KATIBA MPYA - U'CCM', U'CHADEMA', UDINI na USHABIKI

Jul 3, 2012
92
13
Je, tuko tayari kupokea majibu yatakayotokana na Mchakato wa Katiba Mpya?
Katika siku za karibuni kumeibuka mijadala mingi katika siasa za Tanzania. Kwa bahati mbaya, kwa masuala ambayo yanahitaji UTAIFA, Watanzania tumekua tunatumia muda mwingi kujadili kutokana na mapenzi tu ama ya Kisiasa, ama kwa sababu nyingine yeyote ile.
Katika mitandao ya jamii, lugha ya kashfa ndiyo iliyojaa, badala ya hoja mahususi. Hivi sasa, ni rahisi tu, bila kuangalia hoja husika, kubandikana majina „“wewe fisadi“; “wewe magamba“; “wewe CCM“; “wewe CHADEMA“, nk. Ni wazi kwamba hoja yenye maslahi kwa TAIFA, haijibiwi tu kwa kumbandika mtu jina. After all, kila mtu ana haki ya kuchagua chama anacho kitaka. Madhumuni ya Mfumo wa vyama vingi ni kuruhusu fikra mbali mbali. Mwanachama wa CCM au CHADEMA au CUF, UDP, TLP, NCCR, nk hatokua anania nzuri na taifa iwapo atataka Chama Chake tu ndio Kitawale. Madhara ya mfumo wa Chama Kimoja, hata kama kitakua CHADEMA au CUF, UDP, TLP, NCCR, nk ni kwamba tutarudi katika hali ile ile…”wabunge kutetea serikali”
Haya, hayo ya vyama tuyaache. Hivi sasa haya ya Muungano nayo yamesababisha watu kutupiana matusi yasiyo ya maana. Wapo wanaowatukana wenzetu wa visiwani matusi makubwa makubwa, na wapo pia wa visiwani wanaofanya hivyo hivyo. Hii la Uamsho nalo, likaleta mambo mengine. Cha kushangaza pia katika hili, Watu hua hawajadili hoja, ila jazba imekua kubwa. Sitotaka kujikita kwenye masuala ya Muungano katika Mada hii, kwa sababu ya muda. Leo nataka tujitathmini tabia zetu katika mijadala ya kitaifa.
Tukija katika masuala ya kiimani ndio kabisa, wapo “Waislam” waliowaita Wakristo majina ya ajabu ajabu, lakini pia wapo “Wakristo” waliowaita Waislam majina ya ajab pia. Hapa pia, hua ninachokiona ni mashaka tu. Wapo Waislam wanaohisi kwamba Wakristo wanataka kuwakandamiza siku zote; na wapo Wakristo wanaohisi kwamba Waislam ni magaidi always. Pia yapo mambo ambayo pia hayana ushahidi, na wakati mwingine yanasababisha kero tu: kwa mfano, ni rahisi kuona kwenye mitandao ya kijamii, watu wakiandika kwamba, “Waislam siku zote wanafelishwa” na Wakristo, bia kuangalia uhaisia wa shule nyingi zilizo chini ya taasisi za kiislam; na pia wapo Wengine ambao hutukana “Waislam siku zote ni wajinga”, bila kuangalia ukweli kwamba dini yenyewe ya kiislam inahimiza watu kutafuta elimu kokote kule – na ukweli kwamba wapo Maprofesa, Madaktari, Mainjinia, Wahasibu nk ambao ni waislam.
MASWALI KWA WATANZANIA WENZANGU
(a) Mnafahamu kwamba tutake tusitake ni lazima tuishi pamoja?
(b) Unafahamu kwamba kazi ya kuondoa jazba na matusi kwenye siasa inaanza na sisi kukemea vitendo hivyo na kutowachagua viongozi wenye kauli hizo?
(c) Mnafahamu kwamba kazi ya kutokomeza udini haianzi kwa Sheikh au Askofu, ila inaanza na sisi, mmoja mmoja?
(d) Mnafahamu kwamba kwa maendeleo na umoja wa kitaifa ni vema hoja zikatawala na sio ushabiki wa siasa au unasaba wa aina yoyote ile?
Labda nidokeze kwa kusema kua, Mambo haya ambayo kwa sasa yanaonekana kutugawa, moja au kadhaa katika haya yanaweza ndio yakawa majibu ya wananchi katika wakati wa kutoa maoni ya katiba mpya: mfano: Serikali za Majimbo kama inavyopendekezwa na CHADEMA; Serikali tatu za Muungano kama inavyopendekezwa na CUF; Kuvunjwa kabisa kwa Muungano, au hata Mahakama ya Kadhi!
Je, Tuko tayari kupokea maoni kama yatakavyoletwa na watanzania?
Rai yangu ni kwamba tuache USHABIKI katika mchakato huu, tuangalie mustakabali wa Taifa. Tuwe Tayari kupokea maoni yoyote ambayo yataonekana kua ndio chaguo la Watanzania. Tulainishe mioyo yetu kwa ajili ya UTAIFA
Mheshimu mwenzako bia kujali kabila, chama, imani, jinsia, hali yake ya uchumi, ulemavu e.t.c. Tusiseme tu “hatutaki” au “tunataka”. Tuseme “tuheshimu maoni ya watanzania juu ya katiba mpya”. Tuache uchochezi, dhana na fikra potofu dhidi ya Watanzania Wenzetu.
MUNGU BARIKI TANZANIA:
Tafadhali sambaza ujumbe huu juu ya UDINI NA MUSTAKABALI WA TAIFA
 
Back
Top Bottom