Karibuni mjiunge na chama cha kijamii

Jan 29, 2012
39
38
HOTUBA YA UTAMBULISHO WA CHAMA KIPYA CHA SIASA NCHINI CHA CCK

Utangulizi na Shukrani Ndugu wanachama, Waandishi wa habari Na Watanzania wote Leo hii ile ndoto ambayo ilikataliwa kutimia miaka miwili hivi iliyopita hatimaye imetimia leo. Ndoto ya kuweza kuwapatia Watanzania chaguo tofauti la kisiasa nchini lenye kubeba matarajio yao sasa limetimia. Kutimia kwa ndoto hii leo hii ni mwanzo tu wa safari ndefu ya kisiasa kwa wengi wetu.

Ni safari mpya lakini iliyojaa matumaini. Hivyo, ninayofuraha kubwa kuwaambia wanachama wetu waliotuunga mkono kila kona ya nchi hadi kufikia hatua hii kuwa hatutawaangusha kwani tumedhamiria kuchukulia imani mliyoweka juu yetu kwa uzito mkubwa na unaostahili. Kufika hapa tulipofika leo ni juhudi za watu wengi sana ambao hata nikiamua kuwataja kwa majina sitowezakuwatendea wote haki.

Hata hivyo, nitangulishe shukrani za dhati kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini kwa ushirikiano ambao wametupatia hadi kufikia hapa. Wametusahihisha tulipokosea, wametuelekeza tulipotaka ushauri na wakati ulipofika wa wao kufanya usaili wamefanya usaili wa wanachama wetu nchi nzima kwa weledi wa hali ya juu na kujiridhisha kuwa CCK siyo chama cha utani, siyo chama cha msimu, bali ni chama ambacho kimekusudia kujikita na kuzama kabisa katika jamii ya Watanzania na kuwa kweli chama cha jamii hiyo.

Nawashukuru wanachama na viongozi wenzangu ambao wametumia muda mwingi kwa kujitolea kufanya kazi mbalimbali za chama huku wakijua nyuma yake kuna kubezwa, kejeli, kuonekana vibaraka n.k

Hawa wametambua nafasi ya pekee ambayo CCK itakuja kufanya na hivyo waliamua kwa moyo wote kujitolea muda, vipaji na raslimali mbalimbali ili kuweza kufanikisha zoezi zima la kuwez akupata usajili wa kudumu. Ninawashukuru sana. Zaidi hata hivyo nawashukuru wanachama, mashabiki na wapenzi wetu ambao wamekuwa wakitutia moyo na kusimama pamoja nasi japo msukumo wa kutaka kukata tama ulipokuwa mkubwa hasa baada yale ambayo yalitokea katika mwaka wa 2010 ambao wananchi wengi wanajua.

Kutokana na matokeo ya wakati ule tulijifunza kitu kimoja kikubwa kwamba chama ni lazima kitoke kwa wanachama wenyewe. Hivyo, hiki ni chama cha wanachama, chama cha Watanzania.

1. Utambulisho wa CCK na Viongozi wake Napenda kutumia nafasi hii basi kuwatambulisha baadhi ya viongozi wa muda wa CCK ambao nimeambatana nao hapa ili kuweza kuuonesha umma kuwa chama chetu kimejipanga kuweza kujijenga kama chama cha siasa. Nitaanzia upande wangu wa kulia na kuwatambulisha kwenu viongozi hawa:

2.
Kwanini kimeanzishwa na kwanini kiitwe jina hilo Ndugu waandishi na wanachama, Swali kubwa ambalo bila ya shaka linahitaji jibu la moja kwa moja ni kwanini chama kingine kimeanzishwa Tanzania mahali ambapo tayari kuna vyama vingi vya kisiasa?

Swali hili ni swali ambalo litaulizwa labda zaidi na wanachama wa vyama vingine vya upinzani ambao wanaamini kabisa kuwa tayari kuna vyama vya kutosha vya upinzani na hivyo kuja kwa chama kingine cha upinzani itakuwa ni tishio kwa vyama hivyo vingine. Naomba nitoe sababu kubwa tatu tu za kwanini CCK kimeanzishwa na kwanini kinaitwa chama cha kijamii na siyo jina lolote jingine ambalo lingeweza kuonekana la kifahari fahari hivi. i. Hakuna chama kingine katika upinzani chenye msimamo kama wa kwetu.

Kama kungekuwepo na chama kingine chochote ambacho kinawakilisha hata nusu tu ya msimamo wa CCK tusingekuwa na sababu ya kuanzisha chama kingine lakini baada ya kupitia siasa za vyama vyote vya upinzani na kuona vyama hivyo vinavyofanya siasa zao tumegundua kuwa hakuna chama chenye msimamo na mtazamo kama wa kwetu kwenye masuala mbalimbali. Hili nitalielezea kidogo kwenye itikadi ya chama. ii. Wapo Watanzania wengi ambao hawajaridhika na vyama vilivyopo sasa.

Tangu upinzani urudi nchini mwanzoni mwa miaka ya tisini wamekuwepo Watanzania ambao hawajaridhishwa na mapendekezo ya kisiasa ambayo yametolewa na vyama vya upinzani vilivyopo hadi hivi sasa. Hawa ndio wale ambao waliamua kususia uchaguzi au wamebakia ni wapiga kura wa kuangalia majina ya watu na siyo chama chenyewe.

Kwenye taifa la watu karibu milioni 45 ipo nafasi ya kutosha tu kwa chama cha kwetu ambacho kimekuja ili kuwapa wananchi hawa chaguo walilokuwa wakilisubiria kwa muda mrefu. iii. CCK inaitikia changamoto za kizazi kipya; kizazi cha milenia mpya. Vyama karibu vyote vilivyopo sasa vinaitikia wito wa kizazi cha zamani; kizazi kinachopita.

Lakini CCK inaitikia changamoto za kizazi kipya siyo kwa kusahau ya zamani au kubeza kizazi kilichopita bali tunataka kuuleta ujumbe wa kizazi kilichopita kilichounda taifa letu kwenye kizazi kipya. CCK inataka kupokea kijiti cha kupokezana kwa vizazi kutoka kwa wale waliotutangulia. Ni chama kilichoundwa na kuanzishwa na vijana lakini kikiwa kimejikita katika hekima na heshima ya wazee wetu. Tunaamini wazee wetu watatuunga mkono na vijana watakuwa nasi vile vile!

Kwanini kinaitwa chama cha Kijamii?
Ndugu zangu, msingi wa mafanikio ya nchi yoyote ni msisitizo uliopo katika kuinua maisha ya jamii. Tunaamini kabisa kuwa sera zilizopo sasa zilizoundwa na CCM na serikali yake na hasa katika miaka kama ishirini iliyopita zimekuwa kinyume na jamii ya Watanzania. Tulipopata uhuru wazee wetu walitaka kuunda taifa "la jamii ya watu walio huru na sawa". Miaka hamsini sasa baada ya uhuru jamii ya aina hiyo inazidi kutoweka nchini, na njozi hiyo ikiendelea kuwakimbia wengi. Watu walio "huru na sawa" wamebakia kuwa wachache zaidi tena ni wale wenye nguvu za fedha, siasa na nafasi!

Msisitizo wa kuipigania jamii yetu katika ujumla wake wote haupo tena. Hivyo CCK ni chama cha Kijamii kwa sababu msisitizo wa fikra zake, mwelekeo wa sera zake na maono ya uongozi wake ni kuijenga jamii ya kisasa ya Kitanzania. Jamii ambamo watu wake wote watajisikia ni sehemu ya taifa hili na ambapo wakubwa kwa wadogo, wanawake kwa wanaume, weusi na weupe, wa bara na visiwani wanafurahia matunda ya kuwa ndani ya taifa hilo.

Msisitizo wetu ni jamii yetu na sera zetu zitalenga katika kuonesha kuwa ni katika wingi wa tofauti zetu katika jamii yetu ndio utajiri wa taifa letu umefichika! Hiki ni chama cha jamii ya Watanzania! Siyo chama cha tunu fulani fulani tu za maisha! Ni chama cha Kijamii! Itikadi yake Itikadi ya CCK ni uhafidhina wa kijamii na kiuchumi.

Yaani, socio-economic conservatism. Itikadi hii msingi wake ni historia yetu kama taifa na kama jamii ya watu. Tunaamini kuwa tishio kubwa kabisa katika jamii yetu ni kuvunjwa vunjwa kwa familia ya Kiafrika na vile vile matumizi makubwa ya serikali kwenye mambo mengi ambayo kwa kweli serikali isingestahili kuwa inayafanya.

Hivyo, CCK ni chama ambacho kinataka kutetea na kuyahifadhi mambo ya msingi yanayoifanya jamii yetu kuwa ya Kiafrika katika ulimwengu wa kisasa na hasa kutetea na kulinda familia. Tunaamini kabisa kuwa sera zozote na mipango yoyote ya nchi ambayo haiweki mkazo katika kuipa nafuu na kuboresha maisha ya familia sera hizo ni za kutupwa mbali.

Kwa muda mrefu sasa nchi yetu imejiingiza kwenye sera zenye kutukuza kile kinachoitwa "soko" matokeo yake wakati wenye "soko" wakiendelea kufanya vizuri mamilioni ya familia za Watanzania wanaishi maisha ya wasiwasi wa kudumu. Hivyo, tunataka kupendekeza sera ambazo zitalenga kuinua maisha ya wananchi wetu na hivyo kuinua maisha ya familia.

Lakini haya yote yanahitaji uchumi wa kisasa. Uchumi ambao unajiendesha wenyewe kwa kiasi kikubwa na ambao unalindwa vizuri. Sera za sasa za CCM zimeshindwa kutengeneza uchumi wa kisasa na badala yake zimetengeneza uchumi ambao ni watu wachache wananufaika. Hatuwezi kujenga uchumi huo kama tutaendelea kuangalia nje ya Tanzania kwa kutafuta misaada na kukopa badala ya kuweka mkazo katika uzalishaji na ulaji wa ndani.

Hivyo, kinyume na vyama vingine vilivyopo tunatarajia kuwa chama ambacho kinahifadhi mambo ya msingi ya uchumi na kijamii huku kikihakisha tunajenga taifa la kisasa.

Katika kutengeneza itikadi hii mpya chama chetu kitachota pasipo haya wala kuomba radhi katika hazina ya hekima ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na kujifunza huku tukiboresha nadharia zake nyingi ambazo tunaamini ni msingi wa kujenga taifa la watu walio sawa na wenye kuheshimu utu wa watu wote.

HIvyo, tutapinga ubaguzi wa aina yoyote dhidi ya Mtanzania mwingine, tutapigania maadili bora ya viongozi na kuhakikisha kuwa misingi iliyiounda taifa letu ikiwemo kupigania umoja wa Afrika, usawa na haki vinasimamiwa tena. Hatutavumilia kauli za kibaguzi zitakapotolewa na kiongozi au taasisi yeyote; kama Mwalimu alivyosema "Tanzania ni ya wote, na Watanzania ni wote"

3. Malengo/maudhui yake Kwa ufupi malengo ya chama chetu ni kuboresha maisha ya jamii yetu kwa kutumia uwezo wote ambao tumejaliwa na Mwenyezi Mungu. Uwezo wa akili, maliasili, nguvu kazi na hazina mbalimbali tulizojaliwa. Katika kufikia malengo hayo tutashiriki katika siasa za nchi yetu na kusimamisha wagombea wanaotokana na wananchi wenyewe na ambao wataongozwa na misingi hii ya chama hiki kipya.

4.
Hitimisho na jinsi chama kilivyopokewa na wananchi Baada ya matukio ya mwaka 2010 ambapo tulitambua kuwa baadhi ya watu waliotaka kuanzisha chama pamoja nasi walikuwa na lengo la kutaka madaraka tu na siyo kutumikia wananchi tuliamua toka wakati ule kutoshirikisha watu wanaoitwa "vigogo" isipokuwa wale tu ambao hawana mpango wa kutumia chama chetu kupata madaraka ya haraka.

Hivyo, CCK iliamua toka mapema kabisa kuwahusisha wananchi moja kwa moja na kwa ushawishi wa hoja na kuwaonesha kuwa yawezekana chaguo bora liko nje ya vile ambavyo watu wamevipokea au kuaminishwa kuwa ndio chaguo pekee.

Hivyo, tumetiwa moyo jinsi tulivyopokewa mikoani na vijijini ambapo watu walikaa chini kutusikiliza na kutupa nafasi ya kuwashawishi. Hatukutumia magazeti au vyombo vikubwa vya habari na badala yake tumeenda vijiji na miji ambapo tumekutana na wananchi ambao baada ya kutusikiliza wengi walikuwa wanatuambia maneno ya matumaini kuwa "hiki ndicho chama walichokuwa wanakisubiria". Tunawashukuru wananchi hawa hasa wakulima na vijana ambao wamechoshwa na sera mbovu zilizoshindwa kuboresha maisha yao.

5. Mfumo wa siasa hapa nchini Mojawapo ya matatizo makubwa ambayo yanatusumbua sasa hivi nchini na ambayo athari zake zinatoka kizazi kimoja kwenda kingine ni mfumo wetu wa kisiasa nchini. CCK inaamini kuwa mfumo huu wa kisiasa umepitwa na wakati na hauendani kabisa na matamanio ya kujenga taifa la kidemokrasia. Baadhi ya vitu ambavyo tunaamini vimepitwa na wakati na ambavyo vinahitaji kuondolewa mapema zaidi ni suala la ruzuku kwa vyama vya siasa.

Mfumo wa ruzuku uliingizwa kwenye siasa zetu na CCM kwa ajili ya kutafuta njia rahisi ya kupora raslimali zetu na kujinufaisha kwa migongo ya Watanzania. Hakuna sababu wala ulazima wa chama cha siasa kupewa fedha za umma kwa sababu tu ina watu waliochaguliwa kushika nafasi mbalimbali – huu ni wizi wa wazi! Sisi kama CCK tunataka na tutapigania hatimaye kuondolewa kwa mfumo huu wa ruzuku kwa vyama vya siasa kwani vinazawadia uzembe na ubadhirifu.

Iweje chama ambacho kimeshindwa kusimamia serikali yake na ufisadi umeshamiri chini yake bado kinapewa kila mwezi mabilioni ya fedha ambayo hayajafungwa na utendaji kazi wa chama hicho?

Yaani, haijalishi CCM inatawalaje lakini bado inalipwa kila mwezi na Watanzania! Hivyo, kinyume na vyama ambavyo vinaweza kudaiwa kuwa vimeundwa kwa ajili ya ruzuku CCK imeundwa huku ikiwa inatambua kuwa mfumo wa ruzuku ni wa hatari kwenye siasa zetu na kwa kweli ndio umechangia sana kuchelewesha kung'olewa kwa CCM madarakani!

Hivyo, katika mjadala wa Katiba Mpya sisi kama chama tutapigania na kuhakikisha kuwa ruzuku kwa vyama vya siasa zinafutwa ili kila chama kitegemee wanachama wake na akili zake kujiendesha. Kwani TANU ilipewa ruzuku na serikali ya Mkoloni ili ifanye siasa? Si ilitegemea wanachama wake? Kwanini kama wakati huo iliwezekana leo ishindikane?

6.
Ushirikiano na vyama vingine vya upinzani Tunapenda ieleweke mapema kabisa kuwa hatuna uadui na chama chochote cha upinzani na hatuna sababu ya kushindana na chama kingine cha upinzani ambacho malengo yake yanakaribiana nay a kwetu. Ugomvi wetu na mgogoro wetu ni Chama cha Mapinduzi na uongozi wake kwa taifa.

Hivyo, tunatangaza uadui wa kudumu na CCM na tutashirikiana na chama chochote kile ambacho kina lengo la kuona CCM inaondolewa madarakani. Hata hivyo, ushirikiano huo utategemea kukubaliana kwa sera mbalimbali siyo kukubaliana kwa kuondoa CCM tu madarakani.

Endapo hata hivyo, hatutaweza kufanya kazi na vyama vingine vya siasa kwa msingi wa kukubaliana kisera basi sisi wenyewe tutaendelea na juhudi zetu za kuona kuwa serikali ya CCM inadhoofishwa na hatimaye chama hicho kuondolewa madarakani kwa kutumia nguvu za kidemokrasia. Hivyo basi, tunanyosha mkono wa ushirikiano kwa vyama vingine vya upinzani nchini kuwa tuko tayari kushirikiana nao kwa namna ile ambayo vyama vyetu vitakubaliana.

7.
CCK kama chama kipya Chama chetu kina vijana wengi na vile vile nyuma yake wapo wazee ambao hekima yao tunaitegemea. Kina upya wa aina yake lakini vile vile kimejengwa kutoka katika misingi ya taifa. Hivyo, ni chama ambacho ni kipya lakini kinataka kujenga kutoka misingi ile ambayo CCM imeivunja vunja.

Kwa kweli ni chama mbadala hasa wa CCM na kinataka kuwarudishia wananchi wa Tanzania fahari yao. Tunataka kurudisha ule moyo wa uzalendo, kuipenda Tanzania na kuona fahari kuwa sisi ni Watanzania.

Hiki ni chama ambacho wananchi wamekuwa wakikisubiria. Hakina majina makubwa, hakina uwezo mkubwa wa kifedha na hakina raslimali nyingi za kutamba nazo lakini tulichonacho ni ujumbe wa wazi wa mabadiliko ya kweli yenye kutaka kulifanya taifa letu la kisasa kwa kusimamia sheria, uhuru wa habari na maoni, utu na usawa. Hivyo tunawakaribisha Watanzania wote ambao wamekuwa wakisubiria chama kama cha kwetu kujiunga nasi.

8. Hitimisho Kwa vile leo ni siku ya kwanza kutambulisha chama sitopenda kuzungumza mengi zaidi kwani nina uhakika siku zijazo tutaweza kuzungumza mengi zaidi. Sasa hivi kama chama tunajukumu la kujiandaa kuunda uongozi wetu wa kudumu na kujipanga zaidi kama chama na kuhakikisha tunakijenga chama mikoani.

Vile vile sitozungumza mengi zaidi kwa sababu tuna chaguzi mbalimbali ambazo zinakuja na tunataka kuangalia ni jinsi gani tunaweza kushiriki au kuunga mkono mgombea wa chama ambacho tunaamini kinawakilisha matarajio ya jamii husika.

Tunawashukuru kwa kuja kutusikiliza na kutupa nafasi ya kuwapelekea ujumbe kwa Watanzania kuwa "Mabadiliko ni sasa, na mabadiliko ni sisi"! Hatutasubiri tena watu wengine watuletee mabadiliko kwani mabadiliko ni yale ambayo sisi wenyewe tunajiletea. Asanteni. Constantine B. Akitanda Mwenyekiti CCK -Taifa
 
ningependa kujua msimamo wenu kuhusu muungano. kama utakuwa uko sawa na msimamo wangu nikinadi zenji nije niwe balozi wenu
 
Naona mmefanyia kazi utabiri wa Shekeh Yahaya. Kimsingi, kuitikia witu wa mtu aliyekuwa akiongozwa na mashetani maana yake ni kuiweka nchi chini ya majini na mashetani. Ni tatizo hili hili ambalo limepelekea nchi yetu kuwa katika hali ngumu ya kiuchumi, kielimu na kisiasa.
Ningependa kuuliza ni nini hasa mlichoona hakikidhi haja zenu katika siasa za upinzani mpaka mfikie maamuzi haya. Chadema katika siku za karibuni wamekuwa wakifanya vizuri sana. Kwa nini msingewaunga mkono ili kuweza kukamilisha ukombozi wa nchi? Je ni nini kitakachonishawishi nisiamini kwamba ninyi mnatumika kisiasa kupunguza kura za upinzani ambao chadema imeujenga? Hivi ninyi magamba mtaendelea kuigawa nchi yetu hata lini?
 
AKITANDA WEW NI MGENI HAPA AU??UKIPOST KITU KAMA HIKI NI LAZIMA URUDI NA KUJIBU MASWALI SASA WEWE UNAWEKA NA KUKIMBIA KAMA UMEJISAIDIA MAHALI NA KUONDOKA SIO SAWA RUDI HAPA UJIBU MASWALI,MIMI NITAJIUNGA NA CHAMA CHAKO KAMA UTAJIBU KWA UFASAHA HAYA YAFUATAYO

-CCK KINA KATIBA,kama ipo weka hapa kama hamna mna mpango gani
-UCHAGUZI WA CCK ULIFANYIKA LINI-umesema wewe ni mwenyekiti wa CCK taifa,mlichagua lini??
-CCK ina wanachama wangapi kila Mkoa tafadhali
-JE CCK MNA OFISI YA KUDUMU??
-MNAPATA HELA ZENU KUTOKA WAPI??
-MISINGI YENU IKOJE KULE UPANDE WA PILI WA JAMHURI(PEMBA NA UNGUJA)


JIBU HAYO HALAFU NITAULIZA MENGINE BAADA YA MAJIBU YAKO,USISAHAU KUWEKA HAPA FOMU YA KUJIUNGA NA GHARAMA ZENU
 
Yaani umejiunga JF kutangaza chama? Huko nyuma ulikuwa wapi?

Karibu. Naomba katiba ya chama nione kama ina itikadi!
 
crap mnazidi kuongeza utitili wa vyama, badala muwe kitu kimoja mmejaa ubinafsi, hata nchi zilizoendelea zina vya havizidi vinne nyie msiotumia akili mnavyama zaidi ya kumi
 
Mwanakijiji, ni mwenzenu? Ebu weka katiba ya chama tuipitie kama inafaa.
 
Tuna vyama karibu 20 kama sikosei ina maana nyinyi vyama vyote hivi hamkuona chama cha kujiunga nacho ambacho malengo yenu yanafanana? Huu ni usanii unaokuja kwa kimvuli cha Demokrasia. CCJ = CCK = Ubabaishaji na usanii tu.
 
Njaa tu inawasumbua.Watanzania wameshaamua kukumbatia CDM.Mnachohangaikia ni Ruzuku tu na madaraka ndani ya vyama.
 
Richard Kyalo yuko wapi? Mbona mmemtosa? Ni wazi CCJ ndio CCK sasa wako wapi kina nape,sita,mpendazoe???
Kwanin msianzishe chama cha ku-manufacture more teachers and doctors?
 
Back
Top Bottom