April
Member
- Nov 14, 2011
- 35
- 21
Kufuatia kupitishwa kwa SHERIA ya marekebisho ya KATIBA leo Bungeni, Mh. Kafulila atoa maoni yake akitofautiana na maamuzi yaliyopitishwa leo. Mh. Kafulila ameandika waraka huu akiufafanulia UMMA juu ya mchakato huo uliopitishwa jinsi gani hauna TIJA wala hautaleta mabadiliko yoyote ambayo wanaharakati na wananchi kwa ujumla wameazimia.
MAONI YA MH. DAVID KAFULILA
Habari Watanzania,
Nina maoni tofauti kuhusu hiki kinachoendelea kuhusu marekebisho ya sheria ya kusimamia mchakato wa katiba mpya.
Nimejaribu kuomba kuchangia ili niweke maoni yangu wazi lakini imeshindikana, Spika amesema NCCR amepewa mtu mmoja tu Mh. Machali hivyo nikaona ni vema niwajulishe kupitia mtandao maoni yangu.
UTANGULIZI
Hapa ningependa kukumbusha kuwa kutoka NCCR ni mimi David Kafulila na Felix Mkosamali ambao tulikuwa wajumbe wa kamati ya sheria na Utawala. Mh.Mkosamali ni mjumbe wa kudumu kwenye kamati hii, mimi ni miongoni mwa wajumbe walio ongezwa wakati wa kupitia muswada huu. Pia ikumbukwe kuwa ni mimi na Mkosamali ambao tuliungana na CHADEMA kutoka nje katika mkutano wa tano wa Bunge kupinga namna mchakato ulivyoendeshwa. Niliomba kuchangia bungeni lakini imeshindikana kabisa kupata nafasi lakini kwa kuzingatia umuhimu wa jambo hili na nafasi niliyokuwa nayo katika jambo hili naona kuna umuhimu wa kuzungumza kitu kwani hata wale mabalozi wa nchi tano za Ulaya walipokuja bungeni kwenye mkutano wa tano ni mimi niliyekuwa mmoja wa wabunge waliokutana nao kutoa maoni.
MAONI
Nimeshangaa kuona mvutano wa kisiasa kuhusu mabadiliko yaliyoletwa na serikali kwani ninavyofahamu kuna mambo mengi ya msingi katika sheria hii ambayo yalipaswa kubadilishwa, na nilidhani ndiyo yangeletwa kwenye marekebisho ya sheria hii baada ya vikao vya Rais na wadau wengine vikiwemo vyama vya siasa. Mabadiliko yaliyoletwa sio issues za msingi ambazo zingesaidia kuiboresha tume na mchakato mzima wa katiba mpya.
Kwa mfano;
1. Hoja ya kumwondoa DC na Kuweka Mkurugenzi (DED)
Wabunge wengi wa CCM wanataka DC ndio asimamie, wakati hotuba ya kambi rasmi ya upinzani inapendekeza DED.
Ukweli ni kwamba wote DED na DC hawafai kwasababu wote ni sehemu ya serikali na badala yake ilipaswa jukumu hilo litekelezwe na Tume yenyewe ambayo inapaswa kuwa huru.
2.Hapa ndipo inakuja hoja ya mchakato huu mzima wa kura ya maoni kusimamiwa na Tume huru.
Uamuzi wa kuifanya Tume ya sasa ya Uchaguzi kusimamia mchakato huu ni kinyume cha msimamo wetu wa awali kama wapinzani kwasababu moja ya hoja ya mahitaji ya katiba mpya ni tume huru ya uchaguzi, sasa inawezekanaje tume mbovu ya uchaguzi isimamie mchakato wa kupata katiba huru?. Hili lilikuwa muhimu sana. Tungekubaliana kuhusu kupata kwanza tume huru ya uchaguzi kisha tume hiyo isimamie mchakato wa katiba mpya tungekuwa na uhakika wa kupata katiba ambayo watanzania wanaitaka.
3.Hoja ya Tume huru ya kusimamia mchakato wa katiba
Hii pia ni hoja iliyoachwa kwasababu Tume hii ya sasa inateuliwa na Rais na kwa namna ilivyo bado Rais ndio mwenye mamlaka ya kumtoa mjumbe yeyote. Marekebisho yaliyoletwa leo yanapendekeza namna ya kumtoa mjumbe wa tume hii ambaye anayetuhumiwa kukiuka kanuni za maadili, kwamba Rais atateua Kamati ya kufanya maamuzi. Hapa haikupaswa Rais kuteua kamati badala yake ilitakiwa sheria itamke rasmi kamati hiyo itakuwa akina nani ili kamati hiyo iwe huru kuliko iteuliwe na Rais, pengine kosa la mjumbe ni mvutano unaohusu nguvu za serikali kwa tume.
4. Hoja ya Sekretariet huru.
Kwa mujibu wa sheria hii Sekratariet itaundwa na waziri mwenye dhamana. Hii inaondoa uhuru wa utendaji wa sekretariet, ilipaswa Sekretariet iteuliwe na Tume na iwajibike kwa tume ili kupunguza mkono wa serikali kwenye mchakato na utendaji wa kupata katiba mpya.
5. Hoja ya ushiriki wa Jumuiya za kiraia, taasisi za dini vya vyama vya siasa
Marekebisho yaliyoletwa sehemu A, kifungu cha 7 yanatoa uhuru wa jumuiya hizi kushiriki kwa kualikwa na Rais, lakini sehemu hiyo hiyo ya marekebisho kifungu cha 8 inatamka kuwa Rais hafungwi na mapendekezo hayo kuteua watu wengine kuwa wajumbe. Hapa kwa tafsiri rahisi ni kwamba, haki imetolewa kwenye kifungu cha 7 na imepokonywa kwenye kifungu cha 8 kwa kuwaweka wananchi tayari wasishangae itakapotokea mapendekezo yaliyopelekwa na jumuiya yoyote kukataliwa yote. Ingepaswa kuweka wazi kuwa Rais atalazimika kuteua miongoni mwa walipendekezwa na sio nje ya waliopendekezwa.
Kwa ujumla pamoja na sheria hii kupitishwa leo lakini ina matundu makubwa sana kuweza kuifanya isimamie mchakato huu muhimu kwa uhakika. Bado ni sheria ambayo inategemea sana dhamira ya Rais mwenyewe kuliko mfumo tulioweka.
Napenda ifahamike kuwa, sheria hii iliyopitishwa leo haijafanya mabadiliko ya msingi ambayo sisi sote ( wananchi, wanaharakati na wanasiasa) wenye moyo wa dhati wa kuleta mabadiliko kitaifa tulitazamia.
Pamoja katika kujenga Taifa
David Kafulila