
Nov 22, 2007
50,956
22,138
Kauli za Salim, Warioba zautikisa utawala wa Kikwete





Rais Kikwete: Kauli za viongozi waandamizi wastaafu zinasemekana kutikisa serikali yake.

*Wasomi, Wazee wa CCM waonya

Na Waandishi wetu


MAWAZIRI wakuu wa zamani, Jaji Joseph Warioba na Dk Salim Ahmed Salim walikuwa wakizungumza siku moja wakiwa maeneo tofauti, lakini kauli zao kuhusu uendeshaji nchi wa serikali ya awamu ya nne zilifanana na hakuna shaka kwamba, zimeutikisa utawala wa Rais Jakaya Kikwete.


Wote wawili walitoa kauli zinazoonyesha kuwa nchi inayumba na kwamba vita inayoendelea dhidi ya rushwa haiwezi kufanikiwa kama serikali haitapambana kuuondoa mfumo ambao unalea rushwa, huku wakimuelezea Rais Kikwete kuwa anashauriwa vibaya.


Mara baada ya vyombo vya habari kuchapisha habari ya vigogo hao, mweka hazina wa CCM, Amos Makala alijibu kwa maneno makali, akielekezea shutuma zake kwa Warioba ambaye alimtuhumu kuwa hajawahi kuzungumzia mazuri ya Kikwete na kwamba hata wakati akishikilia nafasi ya waziri mkuu, kulikuwa na matatizo.


Kauli ya Makala ilifuatiwa na kauli ya makamu mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa ambaye alisema Warioba na Dk Salim wanao uhuru wa kutoa maoni yao dhidi ya serikali kama ilivyo kwa wananchi wengine.


Wasomi na wanasiasa walioongea na Mwananchi Jumapili wameeleza bayana kuwa kauli hizo za vigogo hao zinaashiria kuwa serikali ya Kikwete inakwenda kombo.


Wanaona kuwa hali hiyo inatokana na serikali kukosa mwelekeo wa baadhi ya viongozi waliopo serikalini na utashi wa kisiasa.


Mkuu wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Bertram Mapunda aliiambia Mwananchi Jumapili kuwa viongozi wa nchi hawana mwelekeo na hawajui pa kuipeleka nchi.

“Viongozi wanatakiwa wawe na vision (uwezo wa kuono mbali). Kwa sasa tunaendaenda tu; hatuna mwelekeo; kiongozi anatakiwa akae chini kufikiria baada ya kupewa madaraka ajue ataipeleka wapi nchi.


Wakati mwingine inatakiwa hata ikibidi achukue likizo ili ajipange namna ya kutekeleza ahadi alizotoa wakati wa kampeni,” alisema Profesa Mapunda bila ya kufafanua kauli yake kuihusisha na matamko ya mawaziri wakuu hao wa zamani.


Naye katibu mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa alidai serikali ya Rais Kikwete haina uongozi mzuri na ndio sababu nchi inaelekea kubaya na akawamwagia sifa Warioba na mkurugenzi wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku kwa kauli zao.


Alisema kitendo cha vigogo hao kuamua kuzungumzia hadharani hali na mwelekeo mbaya wa nchi kutokana na kushamiri kwa vitendo vya ufisadi na rushwa, ni dalili njema na kwamba hiyo inaonyesha wazi kuwa hata wao wameanza kukerwa na wanajiunga na kambi ya wanaharakati katika kutetea haki za wanyonge.


Dk Slaa aliliambia Mwananchi Jumapili jana kuwa kukosekana kwa uongozi mzuri ndiko kunakofanya watendaji wafanye kazi zao kiholale na kuendeleza vitendo vya kifisadi kwa kuwa hawana mtu wa kuwafokea.


Alisema yeye binafsi amekuwa akipiga kelele juu ya kushamiri kwa vitendo vya ufisadi na rushwa hapa nchini, lakini hakuna hatua zinazochukuliwa na hivyo akasema kitendo cha Warioba na Butiku kusimama kidete kusema hadharani udhaifu huo ni dalili njema kwao kwani kilio chao kimesikika.


“Kitendo cha wazee waliowahi kushika nafasi za juu serikalini na ndani ya chama tawala, kuzungumzia hayo hadharani ni dalili njema kwamba, sasa watu wameanza kuona ukweli,” alisema Dk Slaa, ambaye ni mbunge wa Karatu.


Dk Slaa alishangazwa na kitendo cha serikali kushindwa kuchukua hatua kwa watuhumiwa wa kashfa ya ununuzi wa rada na kuiachia Serikali ya Uingereza pekee kufanya kazi hiyo.


“Hawa watuhumiwa watashtakiwa kwa sheria za Uingereza wakati Tanzania ni taifa linalojitegemea,” alisema.

“Niliwahi kutoa mapendekezo kuwa John Chenge na Dk Idris Rashid wafikishwe mahakamani kutokana na tuhuma za ufisadi, lakini serikali iko kimya hadi taasisi ya nje ya SFO (ya kuchunguza jinai kubwa) imekamilisha kazi zake.

”Sasa kama itawafungulia kesi watuhumiwa, watashtakiwa kwa sheria za Kiingereza ambazo hazitakuwa na manufaa kwetu.”

Naye Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahimu Lipumba amewataka Jaji Joseph Warioba, Dk Salim Ahmed Salim na Joseph Butiku kuvaa ujasiri wa baba wa taifa Mwalimu Julius Nyerere kwa kueleza kiini cha matatizo ya kuyumba kwa nchi.


Akizungumza katika mahojiano maalum na Mwananchi, Dk Salim ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, alisema mfumo wa serikali umeoza kwa rushwa pamoja na kwamba serikali inajitahidi kupambana nayo.


“Rais Kikwete anajitahidi na ana nia ya kupambana na rushwa, lakini bado 'system' (mfumo) haijajitayarisha vya kutosha kupambana rushwa,“ alisema Dk Salim ambaye aliwahi kuwa katibu mkuu wa Umoja wa Afrika (OAU).

Kuhusu uchaguzi ujao, Dk Salim alisema kuwa wanachama wa chama hicho wanaotaka kugombea urais sambamba na Jakaya Kikwete, waachwe wapambane naye, lakini akasema hawatamuweza.

Lakini Dk Salim alisema Wanachama wa CCM wana haki ya kupambana na Kikwete kuwania kuteuliwa kugombea urais kwa tiketi ya chama hicho tawala.

Naye Warioba aliwaambia waandishi wa habari kuwa nchi inaelekea kubaya anapoangalia jinsi mambo mbalimbali yanavyoendeshwa, huku akisema kuwa serikali haitaweza kushinda vita dhidi ya rushwa iwapo haitaelekeza nguvu zake katika kupambana na mfumo unaolea tatizo hilo.


Warioba, ambaye alishika nafasi hiyo ya mtendaji mkuu wa serikali kwenye miaka ya themanini, alisema kwa sasa taifa linakabiliwa na matatizo mengi kuanzia ya ukosefu wa maadili ya uongozi, rushwa na hata utaratibu mzima wa kuendesha mambo na kubainisha kuwa kuna pengo kubwa katika kuaminika kwa serikali.


Jaji Warioba alisema hivi sasa kuna dalili ya umoja wa Watanzania kusambaratishwa, watu kugawanywa makundi kwa udini na ukabila pamoja na kuwepo kwa matabaka ya matajiri na maskini.


Naye Butiku wiki hii alipigilia msumari mwingine aliposema utawala wa awamu ya nne bado una kazi kubwa katika mapambano dhidi ya rushwa pamoja na jitahidi za kupambana nayo.


Butiku alisema licha ya serikali kutumia mbinu mbalimbali bado rushwa imeendelea kushamiri kwenye chama na serikali na kwamba sasa imevuruga mfumo wa nchi.
 
Tena ni current topic.Mara nyingine kuangalia kidogo what is current kunasaidia kuondoa duplication.

__________________
KAZI YA MODERATOR NAFIKIRI SI YANGU WALA YAKO

NASHUKURU KUNIJULISHA
 
Tena ni current topic.Mara nyingine kuangalia kidogo what is current kunasaidia kuondoa duplication.

__________________
KAZI YA MODERATOR NAFIKIRI SI YANGU WALA YAKO

NASHUKURU KUNIJULISHA

Hapana,

Ukileta madudu ni wajibu wa kila mtu kusema, haihitaji moderator.

On top of that you are contradicting yourself, mara si kazi yangu, mara unanishukuru.
 
Back
Top Bottom