Sumbalawinyo
JF-Expert Member
- Sep 22, 2009
- 1,282
- 247
CCM
Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam, Haji Manara, amekamatwa na polisi mkoani Dar es Salaam kwa tuhuma za kutapeli magari 18 kwa kutumia jina la chama hicho.
Magari ambayo Manara anadaiwa kutapeli, baadhi yanamilikiwa na watu binafsi na mengine yanamilikiwa na makampuni ya kuuza magari ya jijini Dar es Salaam.
Kigogo huyo wa CCM Mkoa, ambaye pia ni mtoto wa mwanasoka mashuhuri wa zamani nchini, Sunday Manara, alikamatwa juzi kwa tuhuma hizo na kushikiliwa katika kituo cha polisi Magomeni hadi jana mchana alipotolewa kwa dhamana.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Elias Kalinga, alithibitisha kukamatwa kwa Manara na kusema kwamba, magari manne, ambayo anadaiwa kuyatapeli, yanashikiliwa katika kituo hicho na kwamba, uchunguzi wa suala hilo bado unaendelea.
Kalinga aliiambia Nipashe kuwa magari manne yanayoshikiliwa na polisi, yalikutwa kwa watu tofauti, ambako Manara anadaiwa kuyaweka rehani kwa kupewa mkopo wa fedha.
Kamanda Kalinga alisema kuwa magari mengine 14 yaliyosalia, bado yanatafutwa na polisi.
Kamanda Kalinga alisema kuwa kati ya magari, ambayo Manara anatuhumiwa kutapeli, 11 yanamilikiwa na mtu mmoja, sita mtu mmoja na moja linamilikiwa na mtu mwingine.
Alisema wamiliki wa magari hayo, ndio waliowasilisha polisi malalamiko kuhusu utapeli unaodaiwa kufanywa na kada huyo.
Kamanda Kalinga alisema kuwa katika tuhuma hizo, Manara anadaiwa kuwa alitapeli magari hayo kwa nyakati tofauti, baada ya kuwafuata wamiliki wake na kuwalaghai kuwa wanahitaji kuyakodi kwa ajili ya shughuli za chama katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika mwaka jana.
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ngazi za mitaa, vitongozi na vijiji ulifanyika nchini kote Oktoba 25, mwaka jana.
Akikodi analipeleka gari kuweka rehani kwa mtu mwingine ili apewe pesa. Akipewa pesa, siku nyingine anarudi tena kwa mtu yule yule aliyempa pesa amuongeze pesa nyingine na aendelee kulishikilia gari husika, alisema Kamanda Kalinga.
Katika upelelezi wetu, tulionana na uongozi wa juu wa CCM, lakini wamekanusha kuwahi kumtuma kwa shughuli hiyo. Wametwambia CCM wanayo magari ya kutosha, aliongeza:
Tunafanya uchunguzi kubaini kama alikiuka sheria, kama itabainika kuwa alikiuka sheria, atachukuliwa hatua za kisheria.
Habari zilizopatikana jana, zinaeleza kuwa Manara aliachiwa na polisi jana mchana, baada ya Mbunge wa Ilala, Mussa Azan Zungu (CCM) kumchukulia dhamana katika kituo cha polisi alikokuwa akishikiliwa tangu juzi.
CHANZO: NIPASHE